Matendo 21:1-40
21 Sasa tulipokuwa tumejiondoa kwao na kusafiri baharini, tulikwenda kwa mwendo wa moja kwa moja tukaja mpaka Kosi, lakini siku iliyofuata tukaja mpaka Rode, na kutoka huko mpaka Patara.
2 Na tulipokuwa tumepata mashua iliyokuwa ikivuka kwenda Foinike, tukapanda ndani, tukasafiri kwenda zetu.
3 Baada ya kuja mahali tulipoweza kuona kisiwa cha Kipro+ tukakiacha nyuma upande wa kushoto, tukasafiri mpaka Siria,+ tukafika Tiro, kwa maana mashua ilipaswa ipakue shehena yake huko.+
4 Baada ya kuwatafuta, tuliwapata wanafunzi na kukaa huko siku saba. Lakini kupitia roho+ wakarudiarudia kumwambia Paulo asikanyage Yerusalemu.
5 Kwa hiyo tulipokuwa tumekamilisha hizo siku, tukatoka na kuanza kwenda; lakini hao wote, pamoja na wanawake na watoto, wakatupeleka mpaka nje ya jiji. Tukapiga magoti+ pwani, tukasali
6 na kuagana,+ nasi tukapanda ndani ya mashua lakini wao wakarudi nyumbani kwao.
7 Ndipo tukakamilisha safari ya baharini kutoka Tiro tukafika Tolemai, nasi tukawasalimu akina ndugu na kukaa siku moja pamoja nao.
8 Siku iliyofuata tukaondoka tukafika Kaisaria,+ nasi tukaingia katika nyumba ya Filipo mweneza-injili, aliyekuwa mmoja wa wale watu saba,+ nasi tukakaa pamoja naye.
9 Mtu huyu alikuwa na binti wanne, mabikira, waliotoa unabii.+
10 Lakini tulipokuwa tukikaa siku kadhaa, nabii fulani anayeitwa Agabo+ akashuka kutoka Yudea,
11 naye akaja mahali tulipokuwa na kuuchukua mshipi wa Paulo, akafunga miguu na mikono yake mwenyewe na kusema: “Hivi ndivyo inavyosema roho takatifu, ‘Mwanamume ambaye mshipi huu ni wake, Wayahudi watamfunga+ hivi katika Yerusalemu na kumtia+ mikononi mwa watu wa mataifa.’ ”
12 Sasa tuliposikia jambo hilo, sisi na pia watu wa mahali hapo tukaanza kumsihi asipande+ kwenda Yerusalemu.
13 Ndipo Paulo akajibu: “Mnafanya nini kwa kulia+ na kunifanya dhaifu moyoni?+ Muwe na hakika, niko tayari si kufungwa tu bali pia kufa+ Yerusalemu kwa ajili ya jina la Bwana Yesu.”
14 Alipokataa kushawishika, tukakubali kimyakimya maneno haya: “Mapenzi+ ya Yehova na yatendeke.”
15 Sasa baada ya siku hizo tukajitayarisha kwa ajili ya safari, tukaanza kupanda kwenda Yerusalemu.+
16 Lakini wengine kati ya wanafunzi kutoka Kaisaria+ wakaenda pamoja nasi pia, ili kutuleta kwa mtu ambaye nyumbani mwake tulipaswa kukaribishwa, Mnasoni wa Kipro, mwanafunzi wa zamani.
17 Tulipoingia Yerusalemu,+ akina ndugu wakatukaribisha kwa furaha.+
18 Lakini siku iliyofuata Paulo akaingia pamoja nasi kwa Yakobo;+ na wanaume wote wazee walikuwapo.
19 Naye akawasalimu na kuanza kusimulia+ kirefu juu ya mambo ambayo Mungu alifanya katikati ya mataifa kupitia kwa huduma yake.+
20 Baada ya kusikia jambo hilo wakaanza kumtukuza Mungu, nao wakamwambia: “Unaona, ndugu, jinsi kulivyo na maelfu mengi ya waamini walio kati ya Wayahudi; nao wote ni wenye bidii kuhusu Sheria.+
21 Lakini wamesikia uvumi ukitolewa juu yako kwamba wewe umekuwa ukiwafundisha Wayahudi wote kati ya mataifa uasi-imani wa kumwacha Musa,+ ukiwaambia wasiwatahiri+ watoto wao wala kujiendesha katika desturi za kisherehe.
22 Basi, ni nini kinachopaswa kufanywa juu ya hilo? Kwa vyovyote vile watasikia umefika.
23 Kwa hiyo fanya jambo hili tunalokuambia: Tuna wanaume wanne wenye nadhiri juu yao wenyewe.
24 Wachukue watu hawa pamoja nawe+ ujitakase kisherehe pamoja nao na kuwagharimia,+ ili wapate kunyolewa+ vichwa vyao. Na kwa hiyo kila mtu atajua kwamba uvumi mwingi walioambiwa juu yako si kitu, bali kwamba unatembea kwa utaratibu, wewe mwenyewe pia ukishika Sheria.+
25 Kwa habari ya wale waamini kutoka kati ya mataifa, tumetuma watu, tukitoa uamuzi wetu kwamba wanapaswa kujiepusha na vitu vilivyotolewa dhabihu kwa sanamu+ na pia damu+ na vitu vilivyonyongwa,+ na uasherati.”+
26 Ndipo Paulo akawachukua wanaume hao pamoja naye siku iliyofuata akajitakasa kisherehe pamoja nao+ na kuingia ndani ya hekalu, kutoa taarifa juu ya siku ambazo zingetimizwa+ kwa huo utakaso wa kisherehe, mpaka toleo+ litolewe kwa ajili ya kila mmoja wao.+
27 Sasa zile siku saba+ zilipokuwa karibu kumalizika, Wayahudi kutoka Asia walipomwona katika hekalu wakaanza kuuvuruga umati wote,+ nao wakamkamata,
28 wakipaaza sauti: “Wanaume wa Israeli, saidieni! Huyu ndiye mwanamume anayefundisha kila mtu kila mahali dhidi ya watu+ na Sheria na mahali hapa na, zaidi ya hayo, hata aliwaingiza Wagiriki katika hekalu naye amepatia unajisi mahali hapa patakatifu.”+
29 Kwa maana hapo kwanza walikuwa wamemwona Trofimo+ Mwefeso katika jiji akiwa pamoja naye, lakini walikuwa wakiwazia Paulo alikuwa amemwingiza katika hekalu.
30 Na jiji lote likawa na mchafuko,+ na watu wakaanza kukimbia pamoja; nao wakamkamata Paulo wakamkokota nje ya hekalu.+ Na mara moja milango ikafungwa.
31 Na walipokuwa wakitafuta kumuua, kiongozi wa kikosi cha askari-jeshi akaletewa habari kwamba Yerusalemu lote lilikuwa katika mvurugo;+
32 naye mara moja akachukua askari-jeshi na maofisa-jeshi na kuwakimbilia huko chini.+ Walipomwona kiongozi huyo wa kijeshi+ na askari-jeshi, wakaacha kumpiga Paulo.
33 Ndipo kiongozi wa kijeshi akaja karibu akamkamata na kutoa amri afungwe minyororo miwili;+ naye akaanza kuuliza huyo ni nani na alikuwa amefanya nini.
34 Lakini wengine katika umati wakaanza kupaaza sauti kuhusu jambo moja, na wengine kuhusu lingine.+ Kwa hiyo, kwa kuwa hangeweza kujua jambo lolote la hakika kwa sababu ya fujo hizo, akaamuru aletwe kwenye makao ya askari-jeshi.+
35 Lakini alipofika juu ya ngazi, akachukuliwa na wale askari-jeshi kwa sababu ya jeuri ya umati;
36 kwa maana umati wa watu uliendelea kufuata, ukipaaza sauti: “Mwondolee mbali!”+
37 Na alipokuwa karibu kuingizwa katika makao ya askari-jeshi, Paulo akamwambia kiongozi wa kijeshi: “Je, ninaruhusiwa kukuambia jambo fulani?” Akasema: “Je, unaweza kusema Kigiriki?
38 Je, kwa kweli wewe si yule Mmisri ambaye kabla ya siku hizi alichochea uasi+ na kuwaongoza kuingia nyikani wale wanaume elfu nne wenye kutumia visu?”
39 Ndipo Paulo akasema: “Mimi, kwa kweli, ni Myahudi+ wa Tarso+ katika Kilikia, raia wa jiji ambalo si lenye kukosa umashuhuri. Kwa hiyo ninakuomba, uniruhusu niseme na watu hawa.”
40 Baada ya kutoa ruhusa, Paulo, akiwa amesimama juu ya ngazi, akawapungia+ watu mkono wake. Kulipokuwa na kimya kikubwa, akawahutubia kwa lugha ya Kiebrania,+ akisema: