Kwa Waebrania 9:1-28

  • Utumishi mtakatifu katika hekalu la duniani (1-10)

  • Kristo aingia mbinguni akiwa na damu yake (11-28)

    • Mpatanishi wa agano jipya (15)

9  Basi, kwa upande wake, lile agano la zamani lilikuwa na matakwa ya kisheria kwa ajili ya utumishi mtakatifu na mahali pake patakatifu+ duniani.  Kwa maana chumba cha kwanza cha hema kilijengwa, na ndani yake mlikuwa na kinara cha taa+ na meza na mikate ya toleo;*+ nacho kinaitwa Mahali Patakatifu.+  Lakini nyuma ya pazia la pili+ kulikuwa na chumba cha hema kilichoitwa Patakatifu Zaidi.+  Hicho kilikuwa na chetezo cha dhahabu+ na sanduku la agano+ likiwa limefunikwa kabisa kwa dhahabu,+ ambalo ndani yake mlikuwa na mtungi wa dhahabu wenye mana,+ fimbo ya Haruni iliyochipuka,+ na yale mabamba+ ya agano;  na juu yake palikuwa na wale makerubi wenye utukufu waliokifunika kile kifuniko cha upatanisho.*+ Lakini sasa si wakati wa kuzungumzia mambo hayo kirefu.  Baada ya vitu hivyo kujengwa kwa njia hiyo, makuhani huingia katika chumba cha kwanza cha hema kwa ukawaida ili kutoa utumishi mtakatifu;+  lakini kuhani mkuu huingia ndani ya chumba cha pili akiwa peke yake mara moja kwa mwaka,+ akiwa na damu,+ ambayo huitoa kwa ajili yake mwenyewe+ na kwa ajili ya dhambi ambazo watu+ walifanya bila kujua.  Hivyo roho takatifu hufanya iwe wazi kwamba njia ya kuingia mahali patakatifu bado haikuwa imefunuliwa lile hema la zamani lilipokuwa limesimama.+  Hema hili ni mfano kwa ajili ya wakati huu,+ na kulingana na mpango huu, zawadi na dhabihu zinatolewa.+ Hata hivyo, haziwezi kufanya dhamiri ya mtu anayefanya utumishi mtakatifu iwe kamilifu.+ 10  Zinahusu vyakula na vinywaji tu na njia mbalimbali za kujisafisha kisherehe.*+ Hayo yalikuwa matakwa ya kisheria kuhusu mwili+ nayo yalifuatwa mpaka wakati uliowekwa wa kunyoosha mambo. 11  Hata hivyo, Kristo alipokuja akiwa kuhani mkuu wa mambo mema ambayo tayari yamefanyika, aliingia katika hema kubwa na kamilifu zaidi ambalo halikutengenezwa kwa mikono, yaani, si la uumbaji huu. 12  Aliingia mahali patakatifu, si kwa damu ya mbuzi na ya ng’ombe dume wachanga, bali kwa damu yake mwenyewe,+ mara moja kwa wakati wote, na kupata ukombozi wa* milele kwa ajili yetu.+ 13  Kwa maana ikiwa damu ya mbuzi na ya ng’ombe dume+ na majivu ya ndama jike yaliyonyunyizwa juu ya wale ambao wametiwa unajisi hutakasa ili kuusafisha mwili,+ 14  je, damu ya Kristo,+ ambaye kupitia roho inayodumu milele alijitoa mwenyewe kwa Mungu bila dosari, haitazisafisha hata zaidi dhamiri zetu kutoka katika matendo yaliyokufa+ ili tumtolee utumishi mtakatifu Mungu aliye hai?+ 15  Hiyo ndiyo sababu yeye ni mpatanishi wa agano jipya,+ ili kwa sababu kifo kimetokea kusudi waachiliwe huru kupitia fidia+ kutoka kwenye makosa chini ya agano la zamani, wale ambao wameitwa waipokee ahadi ya urithi unaodumu milele.+ 16  Kwa maana palipo na agano, kifo cha mwanadamu anayefanya agano kinahitaji kuthibitishwa, 17  kwa sababu agano huwa halali kifo kinapotokea, kwa kuwa halitumiki ikiwa mwanadamu anayefanya agano bado yuko hai. 18  Kwa hiyo, lile agano la zamani halikuanza kutumika* bila damu. 19  Kwa maana Musa alipowatajia watu wote kila amri ya Sheria, alichukua damu ya wale ng’ombe dume wachanga na ya wale mbuzi, pamoja na maji, sufu nyekundu, na hisopo, na kukinyunyizia kile kitabu* na watu wote, 20  akisema: “Hii ndiyo damu ya agano ambalo Mungu amewaamuru mlishike.”+ 21  Vilevile alilinyunyizia damu lile hema na vyombo vyote vya utumishi mtakatifu.*+ 22  Ndiyo, kulingana na Sheria karibu vitu vyote husafishwa kwa damu,+ na hakuna msamaha unaopatikana bila kumwaga damu.+ 23  Kwa hiyo, ilikuwa muhimu kwa mifano ya uhalisi+ wa vitu vilivyo mbinguni kusafishwa kwa njia hiyo,+ lakini vitu vya mbinguni vinahitaji dhabihu zilizo bora zaidi. 24  Kwa maana Kristo hakuingia mahali patakatifu palipotengenezwa kwa mikono,+ ambapo ni mfano wa uhalisi,+ bali aliingia mbinguni kwenyewe,+ hivi kwamba sasa anaonekana mbele za* Mungu kwa ajili yetu.+ 25  Hilo halikufanywa ili ajitoe mwenyewe mara nyingi, kama kuhani mkuu anavyoingia mahali patakatifu mwaka baada ya mwaka+ akiwa na damu ambayo si yake mwenyewe. 26  La sivyo, ingekuwa lazima ateseke mara nyingi tangu kuwekwa msingi wa ulimwengu. Lakini sasa amejifunua mara moja kwa wakati wote kwenye umalizio wa mifumo ya mambo* ili kuondoa dhambi kupitia dhabihu yake mwenyewe.+ 27  Na kama vile watu wamewekwa akiba kufa mara moja kwa wakati wote, lakini baada ya hapo wapokee hukumu, 28  vivyo hivyo pia Kristo alitolewa mara moja kwa wakati wote ili kubeba dhambi za wengi;+ na mara ya pili atakapotokea itakuwa bila dhambi,* naye ataonwa na wale wanaomtazamia kwa bidii kwa ajili ya wokovu wao.+

Maelezo ya Chini

Au “mikate ya wonyesho.”
Au “mahali pa kufunika dhambi.”
Tnn., “ubatizo wa aina mbalimbali.”
Tnn., “fidia ya; wokovu wa.”
Tnn., “halikuzinduliwa.”
Au “kitabu cha kukunjwa.”
Au “utumishi wa watu wote.”
Tnn., “mbele za uso wa.”
Angalia Kamusi, “Mfumo wa mambo.”
Au “hatakuja kushughulika na dhambi.”