Mathayo 26:1-75
26 Basi Yesu alipokuwa amemaliza kusema yote hayo, aliwaambia wanafunzi wake:
2 “Mnajua kwamba siku mbili tangu sasa kutakuwa na pasaka,+ naye Mwana wa binadamu atatolewa ili atundikwe mtini.”+
3 Ndipo wakuu wa makuhani na wanaume wazee wa watu wakakusanyika pamoja katika ua wa kuhani mkuu aliyeitwa Kayafa,+
4 na kushauriana+ pamoja ili wamkamate Yesu kwa hila na kumuua.
5 Hata hivyo, wao wakawa wakisema: “Si kwenye sherehe, ili ghasia zisitokee katikati ya watu.”+
6 Ikawa kwamba Yesu alipokuwa Bethania+ katika nyumba ya Simoni mwenye ukoma,+
7 mwanamke mwenye chupa ya alabasta iliyo na mafuta ghali yenye marashi+ akamkaribia, naye akaanza kuyamimina juu ya kichwa cha Yesu alipokuwa ameketi mezani.
8 Walipoona hilo wanafunzi wakaghadhibika na kusema: “Hasara hii ni ya nini?+
9 Kwa maana yangaliweza kuuzwa kwa kiasi kikubwa na kupewa maskini.”+
10 Akijua jambo hilo,+ Yesu akawaambia: “Kwa nini mnataka kumsumbua mwanamke huyu? Kwa kuwa amenitendea tendo jema.+
11 Kwa maana ninyi mna maskini+ pamoja nanyi sikuzote, lakini hamtakuwa pamoja nami sikuzote.+
12 Kwa kuwa mwanamke huyu alipotia mafuta haya yenye marashi juu ya mwili wangu, alifanya hivyo ili kunitayarisha kwa ajili ya maziko.+
13 Kwa kweli ninawaambia ninyi, Kokote ambako hii habari njema itahubiriwa katika ulimwengu wote, jambo ambalo mwanamke huyu ametenda litasimuliwa pia kuwa kumbukumbu lake.”+
14 Ndipo mmoja wa wale kumi na wawili, anayeitwa Yuda Iskariote,+ akaenda kwa wakuu wa makuhani
15 na kusema: “Mtanipa nini ili nimsaliti kwenu?”+ Wakamwagizia vipande 30 vya fedha.+
16 Kwa hiyo tangu wakati huo na kuendelea akawa akitafuta nafasi nzuri ya kumsaliti.+
17 Katika siku ya kwanza ya keki zisizo na chachu+ wanafunzi wakamjia Yesu, wakisema: “Ni wapi unapotaka tukutayarishie uile pasaka?”+
18 Akasema: “Nendeni jijini kwa Fulani-wa-fulani,+ mkamwambie, Mwalimu anasema, ‘Wakati wangu uliowekwa uko karibu; nitasherehekea pasaka pamoja na wanafunzi wangu nyumbani mwako.’ ”+
19 Nao wanafunzi wakafanya kama Yesu alivyowaagiza, nao wakatayarisha vitu kwa ajili ya pasaka.+
20 Basi, ilipofika jioni,+ alikuwa ameketi mezani pamoja na wale wanafunzi kumi na wawili.+
21 Walipokuwa wakila, alisema: “Kwa kweli ninawaambia ninyi, Mmoja wenu atanisaliti.”+
22 Wakiwa wamehuzunishwa sana na jambo hilo, kila mmoja wao akaanza kumwambia: “Bwana, je, ni mimi?”+
23 Akajibu, akasema: “Yule anayechovya mkono wake pamoja nami katika bakuli ndiye atakayenisaliti.+
24 Kwa kweli, Mwana wa binadamu anaenda zake, kama ilivyoandikwa+ kumhusu, lakini ole+ wake mtu yule ambaye kupitia kwake Mwana wa binadamu atasalitiwa!+ Ingalikuwa afadhali kwake kama mtu huyo asingalizaliwa.”
25 Yuda, aliyekuwa karibu kumsaliti, akajibu, akasema: “Je, ni mimi, Rabi?” Akamwambia: “Wewe mwenyewe umesema.”
26 Walipokuwa wakiendelea kula, Yesu alichukua mkate+ na, baada ya kutoa baraka, akaumega,+ akawapa wanafunzi, akasema: “Chukueni, mle. Huu unamaanisha mwili wangu.”+
27 Pia, akachukua kikombe+ na, akiisha kushukuru, akawapa, akisema: “Kinyweeni, ninyi nyote;+
28 kwa maana hii inamaanisha+ ‘damu+ yangu ya agano,’+ ambayo itamwagwa kwa ajili ya wengi+ kwa msamaha wa dhambi.+
29 Lakini ninawaambia ninyi, Tangu sasa sitakunywa kamwe divai yoyote ya mzabibu mpaka siku ile nitakapokunywa ikiwa mpya, pamoja nanyi katika ufalme wa Baba yangu.”+
30 Mwishowe, baada ya kuimba sifa,+ wakatoka na kwenda kwenye Mlima wa Mizeituni.+
31 Ndipo Yesu akawaambia: “Ninyi nyote mtakwazika kuhusiana nami usiku huu, kwa maana imeandikwa, ‘Nitampiga mchungaji, nao kondoo wa kundi watatawanyika huku na huku.’+
32 Lakini baada ya kufufuliwa nitawatangulia kuingia Galilaya.”+
33 Lakini Petro akajibu, akamwambia: “Ijapokuwa wengine wote wakwazike kuhusiana nawe, mimi sitakwazika kamwe!”+
34 Yesu akamwambia: “Kwa kweli ninakuambia wewe, Usiku huu, kabla ya jogoo kuwika, utanikana mara tatu.”+
35 Petro akamwambia: “Hata nikilazimika kufa pamoja nawe, mimi sitakukana kamwe.” Wale wanafunzi wengine wote wakasema vivyo hivyo pia.+
36 Ndipo Yesu akaja pamoja nao mpaka mahali+ panapoitwa Gethsemane, naye akawaambia wanafunzi: “Ketini hapa ninapoenda pale na kusali.”+
37 Naye akawachukua Petro na wale wana wawili+ wa Zebedayo pamoja naye, akaanza kuhuzunika na kutaabika sana.+
38 Ndipo akawaambia: “Nafsi yangu ina huzuni sana, kiasi cha kufa.+ Kaeni hapa na mwendelee kukesha pamoja nami.”+
39 Naye akasonga mbele kidogo, akaanguka kifudifudi, akasali+ na kusema: “Baba yangu, ikiwezekana, kikombe hiki+ na kipitilie mbali kutoka kwangu. Lakini, si kulingana na mapenzi yangu,+ bali kulingana na mapenzi yako.”+
40 Naye akaja walipokuwa wanafunzi na kuwakuta wamelala usingizi, naye akamwambia Petro: “Je, hamngeweza kukesha hata saa moja pamoja nami?+
41 Endeleeni kukesha+ na kusali+ sikuzote, ili msiingie katika jaribu.+ Bila shaka, roho inataka, lakini mwili ni dhaifu.”+
42 Tena, kwa mara ya pili,+ akaenda zake na kusali, akisema: “Baba yangu, ikiwa haiwezekani kipitilie mbali ila nikinywe, acha mapenzi yako yatendeke.”+
43 Naye akaja tena na kuwakuta wamelala usingizi, kwa maana macho yao yalikuwa mazito.+
44 Kwa hiyo akawaacha, akaenda zake tena na kusali kwa mara ya tatu,+ akisema mara moja tena neno lilelile.
45 Kisha akaja walipokuwa wanafunzi na kuwaambia: “Wakati kama huu ninyi mnalala usingizi na kupumzika! Tazameni! Saa imekaribia Mwana wa binadamu asalitiwe na kutiwa katika mikono ya watenda-dhambi.+
46 Simameni, twende. Tazama! Msaliti wangu amekaribia.”+
47 Na alipokuwa bado akisema, tazama! Yuda,+ mmoja wa wale kumi na wawili, akaja pamoja na umati mkubwa ukiwa na mapanga+ na marungu kutoka kwa wakuu wa makuhani na wanaume wazee wa watu.+
48 Basi msaliti wake alikuwa amewapa ishara, akisema: “Yeyote yule nitakayembusu, huyo ndiye; mkamateni.”+
49 Naye akaenda moja kwa moja kwa Yesu akasema: “Siku njema, Rabi!”+ na kumbusu+ kwa wororo sana.
50 Lakini Yesu+ akamwambia: “Mwenzangu, uko hapa kwa kusudi gani?” Ndipo wakaja wakaweka mikono juu ya Yesu na kumkamata.+
51 Lakini, tazama! mmoja wa wale waliokuwa pamoja na Yesu akanyoosha mkono wake akauchomoa upanga wake, akampiga mtumwa wa kuhani mkuu akalikata sikio lake.+
52 Ndipo Yesu akamwambia: “Rudisha upanga wako mahali pake,+ kwa maana wale wote wanaouchukua upanga wataangamia kwa upanga.+
53 Au unafikiri kwamba siwezi kumwomba Baba yangu anipe sasa hivi vikosi zaidi ya kumi na viwili vya malaika?+
54 Hata hivyo, Maandiko yangetimizwaje kwamba lazima itendeke hivi?”
55 Ndipo Yesu akauambia umati: “Je, mmetoka mkiwa na mapanga na marungu kana kwamba ni kwenda juu ya mnyang’anyi ili kunikamata?+ Siku baada ya siku nilikuwa nikiketi katika hekalu+ nikifundisha, na bado hamkunikamata.
56 Lakini yote haya yametukia ili maandiko ya manabii yatimizwe.”+ Ndipo wanafunzi wote wakamwacha na kukimbia.+
57 Wale waliomkamata Yesu wakampeleka kwa Kayafa+ kuhani mkuu, ambako waandishi na wanaume wazee walikuwa wamekusanywa pamoja.+
58 Lakini Petro akaendelea kumfuata akiwa mbali kiasi, mpaka katika ua+ wa kuhani mkuu, na, baada ya kuingia ndani, akaketi pamoja na watumishi wa nyumbani ili kuona matokeo.+
59 Wakati huohuo wakuu wa makuhani na Sanhedrini nzima walikuwa wakitafuta ushahidi wa uwongo juu ya Yesu ili wamuue,+
60 lakini hawakupata wowote, ijapokuwa mashahidi wengi wa uwongo walijitokeza.+ Baadaye wawili wakajitokeza
61 na kusema: “Mtu huyu alisema, ‘Ninaweza kuliangusha chini hekalu la Mungu na kulijenga katika siku tatu.’ ”+
62 Ndipo kuhani mkuu akasimama na kumwambia: “Je, huna jibu? Watu hawa wanashuhudia nini juu yako?”+
63 Lakini Yesu akaendelea kukaa kimya.+ Kwa hiyo kuhani mkuu akamwambia: “Kwa Mungu aliye hai ninakuweka chini ya kiapo+ utuambie kama wewe ndiye Kristo+ Mwana wa Mungu!”
64 Yesu akamwambia:+ “Wewe mwenyewe umesema.+ Lakini ninawaambia ninyi, Tangu sasa+ mtamwona Mwana wa binadamu+ akiwa ameketi kwenye mkono wa kuume+ wa nguvu na akija juu ya mawingu ya mbinguni.”+
65 Ndipo kuhani mkuu akayararua mavazi yake ya nje, akisema: “Amekufuru!+ Tunahitaji mashahidi wengine wa nini?+ Tazama! Sasa mmelisikia kufuru.+
66 Mnaonaje?” Wakamjibu: “Anastahili kufa.”+
67 Ndipo wakamtemea mate usoni+ na kumpiga+ ngumi. Wengine wakampiga makofi usoni,+
68 wakisema: “Tutolee unabii, wewe Kristo.+ Ni nani aliyekupiga?”+
69 Basi Petro alikuwa ameketi nje katika ua; na mjakazi akamjia, akisema: “Wewe, pia, ulikuwa pamoja na Yesu Mgalilaya!”+
70 Lakini akakana mbele yao wote, akisema: “Sijui unalosema.”
71 Alipokuwa amekwisha kutoka na kwenda kwenye chumba kilicho langoni, msichana mwingine alimwona na kuwaambia wale waliokuwa hapo: “Mtu huyu alikuwa pamoja na Yesu Mnazareti.”+
72 Naye akakana tena, kwa kiapo: “Simjui mtu huyo!”+
73 Baada ya muda kidogo wale waliokuwa wamesimama kuzunguka wakaja na kumwambia Petro: “Hakika wewe pia ni mmoja wao, kwa maana, kwa kweli, matamshi yako yanakutambulisha wazi.”+
74 Ndipo akaanza kulaani na kuapa: “Simjui mtu huyo!” Na mara jogoo akawika.+
75 Naye Petro akakumbuka maneno ambayo Yesu alisema, yaani: “Kabla ya jogoo kuwika, utanikana mara tatu.”+ Naye akaenda nje akalia kwa uchungu.+