Mathayo 19:1-30
19 Basi Yesu alipokuwa amemaliza maneno hayo, akaondoka Galilaya na kuja kwenye mipaka ya Yudea ng’ambo ya Yordani.+
2 Pia, umati mkubwa ukamfuata, naye akawaponya huko.+
3 Na Mafarisayo wakamjia, wakikusudia kumjaribu na kusema: “Je, ni halali mwanamume kumtaliki mke wake kwa kila sababu?”+
4 Akajibu, akasema: “Je, hamkusoma kwamba yeye aliyewaumba hao kutoka mwanzo aliwafanya mwanamume na mwanamke+
5 na kusema, ‘Kwa sababu hiyo mwanamume atamwacha baba yake na mama yake+ naye atashikamana na mke wake, na hao wawili watakuwa mwili mmoja’?+
6 Hivi kwamba wao si wawili tena, bali mwili mmoja. Kwa hiyo, kile ambacho Mungu ameunganisha mtu yeyote asikitenganishe.”+
7 Wakamwambia: “Basi, kwa nini Musa aliagiza kutoa cheti cha kufukuza na kumtaliki?”+
8 Akawaambia: “Musa, kwa kufikiria ugumu wenu wa moyo,+ aliwapa ruhusa ya kuwataliki wake zenu, lakini haikuwa hivyo kutoka mwanzo.+
9 Ninawaambia kwamba mtu yeyote anayemtaliki mke wake na kumwoa mwingine, ila kwa sababu ya uasherati, anafanya uzinzi.”+
10 Wanafunzi wakamwambia: “Ikiwa hivyo ndivyo ilivyo kati ya mwanamume na mke wake, ni afadhali kutooa.”+
11 Akawaambia: “Si watu wote wanaolipa nafasi neno hilo, ila tu wale walio na hiyo zawadi.+
12 Kwa maana kuna matowashi waliozaliwa namna hiyo kutoka katika tumbo la uzazi la mama yao,+ na kuna matowashi waliofanywa matowashi na watu, na kuna matowashi ambao wamejifanya wenyewe matowashi kwa sababu ya ufalme wa mbinguni. Yule anayeweza kulipa nafasi na alipe nafasi.”+
13 Ndipo akaletewa watoto wachanga, ili aweke mikono yake juu yao na kutoa sala; lakini wanafunzi wakawakemea.+
14 Hata hivyo, Yesu akasema: “Waacheni watoto wachanga, na acheni kuwazuia wasinijie, kwa maana ufalme wa mbinguni ni wa watu walio kama wao.”+
15 Naye akaweka mikono yake juu yao, akaondoka hapo.+
16 Sasa, tazama! mtu fulani akamjia na kusema: “Mwalimu, nifanye wema gani ili niupate uzima wa milele?”+
17 Akamwambia: “Kwa nini unaniuliza juu ya lililo jema?+ Kuna mmoja tu aliye mwema. Ingawa hivyo, ikiwa unataka kuingia katika uzima, zishike amri sikuzote.”+
18 Akamwambia: “Amri gani?”+ Yesu akasema: “Naam, Usiue,+ Usifanye uzinzi,+ Usiibe,+ Usitoe ushahidi wa uwongo,+
19 Mheshimu baba yako na mama yako,+ na, Mpende jirani yako kama wewe mwenyewe.”+
20 Huyo kijana akamwambia: “Nimeyashika yote hayo; ni nini bado ninachokosa?”
21 Yesu akamwambia: “Ikiwa unataka kuwa mkamilifu, nenda ukauze mali zako na uwape maskini nawe utakuwa na hazina mbinguni,+ kisha uje uwe mfuasi wangu.”+
22 Huyo kijana aliposikia maneno hayo, akaenda zake akiwa amehuzunika, kwa maana alikuwa na mali nyingi.+
23 Lakini Yesu akawaambia wanafunzi wake: “Kwa kweli ninawaambia ninyi kwamba itakuwa vigumu kwa tajiri kuingia katika ufalme wa mbinguni.+
24 Tena ninawaambia ninyi, Ni rahisi zaidi ngamia kupita katika tundu la sindano kuliko tajiri kuingia katika ufalme wa Mungu.”+
25 Wanafunzi waliposikia hilo, wakashangaa sana, wakisema: “Ni nani kwa kweli anayeweza kuokolewa?”+
26 Akiwatazama usoni, Yesu akawaambia: “Kwa wanadamu jambo hilo haliwezekani, lakini kwa Mungu mambo yote yanawezekana.”+
27 Ndipo Petro akamjibu na kumwambia: “Tazama! Tumeacha vitu vyote na kukufuata wewe; kwa kweli kutakuwa na nini kwa ajili yetu?”+
28 Yesu akawaambia: “Kwa kweli ninawaambia ninyi, Katika uumbaji-mpya Mwana wa binadamu atakapoketi juu ya kiti chake cha ufalme chenye utukufu, ninyi ambao mmenifuata mtaketi pia juu ya viti vya ufalme kumi na viwili, mkiyahukumu yale makabila kumi na mawili ya Israeli.+
29 Na kila mtu ambaye ameacha nyumba au ndugu au dada au baba au mama au watoto au mashamba kwa ajili ya jina langu atapokea mara nyingi zaidi naye atarithi uzima wa milele.+
30 “Lakini wengi walio wa kwanza watakuwa wa mwisho na wa mwisho watakuwa wa kwanza.+