Mathayo 20:1-34
20 “Kwa maana ufalme wa mbinguni ni kama mtu, mwenye nyumba, aliyetoka asubuhi na mapema kwenda kuajiri wafanyakazi kwa ajili ya shamba lake la mizabibu.+
2 Alipokuwa amekubaliana na wafanyakazi hao awalipe dinari moja kwa siku,+ akawatuma katika shamba lake la mizabibu.
3 Akatoka pia karibu saa tatu,+ akaona wengine wasio na kazi wakiwa wamesimama sokoni;+
4 akawaambia hao, ‘Ninyi pia, nendeni katika shamba la mizabibu, nami nitawapa kilicho haki.’
5 Kwa hiyo wakaenda. Tena akatoka karibu saa sita+ na saa tisa+ na kufanya vivyo hivyo.
6 Mwishowe, karibu saa kumi na moja akatoka, akakuta wengine wakiwa wamesimama, naye akawaambia, ‘Kwa nini mmekuwa mkisimama hapa mchana wote bila kazi?’
7 Wakamwambia, ‘Kwa sababu hakuna mtu ambaye ametuajiri.’ Akawaambia, ‘Ninyi pia nendeni katika shamba la mizabibu.’+
8 “Ilipofika jioni,+ bwana wa shamba la mizabibu akamwambia msimamizi wake, ‘Waite wafanyakazi na kuwalipa mshahara wao,+ ukianza na yule wa mwisho mpaka yule wa kwanza.’
9 Wale watu wa saa kumi na moja walipokuja, wakapokea kila mmoja dinari moja.
10 Kwa hiyo, wale wa kwanza walipokuja, wakakata kauli kwamba wangepokea zaidi; lakini wao pia wakalipwa dinari moja.
11 Walipoipokea wakaanza kumnung’unikia mwenye nyumba+
12 na kusema, ‘Hawa wa mwisho walifanya kazi kwa saa moja; na bado umewafanya kuwa sawa na sisi tuliofanya kazi ngumu mchana kutwa katika lile joto lenye kuchoma!’
13 Lakini akamjibu mmoja wao, akasema, ‘Mwenzangu, sikutendei kosa. Tulikubaliana dinari moja, sivyo?+
14 Chukua kilicho chako uende. Ninataka kumpa huyu wa mwisho sawasawa na wewe.+
15 Je, si halali kwangu kufanya kile ninachotaka na vitu vyangu mwenyewe? Au jicho lako ni ovu+ kwa sababu mimi ni mwema?’+
16 Vivyo hivyo walio wa mwisho watakuwa wa kwanza, na walio wa kwanza watakuwa wa mwisho.”+
17 Alipokuwa akikaribia kupanda kwenda Yerusalemu, Yesu akawapeleka wale wanafunzi kumi na wawili+ faraghani na kuwaambia wakiwa barabarani:
18 “Tazameni! Tunapanda kwenda Yerusalemu, na Mwana wa binadamu atatiwa mikononi mwa wakuu wa makuhani na waandishi, nao watamhukumia kifo,+
19 na watamtia mikononi mwa watu wa mataifa wamdhihaki na kumpiga mijeledi na kumtundika+ juu ya mti, na siku ya tatu atafufuliwa.”+
20 Ndipo mama ya wana wa Zebedayo+ akamkaribia akiwa pamoja na wanawe, akamsujudia na kuomba kitu fulani kutoka kwake.+
21 Akamuuliza: “Unataka nini?” Akamjibu: “Toa agizo ili hawa wanangu wawili waketi, mmoja upande wako wa kuume na mmoja upande wako wa kushoto, katika ufalme wako.”+
22 Yesu akamjibu, akasema: “Hamjui kile mnachoomba. Je, mnaweza kunywa kikombe+ ambacho niko karibu kunywa?” Wakamwambia: “Tunaweza.”
23 Akawaambia: “Kwa kweli mtakunywa kikombe changu,+ lakini kuketi upande wangu wa kuume na upande wangu wa kushoto sina haki ya kutoa, bali wataketi wale ambao Baba yangu amewatayarishia.”+
24 Wale wengine kumi waliposikia jambo hilo, wakawaghadhibikia hao ndugu wawili.+
25 Lakini Yesu akawaita, akasema: “Mnajua kwamba watawala wa mataifa hupiga ubwana juu yao na wakuu hutumia mamlaka juu yao.+
26 Hivyo sivyo ilivyo katikati yenu;+ bali yeyote anayetaka kuwa mkubwa katikati yenu lazima awe mhudumu wenu,+
27 na yeyote anayetaka kuwa wa kwanza katikati yenu lazima awe mtumwa wenu.+
28 Kama vile Mwana wa binadamu alivyokuja, si kuhudumiwa, bali kuhudumu+ na kutoa nafsi yake kuwa fidia badala ya wengi.”+
29 Sasa walipokuwa wakienda kutoka Yeriko+ umati mkubwa ukamfuata.
30 Na, tazama! wanaume wawili vipofu walikuwa wameketi kando ya barabara, waliposikia kwamba Yesu anapitia hapo, wakapaaza sauti, wakisema: “Bwana, uturehemu, Mwana wa Daudi!”+
31 Lakini umati ukasisitiza kuwaambia wakae kimya; na bado wakapaaza sauti kubwa hata zaidi, wakisema: “Bwana, uturehemu, Mwana wa Daudi!”+
32 Kwa hiyo Yesu akasimama, akawaita na kusema: “Mnataka niwatendee nini?”
33 Wakamwambia: “Bwana, tunataka macho yetu yafunguliwe.”+
34 Yesu akawasikitikia, akayagusa macho yao,+ na mara moja wakapata kuona, nao wakamfuata.+