Kulingana na Marko 1:1-45

  • Yohana Mbatizaji ahubiri (1-8)

  • Yesu abatizwa (9-11)

  • Shetani amjaribu Yesu (12, 13)

  • Yesu aanza kuhubiri huko Galilaya (14, 15)

  • Wanafunzi wa kwanza wachaguliwa (16-20)

  • Roho mwovu afukuzwa (21-28)

  • Yesu awaponya watu wengi huko Kapernaumu (29-34)

  • Yesu asali faraghani (35-39)

  • Mtu mwenye ukoma aponywa (40-45)

1  Mwanzo wa habari njema kumhusu Yesu Kristo, Mwana wa Mungu:  Kama ilivyoandikwa katika nabii Isaya: “(Tazama! Ninamtuma mjumbe wangu mbele yako,* ili akutayarishie njia.)+  Kuna mtu anayepaza sauti nyikani: ‘Tayarisheni njia ya Yehova!* Nyoosheni barabara zake.’”+  Yohana Mbatizaji alikuwa nyikani, akiwahubiria watu wabatizwe ili kuonyesha kwamba wametubu na hivyo wasamehewe dhambi zao.+  Watu katika eneo lote la Yudea na wakaaji wote wa Yerusalemu walimwendea, naye akawabatiza* katika Mto Yordani,+ nao wakaungama dhambi zao waziwazi.  Yohana alikuwa akivaa mavazi yaliyofumwa kwa manyoya ya ngamia na alijifunga mshipi wa ngozi kiunoni,+ na alikula nzige na asali ya mwituni.+  Naye alihubiri akisema: “Baada yangu, kuna mtu mwenye nguvu kuliko mimi anayekuja, nami sistahili kuinama ili kufungua kamba za viatu vyake.+  Niliwabatiza ninyi kwa maji, lakini yeye atawabatiza kwa roho takatifu.”+  Siku hizo Yesu alikuja kutoka Nazareti ya Galilaya, na Yohana akambatiza katika Yordani.+ 10  Mara tu alipotoka katika maji akaona mbingu zikifunguka na roho takatifu ikishuka juu yake kama njiwa.+ 11  Sauti ikasikika kutoka mbinguni ikisema: “Wewe ni Mwanangu, mpendwa; nimekukubali.”+ 12  Mara moja roho ikamchochea kuingia nyikani. 13  Basi akakaa nyikani kwa siku 40, akijaribiwa na Shetani.+ Aliishi kati ya wanyama wa mwituni, lakini malaika walikuwa wakimhudumia.+ 14  Baada ya Yohana kukamatwa, Yesu alienda Galilaya+ akihubiri habari njema ya Mungu+ 15  akisema: “Wakati uliowekwa umefika, na Ufalme wa Mungu umekaribia. Tubuni+ na muwe na imani katika habari njema.” 16  Alipokuwa akitembea kando ya Bahari ya Galilaya alimwona Simoni na Andrea ndugu yake+ wakishusha nyavu zao baharini,+ kwa maana walikuwa wavuvi.+ 17  Basi Yesu akawaambia: “Nifuateni, nami nitawafanya muwe wavuvi wa watu.”+ 18  Mara moja wakaziacha nyavu zao na kumfuata.+ 19  Yesu aliposonga mbele kidogo akawaona Yakobo na Yohana, wana wa Zebedayo, kwenye mashua wakitengeneza nyavu zao,+ 20  na bila kukawia akawaita. Nao wakamwacha baba yao Zebedayo katika mashua pamoja na wafanyakazi, kisha wakamfuata Yesu. 21  Wakaenda Kapernaumu. Mara tu Sabato ilipoanza, akaingia katika sinagogi, akaanza kufundisha.+ 22  Nao wakashangazwa na njia yake ya kufundisha, kwa maana alikuwa akiwafundisha kama mtu mwenye mamlaka, si kama waandishi.+ 23  Wakati huohuo, kulikuwa na mtu katika sinagogi lao aliyekuwa na roho mwovu, naye akasema kwa sauti kubwa: 24  “Kwa nini unatusumbua, wewe Yesu Mnazareti?+ Je, umekuja kutuangamiza? Ninajua wewe ni nani, Mtakatifu wa Mungu!”+ 25  Lakini Yesu akamkemea, akisema: “Nyamaza, na umtoke!” 26  Na yule roho mwovu, baada ya kumfanya mtu huyo agaegae na kupiga kelele kwa sauti kubwa, akamtoka. 27  Basi, watu wote wakashangaa sana na kuulizana: “Ni jambo gani hili? Ni fundisho jipya! Hata anawaamuru roho waovu kwa mamlaka, nao wanamtii!” 28  Basi habari kumhusu zikaenea upesi kila mahali katika eneo lote la Galilaya. 29  Ndipo wakatoka kwenye sinagogi na kwenda nyumbani kwa Simoni na Andrea wakiwa na Yakobo na Yohana.+ 30  Sasa mama mkwe wa Simoni+ alikuwa amelala akiugua homa, na mara moja wakamwambia Yesu kumhusu. 31  Yesu akamkaribia, akamshika mkono na kumwinua. Akapona homa, naye akaanza kuwahudumia. 32  Ilipofika jioni, jua lilipotua, watu wakaanza kumletea wote waliokuwa wagonjwa na waliokuwa na roho waovu;+ 33  na jiji lote lilikuwa limekusanyika mlangoni. 34  Basi akawaponya watu wengi waliokuwa na magonjwa mbalimbali,+ akafukuza roho wengi waovu, lakini hakuwaruhusu hao roho waovu waseme, kwa maana walijua yeye ni Kristo.* 35  Asubuhi na mapema, kulipokuwa bado na giza, akaamka na kutoka nje, akaenda mahali pasipo na watu, naye akaanza kusali.+ 36  Hata hivyo, Simoni na wenzake wakamtafuta sana, 37  na walipompata wakamwambia: “Kila mtu anakutafuta.” 38  Lakini akawaambia: “Twendeni mahali pengine, katika miji iliyo karibu, ili nihubiri huko pia, kwa maana nilikuja kwa kusudi hilo.”+ 39  Naye akaenda akihubiri katika masinagogi yao katika Galilaya yote na kuwafukuza roho waovu.+ 40  Mtu fulani mwenye ukoma akamjia, akapiga magoti na kumwomba: “Ikiwa tu unataka, unaweza kunitakasa.”+ 41  Ndipo akamsikitikia, akanyoosha mkono wake, akamgusa na kumwambia: “Ninataka! Takasika.”+ 42  Mara moja ule ukoma ukaisha, akawa safi. 43  Kisha akampa maagizo thabiti na mara moja akamwacha aende, 44  akamwambia: “Usimwambie jambo lolote mtu yeyote, bali nenda ukajionyeshe kwa kuhani na utoe vitu alivyoagiza Musa kwa ajili ya kutakaswa kwako,+ ili kuwa ushahidi kwao.”+ 45  Hata hivyo, baada ya kuondoka, mtu huyo akaanza kueneza habari hizo kila mahali, hivi kwamba Yesu hakuweza kuingia katika jiji lolote waziwazi, bali alikaa nje mahali pasipo na watu. Lakini watu walizidi kumjia kutoka kila upande.+

Maelezo ya Chini

Tnn., “mbele ya uso wako.”
Au “akawatumbukiza; akawazamisha.”
Au labda, “walijua yeye ni nani.”