Kutoka 24:1-18

  • Watu wakubali kushika agano (1-11)

  • Musa akiwa kwenye Mlima Sinai (12-18)

24  Kisha akamwambia Musa: “Panda uje kwangu mimi Yehova, wewe na Haruni, Nadabu na Abihu,+ na wazee 70 wa Israeli, nanyi mwiname chini mkiwa mbali.  Musa anapaswa kunikaribia mimi, Yehova, akiwa peke yake; lakini wale wengine hawapaswi kunikaribia, na watu hawapaswi kupanda pamoja naye.”+  Kisha Musa akaja na kuwaambia watu maneno yote ya Yehova na sheria zote,*+ na watu wote wakajibu hivi kwa sauti moja: “Maneno yote ambayo Yehova amesema, tuko tayari kuyafanya.”+  Basi Musa akaandika maneno yote ya Yehova.+ Kisha akaamka asubuhi na mapema na kujenga madhabahu kwenye sehemu ya chini ya mlima huo na nguzo 12 kulingana na idadi ya makabila 12 ya Israeli.  Baada ya hayo akawatuma wanaume vijana Waisraeli, nao wakatoa dhabihu za kuteketezwa na dhabihu za ng’ombe dume ili ziwe dhabihu za ushirika+ kwa Yehova.  Kisha Musa akachukua nusu ya damu ya wanyama hao na kuitia ndani ya mabakuli, na nusu ya damu hiyo akainyunyiza kwenye madhabahu.  Halafu akachukua kitabu cha agano na kuwasomea watu kwa sauti.+ Nao wakasema: “Mambo yote ambayo Yehova amesema tuko tayari kuyafanya, nasi tutatii.”+  Basi Musa akachukua damu akawanyunyizia watu+ na kusema: “Hii ndiyo damu ya agano ambalo Yehova amefanya pamoja nanyi kulingana na maneno hayo yote.”+  Musa na Haruni, Nadabu na Abihu, na wazee 70 wa Israeli wakapanda mlimani, 10  nao wakamwona Mungu wa Israeli.+ Chini ya miguu yake palikuwa na kitu kilichoonekana kama sakafu ya yakuti, nacho kilikuwa safi kama mbingu zenyewe.+ 11  Hakuwadhuru wanaume hao wenye kuheshimika wa Israeli,+ nao walipata maono ya Mungu wa kweli, wakala na kunywa. 12  Sasa Yehova akamwambia Musa: “Panda uje kwangu mlimani na ukae huku. Nitakupa mabamba ya mawe yenye sheria na amri nitakazoandika ili kuwafundisha watu.”+ 13  Basi Musa akaondoka pamoja na Yoshua mhudumu wake,+ naye Musa akapanda kwenye mlima wa Mungu wa kweli.+ 14  Lakini alikuwa amewaambia wale wazee: “Tungojeeni hapa mpaka tutakaporudi.+ Haruni na Huru+ wako pamoja nanyi. Yeyote aliye na kesi anaweza kuwapelekea.”+ 15  Ndipo Musa akapanda mlimani wingu lilipokuwa likiufunika mlima huo.+ 16  Utukufu wa Yehova+ uliendelea kukaa juu ya Mlima Sinai,+ na wingu likaufunika kwa siku sita. Siku ya saba akamwita Musa kutoka katikati ya lile wingu. 17  Kwa Waisraeli waliokuwa wakitazama, utukufu wa Yehova ulionekana kama moto mkali kwenye kilele cha mlima. 18  Ndipo Musa akaingia ndani ya lile wingu na kupanda mlimani.+ Musa akakaa mlimani siku 40, mchana na usiku.+

Maelezo ya Chini

Tnn., “maamuzi yote ya hukumu.”