Juu ya Nini Tusali mu Jina ya Yesu?

Juu ya Nini Tusali mu Jina ya Yesu?

MARA mingi Yesu alikuwaka nafundisha watu juu ya sala. Wakati alikuwaka ku dunia viongozi wa dini ya Wayahudi walikuwa nasali “kwenye pembe za njia kubwa.” Juu ya nini? “Ili waonekane na watu.” Ni wazi kama walikuwa tu napenda kujionyesha. Wengi walikuwa natoa sala za murefu na kutumia maneno ileile juu waliwaza kama ‘kutumia maneno mengi’ njo kungefanya Mungu awasikie. (Matayo 6:5-8) Yesu alisaidia watu wazuri waelewe kama kutoa sala za vile ilikuwa kuchokea bure. Lakini hakuishia pale. Aliwafundisha namna ya muzuri ya kusali.

Yesu alifundisha kama wakati tunasali tunapaswa kuonyesha ya kama tunapenda jina ya Mungu itakaswe, Ufalme wake ukuye, na mapenzi yake itendeke. Alifundisha pia kama haiko mubaya kuomba Mungu atusaidie mu mambo yetu ya kipekee. (Matayo 6:9-​13; Luka 11:2-4) Alitoa mifano mingi yenye ilionyesha kama kusudi Mungu asikie sala zetu, tunapaswa kuendelea kusali, kuwa na imani, na kuwa wanyenyekevu. (Luka 11:5-​13; 18:1-​14) Mufano wake ulisaidia pia watu wajifunze mambo mingi juu ya sala.​—Matayo 14:23; Marko 1:35.

Kwa kweli, mambo yenye Yesu alifundisha juu ya sala ilisaidia wanafunzi wake wakuwe wanatoa sala za muzuri zaidi. Lakini ni mu usiku wa mwisho wa maisha yake hapa ku dunia njo Yesu alifundishaka wanafunzi wake jambo ya maana sana juu ya sala.

“Mabadiliko Makubwa mu Namna ya Kusali”

Mu usiku wake wa mwisho hapa ku dunia, Yesu alifanya saa ya mingi na iko natia moyo mitume wake waaminifu. Ilikuwa wakati yenye inafaa ya kuwafunulia jambo fulani ya mupya. Yesu aliwaambia hivi. “Mimi ndiye njia na kweli na uzima. Hakuna mwenye anakuja kwa Baba isipokuwa kupitia mimi.” Kisha aliwaambia hii maneno yenye kutia moyo: “Kila jambo lenye munaomba katika jina langu, nitalifanya, ili Baba atukuzwe kuhusiana na Mwana. Mukiomba jambo lolote katika jina langu, nitalifanya.” Ku mwisho-mwisho wa mazungumuzo yake, alisema hivi: “Kufikia sasa hamujaomba hata jambo moja katika jina langu. Muombe na mutapokea, ili furaha yenu ikuwe kamili.”​—Yohana 14:6, 13, 14; 16:24.

Ile ilikuwa maneno ya maana sana. Kitabu fulani inasema kama ile ilikuwa mabadiliko makubwa sana mu namna ya kusali. Hakupenda kusema kama watu wanapaswa kuacha kusali kwa Mungu na kuanza kusali kwake. Lakini alikuwa nafungula njia ya mupya ya kufikisha sala zetu kwa Yehova.

Tunajua kama Mungu anasikilizaka sala za watumishi wake waaminifu. (1 Samweli 1:9-​19; Zaburi 65:2) Tangu wakati Mungu alifanya agano na Waisraeli ili wakuwe watu wake, kila mutu mwenye alipenda Mungu asikie sala yake alipaswa kukubali kama Israeli njo ilikuwa taifa yenye Mungu alikuwa amechagula. Na kisha Sulemani kujenga hekalu, kila mutu mwenye alipenda Mungu asikilize sala yake alipaswa kukubali kama hekalu njo fasi yenye Mungu amechagula juu ya kumuabudia na kutoa zabihu. (Kumbukumbu la Torati 9:29; 2 Mambo ya Nyakati 6:32, 33) Lakini ile namna ya kumuabudu Mungu ingekuwa na mwisho. Mutume Paulo aliandika kama sheria yenye Mungu alipatia Waisraeli na zabihu zenye zilitolewa ku hekalu viilikuwa “kivuli cha mambo ya muzuri yenye yatakuja, lakini hapana umbo ya kweli ya mambo hayo.” (Waebrania 10:1, 2) Kivuli kingepita na pa fasi yake kungekuwa mambo ya kweli kabisa. (Wakolosai 2:17) Tangu mwaka wa 33 kisha kuzaliwa kwa Yesu, haikukuwa tena lazima mutu atii sheria ya Musa juu amukaribie Mungu. Lakini alipaswa tu kumutii Yesu Kristo.​—Yohana 15:14-​16; Wagalatia 3:24, 25.

Jina Lenye Kuwa “Juu Zaidi ya Kila Jina Lingine”

Yesu alitufundisha njia ya muzuri zaidi ya kusali kwa Yehova. Sasa tunapaswa kusali mu jina ya Yesu juu Mungu asikie sala zetu. Nini njo inafanya Yehova asikilize sala zetu wakati tunasali mu jina ya Yesu?

Tulizaliwa katika zambi, njo maana matendo yetu ao zabihu zetu haziwezi kutuondolea zambi ao kutufanya tukuwe na uhusiano na Yehova, Mungu Mutakatifu. (Waroma 3:20, 24; Waebrania 1:3, 4) Lakini Yesu alitoa uzima wake mukamilifu ili kulipia zambi za wanadamu. Ile inasaidia wale wote wenye kuwa na imani katika zabihu yake wakuwe na uhusiano muzuri na Mungu. (Waroma 5:12, 18, 19) Sasa wale wote wenye wanapenda kuwa na uhusiano muzuri na Yehova na wenye wanapenda kusali kwake wanaweza kufanya vile kama wanaonyesha imani katika zabihu ya Yesu na wanasali mu jina yake.​—Waefeso 3:11, 12.

Wakati tunasali mu jina ya Yesu, tunaonyesha kama tunaamini hii mambo tatu: (1) Yesu ni “Mwana-Kondoo wa Mungu” na juu alitoa uzima wake kwa ajili yetu, Mungu anaweza kusamehe zambi zetu. (2) Yehova alimufufua na sasa yeye ni “kuhani mukubwa” na iko anasaidia watu wapate faida ya zabihu yake ya ukombozi. (3) Yeye tu njo “njia” ya kumukaribia Yehova katika sala.​—Yohana 1:29; 14:6; Waebrania 4:14, 15

Wakati tunasali mu jina ya Yesu, tunaonyesha kama tunamuheshimia. Yesu anastahili ile heshima juu Yehova anapenda “katika jina la Yesu kila goti lipigwe . . . , na kila ulimi ukubali waziwazi kama Yesu Kristo ni Bwana kwa utukufu wa Mungu Baba.” (Wafilipi 2:10, 11) Lakini jambo ya maana zaidi ni kwamba wakati tunasali mu jina ya Yesu, tunamutukuza Yehova mwenye alitoa Mwana wake kwa ajili yetu.​—Yohana 3:16.

Tunapaswa kusali kwa “moyo wote.” Haipaswe kuwa desturi tu

Juu ya kutusaidia kuelewa juu ya nini Yesu iko na daraka ya maana sana, Biblia inatumia majina mbalimbali ya cheo juu ya kumuzungumuzia. Ile majina ya cheo inatusaidia tuelewe mambo yote ya muzuri yenye Yesu ametufanyia, yenye iko nafanya sasa, na yenye atatufanyia mu siku zenye ziko nakuya. Biblia inasema kama Yesu amepewa “jina lenye kuwa juu zaidi ya kila jina lingine.” * (Ona kisanduku “ Majina Mbalimbali ya Yesu”) Amepewa mamlaka yote mbinguni na ku dunia.​—Wafilipi 2:9; Matayo 28:18.

Haiko desturi tu

Kama tunapenda Yehova asikilize sala zetu, tunapaswa kusali mu jina ya Yesu. (Yohana 14:13, 14) Lakini hatupendi kusema maneno “mu jina ya Yesu” ikuwe tu desturi. Juu ya nini?

Kwa mufano, wakati mufanyabiashara anaandikaka barua, mara mingi anamaliziaka na maneno yenye kuonyesha heshima. Hata kama anamalizia barua yake na ile maneno, ile haimaanishe kama anakupenda. Iko tu anafuata maagizo ya kuandika barua. Wakati tuko nasali, hatupaswe kutumia maneno “mu jina ya Yesu” sawa maneno ya heshima yenye inamaliziaka barua. Biblia inatuambia ‘tusali bila kuacha.’ Lakini tunapaswa kusali kwa “moyo wote.” Haipaswe kuwa desturi tu.​—1 Watesalonike 5:17; Zaburi 119:145.

Unaweza kufanya nini juu usikuwe unatumia maneno “mu jina ya Yesu” kwa desturi tu? Fikiri sana juu ya sifa za muzuri za Yesu. Fikiri juu ya mambo yenye alishakufanyia na yenye atakufanyia. Wakati unasali kwa Yehova, umushukuru na umusifu juu ya mambo ya muzuri yenye amefanya kupitia mwana wake. Kama unafanya vile utaamini kabisa hii ahadi ya Yesu: “Kama munamuomba Baba jambo lolote, atawapatia ninyi katika jina langu.”​—Yohana 16:23.

^ Kamusi fulani ya Biblia inaonyesha kama jina ya mutu inaweza kumaanisha mambo sawa vile sifa zake, uwezo wake, na mamlaka yenye iko nayo.