Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unayaona Mambo Matakatifu Kama Yehova Anavyoyaona?

Je, Unayaona Mambo Matakatifu Kama Yehova Anavyoyaona?

Je, Unayaona Mambo Matakatifu Kama Yehova Anavyoyaona?

“Mkiwa waangalifu . . . kwamba kusiwe na mwasherati wala yeyote asiyethamini mambo matakatifu.”—WAEBRANIA 12:15, 16.

1. Watumishi wa Yehova wanakataa mtazamo gani uliopo leo?

KWA ujumla, ulimwengu unazidi kupuuza mambo matakatifu. Mwanasosholojia Mfaransa Edgar Morin alisema hivi: “Misingi yote ambayo maadili hutegemea, yaani, Mungu, mazingira, nchi ya mtu ya asili, historia, na akili, inatiliwa shaka tofauti na ilivyokuwa zamani. . . . Watu huchagua na kuamua viwango watakavyofuata.” Hilo linaonyesha “roho ya ulimwengu,” au “roho ambayo sasa hutenda katika wana wa kutotii.” (1 Wakorintho 2:12; Waefeso 2:2) Roho hiyo ya kutoheshimu mambo matakatifu haikubaliwi na wale waliojiweka wakfu kwa Yehova na ambao hujitiisha kwa kupenda chini ya enzi yake kuu. (Waroma 12:1, 2) Badala yake, watumishi wa Mungu wanatambua kwamba utakatifu ni wa maana katika ibada ambayo wanamtolea Yehova. Ni mambo gani yanayopaswa kuwa matakatifu maishani mwetu? Makala hii itazungumzia mambo matano ambayo ni matakatifu kwa watumishi wote wa Mungu. Makala inayofuata itakazia utakatifu wa mikutano yetu ya Kikristo. Lakini kwa kweli neno “takatifu” linamaanisha nini?

2, 3. (a) Maandiko yanakaziaje utakatifu wa Yehova? (b) Tunalionaje jina la Yehova kuwa takatifu?

2 Katika Kiebrania cha Biblia, neno “takatifu” hudokeza wazo la kuweka kando. Katika ibada, neno “takatifu” linatumiwa kuhusiana na kitu kilichowekwa kando ili kisitumiwe kwa mambo ya kawaida. Yehova ni mtakatifu katika maana kamilifu. Anaitwa “Mtakatifu Zaidi.” (Methali 9:10; 30:3) Katika Israeli la kale, kuhani mkuu alivaa kilemba chenye bamba la dhahabu lenye maneno “Utakatifu ni wa Yehova.” (Kutoka 28:36, 37) Katika Maandiko, makerubi na maserafi walio mbinguni ambao wanazunguka kiti cha Ufalme cha Yehova wanatangaza hivi: “Mtakatifu, mtakatifu, mtakatifu ni Yehova.” (Isaya 6:2, 3; Ufunuo 4:6-8) Kurudia-rudia neno hilo hukazia kwamba Yehova ni mtakatifu, safi, na ametakata kabisa. Kwa kweli, yeye ndiye Chanzo cha utakatifu wote.

3 Jina la Yehova ni takatifu. Mtunga-zaburi alisema hivi: “Na walisifu jina lako. Ni kuu na lenye kuogopesha, ni takatifu.” (Zaburi 99:3) Yesu alitufundisha kusali hivi: “Baba yetu uliye mbinguni, jina lako na litakaswe [au lionwe kuwa takatifu].” (Mathayo 6:9) Maria, ambaye alikuwa mama ya Yesu hapa duniani, alitangaza hivi: “Nafsi yangu inamtukuza Yehova . . . Mwenye nguvu amenitendea makuu, nalo jina lake ni takatifu.” (Luka 1:46, 49) Tukiwa watumishi wa Yehova, sisi huliona jina lake kuwa takatifu nasi huepuka kufanya jambo lolote ambalo linaweza kuliletea suto jina hilo takatifu. Zaidi ya hilo, tuna maoni kama ya Yehova kuhusu utakatifu, yaani, tunayaona mambo matakatifu kama Yehova anavyoyaona.—Amosi 5:14, 15.

Kwa Nini Tunamheshimu Sana Yesu

4. Kwa nini Biblia inamtaja Yesu kuwa “Mtakatifu”?

4 Akiwa “mwana mzaliwa-pekee” wa Mungu mtakatifu, Yehova, Yesu aliumbwa akiwa mtakatifu. (Yohana 1:14; Wakolosai 1:15; Waebrania 1:1-3) Kwa hivyo, anaitwa “Mtakatifu wa Mungu.” (Yohana 6:69) Aliendelea kuwa mtakatifu uhai wake ulipohamishwa kutoka mbinguni hadi duniani, kwa sababu Maria alimzaa Yesu kwa uwezo wa roho takatifu. Malaika alikuwa amemwambia hivi: “Roho takatifu itakuja juu yako, . . . kile kitakachozaliwa kitaitwa kitakatifu, Mwana wa Mungu.” (Luka 1:35) Katika sala waliyomtolea Yehova, Wakristo huko Yerusalemu mara mbili walimtaja Mwana wa Mungu kuwa “mtumishi wako mtakatifu Yesu.”—Matendo 4:27, 30.

5. Ni kazi gani takatifu ambayo Yesu alitimiza duniani, na kwa nini damu yake ni yenye thamani?

5 Yesu alipewa kazi takatifu ya kutimiza alipokuwa duniani. Alipobatizwa mwaka wa 29 W.K., Yesu alitiwa mafuta kuwa Kuhani Mkuu wa hekalu kubwa la kiroho la Yehova. (Luka 3:21, 22; Waebrania 7:26; 8:1, 2) Zaidi ya hayo, angekufa kifo cha kidhabihu. Damu yake iliyomwagwa ingeandaa fidia ambayo ingewawezesha wanadamu watenda-dhambi waokolewe. (Mathayo 20:28; Waebrania 9:14) Kwa hiyo, tunaiona damu ya Yesu kuwa takatifu, yenye “thamani.”—1 Petro 1:19.

6. Tunamwonaje Kristo Yesu, na kwa nini?

6 Ili kuonyesha kwamba tunamheshimu sana Mfalme wetu na Kuhani Mkuu, Kristo Yesu, mtume Paulo aliandika hivi: “Mungu alimpandisha [Mwana wake] kwenye cheo cha juu zaidi na kumpa kwa fadhili jina lililo juu ya kila jina lingine, ili katika jina la Yesu kila goti lipigwe la wale walio mbinguni na wale walio duniani na wale walio chini ya nchi, na kila ulimi ukiri waziwazi kwamba Yesu Kristo ni Bwana kwa utukufu wa Mungu Baba.” (Wafilipi 2:9-11) Tunaonyesha kwamba tunayaona mambo matakatifu kama Yehova anavyoyaona kwa kujitiisha kwa shangwe chini ya Kiongozi na Mfalme wetu anayetawala, Kristo Yesu, aliye Kichwa cha kutaniko la Kikristo.—Mathayo 23:10; Wakolosai 1:18.

7. Tunaonyeshaje kwamba tunajitiisha kwa Kristo?

7 Kujitiisha kwa Kristo kunatia ndani pia kuonyesha heshima inayofaa kwa wanaume ambao anawatumia kuongoza kazi ambayo yeye anaelekeza leo. Madaraka ya Wakristo watiwa-mafuta wanaofanyiza Baraza Linaloongoza na ya waangalizi ambao wamewekwa rasmi na Baraza hilo katika ofisi za tawi, wilaya, mizunguko, na makutaniko yanapaswa kuonwa kuwa matakatifu. Hivyo, tunapaswa kujitiisha na kuheshimu sana mpango huo.—Waebrania 13:7, 17.

Watu Watakatifu

8, 9. (a) Waisraeli walikuwa watu watakatifu kwa njia gani? (b) Yehova alikazia jinsi gani kanuni ya utakatifu kwa Waisraeli?

8 Yehova alifanya agano na taifa la Israeli. Uhusiano huo ulifanya taifa hilo jipya liwe la pekee. Walitakaswa, au waliwekwa kando. Yehova mwenyewe aliwaambia hivi: “Mtakuwa watakatifu kwangu, kwa sababu mimi Yehova ni mtakatifu; nami ninawatenga kutoka kwa vikundi vya watu ili muwe wangu.”—Mambo ya Walawi 19:2; 20:26.

9 Mara tu taifa la Israeli lilipoanzishwa, Yehova alikazia umaana wa kanuni ya utakatifu kwa Waisraeli. Hawakupaswa hata kuugusa mlima ambako Amri Kumi zilitolewa ili wasife. Wakati huo, kwa njia fulani Mlima Sinai ulionwa kuwa mtakatifu. (Kutoka 19:12, 23) Ukuhani, maskani, na vyombo vya maskani, vilipaswa pia kuonwa kuwa vitakatifu. (Kutoka 30:26-30) Hali ikoje katika kutaniko la Kikristo?

10, 11. Kwa nini inaweza kusemwa kwamba kutaniko la Kikristo la watiwa-mafuta ni takatifu, na hilo lina matokeo gani kwa “kondoo wengine”?

10 Kutaniko la Kikristo la watiwa-mafuta ni takatifu machoni pa Yehova. (1 Wakorintho 1:2) Kwa kweli, Wakristo wote watiwa-mafuta walio duniani kwa kipindi chochote cha wakati wanafananishwa na hekalu takatifu, ingawa wao si hekalu kubwa la kiroho la Yehova. Yehova anakaa katika hekalu hilo kupitia roho yake takatifu. Mtume Paulo aliandika hivi: “Katika muungano na [Kristo Yesu] jengo lote likiunganishwa pamoja kwa upatano, linakua liwe hekalu takatifu kwa ajili ya Yehova. Katika muungano na yeye, ninyi pia mnajengwa pamoja muwe mahali pa Mungu pa kukaa kwa njia ya roho.”—Waefeso 2:21, 22; 1 Petro 2:5, 9.

11 Paulo aliwaandikia hivi Wakristo watiwa-mafuta: “Je, hamjui kwamba ninyi ni hekalu la Mungu, na kwamba roho ya Mungu inakaa ndani yenu? . . . Hekalu la Mungu ni takatifu, nanyi ni hekalu hilo.” (1 Wakorintho 3:16, 17) Kupitia roho yake, Yehova ‘anakaa’ katikati ya watiwa-mafuta naye ‘anatembea katikati yao.’ (2 Wakorintho 6:16) Yeye anaendelea kumwongoza “mtumwa” wake mwaminifu. (Mathayo 24:45-47) “Kondoo wengine” wanathamini pendeleo lao la kushirikiana na jamii ya hekalu.—Yohana 10:16; Mathayo 25:37-40.

Mambo Matakatifu Katika Maisha Yetu ya Kikristo

12. Ni mambo gani yaliyo matakatifu maishani mwetu, na kwa nini?

12 Haishangazi kwamba mambo mengi yanayohusiana na maisha ya washiriki watiwa-mafuta wa kutaniko la Kikristo na waandamani wao yanaonwa kuwa matakatifu. Uhusiano wetu pamoja na Yehova ni jambo takatifu. (1 Mambo ya Nyakati 28:9; Zaburi 36:7) Ni wenye thamani sana kwetu hivi kwamba haturuhusu chochote wala yeyote aharibu uhusiano tulio nao pamoja na Mungu wetu, Yehova. (2 Mambo ya Nyakati 15:2; Yakobo 4:7, 8) Sala ni ya maana katika kudumisha uhusiano wa karibu pamoja na Yehova. Sala ilikuwa takatifu sana kwa nabii Danieli hivi kwamba aliendeleza kwa uaminifu desturi yake ya kusali kwa Yehova hata uhai wake ulipokuwa hatarini. (Danieli 6:7-11) “Sala za watakatifu,” au Wakristo watiwa-mafuta, zinalinganishwa na uvumba uliotumiwa katika ibada hekaluni. (Ufunuo 5:8; 8:3, 4; Mambo ya Walawi 16:12, 13) Ulinganifu huo unakazia utakatifu wa sala. Ni pendeleo kubwa sana kuwasiliana na Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu wote! Si ajabu kwamba tunaiona sala kuwa takatifu maishani mwetu!

13. Ni nguvu gani iliyo takatifu, nasi tunapaswa kuiruhusu itende kazi maishani mwetu kwa njia gani?

13 Kuna nguvu fulani katika maisha ya Wakristo watiwa-mafuta na waandamani wao ambayo bila shaka wanaiona kuwa takatifu. Nguvu hiyo ni roho takatifu. Roho hiyo ni nguvu ya utendaji ya Yehova, nayo inaitwa kwa kufaa “roho takatifu,” au “roho ya utakatifu” kwa sababu sikuzote inatenda kupatana na mapenzi ya Mungu mtakatifu. (Yohana 14:26; Waroma 1:4) Kupitia roho takatifu, Yehova anawapa watumishi wake nguvu za kuhubiri habari njema. (Matendo 1:8; 4:31) Yehova huwapa roho yake “wale wanaomtii yeye akiwa mtawala,” wale ambao wanaendelea ‘kutembea kwa roho,’ wala si kulingana na tamaa za mwili. (Matendo 5:32; Wagalatia 5:16, 25; Waroma 8:5-8) Roho hiyo yenye nguvu inawawezesha Wakristo kuzaa “matunda ya roho,” yaani, sifa nzuri na kuwa na “matendo matakatifu ya mwenendo na vitendo vya ujitoaji-kimungu.” (Wagalatia 5:22, 23; 2 Petro 3:11) Ikiwa tunaiona roho takatifu kuwa takatifu, tutaepuka kufanya jambo lolote linaloweza kuihuzunisha roho hiyo, au kuizuia isitende kazi maishani mwetu.—Waefeso 4:30.

14. Watiwa-mafuta wanaona pendeleo gani kuwa takatifu, na kondoo wengine wanashiriki katika pendeleo hilo jinsi gani?

14 Pendeleo tulilo nalo la kuitwa kwa jina la Mungu mtakatifu, Yehova, na kuwa Mashahidi wake ni jambo lingine tunaloliona kuwa takatifu. (Isaya 43:10-12, 15) Yehova amewafanya Wakristo watiwa-mafuta wastahili “kuwa wahudumu wa agano jipya.” (2 Wakorintho 3:5, 6) Kwa hiyo, wamepewa kazi ya kuhubiri “habari njema ya ufalme” na ‘kufanya wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.’ (Mathayo 24:14; 28:19, 20) Wanatimiza kwa uaminifu kazi hiyo, na mamilioni ya watu walio mfano wa kondoo wanaitikia, na kwa njia ya mfano wanawaambia hivi watiwa-mafuta: “Tutakwenda pamoja nanyi, kwa maana tumesikia ya kuwa Mungu yupo pamoja nanyi.” (Zekaria 8:23) Kwa njia ya kiroho, watu hao wanyenyekevu wanatumika kwa shangwe wakiwa kama “wakulima” na “watunza-mizabibu” wa “wahudumu [watiwa-mafuta] wa Mungu wetu.” Katika njia hiyo, kondoo wengine wanawasaidia sana watiwa-mafuta kutimiza huduma yao ulimwenguni pote.—Isaya 61:5, 6.

15. Mtume Paulo aliona kazi gani kuwa takatifu, na kwa nini tuna maoni kama yake?

15 Mtume Paulo ni mmoja wa watu ambao waliona huduma ya hadharani kuwa jambo takatifu. Alisema kwamba yeye ni ‘mtumishi wa watu wote wa Kristo Yesu kwa mataifa, akifanya kazi takatifu ya habari njema ya Mungu.’ (Waroma 15:16) Akiwaandikia Wakristo wa Korintho, Paulo alisema kwamba huduma yake ni “hazina.” (2 Wakorintho 4:1, 7) Kupitia huduma yetu ya hadharani, tunatangaza “maneno matakatifu ya Mungu.” (1 Petro 4:11) Kwa hivyo, iwe sisi ni watiwa-mafuta au kondoo wengine, tunaona kushiriki katika kazi ya kutoa ushahidi kuwa pendeleo takatifu.

‘Tuukamilishe Utakatifu Katika Kumwogopa Mungu’

16. Ni nini kitakachotusaidia kuepuka kuwa watu ‘wasiothamini mambo matakatifu’?

16 Mtume Paulo aliwaonya Wakristo wenzake waepuke kuwa watu ‘wasiothamini mambo matakatifu.’ Lakini akawashauri ‘wafuatilie utakaso,’ ‘wakiwa waangalifu . . . kwamba mzizi wowote wenye sumu usichipuke na kusababisha taabu na kwamba wengi wasitiwe unajisi na huo.’ (Waebrania 12:14-16) Maneno ‘mzizi wenye sumu’ yanahusu watu wachache katika kutaniko la Kikristo ambao huenda wakachambua-chambua jinsi mambo yanavyofanywa. Kwa mfano, huenda wasikubaliane na maoni ya Yehova kuhusu utakatifu wa ndoa au uhitaji wa kuwa safi kiadili. (1 Wathesalonike 4:3-7; Waebrania 13:4) Au huenda wakazungumzia na kueneza mawazo ya waasi-imani, “maneno matupu ambayo huchafua mambo matakatifu,” yanayosemwa na wale ambao “wamegeuka kutoka kwenye kweli.”—2 Timotheo 2:16-18.

17. Kwa nini ni lazima watiwa-mafuta wajitahidi daima kuwa na maoni kama ya Yehova kuhusu utakatifu?

17 Paulo aliwaandikia hivi ndugu zake watiwa-mafuta: ‘Wapendwa, acheni tujisafishe wenyewe kila unajisi wa mwili na roho, tukiukamilisha utakatifu katika kumwogopa Mungu.’ (2 Wakorintho 7:1) Maneno hayo yanaonyesha kwamba ni lazima Wakristo watiwa-mafuta, “washiriki wa mwito wa mbinguni,” wajitahidi daima kuhakikisha kwamba wana maoni kama ya Yehova kuhusu utakatifu katika kila sehemu ya maisha yao. (Waebrania 3:1) Vivyo hivyo, mtume Petro aliwahimiza hivi ndugu zake waliozaliwa kwa roho: “Kama watoto watiifu, acheni kufanyizwa kulingana na tamaa mlizokuwa nazo hapo zamani katika hali yenu ya kutojua, bali, kwa kupatana na Mtakatifu aliyewaita, ninyi wenyewe pia iweni watakatifu katika mwenendo wenu wote.”—1 Petro 1:14, 15.

18, 19. (a) Washiriki wa “umati mkubwa” wanaonyesha jinsi gani kwamba wanayaona mambo matakatifu kama Yehova anavyoyaona? (b) Ni jambo gani lingine takatifu katika maisha yetu ya Kikristo litakalozungumziwa katika makala inayofuata?

18 Namna gani washiriki wa “umati mkubwa,” ambao wataokoka “dhiki kuu”? Ni lazima wao pia wathibitishe kwamba wanayaona mambo matakatifu kama Yehova anavyoyaona. Kitabu cha Ufunuo kinasema kwamba wanamtolea Yehova “utumishi mtakatifu” katika ua wa kidunia wa hekalu lake la kiroho. Wanaiamini dhabihu ya fidia ya Kristo, na kwa njia ya mfano, ‘wanafua kanzu zao na kuzifanya nyeupe katika damu ya Mwana-Kondoo.’ (Ufunuo 7:9, 14, 15) Hilo linawapa msimamo safi mbele za Yehova na hivyo wanakuwa na wajibu wa ‘kujisafisha wenyewe kila unajisi wa mwili na roho, wakiukamilisha utakatifu katika kumwogopa Mungu.’

19 Jambo muhimu katika maisha ya Wakristo watiwa-mafuta na waandamani wao ni kuhudhuria mikutano kwa ukawaida ili kumwabudu Yehova na kujifunza Neno lake. Yehova huyaona makusanyiko ya watu wake kuwa matakatifu. Makala inayofuata itazungumzia jinsi na kwa nini tunapaswa kuwa na maoni kama ya Yehova kuhusu mambo matakatifu katika jambo hilo muhimu.

Kwa Kupitia

• Watumishi wa Yehova hukataa mtazamo gani wa kilimwengu?

• Kwa nini Yehova ndiye Chanzo cha mambo yote matakatifu?

• Tunaonyesha jinsi gani kwamba tunaheshimu utakatifu wa Kristo?

• Ni mambo gani tunayopaswa kuyaona kuwa matakatifu maishani mwetu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 23]

Katika Israeli la kale, ukuhani, maskani, na vyombo vya maskani vilipaswa kuonwa kuwa vitakatifu

[Picha katika ukurasa wa 24]

Wakristo watiwa-mafuta walio duniani ni hekalu takatifu

[Picha katika ukurasa wa 25]

Sala na huduma yetu ya hadharani ni mapendeleo matakatifu