Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Naye Atawakaribia”

“Naye Atawakaribia”

“Naye Atawakaribia”

“[Mungu] hayuko mbali sana na kila mmoja wetu.”—MATENDO 17:27.

1, 2. (a) Tunapotazama anga lililojaa nyota, tunaweza kuuliza maswali gani kumhusu Muumba? (b) Biblia hutuhakikishiaje kwamba wanadamu ni wenye thamani sana machoni pa Yehova?

JE, UMEWAHI kutazama anga lililojaa nyota usiku usiokuwa na mawingu na kustaajabu? Idadi hiyo kubwa ya nyota na ukubwa wa anga unastaajabisha. Katika ulimwengu huu mkubwa, dunia ni kama doa tu. Je, hilo linamaanisha kwamba Muumba, ‘Aliye juu, juu ya nchi yote,’ yuko juu sana asiweze kujishughulisha na wanadamu, au yuko mbali sana asiweze kueleweka au kufahamiwa na wanadamu?—Zaburi 83:18.

2 Biblia yatuhakikishia kwamba wanadamu ni wenye thamani sana machoni pa Yehova. Hata Neno la Mungu hututia moyo tumtafute, likisema: “Yeye hayuko mbali sana na kila mmoja wetu.” (Matendo 17:27; 1 Mambo ya Nyakati 28:9) Naam, tukichukua hatua kumkaribia Mungu, atatenda kulingana na jitihada zetu. Kwa njia gani? Maneno ya andiko letu la mwaka wa 2003 hutoa jibu hili lenye kutia moyo: “Naye atawakaribia.” (Yakobo 4:8) Na tuzungumzie baadhi ya baraka ambazo Yehova huwamwagia wale wanaomkaribia.

Zawadi Kutoka kwa Yehova Mwenyewe

3. Yehova huwapa wale wanaomkaribia zawadi gani?

3 Kwanza, watumishi wa Yehova wana zawadi yenye thamani ambayo ameitenga kwa ajili ya watu wake. Uwezo, mali, au elimu ambazo ulimwengu huu unatoa haziwezi kumsaidia mtu kupata zawadi hiyo. Hiyo ni zawadi kutoka kwa Yehova mwenyewe, naye huwapa wale wanaomkaribia. Hiyo ni zawadi gani? Neno la Mungu linajibu: ‘Ukipaza sauti yako upate ufahamu; ukiutafuta kama fedha, na kuutafutia kama hazina iliyositirika; ndipo utakapofahamu kumcha BWANA, na kupata kumjua Mungu. Kwa kuwa BWANA huwapa watu hekima.’ (Mithali 2:3-6) Hebu wazia wanadamu wasio wakamilifu wakiwa na uwezo wa “kumjua Mungu”! Zawadi hiyo—ujuzi unaopatikana katika Neno la Mungu—inalinganishwa na “hazina iliyositirika.” Kwa nini?

4, 5. Kwa nini “kumjua Mungu” kunaweza kulinganishwa na “hazina iliyositirika”? Toa mfano.

4 Sababu moja ni kwamba kumjua Mungu kuna thamani kubwa. Mojawapo ya baraka zenye thamani zaidi za kumjua Mungu ni taraja la uhai udumuo milele. (Yohana 17:3) Lakini ujuzi huo huboresha maisha yetu hata sasa. Kwa mfano, kutokana na uchunguzi wa makini wa Neno la Mungu, tumejibiwa maswali muhimu kama: Mungu anaitwa nani? (Zaburi 83:18) Wafu wako katika hali gani? (Mhubiri 9:5, 10) Kusudi la Mungu ni nini kwa dunia na wanadamu? (Isaya 45:18) Tumekuja kujua kwamba njia bora ya maisha ni kufuata ushauri wenye hekima wa Biblia. (Isaya 30:20, 21; 48:17, 18) Hivyo, tuna mwongozo mzuri unaotusaidia kukabili mahangaiko ya maisha na kujiendesha katika njia inayoleta furaha na uradhi. Zaidi ya yote, kujifunza Neno la Mungu kumetuwezesha kujua sifa nzuri za Yehova na kumkaribia. Je, kuna kitu kingine chochote chenye thamani zaidi ya kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova unaotokana na “kumjua”?

5 Kuna sababu nyingine inayoweza kufanya tulinganishe kumjua Mungu na “hazina iliyositirika.” Kama ilivyo na hazina nyingi, ujuzi huo haupatikani kwa urahisi. Kati ya wakazi wa dunia bilioni sita, waabudu wa Yehova wapatao milioni sita au karibu mtu mmoja kati ya kila watu 1,000 ndio wamepata “kumjua Mungu.” Ili kudhihirisha kwamba kujua kweli ya Neno la Mungu ni pendeleo la pekee, fikiria swali hili moja tu la Biblia: Ni nini hupata wanadamu wanapokufa? Kulingana na Maandiko, tunajua kwamba nafsi hufa na wafu hawafahamu lolote. (Ezekieli 18:4, ZSB) Hata hivyo, dini nyingi za ulimwengu zinaamini isivyo kweli kwamba kitu fulani ndani ya mtu huendelea kuishi baada ya mtu kufa. Hilo ni fundisho la msingi la dini nyingi zinazojiita za Kikristo. Fundisho hilo linapatikana pia katika dini nyingine kama za Wabudha, Wahindu, Wajaini, Waislamu, Washinto, Wasikh, Watao, na Wayahudi. Hebu wazia—mabilioni ya watu ambao wamepotoshwa na fundisho hilo moja lisilo la kweli!

6, 7. (a) Ni nani pekee wanaoweza kupata “kumjua Mungu”? (b) Ni mfano gani unaoonyesha kwamba Yehova ametupatia ufahamu ambao watu wengi “wenye hekima na wenye akili” wamekosa?

6 Kwa nini watu wengi hawajapata “kumjua Mungu”? Kwa sababu mtu hawezi kulielewa Neno la Mungu kabisa bila msaada Wake. Kumbuka kwamba ujuzi huo ni zawadi ambayo Yehova huwapa wale tu walio tayari kuchunguza Neno lake kwa unyofu na kwa unyenyekevu. Huenda watu hao wasiwe “wenye hekima katika njia ya kimwili.” (1 Wakorintho 1:26) Huenda hata wengi wao wakaonwa kuwa watu “wasio na elimu na wa kawaida tu” kulingana na viwango vya ulimwengu. (Matendo 4:13) Hata hivyo, hilo si muhimu. Yehova hututhawabisha kwa kutuwezesha “kumjua,” naye hufanya hivyo kwa sababu ya sifa anazoona moyoni mwetu.

7 Fikiria mfano mmoja. Wasomi wengi wa zile dini zinazojiita za Kikristo wametoa vichapo vingi sana vinavyofafanua Biblia. Huenda vichapo hivyo vya marejeo vikaeleza mambo ya kihistoria kuhusu vitabu vya Biblia, maana ya maneno ya Kiebrania na Kigiriki, na kadhalika. Licha ya elimu yao, je, wasomi hao wamepata “kumjua Mungu” kweli? Je, wanaelewa vizuri kichwa cha Biblia—kutetewa kwa haki ya Yehova ya kutawala kupitia Ufalme wake wa mbinguni? Je, wanajua kwamba Yehova Mungu si sehemu ya Utatu? Sisi tunayafahamu mambo hayo. Kwa nini tuseme hivyo? Kwa sababu Yehova ametupatia ufahamu wa kweli za kiroho ambazo watu wengi “wenye hekima na wenye akili” wamekosa. (Mathayo 11:25) Yehova huwabariki sana wale wanaomkaribia!

‘Yehova Huwalinda Wote Wampendao’

8, 9. (a) Daudi alifafanuaje baraka nyingine ambayo wale wanaomkaribia Yehova hupata? (b) Kwa nini Wakristo wa kweli wanahitaji ulinzi wa Mungu?

8 Wale wanaomkaribia Yehova hufurahia baraka nyingine—ulinzi wake. Mtunga-zaburi Daudi, ambaye alipatwa na magumu na matatizo mengi, aliandika: “BWANA yu karibu na wote wamwitao, wote wamwitao kwa uaminifu. Atawafanyia wamchao matakwa yao, naye atakisikia kilio chao na kuwaokoa. BWANA huwahifadhi [“huwalinda,” NW] wote wampendao.” (Zaburi 145:18-20) Naam, Yehova yu karibu na wale wampendao kwa hiyo anaweza kuitikia upesi vilio vyao wanapoomba msaada.

9 Kwa nini tunahitaji ulinzi wa Mungu? Mbali na kuathiriwa na hali katika ‘nyakati hizi za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo,’ Wakristo wa kweli hushambuliwa sana na Shetani Ibilisi, ambaye ni Adui mkubwa wa Yehova. (2 Timotheo 3:1) Adui huyo mwenye ujanja ameazimia ‘kutunyafua.’ (1 Petro 5:8) Shetani hutunyanyasa, hutuletea mikazo, na kutushawishi. Yeye pia hutafuta mitazamo fulani ya akili na ya moyo anayoweza kuitumia vibaya. Lengo lake ni: kudhoofisha imani yetu na kutuangamiza kiroho. (Ufunuo 12:12, 17) Kwa kuwa tunakabiliana na adui huyo mwenye nguvu nyingi, je, si jambo lenye kutia moyo kujua kwamba ‘Yehova huwalinda wote wampendao’?

10. (a) Yehova huwalindaje watu wake? (b) Ni ulinzi gani ulio muhimu zaidi, na kwa nini?

10 Lakini Yehova hawalindaje watu wake? Ingawa ameahidi kwamba atatulinda, hiyo haimaanishi kwamba hatutapatwa na matatizo yoyote katika ulimwengu huu; wala haimaanishi kwamba atalazimika kufanya miujiza kwa niaba yetu. Hata hivyo, Yehova hutoa ulinzi wa kimwili kwa watu wake kwa ujumla, kwa kuwa hawezi kumruhusu Ibilisi awaangamize waabudu wa kweli duniani! (2 Petro 2:9) Zaidi ya yote, Yehova hutulinda kiroho. Yeye hutuandalia tunachohitaji ili kuvumilia majaribu na kulinda uhusiano wetu pamoja naye. Ulinzi wa kiroho ndio hasa muhimu zaidi. Kwa nini? Maadamu tuna uhusiano na Yehova, hakuna chochote—hata kifo—kinachoweza kutuletea madhara ya kudumu.—Mathayo 10:28.

11. Yehova amefanya maandalizi gani ili kuwalinda watu wake kiroho?

11 Yehova amefanya maandalizi mengi ya kuwalinda kiroho wale wanaomkaribia. Kupitia Neno lake Biblia, yeye hutupatia hekima ya kushinda majaribu mbalimbali. (Yakobo 1:2-5) Tunapata ulinzi kwa kufuata ushauri unaofaa unaopatikana katika Maandiko. Zaidi ya hayo, Yehova ‘huwapa roho takatifu wale wanaomwomba.’ (Luka 11:13) Hiyo ndiyo roho yenye nguvu zaidi ulimwenguni, kwa hiyo inaweza kutusaidia kushinda jaribu au kishawishi chochote kinachoweza kutupata. Yehova hutoa “zawadi zikiwa wanadamu” kupitia Kristo. (Waefeso 4:8) Wanaume hao wanaostahili kiroho hujitahidi kuiga huruma nyingi ya Yehova wanapowasaidia waabudu wenzao.—Yakobo 5:14, 15.

12, 13. (a) Yehova hutumia njia zipi kutuandalia chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa? (b) Unahisije kuhusu maandalizi ambayo Yehova amefanya ili kuboresha hali yetu ya kiroho?

12 Kuna uandalizi mwingine ambao Yehova amefanya ili kutulinda: chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa. (Mathayo 24:45) Kupitia vichapo, kutia ndani magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni!, na pia mikutano na makusanyiko, Yehova hutuandalia tunachohitaji wakati tunapokihitaji. Je, unaweza kukumbuka pindi ambapo ulisikia jambo fulani lililokutia nguvu au kukufariji kwenye mikutano ya Kikristo au kwenye kusanyiko? Je, umewahi kusoma makala fulani katika magazeti yaliyotajwa juu na kuhisi kwamba iliandikwa kwa ajili yako?

13 Silaha ambayo Shetani hutumia kwa matokeo sana ni kivunja-moyo, nasi tunaweza kuathiriwa. Yeye anajua vizuri kwamba tukivunjika moyo kwa muda mrefu, tunaweza kudhoofika na hata kufanya iwe rahisi kwake kutushambulia. (Mithali 24:10) Kwa sababu Shetani anajaribu kutumia vibaya hali hiyo ya kuvunjika moyo, tunahitaji msaada. Mara kwa mara, magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! yamekuwa na makala zinazotusaidia kukabiliana na kuvunjika moyo. Dada mmoja Mkristo aliandika hivi kuhusu makala moja inayozungumzia jambo hilo: “Ninasoma makala hiyo karibu kila siku, na bado mimi hulia ninapoisoma. Naiweka karibu na kitanda changu, mahali ninapoweza kuipata kwa urahisi ninapovunjika moyo. Kwa kusoma makala kama hizi, ninaweza kuhisi mikono ya Yehova ikinikumbatia.” * Je, hatumshukuru Yehova kwa kutuandalia chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa? Kumbuka kwamba maandalizi anayofanya ili kuboresha hali yetu ya kiroho ni uthibitisho kuwa yeye yu karibu nasi na anatulinda.

Kumfikia “Msikiaji wa Sala”

14, 15. (a) Ni baraka gani ambayo Yehova huwapa wale wanaomkaribia? (b) Kwa nini ni pendeleo la pekee sana kuweza kumfikia Yehova kwa sala bila kizuizi?

14 Je, umegundua kwamba kadiri uwezo na mamlaka ya wanadamu yanavyoongezeka, ndivyo mara nyingi inavyokuwa vigumu zaidi kwa wale walio chini yao kuwafikia? Namna gani Yehova Mungu? Je, yeye yuko mbali sana na wanadamu asipendezwe na sala zao? La, hasha! Zawadi ya sala ni baraka nyingine ambayo Yehova huwapa wale wanaomkaribia. Ni pendeleo la pekee sana kuweza kumfikia “Msikiaji wa sala” bila kizuizi. (Zaburi 65:2, NW) Kwa nini?

15 Ona mfano ufuatao: Mkurugenzi mkuu wa kampuni kubwa huwa na shughuli nyingi. Yeye huamua ni mambo gani atakayoshughulikia mwenyewe na ni mambo gani atakayowapa wengine wafanye. Vivyo hivyo, Mtawala Mkuu wa ulimwengu anaweza kuamua ni mambo gani atakayofanya na ni gani atakayowapa wengine wafanye. Fikiria mambo ambayo Yehova amempa Yesu, Mwana wake mpendwa, afanye. Mwana amepewa “mamlaka kufanya kazi ya kuhukumu.” (Yohana 5:27) Malaika ‘wametiishwa kwake.’ (1 Petro 3:22) Yehova amempa Yesu roho Yake takatifu na yenye nguvu ili imsaidie kuwaongoza wanafunzi wake duniani. (Yohana 15:26; 16:7) Kwa hiyo Yesu angeweza kusema: “Nimepewa mamlaka yote mbinguni na juu ya dunia.” (Mathayo 28:18) Hata hivyo, kwa habari ya sala, Yehova amechagua kujihusisha kibinafsi. Hiyo ndiyo sababu Biblia hutuagiza tusali kwa Yehova peke yake, kupitia jina la Yesu.—Zaburi 69:13; Yohana 14:6, 13.

16. Kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova husikiliza sala zetu?

16 Je, kweli Yehova husikiliza sala zetu? Kama hangejali sala zetu, hangetuhimiza “tudumu katika sala” au tumtwike mizigo na mahangaiko yetu. (Waroma 12:12; Zaburi 55:22; 1 Petro 5:7) Watumishi waaminifu wa nyakati za Biblia walikuwa na hakika kabisa kwamba Yehova husikiliza sala. (1 Yohana 5:14) Hivyo, mtunga-zaburi Daudi alisema: “[Yehova] ataisikia sauti yangu.” (Zaburi 55:17) Sisi pia tuna sababu nzuri za kuwa na hakika kwamba Yehova yu karibu na tayari kusikiliza mawazo na mahangaiko yetu yote.

Yehova Huwathawabisha Watumishi Wake

17, 18. (a) Yehova huhisije kuhusu utumishi wa viumbe wake wenye akili—wanadamu na malaika? (b) Eleza jinsi Mithali 19:17 inavyoonyesha kwamba Yehova huthamini matendo yetu ya huruma.

17 Cheo cha Yehova akiwa Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu wote hakiathiriwi na yale ambayo wanadamu wanaweza kufanya au kukataa kufanya. Hata hivyo, Yehova ni Mungu mwenye uthamini. Yeye huthamini na hupendezwa na utumishi mwaminifu wa viumbe wake wenye akili—wanadamu na malaika. (Zaburi 147:11) Kuna baraka nyingine pia ambayo wale wanaomkaribia Yehova hupata: Yeye huwathawabisha watumishi wake.—Waebrania 11:6.

18 Biblia huonyesha wazi kwamba Yehova huthamini yale ambayo waabudu wake hufanya. Kwa mfano, tunasoma: “Amhurumiaye maskini humkopesha BWANA; naye atamlipa kwa tendo lake jema.” (Mithali 19:17) Sheria ya Musa ilionyesha jinsi Yehova anavyowahurumia watu wa hali ya chini. (Mambo ya Walawi 14:21; 19:15) Yehova huhisije tunapomwiga kwa kuwaonyesha huruma watu wa hali ya chini? Tunapompa mtu wa hali ya chini kitu pasipo kutazamia aturudishie, Yehova huona ni kama tumemkopesha Yeye. Yehova anaahidi kulipa deni hilo kwa kutuonyesha kibali na kutubariki. (Mithali 10:22; Mathayo 6:3, 4; Luka 14:12-14) Naam, tunapomwonyesha huruma mwabudu mwenzetu aliye na uhitaji, jambo hilo hugusa moyo wa Yehova. Tunashukuru kama nini kujua kwamba matendo yetu ya huruma yanathaminiwa na Baba yetu wa mbinguni!—Mathayo 5:7.

19. (a) Kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova huthamini tunayofanya katika kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi? (b) Yehova hututhawabishaje kwa utumishi tunaofanya ili kutegemeza Ufalme wake?

19 Yehova hasa huthamini yale tunayofanya kwa ajili ya Ufalme wake. Tunapomkaribia Yehova, ni jambo la kawaida kutaka kutumia wakati, nguvu, na mali zetu ili tushiriki kikamili iwezekanavyo katika kazi ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi. (Mathayo 28:19, 20) Nyakati nyingine, huenda tukahisi kwamba tunatimiza kazi hiyo kwa kiwango kidogo sana. Huenda hata moyo wetu usio mkamilifu ukafanya tuwe na shaka kama Yehova anapendezwa na jitihada zetu. (1 Yohana 3:19, 20) Lakini Yehova huthamini kila zawadi—hata iwe ndogo—ambayo inatolewa kwa moyo wa upendo. (Marko 12:41-44) Biblia hutuhakikishia hivi: “Mungu si asiye mwadilifu ili asahau kazi yenu na upendo mlioonyesha kwa ajili ya jina lake.” (Waebrania 6:10) Naam, Hata utumishi wetu uwe mdogo kadiri gani, Yehova hutukumbuka na kututhawabisha kwa yote tunayofanya ili kutegemeza Ufalme wake. Mbali na baraka tele za kiroho, tunaweza kutazamia maisha yenye furaha katika ulimwengu mpya unaokuja, ambapo Yehova atatoa kwa ukarimu na kutosheleza tamaa za watu wote waadilifu wanaomkaribia!—Zaburi 145:16; 2 Petro 3:13.

20. Katika mwaka wote wa 2003, tunawezaje kuendelea kufikiria maneno ya andiko la mwaka, na matokeo yatakuwa nini?

20 Katika mwaka wote wa 2003, na tujichunguze wenyewe tuone kama tunaendelea kujitahidi kumkaribia Baba yetu wa mbinguni. Tukifanya hivyo, tunaweza kuwa na hakika kwamba atatenda kulingana na ahadi yake, kwa kuwa ‘Mungu hawezi kusema uwongo.’ (Tito 1:2) Ukimkaribia, atakukaribia. (Yakobo 4:8) Matokeo yatakuwa nini? Baraka nyingi sasa na tazamio la kuendelea kumkaribia Yehova milele!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 13 Barua iliyoandikwa kuhusu makala yenye kichwa “Yehova Ni Mkubwa Zaidi Kuliko Mioyo Yetu,” katika toleo la Mnara wa Mlinzi la Mei 1, 2000, ukurasa wa 28-31.

Je, Unakumbuka?

• Yehova huwapa zawadi gani wale wanaomkaribia?

• Yehova hufanya maandalizi gani ili kuwalinda watu wake kiroho?

• Kwa nini ni pendeleo la pekee kumfikia Yehova kwa sala bila kizuizi?

• Biblia huonyeshaje kwamba Yehova huthamini utumishi wa uaminifu wa viumbe wake wenye akili?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 15]

Yehova ametupatia ufahamu wa kweli za kiroho

[Picha katika ukurasa wa 17]

Yehova hutoa ulinzi wa kiroho

[Picha katika ukurasa wa 18]

Yehova yu karibu na tayari kusikiliza sala zetu zote