Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wamjua Shafani na Familia Yake?

Je, Wamjua Shafani na Familia Yake?

Je, Wamjua Shafani na Familia Yake?

ULIPOKUWA ukisoma Biblia yako, je, umewahi kusoma kuhusu Shafani na familia yake iliyokuwa mashuhuri? Walikuwa nani? Walifanya nini? Tunaweza kujifunza nini kutoka kwao?

Biblia humtaja “Shafani, mwana wa Azalia, mwana wa Meshulamu” kwa mara ya kwanza Yosia aliporudisha ibada ya kweli yapata mwaka wa 642 K.W.K. (2 Wafalme 22:3) Katika kipindi cha miaka 36 inayofuata, hadi kuharibiwa kwa Yerusalemu mwaka wa 607 K.W.K., tunapata kuwajua wana wake wanne, Ahikamu, Elasa, Gemaria, na Yezania, na wajukuu wake wawili wa kiume, Mikaya na Gedalia. (Ona chati.) “Familia ya Shafani ilisimamia mambo ya kisheria [katika ufalme wa Yuda] na kushikilia wadhifa wa kuwa mwandishi wa mfalme kuanzia wakati wa Yosia hadi wakati wa Utekwa,” chasema kichapo Encyclopaedia Judaica. Kwa kuchunguza yale ambayo Biblia husema kuhusu Shafani na familia yake, tutaelewa jinsi walivyomtegemeza nabii Yeremia na ibada ya kweli ya Yehova.

Shafani Ategemeza Ibada ya Kweli

Mnamo mwaka wa 642 K.W.K., Mfalme Yosia alipokuwa na umri wa miaka 25 hivi, tunaona Shafani anatumikia akiwa mwandishi na mnakili wa mfalme. (Yeremia 36:10) Kazi hiyo ilihusisha nini? Kichapo cha kitaalamu kilichotajwa juu kinasema kwamba mnakili na mwandishi wa mfalme alikuwa mshauri wake wa karibu, alisimamia mambo ya kifedha, alikuwa balozi stadi, alishughulika na masuala ya nchi za kigeni, alifahamu sheria za kimataifa, na mapatano ya biashara. Kwa hiyo, akiwa mwandishi wa mfalme, Shafani alikuwa miongoni mwa watu mashuhuri zaidi katika ufalme huo.

Miaka kumi kabla ya hapo, Yosia mchanga alikuwa ‘ameanza kumtafuta Mungu wa Daudi babaye.’ Yaonekana Shafani alikuwa na umri mkubwa kuliko Yosia na hivyo angeweza kuwa mshauri mzuri wa kiroho na pia angemwunga mkono Yosia katika kampeni yake ya kwanza ya kurudisha ibada ya kweli. *2 Mambo ya Nyakati 34:1-8.

Kazi ya kurekebisha hekalu ilipokuwa ikiendelea, “kitabu cha torati” kilipatikana, naye Shafani ‘akaanza kukisoma mbele ya mfalme.’ Yosia alishtushwa na mambo aliyosikia na hivyo akatuma wajumbe waliotumainika kwenda kwa Hulda nabii wa kike ili kupata habari kutoka kwa Yehova kuhusu kitabu hicho. Mfalme alionyesha kwamba anamtumaini Shafani na mwana wake Ahikamu kwa kuwaweka wawe miongoni mwa wajumbe hao.—2 Wafalme 22:8-14; 2 Mambo ya Nyakati 34:14-22.

Hili ndilo Andiko pekee linaloonyesha jambo alilofanya Shafani. Katika mistari mingine ya Biblia, anatajwa tu kuwa baba au babu. Mzao mmoja wa Shafani alikuwa na uhusiano wa karibu na nabii Yeremia.

Ahikamu na Gedalia

Kama tulivyotangulia kutaja, mwana wa Shafani, Ahikamu anatajwa kwa mara ya kwanza kuhusiana na wajumbe waliotumwa kwa nabii wa kike Hulda. Kichapo fulani cha kitaalamu kinasema: “Ingawa cheo cha Ahikamu hakitajwi katika Biblia ya Kiebrania, yaonekana alikuwa na cheo cha juu.”

Miaka 15 baada ya kisa hicho, maisha ya Yeremia yalikuwa hatarini. Alipowaonya watu kwamba Yehova anakusudia kuharibu Yerusalemu, “hao makuhani, na manabii, na watu wote, wakamkamata, wakisema, Bila shaka utakufa.” Basi ni nini kilichotukia? Simulizi hilo laendelea kusema: “Mkono wa Ahikamu, mwana wa Shafani, alikuwa pamoja na Yeremia, wasimtie katika mikono ya watu auawe.” (Yeremia 26:1-24) Hilo linaonyesha nini? Kichapo The Anchor Bible Dictionary kinasema: “Kisa hiki kinaonyesha kwamba Ahikamu alikuwa na mamlaka na pia, sawa na washiriki wengine wa familia ya Shafani, alimpenda Yeremia.”

Yapata miaka 20 baadaye, Wababiloni walipoharibu Yerusalemu katika mwaka wa 607 K.W.K. na kupeleka watu wengi uhamishoni, Gedalia mjukuu wa Shafani, mwana wa Ahikamu, aliteuliwa kuwa gavana wa Wayahudi waliosalia. Je, alimtunza Yeremia sawa na walivyofanya washiriki wengine wa familia ya Shafani? Biblia inasema: “Basi Yeremia akaenda kwa Gedalia, mwana wa Ahikamu, huko Mizpa, akakaa pamoja naye.” Baada ya miezi michache, Gedalia aliuawa, na Wayahudi waliosalia wakamchukua Yeremia na kwenda naye Misri.—Yeremia 40:5-7; 41:1, 2; 43:4-7.

Gemaria na Mikaya

Gemaria, mwana wa Shafani na mjukuu wake Mikaya walitimiza fungu muhimu katika mambo yanayotajwa kwenye Yeremia sura ya 36. Ulikuwa mwaka wa 624 K.W.K. hivi, katika mwaka wa tano wa Mfalme Yehoyakimu. Baruku, mwandishi wa Yeremia alisoma kwa sauti maneno ya kitabu cha Yeremia kwenye nyumba ya Yehova, “katika chumba cha Gemaria, mwana wa Shafani.” ‘Mikaya, mwana wa Gemaria, mwana wa Shafani, akayasikia maneno yote ya BWANA yaliyokuwa katika chuo hicho.’—Yeremia 36:9-11.

Mikaya akamwambia baba yake na wakuu wote wengine kuhusu kitabu hicho cha kukunjwa na wote wakataka kusikia yaliyokuwamo. Walitendaje? “Ikawa, walipoyasikia maneno hayo yote, wakatazamana kwa hofu, wakamwambia Baruku, Hatuna budi kumwambia mfalme maneno haya yote.” Hata hivyo, kabla ya kuzungumza na mfalme, walimshauri Baruku hivi: “Enenda ukajifiche, wewe na Yeremia, wala mtu asipajue mlipo.”—Yeremia 36:12-19.

Kama ilivyotarajiwa, mfalme alikataa ujumbe uliokuwa katika kitabu hicho cha kukunjwa, naye akakiteketeza. Baadhi ya wakuu, kutia ndani Gemaria, mwana wa Shafani, ‘walimsihi mfalme asiliteketeze gombo lile, lakini hakukubali kuwasikia.’ (Yeremia 36:21-25) Kitabu Jeremiah—An Archaeological Companion kinakata kauli hivi: “Gemaria alikuwa msaidizi mkuu wa Yeremia katika nyumba ya Mfalme Yehoyakimu.”

Elasa na Yezania

Mnamo mwaka wa 617 K.W.K., Babiloni ilianza kutawala ufalme wa Yuda. Maelfu ya Wayahudi, “wakuu wote, na mashujaa wote, . . . na mafundi wote, na wafua chuma wote,” walipelekwa uhamishoni, kutia ndani nabii Ezekieli. Matania, ambaye jina lake lilibadilishwa na Wababiloni kuwa Sedekia, akawa mfalme kibaraka mpya. (2 Wafalme 24:12-17) Baadaye Sedekia alituma wajumbe kutia ndani Elasa mwana wa Shafani hadi Babiloni. Yeremia alimkabidhi Elasa barua iliyokuwa na ujumbe muhimu kutoka kwa Yehova aupeleke kwa Wayahudi waliotekwa.—Yeremia 29:1-3.

Kwa hiyo, Biblia inaonyesha kwamba Shafani, wana wake watatu, na wajukuu wake wawili walitumia mamlaka yao kumtegemeza Yeremia, nabii mwaminifu na ibada ya kweli. Namna gani Yezania, mwana wa Shafani? Tofauti na washiriki wengine wa familia ya Shafani, yaonekana alijihusisha na ibada ya miungu isiyo ya kweli. Mwaka wa sita wa Ezekieli akiwa uhamishoni Babiloni, au mwaka wa 612 K.W.K. hivi, nabii huyo aliona maono ambapo watu 70 walifukiza uvumba kwa sanamu kwenye hekalu huko Yerusalemu. Miongoni mwao kulikuweko Yezania, ambaye ndiye tu anayetajwa kwa jina. Jambo hilo huenda likadokeza kwamba alikuwa mtu mashuhuri katika kikundi hicho. (Ezekieli 8:1, 9-12) Mfano wa Yezania unaonyesha kwamba mtu hawezi kuwa mwabudu mwaminifu wa Yehova eti kwa sababu tu amelelewa katika familia inayomwogopa Mungu. Kila mtu atatoa hesabu kwa matendo yake.—2 Wakorintho 5:10.

Historia ya Shafani na Familia Yake

Tayari mihuri ilikuwa ikitumiwa huko Yuda wakati familia ya Shafani ilikuwa ikitimiza fungu fulani kuhusiana na mambo yaliyotukia Yerusalemu. Mihuri ilitumiwa kutia sahihi hati au kuzifanya ziwe halali, nayo ilitengenezwa kwa mawe yenye thamani, chuma, pembe za tembo, au glasi. Kwa kawaida jina la mwenye muhuri, la baba yake, na nyakati nyingine cheo chake, kiliandikwa kwenye muhuri huo.

Mamia ya mihuri ya Kiebrania iliyoandikwa kwenye udongo imepatikana. Profesa Nahman Avigad, msomi wa maandishi yaliyochongwa ya Kiebrania alisema: “Maandishi ya Kiebrania yaliyochongwa kwenye mihuri hiyo ndiyo pekee yanayotaja watu wanaojulikana katika Biblia.” Je, kuna maandishi yoyote ambayo yamepatikana na ambayo yanataja Shafani au familia yake? Ndiyo, jina la Shafani na la mwana wake Gemaria linapatikana kwenye muhuri ulio katika ukurasa wa 19 na 21.

Pia wasomi wanasema kwamba labda washiriki wengine wanne wa familia hiyo wanatajwa kwenye maandishi yaliyochongwa kwenye muhuri—Azalia, baba ya Shafani; Ahikamu mwana wa Shafani; Gemaria mwana wa Shafani; na Gedalia, ambaye yaonekana alitajwa kwenye maandishi yaliyochongwa kwenye muhuri fulani kuwa mwenye “mamlaka juu ya Nyumba hiyo.” Muhuri wa nne kati ya mihuri hiyo unadhaniwa kuwa wa Gedalia, mjukuu wa Shafani, ijapokuwa baba yake, Ahikamu, hatajwi. Kutajwa kwa cheo chake kwenye muhuri huo kunaonyesha kwamba alikuwa mmoja wa maofisa wa ngazi za juu zaidi serikalini.

Tunaweza Kujifunza Nini?

Shafani na familia yake wanatuwekea kielelezo kizuri kama nini kwa kutumia mamlaka yao kumtegemeza Yeremia nabii mwaminifu, na ibada ya kweli! Sisi pia tunaweza kutumia mali zetu na mamlaka yetu kutegemeza tengenezo la Yehova na waabudu wenzetu.

Tunachochewa na pia imani yetu inaimarishwa tunaposoma Biblia kwa ukawaida na kufanya utafiti kuhusu mashahidi wa Yehova wa kale kama vile Shafani na familia yake. Wao pia ni sehemu ya ‘wingu kubwa la mashahidi’ ambao tunaweza kuiga kielelezo chao.—Waebrania 12:1.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Shafani alikuwa na umri mkubwa kuliko Yosia, kwa sababu Ahikamu mwana wa Shafani alikuwa mtu mzima wakati Yosia alipokuwa na umri wa miaka 25 hivi.—2 Wafalme 22:1-3, 11-14.

[Sanduku katika ukurasa wa 22]

Hulda—Nabii Mashuhuri wa Kike

Baada ya kusikia “kitabu cha torati” kilichopatikana hekaluni kikisomwa, Mfalme Yosia alimwagiza Shafani na maofisa wengine wanne wa ngazi za juu ‘wakamwulize Yehova’ kuhusu kitabu hicho. (2 Wafalme 22:8-20) Wajumbe hao wangepata jibu wapi? Yeremia na labda Nahumu na Sefania, ambao walikuwa manabii na waandishi wa Biblia, waliishi Yuda wakati huo. Hata hivyo, wajumbe hao walimwendea Hulda, nabii wa kike.

Kitabu Jerusalem—An Archaeological Biography kinasema hivi: ‘Jambo la kushangaza kuhusu kisa hicho ni kwamba hakuna mtu aliyeliona kuwa jambo lisilo la kawaida au lisilofaa kwa wanaume kumwendea nabii wa kike ili awathibitishie ukweli wa maneno ya Kitabu cha Kukunjwa cha Torati. Hulda aliposema kwamba ni neno la Bwana, hakuna mtu aliyepinga mamlaka yake ya kutoa uamuzi huo. Mara nyingi kisa hiki hupuuzwa na wasomi ambao huchunguza daraka la wanawake katika Israeli la kale.’ Bila shaka, ujumbe huo ulitoka kwa Yehova.

[Ramani/Picha katika ukurasa wa 21]

 

Ukoo wa Shafani

Meshulamu

Azalia

Shafani

↓ ↓ ↓ ↓

Ahikamu Elasa Gemaria Yezania

↓ ↓

Gedalia Mikaya

[Picha katika ukurasa wa 20]

Gemaria na wengine walimsihi Yehoyakimu asiteketeze kitabu cha kukunjwa kilichotoka kwa Yeremia

[Picha katika ukurasa wa 22]

Ingawa Yezania alikuwa mshiriki wa familia ya Shafani, alionwa katika maono akiabudu sanamu

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 19]

Courtesy Israel Antiquities Authority

[Picha katika ukurasa wa 21 zemeandaliwa na]

Courtesy Israel Antiquities Authority