Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Onyesha Shauku Katika Familia

Onyesha Shauku Katika Familia

Onyesha Shauku Katika Familia

“THUBUTU kuiteketeza!” Tohru akamwambia mke wake, Yoko. * “Nitaiteketeza,” mke wake akamjibu kwa ukali na kuiwasha moto picha waliyokuwa wamepigwa pamoja. Kisha akasema kwa ujeuri, “Nitaiteketeza nyumba hii!” Tohru naye akaitikia kwa kumchapa kofi Yoko na hivyo akamaliza ubishi huo kwa kutumia jeuri.

Miaka mitatu kabla ya tukio hilo, Tohru na Yoko walikuwa wameanza maisha yao ya ndoa kwa furaha. Hivyo basi, mbona ndoa yao ikatumbukia nyongo? Ingawa Tohru alionekana kuwa mtu mzuri, mke wake alihisi kwamba Tohru hakumpenda na kwamba ni mara chache sana alionyesha anajali hisia zake. Ingawa Yoko alijitahidi kumwonyesha shauku, Tohru hakujali. Yoko alishindwa kuvumilia hali hiyo, hivyo akazidi kuwa mwenye kinyongo na hasira. Alipatwa na matatizo ya kukosa usingizi, wasiwasi, kukosa hamu ya chakula, kukasirika upesi, kushuka moyo, na hata kupatwa na hofu za ghafula. Lakini Tohru hakujali hali yenye mkazo iliyokuwa nyumbani kwake. Aliiona kuwa jambo la kawaida tu.

“Nyakati za Hatari Zilizo Ngumu Kushughulika Nazo”

Leo kuna watu wengi walio na matatizo kama hayo. Mtume Paulo alitabiri kwamba katika nyakati zetu, kutakuwa na watu “wasio na shauku ya kiasili.” (2 Timotheo 3:1-5) Neno la awali la Kigiriki linalotafsiriwa “wasio na shauku ya kiasili” katika andiko hilo lina maana inayokaribiana sana na neno linaloonyesha shauku kati ya washiriki wa familia. Shauku hiyo imekosekana siku hizi. Na hata ikiwapo, huenda washiriki wa familia wakaionyesha mara chache sana.

Wazazi wengi leo hawajui jinsi ya kuwaonyesha watoto wao upendo na shauku. Baadhi yao walilelewa katika familia zisizo na shauku na huenda wasitambue kwamba maisha yanaweza kuwa yenye furaha na yenye kupendeza zaidi ikiwa wataonyesha shauku. Tohru alilelewa katika familia kama hiyo. Alipokuwa mtoto, sikuzote babake alikuwa mwenye shughuli nyingi kazini na alikuja nyumbani usiku sana. Alizungumza na Tohru mara chache sana, na alipofanya hivyo alimtusi. Mamake Tohru alifanya kazi kutwa nzima, na hakuwa na wakati mwingi wa kukaa naye. Televisheni ndiyo iliyokuwa mlezi wake. Familia yao haikupongezana wala kuzungumza.

Huenda utamaduni pia ukachangia hali hiyo. Katika sehemu fulani za Amerika ya Kusini, inambidi mwanamume apuuze mila za kwao ili amwonyeshe mke wake shauku. Katika nchi nyingi za Mashariki na Afrika, kuonyesha shauku kwa maneno au kwa matendo ni jambo lisilopatana na mila za huko. Huenda ikawa vigumu kwa mume kumwambia mke au mtoto wake “Ninakupenda.” Hata hivyo, tunaweza kujifunza kutokana na uhusiano mmoja wa kifamilia ambao ni bora na ambao umedumu kwa muda mrefu.

Mfano Bora wa Uhusiano wa Kifamilia

Uhusiano wa karibu kati ya Yehova Mungu na Mwana wake wa pekee ni mfano bora wa kuigwa na familia. Wao huonyeshana upendo kwa njia inayofaa kabisa. Kwa maelfu ya miaka, kiumbe wa roho ambaye baadaye alikuja kuwa Yesu Kristo, alikuwa na uhusiano wenye furaha pamoja na Baba yake. Aliufafanua uhusiano huo hivi: “Nikawa furaha yake kila siku; nikifurahi daima mbele zake.” (Mithali 8:30) Mwana alikuwa na uhakika kwamba Baba yake alimpenda, hivyo angeweza kuwatangazia wengine kwamba alikuwa furaha yake kila siku. Alifurahi daima mbele za Baba yake.

Hata Yesu alipokuwa mwanadamu hapa duniani, Baba yake alimhakikishia kwamba anampenda sana. Baada ya Yesu kubatizwa, alimsikia Baba yake akisema: “Huyu ni Mwana wangu, mpendwa, ambaye nimemkubali.” (Mathayo 3:17) Huo ulikuwa wonyesho wa upendo wenye kutia moyo kama nini mwanzoni mwa huduma ya Yesu duniani! Bila shaka, aliguswa moyo kumsikia Baba yake akisema kwamba anamkubali. Wakati huo alikumbuka vizuri maisha yake akiwa mbinguni.

Hivyo, Yehova anaweka mfano bora kabisa wa kuionyesha upendo familia yake yote ulimwenguni na anafanya hivyo kikamili kabisa. Sisi pia tunaweza kufurahia shauku ya Yehova tukimkubali Yesu Kristo. (Yohana 16:27) Ingawa hatutasikia maneno yoyote kutoka mbinguni, tutaona upendo wa Yehova ambao ametuonyesha kupitia uumbaji, kutolewa kwa dhabihu ya fidia ya Yesu, na katika njia nyingine. (1 Yohana 4:9, 10) Yehova hata husikiliza sala zetu na kuzijibu kwa njia yenye kutunufaisha kabisa. (Zaburi 145:18; Isaya 48:17) Tunapositawisha uhusiano wa karibu pamoja na Yehova, tunakuwa wenye shukrani hata zaidi kwa utunzaji wake wenye upendo.

Yesu alijifunza kutoka kwa Baba yake jinsi ya kuonyesha hisia-mwenzi, fadhili, na kuwahangaikia wengine. Alieleza hivi: “Mambo yoyote yale [Baba] hufanya, mambo hayo Mwana pia hufanya kwa namna kama hiyo. Kwa maana Baba ana shauku na Mwana na humwonyesha mambo yote afanyayo yeye mwenyewe.” (Yohana 5:19, 20) Sisi pia tunaweza kujifunza jinsi ya kuonyesha shauku kwa kuchunguza mfano wa Yesu alipokuwa duniani.—Wafilipi 1:8.

Jinsi Familia Inavyoweza Kuwa na Shauku

Kwa kuwa “Mungu ni upendo” nasi tumeumbwa “kwa mfano wake,” tunaweza kuhisi na kuonyesha upendo. (1 Yohana 4:8; Mwanzo 1:26, 27) Hata hivyo, lazima tujitahidi kuonyesha sifa hiyo. Ili tuweze kuonyesha shauku kwa mwenzi wetu na watoto wetu, ni lazima kwanza tuhisi shauku hiyo. Uwe macho kuona na kutafakari sifa nzuri walizo nazo, ingawa huenda mwanzoni zisionekane kuwa zenye maana. Huenda ukawaza, ‘hakuna sifa yoyote [ya mke wangu au watoto wangu] inayonivutia.’ Huenda mtu akakosa kuwa na shauku kwa mwenzi wake ikiwa alichaguliwa mwenzi huyo na watu wengine. Huenda wenzi wengine hawakutaka kupata watoto. Hata hivyo, fikiria jinsi Yehova alivyohisi kumhusu mke wake wa mfano, yaani, taifa la Israeli, katika karne ya kumi K.W.K. Ingawa nabii Eliya alifikiri kwamba hakukuwa na watu wengine waliomwabudu Yehova miongoni mwa makabila kumi ya taifa la Israeli, Yehova alichunguza kwa makini na kupata idadi kubwa ya watu—7,000 kwa jumla—waliokuwa na sifa zenye kumpendeza. Je, unaweza kumwiga Yehova kwa kutafuta sifa zenye kupendeza katika washiriki wa familia yako?—1 Wafalme 19:14-18.

Hata hivyo, ni lazima ujitahidi sana ili wengine katika familia wahisi una shauku kuwaelekea. Ukiona wanastahili pongezi kwa jambo fulani, wapongeze. Linapofafanua mke mwema, Neno la Mungu linataja sifa fulani yenye kupendeza ya washiriki wa familia yake: “Wanawe huondoka na kumwita heri; mumewe naye humsifu.” (Mithali 31:28) Ona jinsi washiriki hao wa familia walivyothaminiana. Kwa kumsifu mke wake kwa maneno, baba anaweka kielelezo kizuri kwa mwanawe, akimtia moyo awe akimpongeza mwenzi wake atakapofunga ndoa.

Wazazi wanapaswa pia kuwapongeza watoto wao. Kufanya hivyo kunaweza kuwasaidia watoto wajiheshimu. Kwani, mtu anawezaje ‘kumpenda jirani yake kama yeye mwenyewe’ ikiwa hajiheshimu? (Mathayo 22:39) Kwa upande mwingine, ikiwa wazazi wanawakosoa-kosoa watoto wao, bila hata kuwapongeza, watoto wanaweza kuacha kujiheshimu na huenda ikawa vigumu kwao kuwaonyesha wengine shauku.—Waefeso 4:31, 32.

Unaweza Kupata Msaada

Namna gani ikiwa hukulelewa katika familia yenye upendo? Bado unaweza kujizoeza kuonyesha shauku. Hatua ya kwanza ni kutambua kwamba una tatizo la kuonyesha shauku, kisha ukubali kwamba unahitaji kuboresha hali hiyo. Neno la Mungu, Biblia, linaweza kukusaidia sana. Biblia inaweza kulinganishwa na kioo. Tunapojichunguza kupitia mafundisho ya Biblia yaliyo kama kioo, tunaona kasoro tulizo nazo katika mawazo yetu. (Yakobo 1:23) Kupatana na mafundisho ya Biblia, tunaweza kurekebisha maelekeo yoyote yasiyofaa. (Waefeso 4:20-24; Wafilipi 4:8, 9) Tunahitaji kufanya hivyo kwa ukawaida, ‘bila kuacha kamwe kufanya lililo bora.’—Wagalatia 6:9.

Huenda wengine wakaona vigumu kuonyesha shauku kwa sababu ya malezi au utamaduni wao. Hata hivyo, uchunguzi wa hivi karibuni unaonyesha kwamba matatizo hayo yanaweza kutatuliwa. Dakt. Daniel Goleman, mtaalamu wa akili, anaeleza kwamba ‘hata mazoea fulani ya tangu utotoni ambayo yameota mizizi yanaweza kurekebishwa.’ Zaidi ya karne 19 zilizopita, Biblia ilionyesha kwamba kwa msaada wa roho ya Mungu, hata mazoea yaliyoota mizizi kabisa yanaweza kurekebishwa. Inatushauri hivi: “Uvueni utu wa zamani pamoja na mazoea ya huo, na mjivike wenyewe utu mpya.”—Wakolosai 3:9, 10.

Baada ya kujua tatizo lao, washiriki wa familia wanaweza kujifunza Biblia wakizingatia tatizo hilo. Kwa mfano, mbona usichunguze yale Biblia inayosema kuhusu neno “shauku”? Huenda ukapata andiko kama hili: “Nyinyi mmesikia juu ya uvumilivu wa Yobu na mmeona tokeo alilotoa Yehova, kwamba Yehova ni mwenye wororo sana katika shauku na mwenye rehema.” (Yakobo 5:11) Kisha, chunguza masimulizi ya Biblia kuhusu Ayubu, ukikazia fikira jinsi Yehova alivyomwonyesha shauku nyororo na rehema. Bila shaka, utataka kumwiga Yehova na kuwa mwenye rehema na shauku nyingi nyororo kuelekea familia yako.

Hata hivyo, kwa kuwa sisi si wakamilifu, ‘tunajikwaa mara nyingi’ katika mazungumzo yetu. (Yakobo 3:2) Huenda tukashindwa kuzungumza na washiriki wa familia yetu kwa njia yenye kutia moyo. Huo ndio wakati tunapohitaji sala na kumtegemea Yehova. Usikate tamaa. ‘Sali bila kukoma.’ (1 Wathesalonike 5:17) Yehova atawasaidia wale wanaotamani kuonyeshwa shauku katika familia na pia wale wanaotaka kuionyesha lakini wanashindwa kufanya hivyo.

Isitoshe, kwa fadhili Yehova ametoa msaada katika kutaniko la Kikristo. Yakobo aliandika: “Je, kuna yeyote mgonjwa [kiroho] miongoni mwenu? Acheni awaite kwake wanaume wazee wa kutaniko, na acheni wasali juu yake, wakimpaka mafuta katika jina la Yehova.” (Yakobo 5:14) Naam, wazee katika makutaniko ya Mashahidi wa Yehova wanaweza kusaidia sana familia ambazo washiriki wake wanashindwa kuonyeshana shauku. Ingawa wao si wataalamu wa akili, wazee wanaweza kuwasaidia kwa subira waamini wenzao, si kwa kuwaambia wanayopaswa kufanya, bali kwa kuwakumbusha maoni ya Yehova na kusali pamoja nao na kwa ajili yao.—Zaburi 119:105; Wagalatia 6:1.

Kuhusu Tohru na Yoko, sikuzote wazee Wakristo walisikiliza matatizo yao na kuwafariji. (1 Petro 5:2, 3) Nyakati nyingine, mzee na mke wake wangewatembelea ili Yoko aweze kunufaika kwa kushirikiana na mwanamke Mkristo mwenye uzoefu ambaye ‘angemtia akili kumpenda mume wake.’ (Tito 2:3, 4) Kwa kuonyesha fadhili na huruma kwa mateso na huzuni za Wakristo wenzetu, wazee wanakuwa “mahali pa kujificha na upepo, na mahali pa kujisitiri na dhoruba.”—Isaya 32:1, 2.

Kwa msaada wa wazee wenye fadhili, Tohru alikuja kutambua kwamba hakuwa anaonyesha hisia zake na kwamba katika ‘siku hizi za mwisho,’ Shetani anashambulia familia. (2 Timotheo 3:1) Tohru aliamua kulishughulikia tatizo lake. Alianza kutambua kwamba tatizo lake la kutoweza kuonyesha upendo lilitokana na kutoonyeshwa upendo alipokuwa akikua. Kupitia funzo la makini la Biblia na sala, Tohru alianza kuzingatia hatua kwa hatua mahitaji ya Yoko ya kihisia-moyo.

Ingawa Yoko alikuwa amemkasirikia Tohru, alijitahidi sana kuzingatia sifa zake nzuri alipotambua udhaifu wake mwenyewe na kufahamu jinsi maisha ya Tohru yalivyokuwa utotoni. (Mathayo 7:1-3; Waroma 5:12; Wakolosai 3:12-14) Alimwomba Yehova kwa bidii ili ampatie nguvu za kuendelea kumpenda mume wake. (Wafilipi 4:6, 7) Hatimaye, Tohru alianza kuonyesha shauku, jambo lililomfurahisha mke wake.

Naam, hata ikiwa unaona ni vigumu kuhisi na kuonyesha washiriki wa familia shauku, unaweza kushinda tatizo hilo. Neno la Mungu hutupatia mwongozo ufaao. (Zaburi 19:7) Kwa kutambua uzito wa jambo hilo, kujitahidi kuzingatia sifa nzuri za familia yako, kujifunza na kufuata Neno la Mungu, kumtegemea Yehova kupitia sala ya bidii, na kwa kutafuta msaada wa wazee walio Wakristo wakomavu, unaweza kushinda tatizo ambalo huenda likaonekana kuwa kizuizi kikubwa kinachokutenganisha na familia yako. (1 Petro 5:7) Wewe pia unaweza kufurahi kama vile alivyofurahi mume mmoja huko Marekani. Alitiwa moyo amwonyeshe mke wake shauku. Hatimaye alipopiga moyo konde na kumwambia “Ninakupenda,” alishangaa kuona jinsi mke alivyoitikia. Alisema hivi huku akilengwalengwa na machozi: “Ninakupenda pia, lakini hii ndiyo mara ya kwanza katika muda wa miaka 25 umetamka maneno hayo.” Usingojee muda mrefu hivyo kabla ya kumwonyesha mwenzi wako na watoto wako shauku.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

[Picha katika ukurasa wa 28]

Yehova hutoa msaada kupitia Neno lake, Biblia