Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 4

Kwa Nini Tuheshimu Mamlaka?

Kwa Nini Tuheshimu Mamlaka?

“Waheshimuni watu wa namna zote.”—1 PETRO 2:17.

1, 2. (a) Kwa nini ni vigumu kwetu kuheshimu mamlaka? (b) Tutachunguza maswali gani?

JE, UMEPATA kuona jinsi mtoto mdogo anavyotenda anapoambiwa afanye jambo fulani ambalo hataki kulifanya? Sura yake inaweza kuonyesha wazi kabisa kwamba hataki. Anasikia sauti ya mzazi wake, naye anajua kwamba anapaswa kuheshimu mamlaka ya mzazi wake. Lakini katika kisa hiki, hataki kutii. Hali hiyo inafanana sana na hali ambayo kila mmoja wetu anakabili.

2 Si rahisi kuheshimu mamlaka sikuzote. Je, nyakati nyingine wewe huona ni vigumu kuwaheshimu wale walio na mamlaka fulani juu yako? Ikiwa ndivyo, si wewe tu unayepambana na jambo hilo. Leo, watu wengi sana hawaheshimu mamlaka. Hata hivyo, Biblia inasema kwamba tunahitaji kuwaheshimu wale walio na mamlaka juu yetu. (Methali 24:21) Kwa hakika, lazima tufanye hivyo ikiwa tunataka kukaa katika upendo wa Mungu. Hivyo basi, maswali fulani yanahitaji kujibiwa. Kwa nini inaweza kuwa vigumu sana kwetu kuheshimu mamlaka? Kwa nini Yehova anataka tuheshimu mamlaka, na ni nini kitakachotusaidia kutii? Mwishowe, ni kwa njia gani tunaweza kuonyesha kwamba tunaheshimu mamlaka?

KWA NINI NI VIGUMU?

3, 4. Dhambi na hali ya kutokamilika zilianza jinsi gani, na kwa nini mwelekeo wetu wa kutenda dhambi hufanya iwe vigumu kwetu kuheshimu mamlaka?

3 Acheni tuzungumzie kwa ufupi sababu mbili zinazoonyesha kwa nini inaweza kuwa vigumu sana kwetu kuheshimu wale walio na mamlaka. Kwanza, sisi si wakamilifu; pili, hata wale walio na mamlaka juu yetu si wakamilifu. Dhambi na hali ya kutokamilika ya wanadamu zilianza zamani sana katika bustani ya Edeni wakati ambapo Adamu na Hawa waliasi mamlaka ya Mungu. Kwa hiyo dhambi ya kwanza ilikuwa uasi. Mpaka leo hii tunazaliwa tukiwa na mwelekeo wa kuasi.—Mwanzo 2:15-17; 3:1-7; Zaburi 51:5; Waroma 5:12.

4 Kwa sababu ya mwelekeo wetu wa kutenda dhambi, wengi wetu husitawisha kiburi na majivuno kwa urahisi. Kwa upande mwingine, sifa ya unyenyekevu haipatikani kwa urahisi nasi tunahitaji jitihada nyingi ili kusitawisha na kudumisha sifa hiyo. Hata baada ya kumtumikia Mungu kwa uaminifu kwa miaka mingi, tunaweza kuonyesha ukaidi na kiburi. Kwa mfano, mfikirie Kora. Ijapokuwa alishikamana kwa uaminifu na watu wa Yehova wakati wa dhiki nyingi, alitamani kupata mamlaka zaidi na kwa ushupavu akawachochea watu wamwasi Musa, ambaye alikuwa mwanamume mpole zaidi kuliko watu wote wakati huo. (Hesabu 12:3; 16:1-3) Pia, mfikirie Mfalme Uzia, ambaye alichochewa na kiburi kuingia katika hekalu la Yehova na kufanya kazi takatifu iliyopaswa kufanywa na makuhani tu. (2 Mambo ya Nyakati 26:16-21) Watu hao walipata adhabu kali kwa sababu ya uasi wao. Hata hivyo, sisi sote tunaweza kujifunza mambo muhimu kutokana na mifano yao mibaya. Tunahitaji kupambana na kiburi ambacho hufanya iwe vigumu kwetu kuheshimu mamlaka.

5. Ni kwa njia gani wanadamu wasio wakamilifu wametumia mamlaka yao vibaya?

5 Kwa upande mwingine, wanadamu wasio wakamilifu ambao wana mamlaka wamechangia sana kutoheshimiwa kwa mamlaka. Wengi wao wamekuwa wakatili, wenye kukandamiza, na wametawala kwa mabavu. Katika sehemu kubwa ya historia ya wanadamu, mamlaka imetumiwa vibaya. (Mhubiri 8:9) Kwa mfano, Sauli alikuwa mtu mzuri na mnyenyekevu Yehova alipomchagua awe mfalme. Lakini, alishindwa na kiburi na wivu; kisha akamtesa Daudi ambaye alikuwa mwaminifu. (1 Samweli 9:20, 21; 10:20-22; 18:7-11) Baadaye, Daudi akawa mmoja wa wafalme bora wa Israeli, lakini akatumia mamlaka yake vibaya alipomchukua mke wa Uria Mhiti na kuagiza mtu huyo asiye na hatia awekwe kwenye mstari wa mbele vitani ili auawe. (2 Samweli 11:1-17) Ndiyo, hali ya kutokamilika inafanya iwe vigumu kwa watu kutumia mamlaka vizuri. Na ikiwa wale walio na mamlaka hawamheshimu Yehova, wanatumia mamlaka yao vibaya hata zaidi. Baada ya kueleza jinsi mapapa fulani wa Katoliki walivyoanzisha mateso yaliyoenea sana, kiongozi mmoja wa Uingereza aliandika: “Mamlaka inaharibu watu, na mamlaka kamili inawaharibu kabisa.” Tukiwa na hilo akilini, acheni tufikirie swali hili: Kwa nini tunapaswa kuheshimu mamlaka?

KWA NINI TUHESHIMU MAMLAKA?

6, 7. (a) Kumpenda Yehova kunatuchochea kufanya nini, na kwa nini? (b) Tunaweza kuonyesha jinsi gani kwamba tuna sifa ya kujitiisha?

6 Sababu kuu za kuheshimu mamlaka zinatokana na upendo—kumpenda Yehova, kuwapenda wanadamu wenzetu, na hata kujipenda wenyewe. Kwa sababu tunampenda Yehova kuliko mtu mwingine yeyote, tunataka kuufurahisha moyo wake. (Methali 27:11; Marko 12:29, 30) Tunajua kwamba enzi kuu yake, haki yake ya kutawala ulimwengu, ilitiliwa shaka duniani tangu uasi ulipotokea Edeni. Pia, tunajua kwamba wanadamu wengi wamemuunga mkono Shetani na kuukataa utawala wa Yehova. Sisi, tunafurahi kuwa upande wa Yehova. Tunaposoma maneno yenye kusisimua ya Ufunuo 4:11, mioyo yetu inasisimuka kwelikweli. Hatuna shaka lolote kwamba Yehova ndiye mwenye haki ya kuwa Mtawala wa ulimwengu! Tunaiunga mkono enzi kuu ya Yehova na kuukubali utawala wake kila siku maishani mwetu.

7 Heshima hiyo inatuchochea kufanya mengi zaidi ya kutii tu. Bila shaka, tunamtii Yehova kwa hiari kwa sababu tunampenda. Hata hivyo, kuna nyakati ambapo itakuwa vigumu sana kwetu kutii. Nyakati hizo, kama yule mvulana aliyetajwa mwanzoni, tunahitaji kujifunza kujitiisha. Tunakumbuka kwamba Yesu alijitiisha kwa mapenzi ya Baba yake hata ilipoonekana kuwa vigumu sana. Alimwambia hivi Baba yake: “Acha, si mapenzi yangu, bali yako yatendeke.”—Luka 22:42.

8. (a) Kujitiisha chini ya mamlaka ya Yehova leo kunahusisha nini, na ni nini kinachoonyesha maoni ya Yehova kuhusu jambo hilo? (b) Ni nini kinachoweza kutusaidia kusikiliza shauri na kukubali nidhamu? (Ona sanduku “ Sikiliza Shauri na Kukubali Nidhamu.”)

8 Bila shaka, Yehova hazungumzi na mtu mmoja-mmoja leo; anatumia Neno lake na wanadamu wanaomwakilisha duniani. Hivyo, mara nyingi tunajitiisha kwa mamlaka ya Yehova kwa kuwaheshimu wanadamu ambao ameweka au ambao ameruhusu waendelee kuwa na mamlaka juu yetu. Tukiasi mwongozo wao—kwa mfano kwa kukataa wanapotushauri na kuturekebisha kwa kutumia Maandiko—tunamchukiza Mungu. Waisraeli waliponung’unika na kumwasi Musa, Yehova aliona kwamba walikuwa wakimnung’unikia na kumwasi yeye mwenyewe.—Hesabu 14:26, 27.

9. Kuwapenda wanadamu wenzetu kunatuchochea jinsi gani kuheshimu mamlaka? Toa mfano.

9 Pia, tunaheshimu mamlaka kwa sababu tunawapenda wanadamu wenzetu. Jinsi gani? Wazia kwamba wewe ni askari katika jeshi. Ili jeshi hilo lifanikiwe na hata kuokoka, kila askari anahitaji kuwa na moyo wa ushirikiano, kutii, na kuheshimu maofisa mbalimbali wenye mamlaka. Ikiwa ungeasi mamlaka hiyo, hilo linaweza kuhatarisha askari wengine wote. Ni kweli kwamba majeshi ya wanadamu yanasababisha uharibifu mwingi ulimwenguni leo. Hata hivyo, Yehova ana majeshi ambayo kazi yake ni kuwasaidia watu. Katika mamia ya maandiko, Mungu anatajwa kuwa “Yehova wa majeshi.” (1 Samweli 1:3) Yeye ndiye Amiri-Jeshi wa viumbe wengi wa roho wenye nguvu. Nyakati nyingine, Yehova anawalinganisha watumishi wake walio duniani na jeshi. (Zaburi 68:11; Ezekieli 37:1-10) Tukiasi mwongozo wa wanadamu ambao Yehova amewapa mamlaka juu yetu, je, hatuhatarishi askari wenzetu katika vita vya kiroho? Mkristo anapoasi mwongozo wa wazee waliowekwa rasmi, wengine katika kutaniko wanaweza kuumia. (1 Wakorintho 12:14, 25, 26) Mtoto anapoasi, familia yote inaweza kuumia. Kwa hiyo, tunaonyesha tunawapenda wanadamu wenzetu tunapokuza roho ya heshima na ushirikiano.

10, 11. Ni jambo gani lingine linalotuchochea kutii mamlaka?

10 Pia, tunaheshimu mamlaka kwa sababu sisi wenyewe tunafaidika. Yehova anapotuagiza tuheshimu mamlaka, mara nyingi anataja faida tutakazopata tunapofanya hivyo. Kwa mfano, anawaambia watoto wawatii wazazi wao ili waishi kwa muda mrefu na kwa furaha. (Kumbukumbu la Torati 5:16; Waefeso 6:2, 3) Anatuagiza tuwaheshimu wazee wa kutaniko kwa sababu kutofanya hivyo kutatuletea madhara ya kiroho. (Waebrania 13:7, 17) Naye anatuambia tutii mamlaka za ulimwengu kwa faida yetu wenyewe.—Waroma 13:4.

11 Je, hukubali kwamba kujua kwa nini Yehova anataka tutii kunatusaidia kuheshimu mamlaka? Basi, acheni sasa tuchunguze jinsi tunavyoweza kuheshimu mamlaka katika sehemu tatu muhimu za maisha yetu.

KUONYESHA HESHIMA KATIKA FAMILIA

12. Yehova amempa mume au baba jukumu gani katika familia, na mwanamume anaweza kulitimiza jukumu hilo jinsi gani?

12 Yehova mwenyewe ndiye aliyeanzisha mpango wa familia. Kwa kuwa yeye ni Mungu wa utaratibu, ameweka utaratibu katika familia ili mambo yawe shwari. (1 Wakorintho 14:33) Amempa mume au baba mamlaka ya kuwa kichwa cha familia. Mume anaonyesha kwamba anaheshimu Kichwa chake, Kristo Yesu, kwa kuiga jinsi Yesu anavyotumia ukichwa wake kusimamia kutaniko. (Waefeso 5:23) Hivyo, mume hapaswi kupuuza jukumu lake bali anapaswa kulitekeleza kwa ujasiri; wala hapaswi kuwa mkatili au mkali, badala yake awe mwenye upendo, mwenye usawaziko, na mwenye fadhili. Sikuzote, anakumbuka kwamba mamlaka yake ni ya kadiri—haipiti kamwe mamlaka ya Yehova.

Baba Mkristo anaiga jinsi Kristo anavyotumia ukichwa

13. Ni katika njia gani mke au mama anaweza kutimiza jukumu lake katika familia kwa njia inayompendeza Yehova?

13 Mke au mama anapaswa kuwa msaidizi au kikamilisho cha mume. Yeye pia amepewa mamlaka katika familia kwa kuwa Biblia hutaja “sheria ya mama yako.” (Methali 1:8) Bila shaka, mamlaka yake iko chini ya mamlaka ya mume wake. Mke Mkristo huonyesha kwamba anaheshimu mamlaka ya mume wake kwa kumsaidia atimize jukumu lake akiwa kichwa cha familia. Hamdharau, hatumii hila ili kumshawishi, wala hajaribu kunyakua mamlaka yake. Badala yake, anamuunga mkono na kushirikiana naye. Mume anapofanya maamuzi ambayo hayampendezi, anaweza kueleza maoni yake kwa heshima, lakini bado ataendelea kujitiisha kwake. Ikiwa mume wake si mwamini, huenda hali ikawa ngumu, hata hivyo, kujitiisha kwake kunaweza kumchochea mume wake amtafute Yehova.—1 Petro 3:1.

14. Ni kwa njia gani watoto wanaweza kuwafanya wazazi wao na Yehova wawe na shangwe?

14 Watoto hufurahisha moyo wa Yehova wanapotii baba na mama yao. Pia wanawaletea wazazi wao sifa na shangwe. (Methali 10:1) Katika familia za mzazi mmoja, watoto hufuata kanuni hiyohiyo ya utii wakikumbuka kwamba mzazi huyo anahitaji hata zaidi utegemezo na ushirikiano wao. Familia ambazo washiriki wote wanatimiza majukumu waliyopewa na Mungu huwa na amani na shangwe nyingi. Hilo linamletea sifa Mwanzilishi wa familia zote, Yehova Mungu.—Waefeso 3:14, 15.

KUONYESHA HESHIMA KATIKA KUTANIKO

15. (a) Katika kutaniko, ni kwa njia gani tunaweza kuonyesha kwamba tunaheshimu mamlaka ya Yehova? (b) Ni kanuni gani zinazoweza kutusaidia kuwatii wale wanaoongoza? (Ona sanduku “ Watiini Wale Wanaoongoza.”)

15 Yehova amemweka Mwana wake kuwa Mtawala wa kutaniko la Kikristo. (Wakolosai 1:13) Naye Yesu amempa “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” mgawo wa kushughulikia mahitaji ya kiroho ya watu wa Mungu walio duniani. (Mathayo 24:45-47) Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova linawakilisha jamii ya mtumwa huyo. Kama ilivyokuwa katika makutaniko ya Kikristo ya karne ya kwanza, leo wazee wanapokea maagizo na mashauri kutoka kwa Baraza Linaloongoza, moja kwa moja au kupitia wawakilishi wake, kama vile waangalizi wanaosafiri. Tunapoheshimu mamlaka ya wazee Wakristo tukiwa mtu mmoja-mmoja, tunamtii Yehova.​—Soma 1 Wathesalonike 5:12; Waebrania 13:17.

16. Ni katika njia gani wazee wanawekwa na roho takatifu?

16 Wazee na watumishi wa huduma si wakamilifu. Kama sisi, wanaweza kukosea pia. Hata hivyo, wazee ni “zawadi katika wanadamu,” ambao wameandaliwa ili kulisaidia kutaniko liendelee kuwa imara kiroho. (Waefeso 4:8) Wazee wanawekwa na roho takatifu. (Matendo 20:28) Jinsi gani? Kwa sababu lazima kwanza watimize matakwa yaliyoandikwa katika Neno la Mungu lililoongozwa na roho. (1 Timotheo 3:1-7, 12; Tito 1:5-9) Pia, wazee wanaochunguza sifa za kustahili za ndugu husali kwa bidii ili roho takatifu ya Yehova iwaongoze.

17. Kwa nini wanawake Wakristo nyakati nyingine wanajifunika kichwa wanaposhughulikia mambo fulani ya kutaniko?

17 Katika kutaniko, huenda nyakati nyingine kusiwe na wazee au watumishi wa huduma wa kushughulikia migawo ambayo kwa kawaida ni kazi yao, kama vile kuongoza mkutano wa utumishi wa shambani. Katika nyakati kama hizo, ndugu wengine ambao wamebatizwa wanaweza kutimiza migawo hiyo. Ikiwa hakuna ndugu wowote, basi dada Wakristo wanaostahili wanaweza kushughulikia migawo hiyo. Hata hivyo, mwanamke anaposhughulikia mgawo ambao kwa kawaida hushughulikiwa na mwanamume aliyebatizwa, anapaswa kujifunika kichwa. * (1 Wakorintho 11:3-10) Takwa hilo haliwavunjii heshima wanawake. Badala yake linawapa nafasi ya kuonyesha kwamba wanaheshimu mpango wa Yehova wa ukichwa katika familia na katika kutaniko.

KUHESHIMU MAMLAKA ZA ULIMWENGU

18, 19. (a) Fafanua kanuni zilizo katika Waroma 13:1-7. (b) Ni kwa njia gani tunaonyesha kwamba tunaheshimu mamlaka za ulimwengu?

18 Wakristo wa kweli wanajitahidi sana kufuata kanuni zilizo katika Waroma 13:1-7. Unaposoma mistari hiyo, unaweza kuona kwamba “mamlaka zilizo kubwa” zinazotajwa ni serikali za ulimwengu. Maadamu Yehova anaruhusu serikali hizo za ulimwengu ziendelee kuwapo, zinatimiza mambo muhimu, zikidumisha utaratibu kwa kadiri fulani na kutoa huduma zinazohitajiwa. Tunaonyesha kwamba tunaheshimu mamlaka hizo kwa kutii sheria. Tunahakikisha kwamba tunalipa kodi zozote tunazodaiwa, kujaza kwa usahihi fomu au karatasi zozote zinazohitajiwa na serikali, na kutii sheria zozote zinazotuhusu sisi, familia yetu, biashara yetu, au mali yetu. Hata hivyo, hatuwezi kutii mamlaka za ulimwengu zinapotuagiza tusimtii Mungu. Badala yake tunasema kama mitume wa kale walivyosema: “Lazima tumtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.”—Matendo 5:28, 29; Ona sanduku “ Ni Mamlaka ya Nani Ninayopaswa Kutii?”.

19 Pia, tunaheshimu mamlaka za ulimwengu kupitia mwenendo wetu. Nyakati nyingine, huenda tukashughulika moja kwa moja na maofisa wa serikali. Mtume Paulo alishughulika na watawala kama Mfalme Herode Agripa na Gavana Festo. Watu hao walikuwa na udhaifu mkubwa, lakini Paulo alizungumza nao kwa heshima. (Matendo 26:2, 25) Tunaiga mfano wa Paulo, iwe ofisa tunayezungumza naye ni mtawala mwenye mamlaka kubwa au ni polisi. Shuleni, vijana Wakristo wanajitahidi kuwaheshimu walimu, maofisa, na wafanyakazi wa shule. Bila shaka, hatuwaheshimu tu wale wanaokubali imani yetu; tunaonyesha heshima pia tunaposhughulika na watu ambao wanawapinga Mashahidi wa Yehova. Kwa kweli, watu ambao si waamini wanapaswa kutambua kwamba tuna heshima.—Waroma 12:17, 18; 1 Petro 3:15.

20, 21. Ni faida gani tunazopata kwa kuheshimu mamlaka?

20 Tusiwe wachoyo katika kuwaonyesha wengine heshima. Mtume Petro aliandika hivi: “Waheshimuni watu wa namna zote.” (1 Petro 2:17) Watu wanapotambua kwamba tunawaheshimu kikweli, wanaweza kuchochewa sana. Kumbuka kwamba sifa hiyo inazidi kuwa haba. Hivyo, kuwa wenye heshima ni njia moja ya kutii amri hii ya Yesu: “Acheni nuru yenu iangaze mbele ya watu, ili wapate kuona matendo yenu mazuri na kumpa utukufu Baba yenu aliye mbinguni.”—Mathayo 5:16.

21 Katika ulimwengu huu wenye giza, watu wenye moyo mzuri wanavutwa kwenye nuru ya kiroho. Kwa hiyo, tunapoonyesha heshima katika familia, katika kutaniko, na kwa mamlaka za ulimwengu, tunaweza kuwavutia wengine na kuwachochea waanze kutembea pamoja nasi katika nuru. Hilo ni jambo zuri kama nini! Hata lisipotukia, tuna hakika ya jambo moja. Kuwaheshimu wanadamu kunampendeza Yehova Mungu na kunatusaidia kukaa katika upendo wake. Hakuna thawabu kubwa kuliko hiyo!

^ fu. 17 Nyongeza “Kufunika Kichwa—Wakati Gani na kwa Nini?” inazungumzia jinsi kanuni hiyo inavyoweza kutumiwa katika visa mbalimbali.