Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 17

“Kujijenga Wenyewe juu ya Imani Yenu Iliyo Takatifu Zaidi”

“Kujijenga Wenyewe juu ya Imani Yenu Iliyo Takatifu Zaidi”

“Kwa kujijenga wenyewe juu ya imani yenu iliyo takatifu zaidi, . . . jitunzeni katika upendo wa Mungu.”—YUDA 20, 21.

1, 2. Unahusika katika mradi gani wa ujenzi, na kwa nini ubora wa kazi yako ni muhimu?

KAZI ya ujenzi imepamba moto. Ujenzi huo umekuwa ukiendelea kwa muda fulani, nao utaendelea kwa muda mrefu. Ingawa kazi hiyo ni ngumu, inaridhisha. Hata iweje, umeazimia kutoiacha kamwe wala kulegeza mkono, kwa sababu maisha yako ya sasa na ya wakati ujao yanategemea ubora wa kazi yako. Kwa nini? Kwa sababu jengo lenyewe ni wewe!

2 Mwanafunzi Yuda alikazia kwamba tunapaswa kujijenga. Alipowahimiza Wakristo ‘wajitunze katika upendo wa Mungu,’ alitaja pia jambo kuu ambalo lingewasaidia kufanya hivyo, yaani, ‘kujijenga wenyewe juu ya imani yao iliyo takatifu zaidi.’ (Yuda 20, 21) Ni kwa njia gani unaweza kujijenga mwenyewe na kuimarisha imani yako ili ukae katika upendo wa Mungu? Acheni tuchunguze mambo matatu yanayohusika katika mradi wa kujijenga kiroho.

ENDELEA KUJENGA IMANI KATIKA MATAKWA YA UADILIFU YA YEHOVA

3-5. (a) Shetani angependa kukupotosha uwe na maoni gani kuhusu matakwa ya Yehova? (b) Tunapaswa kuwa na maoni gani kuhusu matakwa ya Mungu, nayo yanapaswa kutufanya tuhisi namna gani? Toa mfano.

3 Kwanza kabisa, tunahitaji kuimarisha imani yetu katika sheria ya Mungu. Kupitia kitabu hiki, umechunguza matakwa mengi ya uadilifu ya Yehova kuhusu mwenendo. Una maoni gani kuyahusu? Shetani angependa kukupotosha uone kwamba sheria, kanuni, na viwango vya Yehova vinabana sana au hata kukandamiza. Amekuwa akitumia mbinu hiyo tangu ilipofaulu katika Edeni. (Mwanzo 3:1-6) Je, atafaulu kukupotosha kwa kutumia mbinu hiyo? Mengi yatategemea mtazamo wako.

4 Kwa mfano: Unapotembea katika bustani maridadi, unaona ua mrefu na imara unaowazuia watu wasiingie katika sehemu fulani. Sehemu hiyo iliyozungukwa na ua inaonekana kuwa yenye kupendeza sana. Mwanzoni, huenda ukaona ua huo kuwa kizuizi kisichohitajika kinachokunyima uhuru. Lakini, unapochungulia ndani ya ua huo, unamwona simba mkali akiotea windo upande ule mwingine! Sasa unatambua kusudi la ua huo—ni ulinzi. Je, kuna mwindaji hatari anayekuotea sasa hivi? Neno la Mungu linaonya: “Tunzeni akili zenu, iweni wenye kulinda. Adui yenu, Ibilisi, anatembea huku na huku kama simba anayenguruma, akitafuta kummeza mtu.”—1 Petro 5:8.

5 Shetani ni mwindaji hatari. Kwa sababu Yehova hataki tuwe windo la Shetani, Ameweka sheria za kutulinda kutokana na “hila” nyingi za mwovu huyo. (Waefeso 6:11) Kwa hiyo, kila tunapotafakari sheria za Mungu, tunapaswa kuona kwamba zimewekwa kwa sababu Baba yetu wa mbinguni anatupenda. Tukiwa na maoni hayo, tutatambua kwamba sheria za Mungu zinatupa usalama na shangwe. Mwanafunzi Yakobo aliandika: “Yeye anayechunguza ndani ya sheria kamilifu iliyo ya uhuru na ambaye hudumu katika hiyo . . . atakuwa mwenye furaha katika kuitenda.”—Yakobo 1:25.

6. Ni njia gani iliyo bora ya kujenga imani katika sheria na kanuni za Mungu za uadilifu? Toa mfano.

6 Kufuata amri za Mungu ndiyo njia bora ya kujenga imani yetu katika Mpaji-sheria na katika hekima ya sheria zake. Kwa mfano, “sheria ya Kristo” inatia ndani amri ya Yesu ya kuwafundisha wengine ‘mambo yote ambayo ameamuru.’ (Wagalatia 6:2; Mathayo 28:19, 20) Wakristo pia huchukua kwa uzito agizo la kuendelea kukutana pamoja kwa ajili ya ibada na ushirika wenye kujenga. (Waebrania 10:24, 25) Amri za Mungu zinatia ndani pia himizo la kusali kwa Yehova kutoka moyoni, mara nyingi na kwa ukawaida. (Mathayo 6:5-8; 1 Wathesalonike 5:17) Tunapoishi kulingana na amri hizo, tunaona wazi zaidi kwamba zina mwongozo wenye upendo. Kuzitii hutupa uradhi na shangwe ambayo haipatikani mahali pengine popote katika ulimwengu huu wenye matatizo mengi. Unapotafakari jinsi ambavyo wewe binafsi umefaidika kwa kutii sheria za Mungu, je, si kweli kwamba imani yako katika sheria hizo imeimarika?

7, 8. Neno la Mungu huwapa uhakikisho gani wale wanaoona kwamba huenda wasiweze kuendelea kuwa waadilifu kadiri miaka inavyosonga?

7 Nyakati nyingine, watu fulani huwa na wasiwasi kwamba itakuwa vigumu sana kushikamana na sheria za Yehova kadiri miaka inavyosonga. Wanaogopa kwamba huenda watashindwa. Ukihisi hivyo wakati wowote, kumbuka maneno haya: “Mimi, Yehova, ni Mungu wako, Yeye anayekufundisha ili ujifaidi mwenyewe, Yeye anayekufanya uende katika njia unayopaswa kutembea ndani yake. Laiti ungesikiliza amri zangu! Ndipo amani yako ingekuwa kama mto, na uadilifu wako kama mawimbi ya bahari.” (Isaya 48:17, 18) Je, umewahi kutua na kufikiria jinsi ambavyo maneno hayo yanatia moyo?

8 Katika andiko hilo, Yehova anatukumbusha kwamba tunapata faida kwa kumtii. Anaahidi kutubariki kwa njia mbili ikiwa tutamtii. Kwanza, amani yetu itakuwa kama mto—tulivu, tele, na isiyokoma. Pili, uadilifu wetu utakuwa kama mawimbi ya bahari. Ukisimama ufuoni na kutazama mawimbi yakiinuka na kushuka, huna shaka lolote kwamba yatakuwako daima. Unajua kwamba mawimbi hayo yataendelea kuinuka na kushuka miaka nenda miaka rudi. Yehova anasema kwamba uadilifu wako, yaani, maisha yako ya kufanya yaliyo sawa, yanaweza kuwa hivyo. Ukiendelea kujitahidi kuwa mwaminifu kwake, hatakuacha kamwe! (Zaburi 55:22) Je, ahadi kama hizo zenye kuchangamsha moyo haziimarishi imani yako katika Yehova na katika matakwa yake ya uadilifu?

“TUSONGE MBELE KUELEKEA UKOMAVU”

9, 10. (a) Kwa nini ukomavu ni mradi mzuri kwa Wakristo? (b) Ni kwa njia gani mtazamo wa kiroho hutusaidia kuwa na furaha?

9 Jambo la pili linaloweza kukusaidia katika mradi wako wa ujenzi linatajwa katika maneno haya yaliyoongozwa na roho: “Na tusonge mbele kuelekea ukomavu.” (Waebrania 6:1) Ukomavu ni mradi mzuri kwa Mkristo. Tofauti na ukamilifu, ambao kwa sasa wanadamu hawawezi kuufikia, ukomavu ni mradi unaoweza kufikiwa. Pia, Wakristo hupata shangwe nyingi katika utumishi wa Yehova kadiri wanavyoendelea kukomaa. Kwa nini?

10 Mkristo mkomavu ni mtu wa kiroho. Anaona mambo jinsi Yehova anavyoyaona. (Yohana 4:23) Paulo aliandika: “Wale wanaopatana na mwili hukaza akili zao juu ya mambo ya mwili, lakini wale wanaopatana na roho juu ya mambo ya roho.” (Waroma 8:5) Mtazamo wa kimwili hutokeza furaha kidogo tu, kwa kuwa hukazia fikira mambo ya kibinafsi, ya wakati huu, na mambo ya kimwili. Mtazamo wa kiroho hutokeza furaha tele, kwa kuwa humkazia fikira Yehova, “Mungu mwenye furaha.” (1 Timotheo 1:11) Mtu wa kiroho hutaka sana kumpendeza Yehova, naye hushangilia hata anapojaribiwa. Kwa nini? Majaribu hutokeza nafasi za kumthibitisha Shetani kuwa mwongo na kujenga ushikamanifu, mambo yanayompendeza Baba yetu wa mbinguni.—Methali 27:11; Yakobo 1:2, 3.

11, 12. (a) Paulo alisema nini kuhusu ‘nguvu za ufahamu’ za Mkristo, nalo neno “zimezoezwa” linamaanisha nini? (b) Ni mazoezi gani ambayo mwili unahitaji ili kukomaa na kuwa na uzoefu?

11 Hali ya kiroho na ukomavu hutokana na mazoezi. Fikiria mstari huu: “Chakula kigumu ni cha watu wakomavu, cha wale ambao kwa kutumia, nguvu zao za ufahamu zimezoezwa kutofautisha yaliyo sawa na yaliyo makosa pia.” (Waebrania 5:14) Paulo aliposema kwamba nguvu za ufahamu “zimezoezwa,” alitumia neno la Kigiriki ambalo yaelekea lilitumika sanasana katika viwanja vya sarakasi vya karne ya kwanza nchini Ugiriki, kwa kuwa linaweza kutafsiriwa ‘zoezwa kama mwanasarakasi.’ Hebu fikiria mazoezi hayo yalitia ndani nini.

Mwanasarakasi huuzoeza mwili wake kwa kufanya mazoezi

12 Tulipozaliwa, miili yetu haikuwa imezoezwa. Kwa mfano, mtoto mchanga hatambui mahali mikono au miguu yake ilipo. Kwa hiyo, yeye hutupa-tupa mikono yake, na hata kujigonga-gonga kwenye uso, jambo ambalo linamuudhi na kumshangaza. Kadiri anavyotumia viungo vyake siku baada ya siku, ndivyo mwili wake unavyozoezwa. Mtoto huyo huanza kutambaa, kisha hutembea, na mwishowe hata anaweza kukimbia. * Lakini namna gani mwanasarakasi? Unapomwona mwanasarakasi akiruka na kujipinda hewani kwa njia yenye kupendeza na bila kukosea hata kidogo, huna shaka lolote kwamba mwili ni kama mashini iliyorekebishwa vizuri. Ustadi wa mwanasarakasi haukujitokeza wenyewe, bali ulitokana na kufanya mazoezi kwa saa nyingi sana. Biblia inasema kwamba mazoezi hayo ya mwili ni “yenye faida kidogo.” Basi, wazia jinsi tunavyoweza kupata faida nyingi kwa kuzoeza nguvu zetu za ufahamu wa kiroho!—1 Timotheo 4:8.

13. Tunaweza kuzoeza nguvu zetu za ufahamu jinsi gani?

13 Katika kitabu hiki, tumezungumzia mambo mengi yatakayokusaidia kuzoeza nguvu zako za ufahamu ili uendelee kuwa mwaminifu kwa Yehova ukiwa mtu wa kiroho. Fikiria kwa makini kanuni na sheria za Yehova na kusali kuzihusu unapofanya maamuzi kila siku maishani. Unapotaka kufanya uamuzi wowote, jiulize: ‘Ni sheria au kanuni gani za Biblia zinazohusika? Ninaweza kuzitumia kwa njia gani? Ni uamuzi gani utakaompendeza Baba yangu wa mbinguni?’ (Methali 3:5, 6; Yakobo 1:5) Kila uamuzi unaofanya kwa njia hiyo utakusaidia zaidi kuzoeza nguvu zako za ufahamu. Mazoezi hayo yatakusaidia kuwa mtu wa kiroho kikweli na kudumu ukiwa hivyo.

14. Ili tukue kiroho tunapaswa kusitawisha hamu gani, hata hivyo tunapaswa kuwa waangalifu kuhusu nini?

14 Ingawa mtu anaweza kufikia ukomavu, bado anahitaji kuendelea kukua kiroho. Ukuzi unategemea chakula. Hivyo, Paulo alisema: “Chakula kigumu ni cha watu wakomavu.” Ili kujenga imani yako unapaswa kuendelea kula chakula kigumu cha kiroho. Unapotumia yale ambayo unajifunza, hiyo ni hekima, nayo Biblia inasema: “Hekima ndilo jambo kuu.” Hivyo, tunahitaji kusitawisha hamu ya kutoka moyoni ya kujifunza kweli zenye thamani kutoka kwa Baba yetu. (Methali 4:5-7; 1 Petro 2:2) Bila shaka, kupata ujuzi na hekima kutoka kwa Mungu hakupaswi kutufanya tuwe na kiburi au wenye majivuno. Tunapaswa kujichunguza mara kwa mara ili kiburi au udhaifu mwingine wowote usitie mizizi na kuota katika moyo wetu. Paulo aliandika: “Endeleeni kujijaribu kama ninyi mko katika imani, endeleeni kuthibitisha ninyi wenyewe jinsi mlivyo.”—2 Wakorintho 13:5.

15. Kwa nini upendo ni muhimu ili kukua kiroho?

15 Hata baada ya ujenzi wa nyumba kukamilika, kazi inaendelea. Ni muhimu kutunza na kurekebisha nyumba hiyo, na huenda upanuzi ukahitajika kulingana na hali. Tunahitaji nini ili kukomaa na kuendelea kuwa watu wa kiroho? Jambo kuu zaidi ni upendo. Lazima upendo wetu kwa Yehova na kwa waamini wenzetu uendelee kukua. Ikiwa hatuna upendo, ujuzi wetu wote na mambo yote tunayofanya yatakuwa bure, naam, kama kelele zisizo na maana yoyote. (1 Wakorintho 13:1-3) Lakini tukiwa na upendo, tunaweza kufikia ukomavu wa Kikristo na kuendelea kukua kiroho.

KAZIA FIKIRA TUMAINI AMBALO YEHOVA ANATOA

16. Shetani huwachochea watu wawe na maoni gani, na Yehova ametupa kifaa gani kinachoweza kutulinda?

16 Acheni tuchunguze jambo lingine kuhusu mradi wako wa ujenzi. Ili kujijenga mwenyewe ukiwa mfuasi wa kweli wa Kristo, unahitaji kuwa mwangalifu kuhusu jinsi unavyofikiri. Shetani, ambaye ni mtawala wa ulimwengu huu, ni stadi wa kuwafanya watu kuwa na maoni yasiyofaa, watazamie mabaya, wawe na mashaka, na wakate tamaa. (Waefeso 2:2) Maoni kama hayo ni hatari kwa Mkristo kama vile mchwa walivyo hatari kwa nyumba ya mbao. Jambo la kupendeza ni kwamba Yehova anatupa kifaa muhimu kinachoweza kutulinda, yaani, tumaini.

17. Neno la Mungu linaonyeshaje umuhimu wa tumaini?

17 Biblia inataja mavazi ya silaha ya kiroho ambayo tunahitaji tunapopigana na Shetani na ulimwengu huu. Vazi moja muhimu ni kofia ya chuma, yaani, “tumaini la wokovu.” (1 Wathesalonike 5:8) Katika nyakati za Biblia, askari-jeshi alijua kwamba angekuwa hatarini ikiwa hangevaa kofia yake ya chuma. Kwa kuwa mara nyingi kofia hiyo ilikuwa ya chuma na upande wa ndani ilikuwa na kitambaa au ngozi, ilizuia kichwa kilipogongwa kisipatwe na madhara yoyote makubwa. Kama vile kofia ya chuma inavyolinda kichwa, tumaini linaweza kulinda akili, yaani, maoni yako.

18, 19. Yesu alituwekea mfano gani wa kuendelea kuwa na tumaini, nasi tunaweza kumwiga kwa njia gani?

18 Yesu aliweka mfano bora wa kuendelea kuwa na tumaini. Kumbuka mambo aliyovumilia usiku wa mwisho wa maisha yake hapa duniani. Rafiki yake wa karibu alilipwa ili amsaliti. Mwingine akamkana. Wengine wakamwacha na kukimbia. Watu wa nchi yake mwenyewe wakamkataa, na kudai auawe kwenye mti wa mateso mikononi mwa askari-jeshi wa Roma. Tunaweza kusema kwamba Yesu alipata majaribu makali kuliko majaribu yoyote tunayoweza kupata. Ni nini kilichomsaidia? Andiko la Waebrania 12:2 linajibu: “Kwa ajili ya shangwe iliyowekwa mbele yake, yeye alivumilia mti wa mateso, akaidharau aibu, naye ameketi kwenye mkono wa kuume wa kiti cha ufalme cha Mungu.” Yesu hakusahau hata kidogo “shangwe iliyowekwa mbele yake.”

19 Ni shangwe gani iliyowekwa mbele ya Yesu? Alijua kwamba uvumilivu wake ungesaidia kutakasa jina takatifu la Yehova. Angetoa uthibitisho mkubwa zaidi wa kwamba Shetani ni mwongo. Hakuna tumaini lingine lolote ambalo lingeweza kumpa Yesu shangwe kubwa kuliko hiyo! Pia, alijua kwamba Yehova angembariki sana kwa sababu ya uaminifu wake, na kwamba baada ya muda mfupi angepata pendeleo la kuungana tena na Baba yake. Nyakati zote zenye majaribu, Yesu alikazia fikira tumaini hilo lenye shangwe. Sisi pia tunapaswa kufanya vivyo hivyo. Tuna shangwe iliyowekwa mbele yetu. Yehova amempa kila mmoja wetu pendeleo la kusaidia kulitakasa jina lake tukufu. Tunaweza kumthibitisha Shetani kuwa mwongo kwa kumtambua Yehova kuwa Mwenye Enzi Kuu na kujitunza wenyewe tukiwa salama salimini katika upendo wa Baba yetu, hata tukikabili majaribu na vishawishi vya namna gani.

20. Ni nini kinachoweza kukusaidia kuendelea kuwa na tumaini na kuwa na maoni yanayofaa?

20 Zaidi ya kuahidi kwamba atawapa watumishi wake waaminifu thawabu, Yehova ana hamu kubwa sana ya kufanya hivyo. (Isaya 30:18; Malaki 3:10) Anafurahi kuwatimizia watumishi wake maombi yanayofaa ya mioyo yao. (Zaburi 37:4) Kwa hiyo, kaza fikira zako kwenye tumaini lililo mbele yako. Usishindwe kamwe na maoni yasiyofaa, yaliyopotoka, na yaliyo kombo ya ulimwengu huu mbovu wa Shetani. Ukiona kwamba roho ya ulimwengu huu inapenya katika akili na moyo wako, mwombe Yehova kwa bidii akupe “amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote.” Amani hiyo itaulinda moyo wako na nguvu zako za akili.—Wafilipi 4:6, 7.

21, 22. (a) “Umati mkubwa” una tumaini gani tukufu? (b) Ni jambo gani katika tumaini la Kikristo linalokuchochea zaidi, nawe umeazimia kufanya nini?

21 Una tumaini zuri kama nini unaloweza kutafakari! Ikiwa wewe ni sehemu ya “umati mkubwa” ambao ‘watatoka katika ile dhiki kuu,’ wazia maisha yanayokungojea hivi punde. (Ufunuo 7:9, 14) Baada ya Shetani na roho wake waovu kuondolewa, utapata burudisho ambalo huenda usiweze kulielewa kwa sasa. Ndiyo, ni nani kati yetu ambaye amewahi kuishi pasipo uvutano wenye kupotosha wa Shetani? Baada ya uvutano huo kuondolewa, kutakuwa na shangwe kama nini kushiriki katika kazi ya kuifanya dunia kuwa paradiso chini ya mwelekezo wa Yesu na wale 144,000 watakaotawala pamoja naye mbinguni! Tunasisimuliwa kama nini na tazamio la kuishi wakati ambapo hakutakuwa na magonjwa na udhaifu wowote, tutakapowakaribisha wapendwa wetu kutoka kaburini, na kuishi jinsi Mungu alivyokusudia tuishi! Tunapozidi kufikia ukamilifu, thawabu kubwa hata zaidi itakuwa ikikaribia, ile ahadi inayotajwa kwenye Waroma 8:21—“uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.”

22 Yehova anataka upate uhuru usio na kifani ambao hata huwezi kuuwazia. Njia ya kupata uhuru huo si nyingine ila kutii. Je, huoni kwamba yakupasa kufanya yote uwezayo sasa kumtii Yehova siku baada ya siku? Hivyo basi, endelea kujijenga mwenyewe juu ya imani yako iliyo takatifu zaidi, ili uendelee kukaa katika upendo wa Mungu milele na milele!

^ fu. 12 Wanasayansi wanasema kwamba sisi husitawisha uwezo wa kutambua mahali mwili wetu ulipo na mahali miguu na mikono yetu ilipo. Kwa mfano, uwezo huo hukuwezesha kupiga makofi ukiwa umefunga macho. Mgonjwa mmoja aliyepoteza uwezo huo alishindwa kusimama, kutembea, au hata kuketi.