Yohana 21:1-25
21 Baada ya mambo haya Yesu alijifunua tena kwa wanafunzi kwenye bahari ya Tiberia; lakini alijifunua hivi.
2 Waliokuwa pamoja ni Simoni Petro na Tomasi, aliyeitwa Pacha,+ na Nathanaeli+ kutoka Kana ya Galilaya na wana wa Zebedayo+ na wengine wawili kati ya wanafunzi wake.
3 Simoni Petro akawaambia: “Ninaenda kuvua samaki.” Wakamwambia: “Sisi pia tutakwenda pamoja nawe.” Wakatoka kwenda, wakapanda ndani ya mashua, lakini usiku huo hawakuvua kitu.+
4 Hata hivyo, ilipokuwa tu inakaribia kuwa asubuhi, Yesu akasimama pwani, lakini wanafunzi, bila shaka, hawakufahamu kwamba ni Yesu.+
5 Basi Yesu akawaambia: “Watoto, je, mna chakula chochote?” Wakamjibu: “Hapana!”
6 Akawaambia: “Utupeni wavu upande wa kuume wa mashua, nanyi mtapata.”+ Basi wakautupa, lakini hawakuweza tena kuuvuta ndani kwa sababu samaki walikuwa wengi sana.+
7 Kwa hiyo mwanafunzi ambaye Yesu alikuwa akimpenda,+ akamwambia Petro:+ “Ni Bwana!” Kwa hiyo Simoni Petro, aliposikia kwamba ni Bwana, akajifunga mwenyewe kwa kujizungushia kiunoni vazi lake la juu, kwa maana alikuwa uchi, akajitumbukiza ndani ya bahari.
8 Lakini wale wanafunzi wengine wakaja katika ile mashua ndogo, kwa maana hawakuwa mbali na nchi kavu, karibu umbali wa meta 90 tu, wakiukokota wavu wenye samaki wengi.
9 Hata hivyo, waliposhuka kwenye nchi kavu wakaona moto wa makaa+ na samaki juu yake na mkate.
10 Yesu akawaambia: “Leteni baadhi ya samaki mliowavua sasa hivi.”
11 Kwa hiyo, Simoni Petro akapanda ndani na kuuvuta wavu kwenye nchi kavu ukiwa umejaa samaki wakubwa 153. Lakini ijapokuwa kulikuwako wengi sana wavu haukupasuka.
12 Yesu akawaambia: “Njooni, mpate kiamsha-kinywa chenu.”+ Hakuna hata mmoja wa wanafunzi aliyekuwa na moyo wa kumuuliza: “Wewe ni nani?” kwa sababu walijua ni Bwana.
13 Yesu akaja, akachukua mkate na kuwapa,+ na samaki vivyo hivyo.
14 Sasa hii ilikuwa ni mara ya tatu+ ambayo Yesu aliwatokea wanafunzi baada ya kufufuliwa kwake kutoka kwa wafu.
15 Basi, walipokuwa wamepata kiamsha-kinywa, Yesu akamwambia Simoni Petro: “Simoni mwana wa Yohana, je, unanipenda kuliko hawa?”+ Akamwambia: “Ndiyo, Bwana, unajua ninakupenda.”+ Akamwambia: “Lisha wana-kondoo wangu.”+
16 Tena akamwambia, mara ya pili: “Simoni mwana wa Yohana, je, unanipenda?”+ Akamwambia: “Ndiyo, Bwana, unajua ninakupenda.” Akamwambia: “Chunga kondoo wangu wadogo.”+
17 Akamwambia mara ya tatu: “Simoni mwana wa Yohana, je, unanipenda?” Petro akahuzunika kwamba alimwambia mara ya tatu: “Je, unanipenda?” Kwa hiyo akamwambia: “Bwana, wewe unajua mambo yote;+ unajua kwamba ninakupenda.” Yesu akamwambia: “Lisha kondoo wangu wadogo.+
18 Kwa kweli kabisa ninakuambia, Ulipokuwa kijana, ulikuwa ukijifunga kiuno na kutembea huku na huku kokote ulikotaka. Lakini utakapozeeka utanyoosha mikono yako na mtu mwingine atakufunga kiuno+ na kukupeleka usikotaka wewe.”+
19 Hilo alisema ili kutoa ishara ni kwa kifo+ cha namna gani yeye angemtukuza Mungu.+ Kwa hiyo, alipokuwa amesema hayo, akamwambia: “Endelea kunifuata.”+
20 Petro alipogeuka, alimwona mwanafunzi ambaye Yesu alikuwa akimpenda,+ akifuata, yule ambaye kwenye mlo wa jioni alikuwa pia ameegemea nyuma kifuani pake akasema: “Bwana, ni nani anayekusaliti?”
21 Basi, alipomwona, Petro akamwambia Yesu: “Bwana, mtu huyu atafanya nini?”
22 Yesu akamwambia: “Ikiwa ni mapenzi yangu akae mpaka nije,+ hilo linakuhusu nini wewe? Wewe endelea kunifuata mimi.”
23 Kwa sababu hiyo, maneno hayo yakaenea kati ya akina ndugu, kwamba mwanafunzi huyo hangekufa. Hata hivyo, Yesu hakumwambia kwamba hangekufa, bali: “Ikiwa ni mapenzi yangu akae+ mpaka nije, hilo linakuhusu nini wewe?”
24 Huyo ndiye mwanafunzi+ ambaye anatoa ushahidi juu ya mambo haya na ambaye aliyaandika mambo haya, na sisi tunajua kwamba ushahidi anaotoa ni wa kweli.+
25 Kwa kweli, kuna mambo mengine mengi pia aliyofanya Yesu, ambayo, kama yangeandikwa kirefu, nadhani ulimwengu wenyewe haungeweza kuwa na nafasi ya kuviweka vitabu vya kukunjwa ambavyo vingeandikwa.+