Yohana 13:1-38
13 Sasa, kwa sababu alijua kabla ya sherehe ya pasaka kwamba saa yake ya kutoka katika ulimwengu huu kwenda kwa Baba ilikuwa imefika,+ Yesu, akiwa amewapenda walio wake mwenyewe waliokuwa ulimwenguni,+ akawapenda mpaka mwisho.
2 Kwa hiyo, mlo wa jioni ulipokuwa ukiendelea, Ibilisi akiwa tayari ameweka ndani ya moyo wa Yuda Iskariote,+ mwana wa Simoni, amsaliti,+
3 yeye, akijua kwamba Baba alikuwa ametia vitu vyote mikononi mwake+ na kwamba alikuja kutoka kwa Mungu na alikuwa akienda kwa Mungu,+
4 alisimama kutoka kwenye mlo wa jioni na kuyaweka kando mavazi yake ya nje. Naye akachukua kitambaa, akajifunga kiunoni.+
5 Kisha akatia maji ndani ya beseni akaanza kuiosha miguu+ ya wanafunzi na kuikausha kwa kitambaa ambacho alikuwa amejifunga kiunoni.
6 Na kwa hiyo akafika kwa Simoni Petro. Huyo akamwambia: “Bwana, je, unaosha miguu yangu?”+
7 Yesu akajibu, akamwambia: “Ninalofanya huelewi sasa, bali utaelewa baada ya mambo haya.”+
8 Petro akamwambia: “Hutaosha kamwe miguu yangu.” Yesu akamjibu: “Nisipokuosha,+ wewe huna sehemu pamoja na mimi.”
9 Simoni Petro akamwambia: “Bwana, si miguu yangu tu, bali pia mikono yangu na kichwa changu.”
10 Yesu akamwambia: “Yule ambaye ameoga+ hahitaji kuoshwa zaidi ya miguu yake, bali yuko safi mwili wote. Nanyi mko safi, lakini si ninyi nyote.”
11 Kwa kweli, alimjua mtu anayemsaliti.+ Ndiyo sababu alisema: “Si wote kati yenu walio safi.”
12 Basi, alipokuwa ameosha miguu yao na kuvaa mavazi yake ya nje, akaketi mezani tena, akawaambia: “Je, mnajua jambo ambalo nimewafanyia ninyi?
13 Ninyi huniita, ‘Mwalimu,’+ na, ‘Bwana,’+ nanyi mnasema sawasawa, kwa maana ndivyo nilivyo.+
14 Kwa hiyo, ikiwa mimi, nijapokuwa Bwana na Mwalimu, niliiosha miguu yenu,+ ninyi pia mnapaswa kuoshana miguu.+
15 Kwa maana niliweka kielelezo kwa ajili yenu, ili, kama vile nilivyowafanyia ninyi, ninyi pia mfanye hivyo.+
16 Kwa kweli kabisa ninawaambia ninyi, Mtumwa si mkuu kuliko bwana wake, wala yule aliyetumwa si mkuu kuliko yule aliyemtuma.+
17 Ikiwa mnajua mambo haya, wenye furaha ni ninyi ikiwa mnayatenda.+
18 Mimi sisemi juu yenu nyote; ninawajua wale ambao nimewachagua.+ Lakini ni ili Andiko lipate kutimizwa,+ ‘Yule aliyekuwa akila mkate wangu amekiinua kisigino chake dhidi yangu.’+
19 Kuanzia dakika hii na kuendelea ninawaambia ninyi kabla ya hilo kutukia,+ ili litakapotukia mwamini kwamba mimi ndiye.
20 Kwa kweli kabisa ninawaambia, Yule anayempokea yeyote ninayemtuma hunipokea mimi pia.+ Naye anayenipokea mimi, humpokea pia yule aliyenituma.”+
21 Baada ya kusema hayo, Yesu akataabika rohoni, naye akatoa ushahidi na kusema: “Kwa kweli kabisa ninawaambia ninyi, Mmoja wenu atanisaliti.”+
22 Wanafunzi wakaanza kutazamana, wasijue kabisa alikuwa akisema hilo kuhusu nani.+
23 Mmoja wa wanafunzi wake alikuwa ameegama kifuani pa Yesu, naye Yesu alimpenda.+
24 Kwa hiyo Simoni Petro akamtolea huyo ishara ya kichwa na kumwambia: “Muulize anasema hilo kuhusu nani.”
25 Kwa hiyo huyo wa mwisho akaegemea nyuma kifuani pa Yesu na kumwambia: “Bwana, ni nani?”+
26 Kwa hiyo Yesu akajibu: “Ni yule ambaye nitampa tonge ambalo ninachovya.”+ Na kwa hiyo, akiisha kuchovya tonge, akalichukua na kumpa Yuda, mwana wa Simoni Iskariote.
27 Na baada ya hilo tonge ndipo Shetani akaingia ndani ya huyo.+ Kwa hiyo, Yesu akamwambia: “Lile unalofanya lifanye upesi zaidi.”
28 Hata hivyo, hakuna hata mmoja kati ya wale waliokuwa wameketi mezani aliyejua amemwambia hili kwa nini.
29 Kwa kweli, baadhi yao walikuwa wakifikiri, kwa kuwa Yuda alikuwa akilishika sanduku la pesa,+ kwamba Yesu alikuwa akimwambia: “Nunua vitu ambavyo tunahitaji kwa ajili ya sherehe,” au kwamba awape maskini kitu fulani.+
30 Kwa hiyo, baada ya yeye kulipokea tonge, akatoka nje mara moja, akaenda. Na wakati huo ulikuwa usiku.+
31 Kwa hiyo alipokuwa ameenda, Yesu akasema: “Sasa Mwana wa binadamu ametukuzwa,+ na Mungu ametukuzwa kuhusiana na yeye.
32 Na Mungu mwenyewe atamtukuza,+ naye atamtukuza mara moja.
33 Watoto wadogo,+ nipo pamoja nanyi muda kidogo zaidi. Ninyi mtanitafuta; na kama vile nilivyowaambia Wayahudi, ‘Ninakoenda ninyi hamwezi kuja,’+ ninawaambia ninyi pia sasa.
34 Ninawapa ninyi amri mpya, kwamba mpendane; kama vile ambavyo nimewapenda ninyi,+ ninyi nanyi mpendane vivyo hivyo.+
35 Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo kati yenu wenyewe.”+
36 Simoni Petro akamwambia: “Bwana, unaenda wapi?” Yesu akajibu: “Ninakoenda huwezi kunifuata sasa, lakini utanifuata baadaye.”+
37 Petro akamwambia: “Bwana, kwa nini siwezi kukufuata sasa? Nitatoa nafsi yangu kwa ajili yako.”+
38 Yesu akajibu: “Je, utaitoa nafsi yako kwa ajili yangu? Kwa kweli kabisa ninakuambia, Jogoo hatawika mpaka uwe umenikana mara tatu.”+