Yohana 7:1-53

7  Basi baada ya mambo hayo Yesu akaendelea kutembea katika Galilaya, kwa maana hakutaka kutembea katika Yudea, kwa sababu Wayahudi walikuwa wakitafuta kumuua.+  Hata hivyo, sherehe ya Wayahudi, ile sherehe ya vibanda,+ ilikuwa karibu.  Kwa hiyo ndugu+ zake wakamwambia: “Ondoka hapa uende Yudea, ili wanafunzi wako pia wapate kuona kazi unazofanya.  Kwa maana hakuna mtu anayefanya jambo lolote katika siri huku yeye mwenyewe akitafuta kujulikana hadharani. Ikiwa unafanya mambo hayo, jionyeshe mwenyewe kwa ulimwengu.”  Kwa kweli, ndugu+ zake walikuwa hawamwamini.+  Kwa hiyo Yesu akawaambia: “Wakati wangu unaofaa haujafika bado,+ lakini wakati wenu unaofaa upo sikuzote.  Ulimwengu hauna sababu ya kuwachukia ninyi, lakini huo unanichukia mimi, kwa sababu ninatoa ushahidi juu yake kwamba kazi zake ni mbovu.+  Pandeni mwende kwenye sherehe; mimi bado sipandi kwenda kwenye sherehe hiyo, kwa sababu wakati wangu unaofaa+ bado haujafika kikamili.”+  Kwa hiyo baada ya kuwaambia mambo haya, akabaki Galilaya. 10  Lakini ndugu zake walipokuwa wamepanda kwenda kwenye sherehe, yeye mwenyewe pia akapanda kwenda, si waziwazi bali kama katika siri.+ 11  Kwa hiyo Wayahudi wakaanza kumtafuta+ kwenye sherehe na kusema: “Yuko wapi yule mtu?” 12  Na umati ulikuwa ukinong’onezana mambo mengi juu yake.+ Baadhi yao wakawa wakisema: “Yeye ni mtu mwema.” Wengine wakawa wakisema: “Sivyo, bali yeye anaupotosha umati.” 13  Bila shaka, hakuna aliyekuwa akisema juu yake hadharani kwa sababu ya kuwaogopa Wayahudi.+ 14  Kufikia sasa sherehe ilipokuwa imefika katikati, Yesu akapanda kuingia hekaluni na kuanza kufundisha.+ 15  Kwa hiyo Wayahudi wakaanza kustaajabu, wakisema: “Mtu huyu amepataje ujuzi wa maandishi,+ na yeye hajajifunza shuleni?”+ 16  Yesu naye akawajibu na kusema: “Yale ninayofundisha si yangu, bali ni yake yeye aliyenituma.+ 17  Ikiwa yeyote anatamani kufanya mapenzi Yake, atajua kama fundisho hilo limetoka kwa Mungu+ au kama ninasema mambo ambayo nimetunga mimi mwenyewe. 18  Yule ambaye husema mambo aliyotunga yeye mwenyewe anatafuta utukufu wake mwenyewe; bali yule anayetafuta utukufu+ wake aliyemtuma, huyo ni wa kweli, na hakuna ukosefu wa uadilifu ndani yake. 19  Musa aliwapa ninyi Sheria,+ sivyo? Lakini hakuna hata mmoja kati yenu anayetii Sheria. Kwa nini mnatafuta kuniua?”+ 20  Umati wakajibu: “Wewe una roho mwovu.+ Ni nani anayetaka kukuua?” 21  Yesu akajibu, akawaambia: “Nilifanya tendo moja,+ nanyi nyote mnastaajabu. 22  Kwa sababu hiyo Musa amewapa tohara+​—⁠si kwamba inatoka kwa Musa, bali kwamba inatoka kwa mababu+⁠—​nanyi mnatahiri mtu siku ya sabato. 23  Ikiwa mtu anatahiriwa siku ya sabato ili sheria ya Musa isivunjwe, je, mnanikasirikia kwa sababu nilimfanya mtu awe na afya nzuri siku ya sabato?+ 24  Acheni kuhukumu kwa sura ya nje, bali hukumuni kwa hukumu ya uadilifu.”+ 25  Kwa hiyo baadhi ya wakaaji wa Yerusalemu wakaanza kusema: “Huyu ndiye mtu ambaye wanatafuta kumuua,+ sivyo? 26  Na bado, oneni! anasema hadharani,+ nao hawamwambii jambo lolote. Je, watawala wanajua kwa hakika kwamba huyu ndiye Kristo?+ 27  Badala yake, sisi tunajua mtu huyu ametoka wapi;+ lakini Kristo atakapokuja, hakuna atakayejua ametoka wapi.”+ 28  Kwa hiyo Yesu akapaaza sauti alipokuwa akifundisha katika hekalu na kusema: “Ninyi mnanijua tena mnajua nimetoka wapi.+ Pia, sikuja kwa uamuzi wangu mwenyewe,+ lakini yule aliyenituma ni halisi,+ nanyi hammjui.+ 29  Mimi ninamjua,+ kwa sababu mimi ni mwakilishi kutoka kwake, na Yeye alinituma.”+ 30  Kwa hiyo wakaanza kutafuta kumkamata,+ lakini hakuna aliyemkamata, kwa sababu saa+ yake ilikuwa haijafika bado. 31  Bado, wengi kati ya umati walimwamini;+ nao wakaanza kusema: “Kristo atakapofika, je, atafanya ishara+ zaidi ya zile ambazo mtu huyu amefanya?” 32  Mafarisayo walisikia umati wakinong’onezana mambo hayo juu yake, nao wakuu wa makuhani na Mafarisayo wakatuma maofisa wamkamate.+ 33  Kwa hiyo Yesu akasema: “Nitaendelea kuwa pamoja nanyi muda kidogo zaidi kabla ya kwenda kwake aliyenituma.+ 34  Mtanitafuta, lakini hamtanipata,+ na mahali nilipo hamwezi kuja.”+ 35  Kwa hiyo Wayahudi wakasema kati yao wenyewe: “Mtu huyu anakusudia kwenda wapi, hata kwamba hatutampata? Je, anakusudia kwenda kwa Wayahudi waliotawanyika+ katikati ya Wagiriki na kuwafundisha Wagiriki? 36  Yanamaanisha nini maneno hayo aliyosema kwamba, ‘Mtanitafuta, lakini hamtanipata, na mahali nilipo hamwezi kuja’?” 37  Basi siku ya mwisho, ile siku kuu ya sherehe,+ Yesu alikuwa amesimama, naye akapaaza sauti, akisema: “Ikiwa yeyote ana kiu,+ acheni aje kwangu na kunywa. 38  Yule ambaye ananiamini,+ kama vile Andiko lilivyosema, ‘Vijito vya maji yaliyo hai vitatiririka kutoka katika sehemu yake ya ndani kabisa.’ ”+ 39  Hata hivyo, alisema hilo kuhusu ile roho ambayo wale waliomwamini wangepokea hivi karibuni; kwa maana kufikia wakati huo roho+ haikuwapo, kwa sababu Yesu hakuwa ametukuzwa+ bado. 40  Kwa hiyo baadhi ya umati ambao walisikia maneno hayo wakaanza kusema: “Kwa hakika huyu ni Yule Nabii.”+ 41  Wengine walikuwa wakisema: “Huyu ndiye Kristo.”+ Lakini wengine walikuwa wakisema: “Je, kwa hakika Kristo+ atakuja kutoka Galilaya?+ 42  Je, Andiko halijasema kwamba Kristo anakuja kutoka kwa uzao wa Daudi,+ na kutoka Bethlehemu+ kijiji ambako Daudi alikaa?”+ 43  Kwa hiyo mgawanyiko juu yake ukatokea kati ya umati.+ 44  Ingawa hivyo, baadhi yao walikuwa wakitafuta kumkamata, lakini hakuna aliyemkamata. 45  Kwa hiyo maofisa wakarudi kwa wakuu wa makuhani na Mafarisayo, na Mafarisayo wakawaambia: “Kwa nini hamkumleta?” 46  Wale maofisa wakajibu: “Mtu mwingine hajapata kamwe kusema kama huyu.”+ 47  Nao Mafarisayo wakajibu: “Je, ninyi pia mmepotoshwa? 48  Je, kuna hata mmoja wa watawala au wa Mafarisayo ambaye amemwamini?+ 49  Lakini umati huu usiojua Sheria ni watu waliolaaniwa.”+ 50  Nikodemo, aliyekuwa amemwendea hapo kwanza, na aliyekuwa mmoja wao, akawaambia: 51  “Je, sheria yetu humhukumu mtu isipokuwa kwanza iwe imesikia+ kutoka kwake na kujua analofanya?” 52  Wakajibu, wakamwambia: “Je, wewe pia umetoka Galilaya? Chunguza uone kwamba hakuna nabii+ atakayeinuliwa kutoka Galilaya.”* Hati Codex Sinaiticus, Codex Vaticanus, na Sinaitic Syriac codex huondoa mstari wa 53 mpaka sura ya 8, mstari wa 11, ambao husomwa (kukiwa na tofauti fulani-fulani katika maandishi mbalimbali na tafsiri za Kigiriki) kama ifuatavyo: 53  Kwa hiyo wakaenda kila mmoja nyumbani kwake.

Maelezo ya Chini