Yohana 18:1-40
18 Akiisha kusema mambo hayo, Yesu akaenda pamoja na wanafunzi wake ng’ambo ya mto wa majira ya baridi kali wa Kidroni+ mpaka mahali palipokuwa na bustani, na yeye na wanafunzi wake wakaingia ndani yake.+
2 Basi Yuda pia, msaliti wake, alipajua mahali hapo, kwa sababu nyakati nyingi Yesu alikuwa amekutana hapo pamoja na wanafunzi wake.+
3 Kwa hiyo Yuda akachukua kikosi cha askari-jeshi na maofisa wa wakuu wa makuhani na wa Mafarisayo nao wakaja hapo wakiwa na mienge na taa na silaha.+
4 Kwa hiyo, Yesu akijua mambo yote ambayo yangempata,+ akatoka na kuwaambia: “Mnamtafuta nani?”
5 Wakamjibu: “Yesu Mnazareti.”+ Akawaambia: “Mimi ndiye.” Basi Yuda, msaliti+ wake, alikuwa pia amesimama pamoja nao.
6 Hata hivyo, alipowaambia: “Mimi ndiye,” wakarudi nyuma+ na kuanguka chini.
7 Kwa hiyo akawauliza tena: “Mnamtafuta nani?” Wakasema: “Yesu Mnazareti.”
8 Yesu akajibu: “Niliwaambia mimi ndiye. Kwa hiyo, ikiwa ni mimi mnayetafuta, acheni hawa waende”;
9 ili neno lipate kutimizwa ambalo yeye alisema: “Kati ya wale ambao umenipa sikumpoteza hata mmoja.”+
10 Ndipo Simoni Petro, kwa kuwa alikuwa na upanga, akauchomoa na kumpiga mtumwa wa kuhani mkuu, akalikata sikio lake la kuume.+ Jina la mtumwa huyo lilikuwa Malko.
11 Hata hivyo, Yesu akamwambia Petro: “Tia upanga ndani ya ala yake.+ Kikombe ambacho Baba amenipa, je, sipaswi kukinywa?”+
12 Basi kikosi cha askari-jeshi na kiongozi wa kijeshi na maofisa wa Wayahudi wakamkamata Yesu na kumfunga,
13 nao wakampeleka kwanza kwa Anasi; kwa maana alikuwa baba-mkwe wa Kayafa, ambaye alikuwa kuhani mkuu mwaka huo.+
14 Kwa kweli, Kayafa ndiye aliyewashauri Wayahudi kwamba ilikuwa kwa faida yao mtu mmoja afe kwa ajili ya watu.+
15 Sasa Simoni Petro na vilevile mwanafunzi mwingine alikuwa akimfuata Yesu.+ Mwanafunzi huyo alijulikana na kuhani mkuu, naye akaingia pamoja na Yesu ndani ya ua wa kuhani mkuu,
16 lakini Petro alikuwa amesimama nje kwenye mlango.+ Kwa hiyo yule mwanafunzi mwingine, ambaye alijulikana na kuhani mkuu, akatoka nje na kusema na mtunza-mlango, akamwingiza Petro ndani.
17 Basi kijakazi, aliye mtunza-mlango, akamwambia Petro: “Wewe pia ni mmoja wa wanafunzi wa mtu huyu, sivyo?” Akasema: “Hapana.”+
18 Sasa wale watumwa na maofisa walikuwa wamesimama huku na huku, kwa kuwa walikuwa wamewasha moto wa makaa,+ kwa sababu kulikuwa na baridi, nao walikuwa wakiota moto. Petro pia alikuwa amesimama pamoja nao akiota moto.
19 Na kwa hiyo mkuu wa makuhani akamuuliza Yesu juu ya wanafunzi wake na juu ya fundisho lake.
20 Yesu akamjibu: “Nimesema na ulimwengu hadharani. Sikuzote nilifundisha katika sinagogi na katika hekalu,+ ambapo Wayahudi wote hukusanyika; nami sikusema jambo lolote katika siri.
21 Kwa nini unaniuliza? Waulize wale ambao wamesikia lile nililowaambia. Ona! Hawa wanajua lile nililosema.”
22 Baada ya kusema mambo hayo, mmoja wa maofisa aliyekuwa amesimama kando akampiga Yesu kofi+ usoni na kusema: “Je, hivyo ndivyo unavyomjibu mkuu wa makuhani?”
23 Yesu akamjibu: “Ikiwa nimesema vibaya, toa ushahidi kuhusu ubaya wenyewe; lakini ikiwa nimesema sawasawa, kwa nini unanipiga?”
24 Basi Anasi akaagiza apelekwe kwa Kayafa kuhani mkuu+ akiwa amefungwa.
25 Sasa Simoni Petro alikuwa amesimama akiota moto. Ndipo wakamwambia: “Wewe pia ni mmoja wa wanafunzi wake, sivyo?” Akakana na kusema: “Hapana.”+
26 Mmoja wa watumwa wa kuhani mkuu, akiwa ni jamaa ya mtu ambaye Petro alikata sikio lake,+ akasema: “Mimi nilikuona katika bustani pamoja naye, sivyo?”
27 Hata hivyo, Petro akakana tena; na mara jogoo akawika.+
28 Basi wakampeleka Yesu kutoka kwa Kayafa mpaka kwenye jumba la gavana.+ Sasa ilikuwa asubuhi. Lakini wao wenyewe hawakuingia ndani ya jumba la gavana, ili wasipate kutiwa unajisi+ bali wapate kula pasaka.
29 Kwa hiyo Pilato akawajia nje na kusema: “Ni shtaka gani ambalo mnaleta juu ya mtu huyu?”+
30 Wakamwambia: “Kama mtu huyu hangekuwa mkosaji, hatungemtia mkononi mwako.”
31 Kwa sababu hiyo Pilato akawaambia: “Mchukueni ninyi wenyewe na kumhukumu kulingana na sheria yenu.”+ Wayahudi wakamwambia: “Si halali kwetu kumuua mtu yeyote.”+
32 Kusudi neno la Yesu litimizwe alilosema ili kutoa ishara ni kifo cha namna gani ambacho angekufa.+
33 Kwa hiyo Pilato akaingia tena ndani ya jumba la gavana naye akamwita Yesu na kumwambia: “Je, wewe ndiye mfalme wa Wayahudi?”+
34 Yesu akajibu: “Je, jambo unalosema umejitungia mwenyewe, au wengine walikuambia juu yangu?”+
35 Pilato akajibu: “Je, mimi ni Myahudi? Taifa lako mwenyewe na wakuu wa makuhani walikutia mikononi mwangu.+ Ulifanya nini?”
36 Yesu akajibu:+ “Ufalme wangu si sehemu ya ulimwengu huu.+ Kama ufalme wangu ungekuwa sehemu ya ulimwengu huu, watumishi wangu wangepigana+ ili nisitiwe mikononi mwa Wayahudi. Lakini, kama ilivyo, ufalme wangu hautoki katika chanzo hiki.”
37 Kwa hiyo Pilato akamwambia: “Kwa hiyo, basi, je, wewe ni mfalme?” Yesu akajibu: “Wewe mwenyewe unasema kwamba mimi ni mfalme.+ Kwa ajili ya hili mimi nimezaliwa, na kwa ajili ya hili nimekuja ulimwenguni, ili nitoe ushahidi juu ya ile kweli.+ Kila mtu aliye upande wa ile kweli+ huisikiliza sauti yangu.”+
38 Pilato akamwambia: “Kweli ni nini?”
Na baada ya kusema hili, akatoka tena kwenda kwa Wayahudi na kuwaambia: “Mimi sioni kosa lolote ndani yake.+
39 Zaidi ya hayo, ninyi mna desturi kwamba niwafungulie mtu kwenye pasaka.+ Kwa hiyo, je, mnataka niwafungulie mfalme wa Wayahudi?”
40 Basi wakapaaza sauti tena, wakisema: “Si mtu huyu, bali Baraba!” Basi Baraba alikuwa mnyang’anyi.+