Yohana 19:1-42
19 Kwa hiyo, wakati huo Pilato akamchukua Yesu na kumpiga mijeledi.+
2 Nao askari-jeshi wakasokota taji la miiba na kuliweka juu ya kichwa chake nao wakampamba kwa vazi la nje la zambarau;+
3 nao wakaanza kumjia na kusema: “Siku njema, ewe Mfalme wa Wayahudi!” Pia wakawa wakimpiga makofi usoni.+
4 Naye Pilato akaenda nje tena na kuwaambia: “Oneni! Namleta nje kwenu kusudi mjue kwamba sioni kosa lolote ndani yake.”+
5 Basi Yesu akaja nje, akiwa amevaa taji lenye miiba na vazi la nje la zambarau. Naye akawaambia: “Tazameni! Mwanamume!”
6 Hata hivyo, wakuu wa makuhani na maofisa walipomwona, wakapaaza sauti, wakisema: “Mtundike mtini! Mtundike mtini!”+ Pilato akawaambia: “Mchukueni ninyi wenyewe mkamtundike mtini, kwa maana mimi sioni kosa lolote ndani yake.”+
7 Wayahudi wakamjibu: “Sisi tuna sheria,+ na kulingana na sheria anapaswa kufa, kwa sababu alijifanya mwenyewe kuwa mwana wa Mungu.”+
8 Kwa hiyo, Pilato aliposikia maneno hayo, akaogopa zaidi;
9 naye akaingia ndani ya jumba la gavana tena na kumwambia Yesu: “Wewe ni mtu wa kutoka wapi?” Lakini Yesu hakumjibu.+
10 Kwa sababu hiyo Pilato akamwambia: “Je, husemi nami?+ Je, hujui nina mamlaka ya kukufungua na nina mamlaka ya kukutundika mtini?”
11 Yesu akamjibu: “Wewe hungekuwa na mamlaka hata kidogo juu yangu kama usingepewa kutoka juu.+ Ndiyo sababu mtu aliyenitia mikononi mwako ana dhambi kubwa zaidi.”
12 Kwa sababu hii Pilato akazidi kutafuta jinsi ya kumfungua. Lakini Wayahudi wakapaaza sauti, wakisema: “Ukimfungua mtu huyu, wewe si rafiki ya Kaisari. Kila mtu anayejifanya mfalme anasema vibaya juu ya Kaisari.”+
13 Kwa hiyo Pilato, baada ya kusikia maneno hayo, akamleta Yesu nje, naye akaketi juu ya kiti cha hukumu mahali panapoitwa Sakafu ya Jiwe, lakini, katika Kiebrania, Gabatha.
14 Sasa kulikuwa na matayarisho+ ya pasaka; karibu saa sita. Naye akawaambia Wayahudi: “Oneni! Mfalme wenu!”
15 Hata hivyo, wakapaaza sauti: “Mwondolee mbali! Mwondolee mbali! Mtundike mtini!” Pilato akawaambia: “Je, nimtundike mtini mfalme wenu?” Wakuu wa makuhani wakajibu: “Sisi hatuna mfalme ila Kaisari.”+
16 Kwa hiyo, wakati huo akamtia mikononi mwao, wakamtundike mtini.+
Basi wakamchukua Yesu.
17 Naye, akajibebea mti wa mateso,+ akaenda+ pale panapoitwa Mahali pa Fuvu la Kichwa, panapoitwa Golgotha katika Kiebrania;+
18 na huko wakamtundika mtini,+ na watu wengine wawili pamoja naye, mmoja upande huu na mmoja upande huu, lakini Yesu katikati.+
19 Pilato akaandika pia tangazo na kuliweka juu ya huo mti wa mateso. Liliandikwa: “Yesu Mnazareti Mfalme wa Wayahudi.”+
20 Kwa hiyo wengi wa Wayahudi walilisoma tangazo hilo, kwa sababu mahali ambapo Yesu alitundikwa palikuwa karibu na jiji;+ nalo liliandikwa kwa Kiebrania, kwa Kilatini, kwa Kigiriki.
21 Hata hivyo, wakuu wa makuhani wa Wayahudi wakaanza kumwambia Pilato: “Usiandike ‘Mfalme wa Wayahudi,’ bali kwamba alisema, ‘Mimi ni Mfalme wa Wayahudi.’ ”
22 Pilato akajibu: “Yale ambayo nimeandika, nimeandika.”
23 Sasa wakati askari-jeshi walipokuwa wamemtundika Yesu mtini, wakachukua mavazi yake ya nje na kufanya sehemu nne, kwa kila askari-jeshi sehemu moja, na vazi la ndani. Lakini lile vazi la ndani lilikuwa halina mshono, likiwa limefumwa kutoka juu mpaka urefu wake wote.+
24 Kwa hiyo wakaambiana: “Tusilirarue, bali na tuamue kwa kura juu yake litakuwa la nani.” Hii ilikuwa ili andiko lipate kutimizwa: “Waligawana mavazi yangu ya nje, nalo vazi langu walilipigia kura.”+ Ndivyo hasa hao askari-jeshi walivyofanya mambo hayo.
25 Hata hivyo, kando ya mti wa mateso wa Yesu, walikuwa wamesimama mama+ yake na dada ya mama yake; Maria+ mke wa Klopa, na Maria Magdalene.+
26 Kwa hiyo Yesu, alipomwona mama yake na mwanafunzi ambaye alimpenda+ wamesimama kando, akamwambia mama yake: “Mwanamke, ona! Mwana wako!”
27 Halafu akamwambia mwanafunzi huyo: “Ona! Mama yako!” Na tangu saa hiyo na kuendelea mwanafunzi huyo akampeleka nyumbani kwake.
28 Baada ya hayo, Yesu alipojua kwamba kufikia sasa mambo yote yalikuwa yametimizwa, ili andiko lipate kutimizwa, akasema: “Nina kiu.”+
29 Chombo kimoja kilichojaa divai kali kilikuwa hapo. Kwa hiyo wakaweka sifongo iliyojaa divai kali juu ya kijiti cha hisopo na kukileta kwenye kinywa chake.+
30 Sasa, alipokuwa amepokea ile divai kali, Yesu akasema: “Imetimizwa!”+ na, akiinamisha kichwa chake, akaitoa roho yake.+
31 Basi Wayahudi, kwa kuwa yalikuwa ni Matayarisho,+ ili miili hiyo isipate kukaa+ juu ya miti ya mateso siku ya Sabato, (kwa maana siku ya Sabato hiyo ilikuwa kuu,)+ wakamwomba Pilato aagize miguu yao ivunjwe na miili iondolewe.
32 Kwa hiyo, askari-jeshi wakaja na kuvunja miguu ya mtu wa kwanza na ile ya yule mtu mwingine aliyekuwa ametundikwa mtini pamoja naye.
33 Lakini walipokuja kwa Yesu, kwa kuwa waliona kwamba tayari alikuwa amekufa, hawakuivunja miguu yake.
34 Lakini mmoja wa hao askari-jeshi akauchoma ubavu wake kwa mkuki,+ na mara moja damu na maji vikatoka.
35 Na yeye ambaye ameona hilo ametoa ushahidi, nao ushahidi wake ni wa kweli, na mtu huyo anajua kwamba yeye husema mambo ya kweli, ili ninyi pia mweze kuamini.+
36 Kwa kweli, mambo haya yalitendeka kusudi andiko litimizwe: “Hakuna mfupa wake hata mmoja utakaovunjwa.”+
37 Na, tena, andiko tofauti linasema: “Watamtazama Yule waliyemchoma.”+
38 Basi baada ya mambo haya Yosefu kutoka Arimathea, aliyekuwa mwanafunzi wa Yesu lakini kwa siri kwa sababu alikuwa akiwaogopa Wayahudi,+ alimwomba Pilato apate kuondoa mwili wa Yesu; naye Pilato akampa ruhusa.+ Kwa hiyo akaja na kuuondoa mwili wake.+
39 Nikodemo pia, yule mtu aliyemjia usiku mara ya kwanza, akaja akileta msokoto wa manemane na udi, karibu ratili mia moja.+
40 Basi wakauchukua mwili wa Yesu na kuufunga kwa vitambaa pamoja na manukato,+ sawa na jinsi Wayahudi walivyo na desturi ya kutayarisha kwa ajili ya maziko.
41 Ilitukia kwamba, mahali alipotundikwa mtini palikuwa na bustani, na katika bustani hiyo kaburi jipya,+ ambalo bado hakuna yeyote aliyekuwa amelazwa ndani yake.
42 Basi, kwa sababu ya matayarisho+ ya Wayahudi, wakamlaza Yesu humo, kwa kuwa kaburi hilo lilikuwa hapo karibu.