Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Anatutazama kwa Faida Yetu

Yehova Anatutazama kwa Faida Yetu

Yehova Anatutazama kwa Faida Yetu

“Macho [ya Yehova] yanaenda huku na huku duniani kote ili aonyeshe nguvu zake kwa ajili ya wale ambao moyo wao ni mkamilifu kumwelekea yeye.”—2 NYA. 16:9.

1. Kwa nini Yehova anatuchunguza?

YEHOVA ni Baba mkamilifu. Anatujua vizuri sana hivi kwamba anajua hata “mwelekeo wa fikira” zetu. (1 Nya. 28:9) Hata hivyo, hatuchunguzi ili kupata tu makosa. (Zab. 11:4; 130:3) Badala yake, anataka kutulinda kwa upendo kutokana na jambo lolote linaloweza kuharibu uhusiano wetu pamoja naye au matarajio yetu ya kupata uzima wa milele.—Zab. 25:8-10, 12, 13.

2. Yehova anatumia nguvu zake kwa ajili ya nani?

2 Yehova ni Mweza-Yote, naye anaona kila kitu. Kwa sababu hiyo, anaweza kuwasaidia washikamanifu wake wakati wowote wanapomwomba msaada, naye anaweza kuwategemeza wanapopata majaribu. Andiko la 2 Mambo ya Nyakati 16:9 linasema: “Macho [ya Yehova] yanaenda huku na huku duniani kote ili aonyeshe nguvu zake kwa ajili ya wale ambao moyo wao ni mkamilifu kumwelekea yeye.” Ona kwamba Yehova anatumia nguvu zake kwa ajili ya wale wanaomtumikia kwa moyo kamili, moyo ulio safi na mnyoofu. Hatumii nguvu zake kwa ajili ya watu ambao ni wadanganyifu au wanafiki.—Yos. 7:1, 20, 21, 25; Met. 1:23-33.

Tembea Pamoja na Mungu

3, 4. Ni nini maana ya “kutembea pamoja na Mungu,” na ni mifano gani ya Biblia inayotusaidia kuelewa jambo hilo?

3 Wengi hawaamini kwamba Muumba wa mbingu na dunia anawaruhusu wanadamu watembee pamoja naye kwa njia ya mfano. Lakini, hivyo ndivyo Yehova anavyotaka tufanye. Katika nyakati za Biblia, Enoko na Noa ‘walitembea pamoja na Mungu.’ (Mwa. 5:24; 6:9) Musa “aliendelea kuwa imara kama mtu anayemwona Yeye asiyeonekana.” (Ebr. 11:27) Mfalme Daudi alitembea kwa unyenyekevu pamoja na Baba yake wa mbinguni. Alisema hivi: “Kwa sababu [Yehova] yuko upande wa mkono wangu wa kuume, sitatikiswa.”—Zab. 16:8.

4 Bila shaka, hatuwezi kuushika mkono wa Yehova na kutembea naye kihalisi. Lakini tunaweza kufanya hivyo kwa njia ya mfano. Jinsi gani? Mtunga-zaburi Asafu aliandika hivi: “Niko pamoja nawe daima; umeushika mkono wangu wa kuume. Utaniongoza kwa shauri lako.” (Zab. 73:23, 24) Kwa ufupi, tunatembea pamoja na Yehova tunapofuata kwa makini shauri lake, ambalo tunapokea hasa kupitia Neno lake lililoandikwa na kupitia “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.”—Mt. 24:45; 2 Tim. 3:16.

5. Yehova anawatazama jinsi gani washikamanifu wake kama baba mwenye upendo, nasi tunapaswa kuwa na maoni gani kumhusu?

5 Kwa kuwa Yehova anawathamini wale wanaotembea pamoja naye, anawatazama kama baba mwenye upendo, anawajali, anawalinda, na kuwafundisha. Mungu anasema hivi: “Nitakufanya uwe na ufahamu na kukufundisha katika njia unayopaswa kuiendea. Nitakupa shauri jicho langu likiwa linakutazama.” (Zab. 32:8) Jiulize hivi: ‘Je, ninajiwazia nikitembea pamoja na Yehova nikiwa nimeushika mkono wake na kusikiliza hekima yake na kujua kwamba ananitazama kwa upendo? Je, mawazo, maneno, na matendo yangu yanaonyesha kwamba ninatambua kuwa Yehova yupo? Na ninapokosea, je, ninamwona Yehova kuwa Baba mwenye upendo na mwenye rehema anayetaka kuwasaidia watu wanaotubu ili wawe na uhusiano wa karibu pamoja naye badala ya kumwona kuwa Mungu mkali na asiyejali?’—Zab. 51:17.

6. Yehova ana uwezo gani ambao wazazi wanadamu hawana?

6 Nyakati nyingine, Yehova anaweza kutusaidia hata kabla hatujatenda jambo lisilofaa. Kwa mfano, anaweza kuona kwamba moyo wetu wenye hila umeanza kutamani mambo yasiyofaa. (Yer. 17:9) Katika hali kama hiyo, anaweza kuchukua hatua haraka kuliko wazazi wanadamu kwa sababu “macho yake yanayong’aa” yana uwezo wa kuona ndani yetu kabisa, kuchunguza fikira zetu za ndani kabisa. (Zab. 11:4; 139:4; Yer. 17:10) Fikiria jinsi Mungu alivyoshughulikia hali fulani iliyotokea katika maisha ya Baruku, rafiki wa karibu na mwandishi wa nabii Yeremia.

Alimhangaikia Baruku Kama Baba Mwenye Upendo

7, 8. (a) Baruku alikuwa nani, na ni tamaa gani zisizofaa ambazo huenda zilianza kusitawi katika moyo wake? (b) Ni kwa njia gani Yehova alimhangaikia Baruku kama baba mwenye upendo?

7 Baruku alikuwa mwandishi stadi aliyetumikia kwa uaminifu pamoja na Yeremia katika mgawo mgumu wa kutangaza hukumu za Yehova huko Yuda. (Yer. 1:18, 19) Wakati fulani, Baruku, ambaye huenda alitoka katika familia maarufu, alianza kujitafutia mambo “makuu.” Labda alianza kusitawisha tamaa ya kichoyo ya kutaka makuu au alitamani kutajirika. Vyovyote vile, Yehova aliona kwamba mawazo hayo hatari yameanza kusitawi katika moyo wa Baruku. Akizungumza kupitia Yeremia, Yehova alishughulikia haraka jambo hilo kwa kumwambia hivi Baruku: “Umesema: ‘Ole wangu, sasa, kwa maana Yehova ameongeza huzuni juu ya maumivu yangu! Nimechoka kwa sababu ya kuugua kwangu, nami sikupata mahali pa kupumzika.’” Kisha Mungu akasema: “Unaendelea kujitafutia makuu. Usiendelee kuyatafuta.”—Yer. 45:1-5.

8 Ingawa Yehova alimpa Baruku shauri thabiti, hakutenda kwa hasira. Badala yake, alimjali kikweli kama baba mwenye upendo. Inaelekea Mungu aliona kwamba tamaa ya Baruku haikutokana na moyo mwovu au moyo uliopotoka. Pia, Yehova alijua kwamba Yerusalemu na Yuda zilikuwa katika siku za mwisho, naye hakutaka Baruku ajikwae wakati huo hatari. Kwa hiyo, ili kumsaidia mtumishi wake aone mambo waziwazi, Mungu alimkumbusha kwamba ‘Ataleta msiba juu ya wote wenye mwili,’ naye akaongeza kwamba ikiwa Baruku atatenda kwa hekima, ataishi. (Yer. 45:5) Ni kana kwamba Mungu alisema: ‘Fungua macho, Baruku. Kumbuka mambo ambayo yatapata Yuda na Yerusalemu zenye dhambi hivi karibuni. Endelea kuwa mwaminifu na uishi! Nitakulinda.’ Inaonekana Yehova aliugusa moyo wa Baruku, kwa maana Baruku alirekebisha maoni yake na kuokoka uharibifu wa Yerusalemu, uliotukia miaka 17 baadaye.

9. Unaweza kujibu jinsi gani maswali yaliyo katika fungu?

9 Unapotafakari kuhusu simulizi la Baruku, fikiria maswali na maandiko haya: Njia ambayo Mungu alitumia kumshughulikia Baruku inaonyesha nini kumhusu Yehova na maoni yake kuhusu watumishi wake? (Soma Waebrania 12:9.) Kwa kuwa tunaishi katika nyakati hatari, tunaweza kujifunza nini kutokana na shauri ambalo Mungu alimpa Baruku na kutokana na jinsi Baruku alivyoitikia? (Soma Luka 21:34-36.) Wazee Wakristo wanaweza kumwiga Yeremia jinsi gani katika kuonyesha kwamba wanawahangaikia watumishi wa Yehova kama Yehova anavyofanya?—Soma Wagalatia 6:1.

Mwana Aliiga Upendo wa Baba

10. Ni uwezo gani ambao Yesu amepewa ili atimize daraka lake akiwa Kichwa cha kutaniko la Kikristo?

10 Katika nyakati za kabla ya Ukristo, Yehova alifunua upendo wake kwa watu wake kupitia manabii wake na watumishi wengine waaminifu. Katika siku zetu, upendo huo unaonyeshwa hasa na Kichwa cha kutaniko la Kikristo, Yesu Kristo. (Efe. 1:22, 23) Hivyo, katika kitabu cha Ufunuo, Yesu anafananishwa na mwana-kondoo mwenye “macho saba, macho ambayo yanamaanisha roho saba za Mungu ambazo zimetumwa katika dunia nzima.” (Ufu. 5:6) Ndiyo, Yesu ana utambuzi kamili kwa sababu ametiwa nguvu kikamili na roho takatifu ya Mungu. Yeye pia anaona jinsi tulivyo kwa ndani, na hakuna jambo linalotendeka bila yeye kujua.

11. Kristo anatimiza daraka gani, na mtazamo wake kutuelekea unaonyesha nini kuhusu mtazamo wa Baba yake?

11 Hata hivyo, sawa na Yehova, Yesu si kama polisi anayetutazama akiwa mbinguni. Yesu anatuchunguza kwa upendo. Jina la Yesu la cheo “Baba wa Milele,” linatukumbusha daraka ambalo atatimiza katika kuwapa uzima wa milele wote wanaomwamini. (Isa. 9:6) Zaidi ya hayo, akiwa Kichwa cha kutaniko la Kikristo, Kristo anaweza kuwachochea Wakristo wakomavu na walio tayari kutumika, hasa wazee, kuwafariji au kuwashauri wale wanaohitaji kufarijiwa au kushauriwa.—1 The. 5:14; 2 Tim. 4:1, 2.

12. (a) Barua kwa makutaniko saba ya Asia Ndogo zinaonyesha nini kumhusu Yesu? (b) Wazee wanaonyesha jinsi gani mtazamo wa Kristo kuelekea kondoo wa Mungu?

12 Barua za Kristo kwa wazee wa makutaniko saba ya Asia Ndogo zinaonyesha kwamba anapendezwa sana na kondoo. (Ufu. 2:1–3:22) Katika barua hizo, Yesu alionyesha kwamba alijua mambo yaliyokuwa yakitendeka katika kila kutaniko na jinsi alivyowahangaikia sana wafuasi wake. Na anajua hata zaidi mambo yanayotendeka leo kwa kuwa maono ya Ufunuo yanatimizwa katika “siku ya Bwana.” * (Ufu. 1:10) Upendo wa Kristo unaonyeshwa mara nyingi kupitia wazee ambao wanatumikia wakiwa wachungaji wa kiroho wa kutaniko. Inapohitajika, anaweza kuwachochea wachungaji hao ambao ni “zawadi katika wanadamu” kutoa faraja, kuwatia watu moyo, na kuwashauri. (Efe. 4:8; Mdo. 20:28; soma Isaya 32:1, 2.) Je, unaona kwamba jitihada zao zinaonyesha kuwa Kristo anapendezwa nawe kibinafsi?

Msaada kwa Wakati Unaofaa

13-15. Mungu anaweza kuamua kujibu sala zetu jinsi gani? Toa mifano.

13 Je, umewahi kusali kwa bidii ili upate msaada na sala hiyo ikajibiwa wakati ulipotembelewa na kutiwa moyo na Mkristo mkomavu? (Yak. 5:14-16) Au labda ulipata msaada kupitia hotuba katika mkutano wa Kikristo au kichapo chetu kimoja. Mara nyingi Yehova anajibu sala katika njia hizo. Kwa mfano, baada ya mzee mmoja kutoa hotuba, alifikiwa na dada fulani ambaye alikuwa ametendewa isivyo haki majuma machache kabla ya hapo. Badala ya kulalamika kuhusu tatizo lake, dada huyo alieleza jinsi alivyothamini sana habari fulani za Kimaandiko katika hotuba hiyo. Habari hizo zilihusu hali yake na zilimfariji sana. Alifurahi kama nini kwamba alihudhuria mkutano huo!

14 Kuhusiana na msaada tunaopata kupitia sala, fikiria mfano wa wanaume watatu waliojifunza kweli za Biblia walipokuwa gerezani na kuwa wahubiri ambao hawajabatizwa. Kwa sababu ya kisa fulani cha jeuri, wafungwa wote katika gereza hilo walinyimwa mapendeleo fulani. Jambo hilo lilisababisha uasi. Ili kuonyesha kwamba wameasi, wafungwa waliamua kwamba hawatarudisha sahani zao baada ya kupata kiamsha-kinywa asubuhi iliyofuata. Wahubiri hao watatu wangefanya nini? Ikiwa wangeunga mkono uasi huo, wangekosa kutii shauri la Yehova kwenye Waroma 13:1. Kama hawangeunga mkono uasi huo, wangeshambuliwa na wafungwa wenzao wenye hasira.

15 Kwa kuwa wanaume hao watatu hawangeweza kuwasiliana, walisali ili wapate hekima. Asubuhi iliyofuata, wote watatu waligundua kwamba wamefanya uamuzi uleule—walikataa kiamsha-kinywa. Walinzi walipokuja baadaye ili kukusanya sahani, wanaume hao watatu hawakuwa na sahani ambazo wangerudisha. Walifurahi kama nini kwamba “msikiaji wa sala” alisikia sala zao!—Zab. 65:2.

Kutarajia Wakati Ujao Bila Wasiwasi

16. Kazi ya kuhubiri inaonyesha jinsi gani kwamba Yehova anawajali watu walio kama kondoo?

16 Kazi ya ulimwenguni pote ya kuhubiri ni jambo lingine linaloonyesha kwamba Yehova anawahangaikia watu wenye moyo mnyoofu popote pale wanapoishi. (Mwa. 18:25) Yehova anaweza kuwaongoza watumishi wake kwa watu walio kama kondoo hata ikiwa watu hao wanaishi katika maeneo ambako habari njema hazijahubiriwa, na mara nyingi anatumia malaika ili kufanya hivyo. (Ufu. 14:6, 7) Kwa mfano, kupitia malaika, Mungu alimwongoza Filipo, mweneza-injili wa karne ya kwanza amtafute ofisa Mwethiopia na kumfafanulia Maandiko. Kulikuwa na matokeo gani? Mtu huyo alikubali habari njema na kuwa mfuasi aliyebatizwa wa Yesu. *Yoh. 10:14; Mdo. 8:26-39.

17. Kwa nini hatupaswi kuhangaika kupita kiasi kuhusu wakati ujao?

17 Kadiri mfumo wa mambo wa sasa unavyokaribia kwisha, “maumivu ya taabu” yaliyotabiriwa yataendelea. (Mt. 24:8) Kwa mfano, huenda bei za vyakula zikapanda sana kwa sababu ya ongezeko la idadi ya watu, hali mbaya sana ya hewa, au matatizo ya kiuchumi. Huenda ikawa vigumu zaidi kupata kazi, na huenda wafanyakazi wakalazimika kufanya kazi kwa saa nyingi zaidi. Vyovyote itakavyokuwa, wote wanaotanguliza mambo ya kiroho na kuendelea kuwa na ‘jicho rahisi’ hawapaswi kuhangaika kupita kiasi. Wanajua kwamba Mungu anawapenda na atawatunza. (Mt. 6:22-34) Kwa mfano, fikiria jinsi ambavyo Yehova alimtunza Yeremia wakati wa mwisho wenye msukosuko wa Yerusalemu mwaka wa 607 K.W.K.

18. Yehova alionyesha jinsi gani kwamba anampenda Yeremia wakati Yerusalemu lilipozingirwa?

18 Wababiloni walipokaribia kumaliza kuzingira Yerusalemu, Yeremia alifungwa katika Ua wa Walinzi. Angepata chakula jinsi gani? Ikiwa angekuwa huru, angekitafuta. Lakini sasa angeweza tu kukipata kutoka kwa watu waliokuwa karibu naye, na wengi wao walimchukia! Hata hivyo, Yeremia hakuwategemea wanadamu, bali alimtegemea Mungu ambaye aliahidi kumtunza. Je, Yehova alitimiza ahadi yake? Bila shaka! Alihakikisha kwamba kila siku Yeremia alipata “mkate wa mviringo . . . mpaka mkate wote ulipokwisha jijini.” (Yer. 37:21) Yeremia, na pia Baruku, Ebed-meleki, na wengine, waliokoka wakati huo wa njaa, magonjwa, na kifo.—Yer. 38:2; 39:15-18.

19. Tunapongojea wakati ujao, tunapaswa kuazimia kufanya nini?

19 Ndiyo, “macho ya Yehova yako juu ya waadilifu, na masikio yake yanaielekea dua yao.” (1 Pet. 3:12) Je, unafurahi kwamba Baba yako wa mbinguni anakutazama? Je, unahisi ukiwa salama salimini kwa sababu unajua kwamba anakutazama kwa faida yako? Basi, azimia kuendelea kutembea pamoja na Mungu, hata mambo yawe namna gani wakati ujao. Tunaweza kuwa na hakika kwamba sikuzote Yehova, kama baba mwenye upendo, atawachunguza washikamanifu wake wote.—Zab. 32:8; soma Isaya 41:13.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 12 Ingawa barua hizo zinawahusu hasa wafuasi wa Kristo watiwa-mafuta, kanuni zake zinawahusu watumishi wote wa Mungu.

^ fu. 16 Mfano mwingine unaoonyesha jinsi Mungu anavyotoa mwongozo unapatikana katika Matendo 16:6-10. Andiko hilo linasema kwamba Paulo na wenzake “walikatazwa na roho takatifu” wasihubiri katika Asia na Bithinia. Badala yake, walitumwa Makedonia, ambako watu wengi wapole waliikubali injili.

Je, Unaweza Kueleza?

• Tunaweza kuonyesha jinsi gani kwamba ‘tunatembea pamoja na Mungu’?

• Yehova alionyesha jinsi gani kwamba anampenda Baruku?

• Akiwa Kichwa cha kutaniko la Kikristo, Yesu anaiga jinsi gani sifa za Baba yake?

• Tunaweza kuonyesha jinsi gani kwamba tunamtegemea Mungu katika nyakati hizi za hatari?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 9]

Kama Yeremia alivyomhangaikia Baruku, wazee Wakristo leo wanamwiga Yehova kwa kuwahangaikia wengine

[Picha katika ukurasa wa 10]

Yehova anaweza kutupa msaada jinsi gani kwa wakati unaofaa?