Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Luka

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Luka

Neno la Yehova Liko Hai

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Luka

INASEMEKANA kwamba Injili ya Mathayo iliandikwa hasa kwa ajili ya Wayahudi, nayo Injili ya Marko ikaandikwa kwa ajili ya wasio Wayahudi. Hata hivyo, Injili ya Luka iliandikwa kwa ajili ya watu wa mataifa yote. Kitabu hicho cha Luka kilichoandikwa mwaka wa 56-58 W.K. hivi, kinasimulia kwa undani kuhusu maisha na huduma ya Yesu.

Akiwa na mtazamo wa tabibu mwenye kujali na mwangalifu, Luka anafuata “mambo yote tangu mwanzo kwa usahihi” na masimulizi yake yanahusu kipindi cha miaka 35—kuanzia mwaka wa 3 K.W.K. mpaka 33 W.K. (Luka 1:3) Asilimia 60 hivi ya mambo yaliyo katika Injili ya Luka hayapatikani katika zile Injili nyingine.

HUDUMA YA MAPEMA

(Luka 1:1–9:62)

Baada ya kueleza kwa undani kuhusu kuzaliwa kwa Yohana Mbatizaji na kwa Yesu, Luka anatuambia kwamba Yohana alianza huduma yake katika mwaka wa 15 wa utawala wa Kaisari Tiberio, yaani, mwanzoni mwa mwaka wa 29 W.K. (Luka 3:1, 2) Yohana anambatiza Yesu baadaye mwaka huohuo. (Luka 3:21, 22) Kufikia mwaka wa 30 W.K., ‘Yesu anarudi Galilaya na kuanza kufundisha katika masinagogi yao.’—Luka 4:14, 15.

Yesu anaanza safari yake ya kwanza ya kuhubiri Galilaya. Anauambia umati hivi: “Ni lazima nitangaze habari njema ya ufalme wa Mungu kwenye majiji mengine pia.” (Luka 4:43) Anamchukua Simoni yule mvuvi pamoja na watu wengine. Anasema hivi: “Tangu sasa na kuendelea utakuwa ukiwavua watu wakiwa hai.” (Luka 5:1-11; Mt. 4:18, 19) Wale mitume 12 wako pamoja na Yesu anapofunga safari yake ya pili ya kuhubiri Galilaya. (Luka 8:1) Katika safari yake ya tatu, anawatuma wale 12 “kuhubiri ufalme wa Mungu na kuponya.”—Luka 9:1, 2.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

1:35—Je, yai la uzazi la Maria lilihusika katika mimba yake? Ili mtoto wa Maria awe mzao wa kweli wa Abrahamu, Yuda, na Daudi, kama Mungu alivyokuwa ameahidi, ilikuwa lazima yai la uzazi la Maria lihusike katika mimba yake. (Mwa. 22:15, 18; 49:10; 2 Sam. 7:8, 16) Hata hivyo, roho takatifu ya Yehova ilitumiwa kuhamisha uhai mkamilifu wa Mwana wa Mungu na hivyo kutungisha mimba hiyo. (Mt. 1:18) Inaelekea kwamba hilo liliondoa kabisa kutokamilika kokote katika yai la uzazi la Maria na kulinda kiini-tete kilichokuwa kikikua kisipatwe na madhara yoyote tangu mwanzo.

1:62—Je, Zekaria alikuwa bubu na kiziwi? Hapana. Uwezo wake wa kuzungumza tu ndio ulioathiriwa. Wengine walimuuliza “kwa ishara” jina ambalo alitaka mtoto aitwe lakini si kwa sababu Zekaria alikuwa kiziwi. Inaelekea sana kwamba alisikia yale ambayo mke wake alisema kuhusu jina la mwana wao. Labda wengine walimuuliza Zekaria kuhusu hilo kwa kufanya ishara. Uhakika wa kwamba Zekaria alihitaji kurudishiwa tu uwezo wake wa kuzungumza unaonyesha kwamba hakuwa kiziwi.—Luka 1:13, 18-20, 60-64.

2:1, 2—Maneno “uandikisho huu wa kwanza” yanatusaidia jinsi gani kukadiria wakati wa kuzaliwa kwa Yesu? Chini ya Kaisari Augusto, kulikuwa na zaidi ya uandikisho mmoja—wa kwanza ulitukia mwaka wa 2 K.W.K. kupatana na Danieli 11:20 na wa pili ukawa mwaka wa 6 au 7 W.K. (Mdo. 5:37) Kirenio alikuwa gavana wa Siria wakati wa uandikisho wa kwanza na wa pili, na ni wazi kwamba alishikilia cheo hicho mara mbili. Luka anapotaja uandikisho wa kwanza anatusaidia kujua kwamba Yesu alizaliwa katika mwaka wa 2 K.W.K.

2:35—“Upanga mrefu” ungeichoma nafsi ya Maria jinsi gani? Maneno hayo yalionyesha kwamba Maria angefadhaika kuwaona watu wengi wakimkataa Yesu kuwa Masihi na huzuni ambayo ingempata wakati Yesu angekufa kifo chenye maumivu makali.—Yoh. 19:25.

9:27, 28—Kwa nini Luka anasema kugeuka sura kulitukia “siku nane” baada ya Yesu kuwaahidi wanafunzi wake kwamba baadhi yao ‘hawangeonja kifo kamwe’ mpaka kwanza wamwone akija katika Ufalme wake, lakini Mathayo na Marko wanasema kwamba kulitukia “siku sita baadaye”? (Mt. 17:1; Marko 9:2) Inaonekana Luka anaongeza siku mbili za ziada—siku ya kutolewa kwa ahadi na siku ya utimizo.

9:49, 50—Kwa nini Yesu hakumzuia mtu fulani asifukuze roho waovu, ijapokuwa mtu huyo hakuwa akimfuata? Yesu hakumzuia mtu huyo kwa kuwa kutaniko la Kikristo halikuwa limeanzishwa. Hivyo, mtu huyo hakuhitajiwa kumfuata Yesu kihalisi ili aweke imani katika jina la Yesu na kufukuza roho waovu.—Marko 9:38-40.

Mambo Tunayojifunza:

1:32, 33; 2:19, 51. Maria alihifadhi moyoni mwake matukio na maneno yaliyotimiza unabii. Je, tunahifadhi moyoni mwetu yale ambayo Yesu alitabiri kuhusu “umalizio wa mfumo wa mambo,” tukilinganisha yale aliyosema na yale yanayotukia leo?—Mt. 24:3.

2:37. Mfano wa Ana unatufundisha kwamba tunapaswa kumwabudu Yehova daima, ‘kudumu katika sala,’ na kutoacha “kukusanyika pamoja sisi wenyewe” katika mikutano ya Kikristo.—Rom. 12:12; Ebr. 10:24, 25.

2:41-50. Yosefu alitanguliza mambo ya kiroho katika maisha yake na aliitunza familia yake kimwili na kiroho. Kwa njia hiyo, aliwawekea vichwa vya familia mfano mzuri.

4:4. Tunapaswa kufikiria mambo ya kiroho kila siku.

6:40. Mwalimu wa Neno la Mungu anapaswa kuwawekea wanafunzi wake mfano unaofaa. Anapaswa kutenda kulingana na yale anayofundisha.

8:15. Ili ‘kulihifadhi Neno na kuzaa matunda kwa uvumilivu,’ ni lazima tulielewe, tulithamini, na tulishike Neno la Mungu. Ni lazima tusali na kutafakari tunapoisoma Biblia na vichapo vinavyotegemea Biblia.

HUDUMA YA YESU YA BAADAYE

(Luka 10:1–24:53)

Yesu anawatuma wengine 70 wamtangulie kuingia katika majiji na maeneo ya Yudea. (Luka 10:1) Anasafiri “kutoka jiji mpaka jiji na kutoka kijiji mpaka kijiji, akifundisha.”—Luka 13:22.

Siku tano kabla ya Pasaka ya 33 W.K., Yesu anaingia Yerusalemu akiwa amempanda mwana-punda. Wakati umefika wa kutimizwa kwa maneno haya aliyokuwa amewaambia wanafunzi wake: “Mwana wa binadamu lazima apatwe na mateso mengi na kukataliwa na wanaume wazee na wakuu wa makuhani na waandishi, na kuuawa, na siku ya tatu afufuliwe.”—Luka 9:22, 44.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

10:18—Yesu alikuwa akizungumzia nini alipowaambia wale wanafunzi 70 hivi: “Nilianza kumwona Shetani akiwa tayari ameanguka kama umeme kutoka mbinguni”? Yesu hakuwa akisema kwamba tayari Shetani alikuwa amefukuzwa kutoka mbinguni. Hilo halikutukia mpaka muda mfupi baada ya Kristo kuwekwa kuwa Mfalme wa kimbingu katika 1914. (Ufu. 12:1-10) Hatuwezi kusema kwa uhakika ikiwa alikuwa akizungumzia tukio la wakati ujao kana kwamba limetukia, hata hivyo ni wazi Yesu alikuwa akikazia kwamba jambo hilo lingetukia bila shaka.

14:26—Wafuasi wa Kristo wanapaswa ‘kuwachukia’ watu wao wa ukoo katika maana gani? Katika Biblia, neno ‘chukia’ linaweza kumaanisha kumpenda mtu fulani kwa kadiri ndogo kuliko mwingine. (Mwa. 29:30, 31) Wakristo wanapaswa ‘kuwachukia’ watu wao wa ukoo katika maana ya kwamba wanawapenda kwa kadiri ndogo kuliko wanavyompenda Yesu.—Mt. 10:37.

17:34-37—Ni nani “tai,” na ni nini ule “mzoga” ambao tai wanakusanyika kuuzunguka? Wale ‘watakaochukuliwa,’ au kukombolewa, wanalinganishwa na tai wanaoona mbali. “Mzoga” ambao wanakusanyika kuuzunguka ni Kristo wa kweli wakati wa kuwapo kwake kusikoonekana na chakula cha kiroho ambacho Yehova anawaandalia.—Mt. 24:28.

22:44—Kwa nini Yesu alipata maumivu makali? Ilikuwa hivyo kwa sababu kadhaa. Yesu alihangaika alipofikiria jinsi kuuawa kwake kama mhalifu kungemwathiri Yehova Mungu na jina Lake. Zaidi ya hilo, Yesu alijua vizuri kwamba uhai wake wa milele na wakati ujao wa wanadamu wote ulitegemea kudumu kwake akiwa mwaminifu.

23:44—Je, lile giza la muda wa saa tatu lilisababishwa na kupatwa kwa jua? Hapana. Kupatwa kwa jua kunatukia tu wakati wa mwezi mpya, wala si wakati wa mwezi mpevu, kama inavyokuwa wakati wa Pasaka. Giza lililotokea siku ambayo Yesu alikufa lililetwa kimuujiza na Mungu.

Mambo Tunayojifunza:

11:1-4. Kulinganisha maagizo haya na sala ya kielelezo iliyo na maneno tofauti kidogo ambayo ilitolewa katika Mahubiri ya Mlimani miezi 18 mapema, kunaonyesha wazi kwamba hatupaswi kurudia-rudia tu maneno fulani tunaposali.—Mt. 6:9-13.

11:5, 13. Ijapokuwa Yehova yuko tayari kujibu sala zetu, tunapaswa kusali kwa bidii.—1 Yoh. 5:14.

11:27, 28. Furaha ya kweli inatokana na kufanya mapenzi ya Mungu kwa uaminifu wala haitokani na uhusiano wa kifamilia au utajiri wa kimwili.

11:41. Moyo wenye upendo na utayari ndio unaopaswa kutuchochea kutoa zawadi za rehema.

12:47, 48. Yule ambaye amepewa wajibu mkubwa zaidi lakini anakosa kuutimiza analaumika zaidi kuliko yule asiyejua au kuelewa vizuri wajibu wake.

14:28, 29. Ni jambo la hekima kuishi kulingana na mapato yetu.

22:36-38. Yesu hakuwaambia wanafunzi wake wabebe silaha ya kujilinda. Badala yake, kuwa na mapanga usiku ambao Yesu alisalitiwa kulimwezesha Yesu kuwafundisha somo muhimu: “Wale wote wanaouchukua upanga wataangamia kwa upanga.”—Mt. 26:52.

[Picha katika ukurasa wa 31]

Yosefu aliweka mfano mzuri akiwa kichwa cha familia

[Picha katika ukurasa wa 32]

Luka ndiye aliyeandika kwa undani zaidi kuhusu maisha na huduma ya Yesu