Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Anasikia Vilio Vyetu Vya Kuomba Msaada

Yehova Anasikia Vilio Vyetu Vya Kuomba Msaada

Yehova Anasikia Vilio Vyetu Vya Kuomba Msaada

“Macho ya Yehova yanawaelekea waadilifu, na masikio yake yanakielekea kilio chao cha kuomba msaada.”—ZAB. 34:15.

1, 2. (a) Watu wengi leo wanahisi namna gani? (b) Kwa nini hilo halitushangazi?

JE, UNAKUMBWA na taabu? Ikiwa ndivyo, ujue kwamba kuna wengine wanaokumbwa na taabu kama wewe. Mamilioni ya watu wanapambana na matatizo ya maisha ya kila siku katika mfumo huu mbovu wa mambo. Ni vigumu sana kwa wengine kuvumilia. Wanahisi tu kama mtunga-zaburi Daudi ambaye aliandika hivi: “Nimekufa ganzi na kupondwa kupita kiasi; nimenguruma kwa sababu ya kuugua kwa moyo wangu. Moyo wangu mwenyewe umepiga-piga kwa nguvu, nguvu zangu zimeniacha, na nuru ya macho yangu mwenyewe haiko pamoja nami.”—Zab. 38:8, 10.

2 Tukiwa Wakristo, hatushangazwi na taabu za maisha. Tunaelewa kwamba “maumivu ya taabu” ni sehemu ya ishara iliyotabiriwa ya kuwapo kwa Yesu. (Marko 13:8; Mt. 24:3) Neno la lugha ya awali linalotafsiriwa “maumivu ya taabu” linamaanisha maumivu makali sana ya kuzaa. Neno hilo linaonyesha kikweli mateso makali ambayo watu wanapata katika nyakati hizi “za hatari,” au “kali sana,” ambazo ni “ngumu kushughulika nazo”!—2 Tim. 3:1; Kingdom Interlinear.

Yehova Anaelewa Taabu Zetu

3. Watu wa Mungu wanajua vizuri nini?

3 Watu wa Yehova wanajua vizuri kwamba hawawezi kuepuka madhara ya taabu, na inaelekea sana kwamba hali mbaya zitakuwa mbaya hata zaidi. Tukiwa watumishi wa Mungu tunakabili matatizo yanayowakumba wanadamu wote kwa ujumla na pia tunakabiliana na ‘adui, Ibilisi,’ ambaye ameazimia kuiharibu imani yetu. (1 Pet. 5:8) Ni rahisi sana kuhisi kama Daudi aliyesema hivi: “Shutuma imeuvunja moyo wangu, nalo jeraha haliwezi kuponywa. Nami niliendelea kutumainia mtu fulani aonyeshe kusikitika, lakini hapakuwa na yeyote; na watu wa kufariji, lakini sikupata yeyote”!—Zab. 69:20.

4. Ni nini kinachotufariji tunapokumbwa na taabu?

4 Je, Daudi alimaanisha kwamba hakuwa na tumaini lolote? Hapana. Angalia maneno aliyoongezea katika zaburi hiyo: “Yehova anawasikiliza maskini, wala kwa kweli hatawadharau wafungwa wake mwenyewe,” au “watu wake wafungwa.” (Zab. 69:33; Biblia Habari Njema) Kwa ujumla, huenda nyakati nyingine tukahisi kwamba sisi ni wafungwa wa taabu au mateso yetu. Huenda ikaonekana kwamba wengine hawaelewi hali yetu, na labda kwa kweli hawaelewi. Lakini kama Daudi, tunaweza kufarijiwa kujua kwamba Yehova anaelewa kikamili taabu zetu.—Zab. 34:15.

5. Mfalme Sulemani alikuwa na uhakika gani?

5 Sulemani, mwana wa Daudi, alikazia jambo hilo la hakika hekalu la Yerusalemu lilipokuwa likiwekwa wakfu. (Soma 2 Mambo ya Nyakati 6:29-31.) Alimsihi Yehova asikie sala ya kila mtu mwenye moyo mnyoofu ambaye Angemfikia kuhusu “pigo lake na maumivu yake mwenyewe.” Mungu angeitikia jinsi gani sala za watu hao wenye taabu? Sulemani alionyesha uhakika wake wa kwamba Mungu hangesikia tu sala zao bali pia angechukua hatua ya kuwasaidia. Kwa nini? Kwa sababu anajua vema mambo yaliyo katika “moyo wa wanadamu.”

6. Tunaweza kukabiliana jinsi gani na mahangaiko, na kwa nini?

6 Sisi pia tunaweza kumfikia Yehova katika sala kuhusu ‘pigo letu na maumivu yetu wenyewe,’ kuhusu taabu zetu binafsi. Kujua kwamba anaelewa taabu zetu na kwamba anatujali kunapaswa kutufariji. Mtume Petro alithibitisha hilo aliposema hivi: ‘Tupeni mahangaiko yenu yote juu yake, kwa sababu yeye anawajali ninyi.’ (1 Pet. 5:7) Yehova anahangaishwa kikweli na yale yanayotupata. Yesu alikazia jinsi Yehova anavyotutunza kwa upendo, aliposema hivi: “Je, shomoro wawili hawauzwi kwa sarafu ya thamani ndogo? Na bado hakuna hata mmoja wao atakayeanguka chini bila Baba yenu kujua. Lakini nywele zenyewe za kichwa chenu zimehesabiwa zote. Kwa hiyo msiogope: Ninyi ni bora kuliko shomoro wengi.”—Mt. 10:29-31.

Tegemea Msaada wa Yehova

7. Tunaweza kuwa na uhakika wa kupata msaada gani?

7 Bila shaka, tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova yuko tayari naye anaweza kutusaidia tunapokabili taabu. “Kwetu Mungu ni kimbilio na nguvu, msaada unaopatikana kwa utayari wakati wa taabu.” (Zab. 34:15-18; 46:1) Mungu anatusaidia kwa njia gani? Fikiria yale yanayosemwa katika 1 Wakorintho 10:13: “Mungu ni mwaminifu, naye hatawaacha ninyi mjaribiwe kupita mnavyoweza kuhimili, bali pamoja na hilo jaribu ataifanya pia njia ya kutokea kusudi mweze kulivumilia.” Yehova anaweza kuongoza mambo na kuondoa taabu yetu, au anaweza kutupa nguvu tunazohitaji ili tuvumilie. Kwa vyovyote vile, Yehova anatusaidia.

8. Tunapaswa kufanya nini ili tufaidike na msaada wa Mungu?

8 Tunapaswa kufanya nini ili tufaidike na msaada huo? Tunashauriwa hivi: ‘Tupeni mahangaiko yenu yote juu yake.’ Hilo linamaanisha kwamba kwa njia ya mfano tunampa Yehova daraka la kushughulikia mahangaiko na masumbuko yetu yote. Tunajitahidi kuacha kuhangaika, nasi tunamtegemea kwa subira ili ashughulikie mahitaji yetu. (Mt. 6:25-32) Ili tumtegemee kwa njia hiyo, tunahitaji unyenyekevu. Hatupaswi kutegemea nguvu au hekima yetu wenyewe. Tunapojinyenyekeza “chini ya mkono wenye nguvu wa Mungu,” tunatambua hali yetu ya chini. (Soma 1 Petro 5:6.) Kufanya hivyo kunatusaidia kukabiliana na hali yoyote ambayo Mungu anaruhusu. Huenda tukatamani sana kupata kitulizo haraka, lakini tuna hakika kwamba Yehova anajua wakati unaofaa kabisa wa kutusaidia na jinsi ya kufanya hivyo.—Zab. 54:7; Isa. 41:10.

9. Ni mzigo wa aina gani ambao Daudi alihitaji kumtupia Yehova?

9 Kumbuka maneno ya Daudi yaliyoandikwa katika Zaburi 55:22: “Mtupie Yehova mzigo wako, naye mwenyewe atakutegemeza. Hatamwacha kamwe mwadilifu atikisike.” Daudi alipoandika maneno hayo, alikuwa na taabu nyingi sana. (Zab. 55:4) Inaeleweka kwamba zaburi hii iliandikwa wakati Absalomu, mwana wake, alipopanga njama ya kunyakua ufalme wake. Ahithofeli, mshauri aliyetegemeka zaidi wa Daudi aliunga mkono njama hiyo. Daudi alilazimika kukimbia kutoka Yerusalemu ili aokoe uhai wake. (2 Sam. 15:12-14) Hata katika hali hizo ngumu sana, Daudi aliendelea kumtegemea Mungu, naye hakukatishwa tamaa.

10. Ni lazima tufanye nini tunapokabili taabu?

10 Ni jambo la maana sana tumfikie Yehova katika sala kama Daudi, na kumweleza taabu zozote ambazo huenda tunakabili. Acheni tuchunguze yale ambayo mtume Paulo alituhimiza tufanye kuhusiana na hilo. (Soma Wafilipi 4:6, 7.) Matokeo yatakuwa nini tukisali kwa bidii? “Amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote itailinda mioyo [yetu] na nguvu [zetu] za akili kwa njia ya Kristo Yesu.”

11. “Amani ya Mungu” inalinda mioyo na nguvu zetu za akili kwa njia gani?

11 Je, sala itabadili hali yako? Inaweza. Lakini, tunapaswa kutambua kwamba nyakati nyingine Yehova hajibu sala zetu kwa njia ambayo tunataka. Hata hivyo, sala inatusaidia kudumisha usawaziko wetu wa kiakili, ili taabu zetu zisitulemee. “Amani ya Mungu” inaweza kutuletea utulivu tunapolemewa sana na mahangaiko. Kama kikosi cha askari-jeshi ambacho kimepewa kazi ya kulinda mji usishambuliwe na maadui, ndivyo “amani ya Mungu” itakavyolinda mioyo yetu na nguvu zetu za akili. Itatuwezesha pia kuondoa mashaka, woga, na mawazo yasiyofaa na kutuzuia tusitende haraka-haraka na kwa njia isiyo ya hekima.—Zab. 145:18.

12. Toa mfano unaoonyesha jinsi mtu anavyoweza kuwa na amani ya akili.

12 Tunaweza kuwa na amani ya akili jinsi gani tunapokuwa na taabu? Fikiria mfano mmoja ambao kwa njia fulani unalingana na hali zetu. Huenda mtu akafanya kazi chini ya msimamizi mwenye matusi. Hata hivyo, mtu huyo anamwambia mwenye kampuni hiyo jinsi anavyohisi. Mwenye kampuni ni mtu mwenye fadhili na usawaziko. Anamhakikishia mtu huyo kwamba anaelewa hali yake na kumfunulia kwamba msimamizi huyo atafutwa kazi hivi karibuni. Hilo litamfanya mtu huyo ahisi namna gani? Kuamini ahadi hiyo na kujua hatua ambayo itachukuliwa, kutatia nguvu azimio lake la kuendelea na kazi, hata ikiwa kwa muda atapata matatizo mengine. Vivyo hivyo, tunajua kwamba Yehova anaelewa hali yetu, naye anatuhakikishia kwamba hivi karibuni “mtawala wa ulimwengu huu atatupwa nje.” (Yoh. 12:31) Ni jambo lenye kufariji kama nini!

13. Zaidi ya kusali, ni lazima tufanye nini kingine?

13 Basi, je, inatosha tu kumwambia Yehova matatizo yetu katika sala? Haitoshi. Tunahitaji kufanya mengi zaidi. Tunahitaji kutenda kupatana na sala zetu. Mfalme Sauli alipowatuma watu nyumbani kwa Daudi ili wamuue, Daudi alisali hivi: “Unikomboe kutoka kwa adui zangu, Ee Mungu wangu; unilinde kutoka kwa wale wanaoinuka dhidi yangu. Unikomboe kutoka kwa wanaotenda mambo yenye kuumiza, na uniokoe kutoka kwa watu wenye hatia ya damu.” (Zab. 59:1, 2) Zaidi ya kusali, Daudi alimsikiliza mke wake naye akachukua hatua iliyohitajiwa ili kuponyoka. (1 Sam. 19:11, 12) Vivyo hivyo, tunaweza kusali ili tupate hekima itakayotusaidia kushughulikia na labda hata kuboresha hali zetu ngumu.—Yak. 1:5.

Jinsi Tunavyoweza Kuwa na Nguvu za Kuvumilia

14. Ni nini kinachoweza kutusaidia kuvumilia tunapokabili taabu?

14 Huenda taabu zetu zisiondolewe mara moja. Zinaweza hata kuendelea kwa muda fulani. Ikiwa hivyo, ni nini kitakachotusaidia kuvumilia? Kwanza, kumbuka kwamba tunapoendelea kumtumikia Yehova kwa uaminifu hata tunapokabili matatizo, tunathibitisha kwamba tunampenda. (Mdo. 14:22) Kumbuka shtaka la Shetani kumhusu Ayubu: “Je, Ayubu angekuabudu ikiwa hangekuwa akipata faida yoyote? Sikuzote umemlinda yeye na familia yake na kila kitu alicho nacho. Unabariki kila kitu anachofanya, nawe umempa ng’ombe wa kutosha kujaza nchi yote. Lakini sasa jaribu kuchukua kila kitu alicho nacho—atakulaani mbele za uso wako.” (Ayu. 1:9-11, Today’s English Version) Ayubu alithibitisha kwa utimilifu wake kwamba shtaka hilo ni uwongo mtupu. Tunapovumilia taabu, sisi pia tunapata nafasi ya kuthibitisha kwamba Shetani ni mwongo. Kwa njia hiyo, uvumilivu wetu unatia nguvu tumaini na uhakika wetu.—Yak. 1:4.

15. Ni mifano gani inayoweza kututia nguvu?

15 Pili, kumbuka kwamba ‘mambo yaleyale kwa njia ya mateso yanatimizwa katika ushirika mzima wa ndugu zako ulimwenguni.’ (1 Pet. 5:9) Ndiyo, ‘hakuna jaribu ambalo limekupata wewe ila lile lililo kawaida kwa watu.’ (1 Kor. 10:13) Kwa hivyo, unaweza kupata nguvu na ujasiri ukitafakari kuhusu mifano ya wengine badala ya kukazia fikira matatizo yako. (1 The. 1:5-7; Ebr. 12:1) Tumia wakati kufikiria mifano ya watu unaowafahamu ambao wamevumilia kwa uaminifu taabu zenye kuumiza sana. Je, umechunguza masimulizi ya maisha ambayo yamechapishwa ili kupata masimulizi ya watu ambao wamekabili hali kama zako? Masimulizi hayo yanaweza kukutia nguvu sana.

16. Mungu anatutia nguvu jinsi gani tunapokabili majaribu mbalimbali?

16 Tatu, kumbuka kwamba Yehova ndiye “Baba ya rehema nyororo na Mungu wa faraja yote, ambaye hutufariji katika dhiki yetu yote, ili tuweze kuwafariji wale walio katika namna yoyote ya dhiki kupitia faraja ambayo sisi wenyewe tunafarijiwa na Mungu.” (2 Kor. 1:3, 4) Ni kana kwamba Mungu anasimama kando yetu ili kututia moyo na kututia nguvu, si katika dhiki yetu ya sasa tu bali “katika dhiki yetu yote.” Hilo linatuwezesha kuwafariji wengine walio “katika namna yoyote ya dhiki.” Paulo alijionea ukweli wa maneno hayo.—2 Kor. 4:8, 9; 11:23-27.

17. Biblia inaweza kutusaidia jinsi gani kushughulikia taabu tunazokabili maishani?

17 Nne, tuna Neno la Mungu, Biblia, ambalo “ni lenye faida kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo, kwa kutia nidhamu katika uadilifu, ili mtu wa Mungu awe na uwezo kamili, akiwa na vifaa kamili kwa ajili ya kila kazi njema.” (2 Tim. 3:16, 17) Neno la Mungu halitufanyi tu tuwe na “uwezo” na ‘vifaa kwa ajili ya kila kazi njema.’ Linatuwezesha pia kushughulikia taabu zinazotukumba maishani. Linatufanya tuwe na “uwezo kamili” na “vifaa kamili.” Neno la lugha ya awali linalotafsiriwa ‘kuwa na vifaa kamili’ kihalisi linamaanisha “kuwa na kila kitu.” Huenda neno hilo lilitumiwa zamani kuhusu mashua ambayo ilikuwa imetiwa kila kitu kilichohitajiwa kwa ajili ya safari au kuhusu mashini iliyokuwa na uwezo wa kufanya kazi yoyote ile iliyokusudiwa. Vivyo hivyo, kupitia Neno lake, Yehova anatupa kila kitu tunachohitaji ili kushughulikia hali yoyote ambayo huenda tukakabili. Kwa hivyo, tunaweza kusema, “Mungu akiruhusu taabu yoyote, ninaweza kuivumilia kwa msaada wake.”

Kukombolewa Kutoka Katika Taabu Zetu Zote

18. Tunaweza kuvumilia kwa uaminifu tukikazia fikira jambo gani?

18 Tano, sikuzote kazia fikira ukweli mzuri ajabu wa kwamba hivi karibuni Yehova atawaondolea wanadamu taabu zote. (Zab. 34:19; 37:9-11; 2 Pet. 2:9) Kwa kweli, Mungu hatatukomboa tu kutoka katika taabu za leo bali pia atatupa nafasi ya kupata uzima wa milele, iwe mbinguni pamoja na Yesu au katika paradiso duniani.

19. Tunaweza jinsi gani kuvumilia kwa uaminifu?

19 Tutaendelea kupambana na taabu za ulimwengu huu mbovu mpaka tutakapokombolewa. Tunatamani sana wakati ambapo taabu hizo hazitakuwapo tena. (Zab. 55:6-8) Acheni tukumbuke kwamba tunapovumilia kwa uaminifu tunathibitisha kwamba Ibilisi ni mwongo. Na tutiwe nguvu na sala zetu na undugu wetu wa Kikristo, tukikumbuka kwamba ndugu zetu Wakristo wanapata majaribu kama yetu. Endelea kuwa na uwezo kamili na vifaa kamili kwa kutumia vizuri Neno la Mungu. Usiyumbe-yumbe kamwe katika kutegemea utunzaji wenye upendo wa “Mungu wa faraja yote.” Kumbuka kwamba “macho ya Yehova yanawaelekea waadilifu, na masikio yake yanakielekea kilio chao cha kuomba msaada.”—Zab. 34:15.

Je, Unaweza Kujibu?

• Daudi alihisi namna gani kuhusu taabu alizokabili?

• Mfalme Sulemani alikuwa na uhakika gani?

• Ni nini kinachoweza kutusaidia kukabiliana na hali ambazo Yehova anaruhusu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 13]

Sulemani alikuwa na hakika kwamba Yehova angewasaidia watu Wake wenye taabu

[Picha katika ukurasa wa 15]

Daudi alimtupia Yehova mzigo wake kupitia sala kisha akatenda kupatana na sala zake