Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kulinda Utambulisho Wetu wa Kikristo

Kulinda Utambulisho Wetu wa Kikristo

Kulinda Utambulisho Wetu wa Kikristo

“‘Ninyi ni mashahidi wangu,’ asema Yehova.”—ISAYA 43:10.

1. Ni watu wa aina gani ambao Yehova huwavuta kwake?

UNAPOKUWA kwenye Jumba la Ufalme, tazama kwa makini watu wanaokuzunguka. Unaona nani katika mahali hapo pa ibada? Huenda ukaona vijana wanyoofu wakisikiliza kwa makini hekima ya Biblia. (Zaburi 148:12, 13) Pia yaelekea utaona vichwa vya familia wanaojitahidi kumpendeza Mungu huku wakiishi katika ulimwengu usioheshimu maisha ya familia. Labda utaona wazee wapendwa, wanaoishi kupatana na wakfu wao kwa Yehova wakiwa imara licha ya matatizo yanayosababishwa na uzee. (Methali 16:31) Wote wanampenda sana Yehova. Naye aliona inafaa kuanzisha uhusiano pamoja nao. Mwana wa Mungu alisema hivi: “Hakuna mtu anayeweza kuja kwangu isipokuwa Baba, aliyenituma, amvute.”—Yohana 6:37, 44, 65.

2, 3. Kwa nini inaweza kuwa vigumu kudumisha utambulisho wa Kikristo ulio wazi?

2 Je, hatufurahi kuwa kati ya watu walio na kibali na baraka za Yehova? Hata hivyo, si rahisi kujitambulisha waziwazi kuwa Wakristo katika ‘nyakati hizi za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.’ (2 Timotheo 3:1) Inakuwa hivyo hasa kwa vijana ambao wanalelewa katika familia za Kikristo. Kijana mmoja alikiri hivi: “Ingawa nilikuwa nikihudhuria mikutano ya Kikristo, sikuwa na miradi hususa ya kiroho, na kwa kweli, sikuwa nimesitawisha tamaa ya kumtumikia Yehova.”

3 Wengine ambao huenda wakatamani kwa unyoofu kumtumikia Yehova, wanaweza kukengeushwa na msongo mkali wa marika, uvutano wa ulimwengu, na maelekeo ya dhambi. Tunapokuwa chini ya mkazo mwingi, huenda hatua kwa hatua tukapoteza utambulisho wetu wa Kikristo. Kwa mfano, leo watu wengi katika ulimwengu huona viwango vya Biblia vya maadili kuwa vimepitwa na wakati au visivyofaa katika ulimwengu wa kisasa. (1 Petro 4:4) Wengine huhisi kwamba si lazima kumwabudu Mungu kwa njia anayoonyesha. (Yohana 4:24) Katika barua yake kwa Waefeso, Paulo anautaja ulimwengu kuwa una “roho,” au mtazamo ulioenea. (Waefeso 2:2) Roho hiyo huweka mkazo juu ya watu ili wafikiri kama jamii isiyomjua Yehova.

4. Yesu alikaziaje uhitaji wa kulinda utambulisho wetu wa Kikristo ulio wazi?

4 Hata hivyo, tukiwa watumishi wa Yehova waliojiweka wakfu, tunatambua kwamba lingekuwa jambo la kuhuzunisha kwa yeyote kati yetu—kijana au mzee—kupoteza utambulisho wetu wa Kikristo. Kuwa na maoni yanayofaa kuhusu utambulisho wa Kikristo kunaweza kutegemea tu viwango vya Yehova na mambo anayotarajia kutoka kwetu. Hiyo ni kwa sababu tumeumbwa kwa mfano wake. (Mwanzo 1:26; Mika 6:8) Biblia inafananisha utambulisho wetu wa Kikristo ulio wazi na mavazi ya nje, yanayovaliwa ili kuonwa na wote. Kuhusu nyakati zetu, Yesu alionya hivi: “Tazama! Ninakuja kama mwizi. Mwenye furaha ni yule anayekaa macho na kutunza mavazi yake ya nje, ili asipate kutembea akiwa uchi na watu waitazame aibu yake.” * (Ufunuo 16:15) Hatungependa kuvua sifa zetu za Kikristo na viwango vya mwenendo na kuruhusu ulimwengu wa Shetani utufinyange. Ikiwa jambo hilo lingetokea, tungepoteza ‘mavazi hayo ya nje.’ Hali hiyo ingekuwa yenye kusikitisha na yenye kuaibisha.

5, 6. Kwa nini ni muhimu kuwa thabiti kiroho?

5 Utambulisho wa Kikristo ulio wazi huwa na matokeo makubwa sana juu ya maisha ya mtu. Jinsi gani? Mwabudu wa Yehova akipoteza utambulisho wake ulio wazi, huenda akakengeushwa na kukosa mwelekeo au miradi hususa. Biblia inatuonya mara kwa mara kuhusu hali kama hiyo ya kusitasita. Mwanafunzi Yakobo alionya hivi: “Yeye anayetia shaka ni kama wimbi la bahari linaloendeshwa na upepo na kupeperushwa huku na huku. Kwa kweli, mtu huyo asidhani kwamba atapokea kitu chochote kutoka kwa Yehova; yeye ni mtu anayesitasita, asiye imara katika njia zake zote.”—Yakobo 1:6-8; Waefeso 4:14; Waebrania 13:9.

6 Tunawezaje kulinda utambulisho wetu wa Kikristo? Ni nini kinachoweza kutusaidia kuboresha uwezo wa kutambua pendeleo letu kubwa la kuwa waabudu wa Aliye Juu Zaidi? Tafadhali chunguza njia zifuatazo.

Imarisha Kabisa Utambulisho Wako wa Kikristo

7. Kwa nini ni muhimu kumwomba Yehova atuchunguze?

7 Endelea kuimarisha uhusiano wako pamoja na Yehova. Kitu chenye thamani zaidi alicho nacho Mkristo ni uhusiano wake pamoja na Mungu. (Zaburi 25:14; Methali 3:32) Tukianza kuwa na shaka kuhusu utambulisho wetu wa Kikristo, tunapaswa kuchunguza kwa makini ubora na kina cha uhusiano huo. Kwa kufaa, mtunga-zaburi aliomba hivi: “Unichunguze, Ee Yehova, na kunijaribu; usafishe figo zangu na moyo wangu.” (Zaburi 26:2) Kwa nini ni muhimu kuchunguzwa na Yehova? Kwa sababu hatuwezi kuchanganua nia na maelekeo yetu ya ndani kabisa bila kukosea. Ni Yehova tu anayeweza kuelewa utu wetu wa ndani, yaani, nia yetu, mawazo yetu, na hisia zetu.—Yeremia 17:9, 10.

8. (a) Tunaweza kunufaikaje kwa kujaribiwa na Yehova? (b) Umesaidiwaje kufanya maendeleo ukiwa Mkristo?

8 Kwa kumwomba Yehova atuchunguze, tunamwalika atujaribu. Huenda akaruhusu hali fulani zitokee ambazo hufunua nia yetu ya kweli na hali yetu ya moyoni. (Waebrania 4:12, 13; Yakobo 1:22-25) Tunapaswa kukubali kujaribiwa kwa njia hiyo kwa sababu majaribu hutupa nafasi ya kuonyesha kina cha ushikamanifu wetu kwa Yehova. Kujaribiwa huko kunaweza kuonyesha kama tuko “kamili na timamu katika mambo yote, bila kukosa kitu chochote.” (Yakobo 1:2-4) Na tunapojaribiwa, tunaweza kukua kiroho.—Waefeso 4:22-24.

9. Kwa nini ni muhimu kujihakikishia kwamba yale ambayo Biblia hufundisha ni kweli? Eleza.

9 Jihakikishie kweli ya Biblia. Utambulisho wetu tukiwa watumishi wa Yehova unaweza kudhoofika usipotegemea kabisa ujuzi wa Biblia. (Wafilipi 1:9, 10) Kila Mkristo, kijana au mzee anahitaji kujihakikishia na kuridhika kwamba mambo anayoamini ndiyo kweli inayopatikana katika Biblia. Paulo aliwahimiza waamini wenzake hivi: “Hakikisheni mambo yote; shikeni sana yaliyo mazuri.” (1 Wathesalonike 5:21) Vijana Wakristo wanaotoka katika familia zinazomwogopa Mungu wanapaswa kutambua kwamba hawawezi kuwa Wakristo wa kweli kwa sababu tu ya imani ya wazazi wao. Daudi, baba ya Sulemani, alimhimiza ‘amjue Mungu wa baba yake, amtumikie kwa moyo kamili.’ (1 Mambo ya Nyakati 28:9) Haingetosha tu kijana Sulemani kutazama jinsi baba yake alivyositawisha imani katika Yehova. Alipaswa kumjua Yehova yeye mwenyewe, naye alifanya hivyo. Alimsihi Mungu hivi: “Sasa unipe hekima na ujuzi ili nitoke mbele ya watu hawa na ili niingie ndani.”—2 Mambo ya Nyakati 1:10.

10. Kwa nini si vibaya kuuliza maswali manyoofu kwa nia nzuri?

10 Imani yenye nguvu husitawishwa kupitia ujuzi. Paulo alisema: “Imani hufuata jambo lililosikiwa.” (Waroma 10:17) Alimaanisha nini? Alimaanisha kwamba kwa kujifunza Neno la Mungu, tunaimarisha imani yetu na uhakika wetu katika Yehova, ahadi zake, na tengenezo lake. Tunaweza kupata majibu yanayotoa uhakikisho kwa kujiuliza maswali manyoofu kuhusu Biblia. Isitoshe, kwenye Waroma 12:2, tunapata shauri hili la Paulo: “Mjihakikishie wenyewe mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.” Tunawezaje kufanya hivyo? Kwa kupata “ujuzi sahihi wa ile kweli.” (Tito 1:1) Roho ya Yehova inaweza kutusaidia kuelewa hata habari zilizo ngumu. (1 Wakorintho 2:11, 12) Tunapaswa kusali ili kupata msaada wa Mungu tunapokosa kuelewa jambo fulani. (Zaburi 119:10, 11, 27) Yehova anataka tuelewe Neno lake, tuliamini, na kulitii. Yeye hufurahia maswali manyoofu yanayoulizwa kwa nia nzuri.

Azimia Kumpendeza Mungu

11. (a) Ni tamaa gani ya asili inayoweza kutunasa? (b) Tunawezaje kupata ujasiri wa kupinga msongo wa marika?

11 Jitahidi kumpendeza Mungu, si mwanadamu. Ni jambo la kawaida kujitambulisha na kikundi fulani. Kila mtu anahitaji marafiki, na tunapokubaliwa na wengine tunafurahi na kuhisi usalama. Wakati wa kubalehe na pia baadaye maishani, msongo wa marika unaweza kuwa wenye nguvu na kumfanya mtu atake sana kuwaiga au kuwapendeza wengine. Lakini sikuzote marafiki na marika hawapendezwi na hali yetu nzuri. Nyakati nyingine wanataka tu mtu wa kushirikiana naye katika kufanya mabaya. (Methali 1:11-19) Mkristo anaposhindwa na msongo wa marika usiofaa, kwa kawaida yeye hujaribu kuficha utambulisho wake. (Zaburi 26:4) Mtume Paulo alionya hivi: “Usiruhusu ulimwengu unaokuzunguka ufinyange tabia yako.” (Waroma 12:2, The Jerusalem Bible) Yehova huandaa nguvu tunazohitaji ili kupinga mkazo wowote ambao hufanya tujipatanishe na ulimwengu.—Waebrania 13:6.

12. Ni kanuni na kielelezo gani kinachoweza kutuimarisha tuendelee kuwa thabiti katika imani tumaini letu katika Mungu linapohusika?

12 Mkazo unapotisha kuharibu utambulisho wetu wa Kikristo, tunapaswa kukumbuka kwamba ushikamanifu wetu kwa Mungu ni muhimu zaidi kuliko maoni au maelekeo ya wengi. Maneno haya ya Kutoka 23:2 hutumika kama kanuni ya kutulinda: “Usiufuate umati kwa ajili ya makusudio maovu.” Waisraeli wengi walipotilia shaka uwezo wa Yehova wa kutimiza ahadi Zake, Kalebu alikataa kwa uthabiti kufuata walio wengi. Alikuwa na uhakika kwamba ahadi za Mungu zilikuwa zenye kutegemeka, naye alithawabishwa sana kwa msimamo wake. (Hesabu 13:30; Yoshua 14:6-11) Je, wewe pia uko tayari kupinga mkazo unaotokana na maoni ya wengi ili kulinda uhusiano wako pamoja na Mungu?

13. Kwa nini ni jambo la hekima kuwajulisha wengine msimamo wetu wa Kikristo?

13 Jitambulishe kuwa Mkristo. Ule usemi kwamba kinga ni bora kuliko tiba unaweza kutumika pia tunapotetea utambulisho wetu wa Kikristo. Katika siku za Ezra, jitihada za Waisraeli waaminifu za kufanya mapenzi ya Yehova zilipopingwa, walisema hivi: “Sisi ni watumishi wa Mungu wa mbingu na dunia.” (Ezra 5:11) Tunaweza kuishiwa na nguvu kwa woga iwapo tutaathiriwa na jinsi watu wenye uadui wanavyoitikia na pia uchambuzi wao. Ikiwa sikuzote tutajaribu kumpendeza kila mtu, hatutakuwa na matokeo sana katika kujitambulisha. Kwa hiyo, usitishwe. Sikuzote ni vizuri kuwajulisha wengine waziwazi kwamba wewe ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Kwa heshima na kwa uthabiti, unaweza kuwaeleza wengine viwango, imani, na msimamo wako ukiwa Mkristo. Wajulishe wengine kwamba umeazimia kudumisha viwango vya Yehova vya juu kuhusu maadili. Wajulishe waziwazi kwamba huwezi kulegeza msimamo wako wa utimilifu wa Kikristo. Onyesha kwamba unajivunia viwango vyako vya maadili. (Zaburi 64:10) Kusimama imara ukiwa Mkristo kunaweza kukutia nguvu, kukulinda, na hata kuwachochea wengine watake kumjua Yehova na watu wake.

14. Je, tunapaswa kuvunjwa moyo na dhihaka au upinzani? Eleza.

14 Naam, huenda wengine wakakudhihaki au kukupinga. (Yuda 18) Wengine wasipoitikia vizuri jitihada zako za kuwaeleza viwango vyako, usivunjike moyo. (Ezekieli 3:7, 8) Hata uwe umeazimia kadiri gani, hutawasadikisha kamwe watu wasiotaka kusadikishwa. Mkumbuke Farao. Yeye hakusadiki kwamba Musa alikuwa akisema kwa niaba ya Yehova licha ya mapigo au miujiza, na hata kifo cha mzaliwa wake wa kwanza. Kwa hiyo, usiruhusu woga wa mwanadamu ufanye uishiwe na nguvu. Tumaini na imani katika Mungu zinaweza kutusaidia kushinda woga.—Methali 3:5, 6; 29:25.

Jifunze Kutokana na Yaliyopita, Jenga kwa Ajili ya Wakati Ujao

15, 16. (a) Urithi wetu wa kiroho ni nini? (b) Tunaweza kunufaikaje kwa kutafakari urithi wetu wa kiroho tukitumia Neno la Mungu?

15 Thamini urithi wako wa kiroho. Kwa kutumia Neno la Mungu, Wakristo watanufaika kwa kutafakari urithi wao mkubwa wa kiroho. Urithi huo unatia ndani kweli ya Neno la Yehova, tumaini la uzima wa milele, na pendeleo la kumwakilisha Mungu tukiwa watangazaji wa habari njema. Je, unaweza kuona daraka lako miongoni mwa Mashahidi wake, ambao wakiwa kikundi wana pendeleo la kufanya kazi ya kuhubiri Ufalme inayookoa uhai? Kumbuka kwamba Yehova tu ndiye anayetoa uhakikisho huu: “Ninyi ni mashahidi wangu.”—Isaya 43:10.

16 Unaweza kujiuliza maswali kama vile: ‘Urithi huo wa kiroho ni wenye thamani kadiri gani kwangu? Je, ninauthamini sana hivi kwamba ninatanguliza mapenzi ya Mungu maishani mwangu? Je, ninauthamini sana hivi kwamba unaniimarisha kupinga kishawishi chochote kinachoweza kufanya niupoteze?’ Pia urithi wetu wa kiroho unaweza kutupa hali ya usalama wa kiroho ambayo inaweza kupatikana tu katika tengenezo la Yehova. (Zaburi 91:1, 2) Kuchunguza matukio muhimu katika historia ya tengenezo la Yehova la kisasa kunaweza kukazia akilini mwetu uhakika wa kwamba hakuna mtu au kitu chochote kinachoweza kuwaondoa watumishi wa Yehova duniani.—Isaya 54:17; Yeremia 1:19.

17. Ni nini kingine kinachohitajiwa badala ya kutegemea tu urithi wetu wa kiroho?

17 Bila shaka, hatuwezi kutegemea tu urithi wetu wa kiroho. Lazima kila mmoja wetu asitawishe uhusiano wa karibu sana pamoja na Mungu. Baada ya Paulo kujitahidi sana kujenga imani ya Wakristo huko Filipi, aliwaandikia hivi: “Kwa hiyo, wapendwa wangu, kwa jinsi ambavyo mmekuwa mkitii sikuzote, si wakati wa kuwapo kwangu tu, bali kwa utayari zaidi sasa wakati wa kutokuwapo kwangu, endeleeni kuufanyia kazi wokovu wenu wenyewe kwa kuogopa na kutetemeka.” (Wafilipi 2:12) Hatuwezi kumtegemea mtu mwingine ili kupata wokovu.

18. Utendaji wa Kikristo unawezaje kuboresha utambulisho wetu wa Kikristo?

18 Shiriki katika utendaji wa Kikristo kadiri uwezavyo. Inasemekana kwamba “kazi huathiri sana utu wa mtu.” Leo Wakristo wamepewa kazi muhimu sana ya kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu uliosimamishwa. Paulo alisema: “Kwa maana kama nilivyo, kwa kweli, mtume kwa mataifa, naitukuza huduma yangu.” (Waroma 11:13) Kazi yetu ya kuhubiri hututofautisha na ulimwengu, na tunapoifanya tunaboresha utambulisho wetu wa Kikristo. Kushiriki katika utendaji mwingine wa Kikristo kadiri tuwezavyo, kama vile mikutano ya Kikristo, programu za kujenga mahali pa ibada, jitihada za kuwasaidia wenye uhitaji, na mambo kama hayo, kunaweza kuimarisha utambulisho wetu wa Kikristo.—Wagalatia 6:9, 10; Waebrania 10:23, 24.

Utambulisho Ulio Wazi Huleta Manufaa Halisi

19, 20. (a) Umepata manufaa gani binafsi kwa kuwa Mkristo? (b) Ni nini hutupa msingi wa utambulisho wa kweli?

19 Ebu fikiria kwa muda mfupi baraka nyingi na manufaa tunayopata kwa sababu ya kuwa Wakristo wa kweli. Tuna pendeleo la kutambuliwa kibinafsi na Yehova. Nabii Malaki alisema hivi: “Wale wenye kumwogopa Yehova wakasemezana, kila mmoja na mwenzake, na Yehova akaendelea kutoa uangalifu na kusikiliza. Na kitabu cha kumbukumbu kikaanza kuandikwa mbele zake kwa ajili ya wale wenye kumwogopa Yehova na kwa ajili ya wale wanaolifikiria jina lake.” (Malaki 3:16) Tunaweza kuonwa na Mungu kuwa marafiki wake. (Yakobo 2:23) Maisha yetu huboreshwa na kuwa na kusudi lililo wazi, yanakuwa na maana, na miradi inayofaa na yenye matokeo. Na tumepewa tumaini la kuishi milele wakati ujao.—Zaburi 37:9.

20 Kumbuka kwamba Mungu ndiye anayeamua jinsi ulivyo na thamani na pia utambulisho wako halisi wala si maoni ya watu. Huenda wengine wakatuona kulingana na viwango vya kibinadamu ambavyo vimepungukiwa. Lakini upendo wa Mungu na kupendezwa nasi binafsi hufanya tuwe wenye thamani halisi—sisi ni watu wake. (Mathayo 10:29-31) Kisha, upendo wetu kwa Mungu unaweza kutupa utambulisho na mwongozo ulio wazi zaidi maishani. “Ikiwa yeyote anampenda Mungu, huyo anajulikana naye.”—1 Wakorintho 8:3.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Huenda maneno hayo yakarejelea kwa njia isiyo ya moja kwa moja kazi za ofisa wa hekalu la mlimani huko Yerusalemu. Wakati wa makesha ya usiku alitembea hekaluni ili kuona ikiwa walinzi Walawi walikuwa macho au walikuwa wamelala mahali pao pa kazi. Mlinzi yeyote aliyepatikana amelala alipigwa kwa kijiti, na huenda mavazi yake ya nje yalichomwa kama adhabu ya kumwaibisha.

Je, Unakumbuka?

• Kwa nini ni muhimu Wakristo kulinda utambulisho wao wa kiroho?

• Tunawezaje kuimarisha kabisa utambulisho wetu wa Kikristo?

• Tunapokabili suala la ni nani tutakayempendeza, ni mambo gani yanayoweza kutusaidia tufanye uamuzi unaofaa?

• Utambulisho wetu ulio wazi unawezaje kuwa na matokeo juu ya wakati wetu ujao tukiwa Wakristo?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 21]

Kushiriki katika utendaji wa Kikristo kadiri tuwezavyo kunaweza kuboresha utambulisho wetu wa Kikristo