Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Ukilazimishwa Uingie Katika Utumishi’

‘Ukilazimishwa Uingie Katika Utumishi’

‘Ukilazimishwa Uingie Katika Utumishi’

“WEWE! Acha unachofanya na uje hapa mara moja unibebee furushi hili.” Unafikiri Myahudi mwenye shughuli nyingi katika karne ya kwanza angefanya nini ikiwa angeambiwa hivyo na askari-jeshi Mroma? Katika Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu alipendekeza hivi: “Mtu fulani aliye na mamlaka akikulazimisha uingie katika utumishi wa kilometa moja, nenda pamoja naye kilometa mbili.” (Mathayo 5:41) Wasikilizaji wa Yesu wangeelewaje shauri hilo? Nalo lapaswa kumaanisha nini kwetu leo?

Ili kupata majibu, tunahitaji kujua kilichomaanishwa na utumishi wa lazima katika nyakati za kale. Zoea hilo lilijulikana sana na wakaaji wa Israeli katika siku za Yesu.

Utumishi wa Lazima

Tangu karne ya 18 K.W.K., kumekuwa na uthibitisho kwamba kulikuwa na kazi ya lazima (au kazi ngumu ya kulazimishwa) katika Mashariki ya Karibu. Maandishi ya serikali kutoka jiji la kale la Siria la Alalakh yanataja vikundi vya watu walioandikishwa na serikali ili kufanya kazi za kibinafsi. Huko Ugarit, kwenye pwani ya Siria, wakulima waliokodi mashamba waliandikishwa ili kufanya kazi hizo isipokuwa waruhusiwe na mfalme kutozifanya.

Bila shaka, mara nyingi watu walioshindwa au kutekwa walipewa mgawo wa kufanya kazi ya lazima. Wasimamizi wa kazi Wamisri waliwalazimisha Waisraeli wawatumikie kwa kutengeneza matofali. Baadaye, Waisraeli waliwatumikisha Wakanaani waliokuwa katika Nchi ya Ahadi, na mazoea hayo yaliendelezwa na Daudi na Sulemani.—Kutoka 1:13, 14; 2 Samweli 12:31; 1 Wafalme 9:20, 21.

Waisraeli walipoomba wapewe mfalme, Samweli aliwaeleza fungu ambalo lingekuwa haki ya mfalme. Angechukua raia zake kutumika kama waendesha-magari na wapanda-farasi, walime na kuvuna, watengeneze silaha, na kadhalika. (1 Samweli 8:4-17) Hata hivyo, wakati hekalu la Yehova lilipokuwa likijengwa, huku wageni wakitumikishwa katika kazi ya lazima, “Sulemani hakumfanya yeyote kati ya wana wa Israeli kuwa mtumwa; kwa maana wao walikuwa ndio mashujaa wa vita na watumishi wake na wakuu wake na maamiri wasaidizi wake na wakuu wa waendesha-magari wake na wakuu wa wapanda-farasi wake.”—1 Wafalme 9:22.

Andiko la 1 Wafalme 5:13, 14 linasema hivi kuhusu Waisraeli walioajiriwa katika miradi ya ujenzi: “Mfalme Sulemani akaendelea kuwaleta wale wote walioandikishwa kufanya kazi ya kulazimishwa kutoka katika Israeli yote; na wale walioandikishwa kufanya kazi ya kulazimishwa jumla yao ikawa watu 30,000. Naye akawa akiwapeleka Lebanoni kwa zamu za 10,000 kwa mwezi. Wakaendelea kukaa katika Lebanoni kwa mwezi mmoja, na kwa miezi miwili nyumbani kwao.” Msomi mmoja anasema: “Hakuna shaka yoyote kwamba wafalme wa Israeli na Yuda walitumia vikundi vya wale waliofanya kazi za lazima ili wawafanyie kazi bila malipo kwenye majengo yao na kwenye mashamba yaliyomilikiwa na mfalme.”

Mzigo huo ulikuwa mzito wakati wa utawala wa Sulemani. Mzigo huo ulikuwa wenye kulemea sana hivi kwamba wakati Rehoboamu alipotisha kuuongeza, Waisraeli wote waliasi na kumpiga kwa mawe ofisa aliyewekwa juu ya wale walioandikishwa kufanya kazi ya kulazimishwa. (1 Wafalme 12:12-18) Hata hivyo, kazi ya kulazimishwa bado iliendelea. Asa, mjukuu wa kiume wa Rehoboamu, aliita watu wa Yuda kujenga majiji ya Geba na Mispa, na “hakuna yeyote aliyeachwa.”—1 Wafalme 15:22.

Chini ya Utawala wa Roma

Mahubiri ya Mlimani yanaonyesha kwamba Wayahudi wa karne ya kwanza walijua kwamba wangeweza ‘kulazimishwa kuingia katika utumishi.’ Maneno hayo yametafsiriwa kutokana na neno la Kigiriki ag·ga·reuʹo, ambalo hapo awali lilihusianishwa na kazi iliyofanywa na wajumbe Waajemi. Walikuwa na mamlaka ya kutumia kwa nguvu wanaume, farasi, meli, au kitu kingine chochote walichohitaji ili kuharakisha shughuli za umma.

Katika siku za Yesu, Israeli ilitawaliwa na Waroma, ambao walikuwa na mfumo kama huo. Katika mikoa ya Nchi za Mashariki, mbali na kodi za kawaida, watu wangeweza kulazimishwa kufanya kazi kwa ukawaida au katika hali zisizo za kawaida. Bila shaka, wengi hawangependa kazi hizo. Isitoshe, lilikuwa jambo la kawaida kwa wanyama, madereva, au magari ya kukokotwa kuchukuliwa kwa nguvu ili kusafirisha maofisa wa Serikali. Kulingana na mwanahistoria Michael Rostovtzeff, watu wenye mamlaka “walijaribu kudhibiti na kupanga [desturi hiyo] katika utaratibu fulani, lakini hawakufanikiwa, kwa kuwa maadamu desturi hiyo iliendelea kuwapo, ilitokeza madhara. Sheria nyingi zilitolewa na manaibu wa maliwali waliojaribu kwa unyoofu kukomesha utumizi mbaya wa mamlaka na ukandamizaji ambao ulikuwa kawaida ya mfumo huo . . . Lakini desturi hiyo iliendelea kuwakandamiza watu.”

“Mtu yeyote angeweza kulazimishwa kubeba mzigo wa askari kwa umbali fulani,” asema msomi mmoja Mgiriki, na “mtu yeyote angeweza kulazimishwa kufanya utumishi wowote ambao Waroma waliamua.” Hivyo ndivyo ilivyokuwa kwa Simoni wa Kirene, ambaye askari-jeshi Waroma ‘walimlazimisha’ kubeba mti wa mateso wa Yesu.—Mathayo 27:32.

Pia vitabu vya Marabi vinataja desturi hiyo iliyochukiwa. Kwa mfano, rabi mmoja alikamatwa ili asafirishe mihadasi hadi kwenye jumba fulani la mfalme. Wafanyakazi wangeweza kuchukuliwa kutoka kwa waajiri wao na kupewa kazi nyingine, na bado waajiri walipaswa kuwalipa mishahara yao. Wanyama wa kubeba mizigo au ng’ombe wangeweza kuchukuliwa kwa nguvu. Ikiwa wangerudishwa, yaelekea wangekuwa katika hali mbaya hivi kwamba hawangeweza kufanya kazi tena. Unaweza kuelewa ni kwa nini watu waliona kutwaliwa kwa wanyama wao kwa muda kuwa kana kwamba walichukuliwa kabisa. Hivyo, methali moja ya Kiyahudi ilisema: “Angareia ni kama kifo.” Mwanahistoria mmoja anasema: “Kijiji kingeweza kuharibiwa kwa sababu ya kuchukuliwa kinguvu kwa ng’ombe wa kulima kwa ajili ya utumishi wa lazima badala ya kuchukuliwa kwa wanyama wa kubeba mizigo.”

Unaweza kuwazia jinsi utumishi huo ulivyochukiwa hasa kwa kuwa mara nyingi wale waliowalazimisha walikuwa na kiburi na hawakufuata haki. Kwa kufikiria chuki waliyokuwa nayo kuelekea serikali za watu wasio Wayahudi ambazo ziliwatawala, Wayahudi walichukia sana aibu ya kulazimishwa kufanya kazi hizo zenye kukera. Leo hakuna sheria inayotueleza kihususa umbali ambao raia angeweza kulazimishwa kubeba mzigo. Yaelekea wengi hawangekubali kwenda hatua moja zaidi ya ile iliyotakiwa na sheria.

Hata hivyo, hii ndiyo desturi ambayo Yesu alikuwa akitaja aliposema: “Mtu fulani aliye na mamlaka akikulazimisha uingie katika utumishi wa kilometa moja, nenda pamoja naye kilometa mbili.” (Mathayo 5:41) Walipomsikia akisema hivyo, lazima wengine wawe walifikiri kwamba hakuwa na busara. Kwa kweli alimaanisha nini?

Jinsi Wakristo Wanavyopaswa Kuitikia

Kwa ufupi, Yesu alikuwa akiwaambia wasikilizaji wake kwamba ikiwa wangelazimishwa kufanya kazi fulani halali na wenye mamlaka, wangepaswa kuifanya kwa kupenda na bila hasira. Hivyo wangemlipa “Kaisari vitu vya Kaisari” bila kupuuza daraka la kumlipa “Mungu vitu vya Mungu.”—Marko 12:17. *

Isitoshe, mtume Paulo aliwahimiza hivi Wakristo: “Kila nafsi na ijitiishe kwa mamlaka zilizo kubwa, kwa maana hakuna mamlaka isipokuwa kwa njia ya Mungu; mamlaka zilizopo zimesimamishwa na Mungu katika vyeo vyao vya kadiri. Kwa hiyo yeye anayepinga mamlaka amechukua msimamo kupingana na mpango wa Mungu . . . Ikiwa unafanya mabaya, ogopa: kwa maana haichukui upanga bila kusudi.”—Waroma 13:1-4.

Hivyo, Yesu na Paulo walikubali kwamba mfalme au serikali ilikuwa na haki ya kuadhibu wale waliovunja amri zao. Adhabu ya aina gani? Mwanafalsafa Mgiriki Epictetus, wa karne ya kwanza na ya pili W.K., anatoa jibu moja: “Uhitaji usiotazamiwa unapotokea na askari achukue mwana-punda wako, mwachie. Usishindane naye, usilalamike, usije ukapigwa makonde na pia kumpoteza punda wako.”

Hata hivyo, pindi fulani katika nyakati za kale na sasa, Wakristo wamehisi kwamba hawawezi kutii amri za serikali kwa dhamiri nzuri. Wakati mwingine matokeo yamekuwa mabaya. Wakristo fulani wamehukumiwa kifo. Wengine wamefungwa gerezani kwa miaka mingi kwa sababu ya kukataa kushiriki katika mambo ambayo waliona kuwa yatafanya wavunje msimamo wao wa kutokuwamo. (Isaya 2:4; Yohana 17:16; 18:36) Kwenye pindi nyingine, Wakristo wamehisi kwamba wanaweza kukubali kufanya mambo wanayoambiwa wafanye. Kwa mfano, Wakristo fulani huhisi kwamba wanaweza kwa dhamiri safi kufanya kazi fulani za kunufaisha jamii ambazo si za kijeshi chini ya usimamizi wa serikali. Huenda kazi hizo zikatia ndani kuwasaidia walio wazee au wasiojiweza, kutumika kama wazima-moto, kusafisha fuo, kufanya kazi bustanini, misituni, au kwenye maktaba, na kadhalika.

Kwa kawaida, hali hutofautiana katika nchi mbalimbali. Kwa hiyo, ili kuamua kutii au kutotii amri hizo, kila Mkristo anapaswa kufuata dhamiri yake iliyozoezwa na Biblia.

Kwenda Kilometa ya Pili

Kanuni ambayo Yesu alifundisha ya kuwa tayari kufanya kazi zilizo halali, haihusu tu matakwa ya serikali bali pia shughuli za wanadamu za kila siku. Kwa mfano, huenda mtu mwenye mamlaka juu yako akakuomba ufanye kazi fulani usiyoipenda lakini ambayo haipingani na sheria ya Mungu. Utafanyaje? Huenda ukakasirika na kuhisi kwamba anakupotezea wakati na nguvu zako isivyo lazima. Huenda kufanya hivyo kukatokeza uadui. Kwa upande mwingine, ukikubali huku ukiwa umenuna, huenda ukapoteza amani yako ya moyoni. Suluhisho ni nini? Fanya kama vile Yesu alivyopendekeza, yaani, nenda kilometa ya pili. Usifanye tu kazi ambayo umeombwa kufanya, bali fanya zaidi ya hiyo. Ifanye kwa kupenda. Ukiwa na mtazamo huo, hutahisi kwamba unatendewa vibaya, na bado utaendelea kuwa na uhuru wa kufanya utakavyo.

Mwandishi mmoja anasema hivi: “Katika maisha yao yote, watu wengi hufanya tu mambo ambayo wamelazimishwa kufanya. Watu hao huona kuwa maisha ni magumu, nao huwa wamechoka daima. Wengine hufanya zaidi ya yale waliyopaswa kufanya, na kujitoa kwa hiari.” Kwa kweli, katika hali nyingi, mtu anaweza kuamua kwenda kilometa moja tu kwa kulazimishwa—au mbili. Akienda kilometa moja, huenda akadai haki zake. Akienda kilometa mbili, huenda akathawabishwa sana. Wewe ni nani kati ya hao? Huenda ukawa mwenye furaha na mwenye matokeo zaidi ikiwa hutaona kazi ambazo umepewa kuwa wajibu tu au mambo unayopaswa kufanya, bali mambo ambayo unataka kufanya.

Namna gani ikiwa una mamlaka? Ni wazi kwamba, si jambo la upendo wala la Kikristo kutumia mamlaka yako kuwalazimisha wengine wafanye mambo unayowaambia. Yesu alisema: “Watawala wa mataifa hupiga ubwana juu yao na wakuu hutumia mamlaka juu yao.” Lakini hiyo si njia ya Kikristo. (Mathayo 20:25, 26) Ingawa huenda mtu mwenye mamlaka akadai kwa nguvu jambo fulani lifanywe na likafanywa, kutakuwa na mahusiano mazuri zaidi kati ya wote wanaohusika ikiwa maombi yatatolewa kwa fadhili na kwa njia inayofaa na wale wanaoombwa watakubali kwa heshima na kwa furaha. Naam, kuwa tayari kwenda kilometa mbili badala ya moja kunaweza kufanya maisha yako yawe yenye kuthawabisha kwelikweli.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 18 Kwa habari kamili kuhusu kinachomaanishwa kwa Wakristo ‘kumlipa Kaisari vitu vya Kaisari, lakini Mungu vitu vya Mungu,’ ona Mnara wa Mlinzi, Mei 1, 1996, ukurasa wa 15-20.

[Sanduku katika ukurasa wa 25]

JINSI KAZI YA KULAZIMISHWA ILIVYOTUMIWA VIBAYA ZAMANI

Sheria zilizowekwa ili kuzuia matumizi mabaya ya kazi ya kulazimishwa zinaonyesha kwamba mara nyingi kazi hiyo ilitumiwa kama kisingizio cha kupata huduma bila malipo. Mnamo mwaka wa 118 K.W.K., Ptolemy Euergetes wa Pili wa Misri alitoa amri kwamba maofisa “hawatamlazimisha mkaaji yeyote wa nchi hiyo kuwafanyia kazi za kibinafsi au kuchukua ng’ombe wao kwa matumizi ya kibinafsi.” Isitoshe: “Hakuna mtu atakayechukua . . . mashua ili kuitumia kwa faida yake kwa kisingizio chochote kile.” Katika maandishi ya mwaka wa 49 W.K., kwenye Hekalu la Great Oasis, Misri, naibu wa liwali Mroma Vergilius Capito alikiri kwamba askari-jeshi walikuwa wamechukua vitu kwa njia isiyo halali, naye alihakikisha kwamba “hakuna mtu atakayechukua . . . chochote, isipokuwa niwe nimemwandikia barua ya kumruhusu.”

[Picha katika ukurasa wa 24]

Simoni wa Kirene alilazimishwa kuingia katika utumishi

[Picha katika ukurasa wa 26]

Mashahidi wengi wamekaa gerezani kwa muda mrefu kwa sababu ya kushikilia msimamo wao wa Kikristo