Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, “Ukristo” Wenye Kubadilika-Badilika-Unakubaliwa na Mungu?

Je, “Ukristo” Wenye Kubadilika-Badilika-Unakubaliwa na Mungu?

Je, “Ukristo” Wenye Kubadilika-Badilika-Unakubaliwa na Mungu?

TUSEME umempa mchoraji kazi ya kuchora picha yako. Anapomaliza, unafurahi; picha hiyo inafanana na sura yako kabisa. Unawafikiria watoto wako, wajukuu wako, na wajukuu wao wakiitazama kwa furaha kubwa.

Hata hivyo, vizazi kadhaa baadaye mmoja wa wazao wako anaona nywele ambazo zimepungua kwenye utosi hazipendezi, hivyo anafanya ziongezwe. Mwingine anaona pua lako halipendezi na anafanya libadilishwe. Vizazi vinavyofuata vinafanya “marekebisho” mengine hivi kwamba mwishowe picha hiyo inakuwa tofauti na sura yako. Kama ungalijua wangalifanya hivyo, ungalihisije? Yaelekea ungaliudhika sana.

Kwa kusikitisha, picha hiyo yaonyesha hasa vile hali ilivyo katika kanisa ambalo ni la Kikristo kwa jina tu. Historia yaonyesha kwamba punde baada ya kifo cha mitume wa Kristo, “Ukristo” rasmi ulianza kubadilika, kama vile Biblia ilivyotabiri.—Mathayo 13:24-30, 37-43; Matendo 20:30. *

Bila shaka, ni jambo lifaalo kabisa kutumia kanuni za Biblia katika tamaduni tofauti-tofauti na vizazi tofauti-tofauti. Ni jambo lisilofaa kabisa kubadili mafundisho ya Biblia ili yapatane na maoni ya wengi. Na hivyo ndivyo imefanyika. Kwa mfano, fikiria jinsi ambavyo mafundisho kadhaa muhimu yamebadilishwa.

Kanisa Laungana na Serikali

Yesu alifundisha kwamba utawala, au Ufalme wake, ni wa mbinguni na, kwa wakati ufaao, utaharibu tawala zote za wanadamu na utawale juu ya dunia yote. (Danieli 2:44; Mathayo 6:9, 10) Hautatawala kupitia mifumo ya kisiasa ya wanadamu. “Ufalme wangu si sehemu ya ulimwengu huu,” Yesu akasema. (Yohana 17:16; 18:36) Hivyo, ingawa wanafunzi wa Yesu walitii sheria, wao walijiepusha na siasa.

Hata hivyo, kufikia wakati wa Maliki Konstantino wa Roma katika karne ya nne, wengi waliodai kuwa Wakristo walikosa subira katika kungojea kurudi kwa Kristo na kusimamishwa kwa Ufalme wa Mungu. Polepole, maoni yao kuhusu siasa yakabadilika. “Kabla ya Konstantino,” chasema kitabu Europe—A History, “Wakristo hawakujaribu kutwaa mamlaka [ya kisiasa] ili kuendeleza harakati zao. Baada ya Konstantino, Ukristo na mamlaka za juu za kisiasa zikaungana.” Ukristo huo uliokuwa umebadilishwa ukawa dini rasmi ya “watu wote,” au “katoliki,” ya Milki ya Roma.

Ensaiklopedia Great Ages of Man yasema kwamba kwa sababu ya muungano huo wa Kanisa na Serikali, “kufikia mwaka wa 385 A.D., miaka 80 tu baada ya mnyanyaso mkubwa wa mwisho dhidi ya Wakristo, Kanisa lenyewe lilikuwa linaanza kuwaua wazushi, na makasisi wake walikuwa na uwezo uliokuwa karibu kutoshana na uwezo wa maliki.” Hivyo, huo ukawa mwanzo wa enzi ambamo upanga, badala ya ushawishi, ulitumiwa kugeuza imani za watu, na makasisi wenye majina ya vyeo na wenye kupenda ukubwa wakachukua mahali pa wahubiri wanyenyekevu wa karne ya kwanza. (Mathayo 23:9, 10; 28:19, 20) Mwanahistoria H. G. Wells aliandika juu ya “tofauti kubwa iliyoko kati ya” Ukristo wa karne ya nne “na mafundisho ya Yesu wa Nazareti.” ‘Tofauti hizo kubwa’ hata ziliathiri mafundisho ya msingi kuhusu Mungu na Kristo.

Mafundisho Kuhusu Mungu Yabadilika

Kristo na wanafunzi wake walifundisha kwamba kuna ‘Mungu mmoja tu Baba,’ anayetambuliwa kwa jina lake binafsi, Yehova, ambalo laonekana mara 7,000 hivi katika hati za zamani za Biblia. (1 Wakorintho 8:6; Zaburi 83:18) Yesu aliumbwa na Mungu; yeye ni “mzaliwa wa kwanza wa kila kiumbe,” yasema Biblia ya Douay Version ya Wakatoliki kwenye Wakolosai 1:15. Hivyo, akiwa kiumbe Yesu alisema wazi hivi: “Baba ni mkubwa zaidi kuliko mimi.”—Yohana 14:28.

Lakini kufikia karne ya tatu, makasisi fulani wenye uwezo waliopenda sana fundisho la utatu la Pilato, mwana-falsafa Mgiriki aliyekuwa mpagani, walianza kubadili mafundisho kuhusu Mungu ili kumfanya awe sehemu ya Utatu. Katika karne zilizofuata, fundisho hilo likamkweza Yesu kinyume cha Maandiko na kumfanya kuwa sawa na Yehova na kuifanya roho takatifu ya Mungu, au kani ya utendaji, kuwa mtu.

Kuhusu kukubali kwa kanisa dhana ya Utatu, kichapo New Catholic Encyclopedia chasema hivi: “Tungo hili ‘Mungu mmoja katika Watu watatu’ halikuwa na msingi imara, hata halikukubaliwa kabisa katika maisha na imani ya Kikristo, kabla ya karne ya nne kumalizika. Lakini tungo hilo hasa ndilo la kwanza kabisa kuitwa fundisho la Utatu. Miongoni mwa Mababa wa Kimitume, hakukuwa na jambo lolote lenye kukaribia maoni yoyote ya aina hiyo.”

Vivyo hivyo, kichapo The Encyclopedia Americana chasema: “Fundisho la Utatu la karne ya nne halikuonyesha kwa usahihi fundisho la mapema la Kikristo kuhusu utu wa Mungu; bali lilipotoa fundisho hilo.” Kichapo The Oxford Companion to the Bible huutaja Utatu kuwa mojawapo ya “imani [kadhaa] zilizotungwa baadaye.” Hata hivyo, Utatu haukuwa ndio dhana pekee ya kipagani iliyokubaliwa katika kanisa.

Mafundisho Kuhusu Nafsi Yabadilika

Leo watu wengi wanaamini kwamba wanadamu wana nafsi isiyoweza kufa ambayo hubaki hai baada ya mwili kufa. Lakini je, unajua kwamba fundisho hilo la kanisa pia liliongezwa baadaye? Yesu alithibitisha kweli ya Biblia kwamba wafu “hawajui neno lo lote,” yaani wamelala usingizi. (Mhubiri 9:5; Yohana 11:11-13) Uhai unarudishwa kupitia ufufuo—‘kusimama tena’ kutoka katika usingizi wa kifo. (Yohana 5:28, 29) Nafsi isiyoweza kufa, ikiwa ingalikuwako, haingalihitaji kufufuliwa, kwa kuwa hali ya kutoweza kufa huzuia kifo.

Yesu hata alithibitisha fundisho la Biblia la ufufuo kwa kufufua watu kutoka kwa wafu. Ebu fikiria mfano wa Lazaro, aliyekuwa mfu kwa siku nne. Yesu alipomfufua, Lazaro alitoka kaburini akiwa binadamu hai anayepumua. Wakati alipofufuka, hakuna nafsi isiyoweza kufa ambayo ilitoka katika paradiso ya mbinguni, ikarudi ndani ya mwili wake. Kama hali ilikuwa hivyo, Yesu hakumtendea kwa fadhili kwa kumfufua!—Yohana 11:39, 43, 44.

Basi, nadharia ya nafsi isiyoweza kufa ilianzaje? Kichapo The Westminster Dictionary of Christian Theology chasema kwamba dhana hiyo “yatokana zaidi na falsafa ya Kigiriki kuliko ufunuo wa Biblia.” Kichapo The Jewish Encyclopedia chaeleza: “Itikadi kwamba nafsi huendelea kuwa hai baada ya mwili kufa haitokani na imani safi, bali yatokana na udadisi wa kifalsafa au wa kitheolojia, kwa hiyo haifundishwi waziwazi mahali popote katika Maandiko Matakatifu.”

Mara nyingi, uwongo mmoja huongoza kwenye uwongo mwingine, na ndivyo ilivyo na fundisho juu ya nafsi isiyoweza kufa. Fundisho hilo lilitokeza ile dhana ya kipagani juu ya kuteswa milele katika helo yenye moto. * Hata hivyo, Biblia yasema wazi kwamba “mshahara ambao dhambi hulipa ni kifo”—si kuteswa milele. (Waroma 6:23) Hivyo, inapoelezea ufufuo, Biblia ya King James Version yasema: “Bahari iliwatoa wafu waliokuwamo ndani yake; na kifo na helo zikawatoa wafu waliokuwamo ndani yake.” Vilevile, Biblia ya Douay yasema kwamba “bahari . . . na kifo na helo ziliwatoa wafu wao.” Naam, kwa ufupi, wale walio katika helo wamekufa, ‘wamelala usingizi,’ kama Yesu alivyosema.—Ufunuo 20:13.

Je, unaamini kwelikweli kwamba fundisho la kuhukumiwa kukaa helo milele huvuta watu kwa Mungu? La. Watu wenye haki na wenye upendo huliona kuwa wazo lenye kuchukiza! Kwa upande mwingine, Biblia hufundisha kwamba “Mungu ni upendo” na kwamba ukatili, hata kwa wanyama, humchukiza sana.—1 Yohana 4:8; Mithali 12:10; Yeremia 7:31; Yona 4:11.

Kuubadili Ukristo Leo

Kubadili mafundisho kuhusu Mungu na Ukristo kunaendelea leo. Hivi majuzi, profesa mmoja wa dini alitaja shindano katika kanisa lake la Kiprotestanti kuwa shindano “la mamlaka ya Maandiko na kanuni za imani dhidi ya mamlaka ya kigeni na dhana za kibinadamu, na uaminifu wa kanisa kwa ukichwa wa Kristo dhidi ya kurekebisha na kuubadili Ukristo ili upatane na maoni ya kizazi fulani. Jambo linaloshindaniwa ni hili: Ni nani anayeamua kanisa linafuata nini . . . Je, ni Maandiko Matakatifu au ni dhana inayokubaliwa wakati huo?”

Kwa kusikitisha, “dhana inayokubaliwa wakati huo” bado ndiyo huelekea kushinda. Kwa mfano, ni wazi kwamba makanisa mengi yamebadili msimamo wao kuhusu masuala mbalimbali ili yaonekane kwamba yanapenda maendeleo na yako tayari kukubali mawazo mapya. Hasa katika mambo ya kiadili, makanisa yamekuwa yenye kupendelea sana mabadiliko, kama ilivyotajwa katika makala ya kwanza. Lakini Biblia inasema wazi kwamba uasherati, uzinzi, na ugoni-jinsia moja ni dhambi nzito mbele za Mungu na kwamba wale wafanyao dhambi hizo “hawatarithi ufalme wa Mungu.”—1 Wakorintho 6:9, 10; Mathayo 5:27-32; Waroma 1:26, 27.

Mtume Paulo alipoandika maneno yaliyonukuliwa juu, Wagiriki na Waroma ambao aliishi miongoni mwao walifanya uovu wa kila aina. Paulo angesababu hivi: “Mungu aliteketeza Sodoma na Gomora kwa sababu ya dhambi nzito za kingono, lakini alifanya hivyo miaka 2,000 iliyopita! Bila shaka, hawezi kufanya hivyo katika kizazi hiki kilichoelimika.’ Lakini hakusababu hivyo; alikataa kuipotosha kweli ya Biblia.—Wagalatia 5:19-23.

Tazama Ukristo wa Awali

Akizungumza na viongozi wa dini ya Kiyahudi wa wakati wake, Yesu alisema kwamba ibada yao ni ‘bure kwa sababu walifundisha amri za watu kuwa mafundisho.’ (Mathayo 15:9) Viongozi hao wa kidini waliifanyia Sheria ya Yehova, iliyotolewa kupitia Musa, jambo lilelile ambalo makasisi wa Jumuiya ya Wakristo waliyafanyia, na bado wanayafanyia, mafundisho ya Kristo—walifunika kweli ya Mungu kwa mapokeo. Lakini Yesu aliondoa uwongo wote kwa manufaa ya watu wenye mioyo minyofu. (Marko 7:7-13) Yesu alisema kweli, iwe ilipendwa au la. Sikuzote neno la Mungu lilikuwa ndilo mamlaka yake.— Yohana 17:17.

Yesu ni tofauti kama nini na wengi ambao hudai kuwa Wakristo! Kwa kweli, Biblia ilitabiri: “Watu watatamani sana mambo mapya na kukusanya . . . walimu kulingana na mapendezi yao; kisha badala ya kusikiliza kweli, watageukia hekaya.” (2 Timotheo 4:3, 4, The Jerusalem Bible) Baadhi ya “hekaya” hizo ambazo tumechunguza zinaharibu kiroho, ilhali Neno la Mungu hujenga, nalo huongoza kwenye uhai udumuo milele. Hiyo ndiyo kweli ambayo Mashahidi wa Yehova wanakutia moyo uichunguze.—Yohana 4:24; 8:32; 17:3.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Katika mfano wa ngano na magugu na wa barabara pana na yenye kufinyana (Mathayo 7:13, 14), Yesu alionyesha kwamba katika enzi zote ni watu wachache tu ambao wangeendelea kufuata Ukristo wa kweli. Hata hivyo, watu wengi walio kama magugu ambao wangejiendeleza na kuendeleza mafundisho yao kuwa eti Ukristo halisi, wangefanya iwe vigumu kuwatambua Wakristo wa kweli. Hali hiyo ndiyo inayozungumziwa katika makala yetu.

^ fu. 19 “Helo” limetafsiriwa kutoka kwa neno la Kiebrania Sheoli na neno la Kigiriki Hadesi, maneno hayo mawili yanamaanisha tu “kaburi.” Hivyo, ingawa watafsiri wa Kiingereza wa Biblia ya King James Version walitafsiri neno Sheoli mara 31 kuwa “helo,” pia walilitafsiri mara 31 kuwa “kaburi” na mara 3 kuwa “shimo,” hivyo wakionyesha kwamba kwa ujumla maneno hayo yana maana moja tu.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 7]

Chanzo cha Jina Mkristo

Kwa angalau miaka kumi baada ya kifo cha Yesu, wafuasi wake walijulikana kuwa watu wa “Ile njia.” (Matendo 9:2; 19:9, 23; 22:4) Kwa nini? Kwa sababu imani katika Yesu Kristo, ambaye ndiye “njia na kweli na uhai,” ndiyo iliyokuwa jambo muhimu zaidi maishani mwao. (Yohana 14:6) Ndipo wakati fulani baada ya mwaka wa 44 W.K., huko Antiokia ya Siria, wanafunzi wa Yesu ‘kwa uongozi wa kimungu wakaitwa Wakristo.’ (Matendo 11:26) Jina hilo lilikubaliwa upesi, hata miongoni mwa maofisa wa umma. (Matendo 26:28) Jina hilo jipya halikubadili njia ya maisha ya Kikristo, ambayo iliendelea kufuata kigezo cha Kristo.—1 Petro 2:21.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Kwa huduma yao ya hadharani, Mashahidi wa Yehova huelekeza watu kwenye Neno la Mungu, Biblia

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 4]

Tatu kutoka kushoto: United Nations/Photo by Saw Lwin