Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Muziki Unaomfurahisha Mungu

Muziki Unaomfurahisha Mungu

Muziki Unaomfurahisha Mungu

Muziki umefafanuliwa kuwa “mojawapo ya sanaa za zamani zaidi na za asili zaidi.” Kama lugha, muziki ni zawadi ya ajabu ambayo hutofautisha wanadamu na wanyama. Muziki huchochea hisia. Muziki unaweza kukufurahisha, unaweza kudumu akilini. Zaidi ya yote, muziki unaweza kumfurahisha Mungu.

KAMA Biblia ionyeshavyo, Waisraeli walipenda muziki. Muziki ulikuwa “sanaa maarufu nyakati za kale za Biblia,” kichapo Unger’s Bible Dictionary chasema. Ukiwa sehemu ya maisha ya kila siku, muziki wa kuimbwa na muziki wa ala ulitumiwa katika ibada yao. Lakini muziki wa kuimbwa ndio uliotumiwa zaidi.

Mfalme Daudi aliweka rasmi wawakilishi miongoni mwa Walawi “juu ya kazi ya kuimba” katika tabenakulo, kabla ya kuzinduliwa kwa hekalu lililojengwa na Solomoni mwana wake. (1 Mambo ya Nyakati 6:31, 32) Wakati sanduku la agano, lililowakilisha kuwapo kwa Yehova, lilipofika Yerusalemu, Daudi aliwatayarisha baadhi ya Walawi ili “wamfanyie ukumbusho, na shukrani, na sifa, BWANA.” Waliimba pamoja na kupiga ‘vinanda na vinubi, na matoazi, na baragumu.’ Watu hao ‘walitajwa majina, ili kumshukuru BWANA, kwa kuwa fadhili zake ni za milele.’—1 Mambo ya Nyakati 16:4-6, 41; 25:1.

Korasi “fadhili za [Yehova] ni za milele” yapatikana mara nyingi katika Zaburi, kitabu cha Biblia kinachohusianishwa sana na muziki. Kwa mfano, korasi hiyo inafanyiza sehemu ya pili ya kila mstari katika mistari 26 ya Zaburi 136. “Ufupi wake huifanya iwe rahisi kuimbwa na watu,” asema msomi mmoja wa Biblia. “Yeyote ambaye ameisikia anaweza kuikumbuka.”

Maandishi yanayotangulia sura fulani za zaburi yaonyesha kwamba ala za muziki zilitumiwa sana. Zaburi 150 hutaja baragumu, kinubi, matari, filimbi, na matoazi, mbali na vinanda. Hata hivyo, watu hasa ndio wanaosihiwa waimbe. Mstari wa 6 wahimiza: “Kila mwenye pumzi na amsifu BWANA. Haleluya.”

Kwa kuwa muziki unadhihirisha hisia zetu, mawazo ya huzuni yalichochea watu kuimba nyimbo za maombolezo au za kurudia-rudia nyakati za Biblia. Hata hivyo, nyimbo za aina hiyo hazikuwa nyingi katika orodha ya muziki wa Waisraeli. “Ni wakati wa kuomboleza tu ambapo watu walipendelea nyimbo za kurudia-rudia badala ya muziki wenye sauti tamu au wenye kubadilika-badilika na wenye kukazia maneno halisi,” yasema ensaiklopedia ya Biblia iitwayo Insight on the Scriptures. *

Yesu na mitume wake waaminifu walimwimbia Yehova sifa usiku uliotangulia kifo cha Yesu na yaelekea waliimba maneno ya Zaburi za Haleli. (Zaburi 113-118) Ni lazima nyimbo hizo ziliwaimarisha mitume wa Yesu kama nini kuweza kukabili kifo cha Bwana-Mkubwa wao! Isitoshe, ni lazima azimio lao la kubaki wakiwa watumishi waaminifu wa Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu aliye Mkuu Kuliko Wote, Yehova, liwe liliimarika sana walipoimba mara tano korasi “kwa maana fadhili zake ni za milele.”—Zaburi 118:1-4, 29.

Wakristo wa mapema wa Efeso na Kolosai waliimba “zaburi na sifa kwa Mungu” (kihalisi, “nyimbo”). Walikuwa pia na “nyimbo za kiroho” walizoimba katika mioyo yao. (Waefeso 5:19; Wakolosai 3:16) Kwa nyimbo na usemi pia walitumia vinywa vyao kwa kufaa kutoa sifa. Je, Yesu hakusema kwamba “kutoka katika wingi wa moyo kinywa husema”?—Mathayo 12:34.

Muziki Usiomfurahisha Mungu

Si muziki wote unaotajwa katika Biblia ulimfurahisha Mungu. Fikiria jambo lililotukia kwenye Mlima Sinai, ambapo Musa alipokea Sheria, kutia ndani zile Amri Kumi. Musa aliposhuka kutoka mlimani, alisikia nini? “Si sauti ya watu wapigao kelele kwa sababu ya kushinda vitani,” “wala si sauti ya watu wapigao kelele kwa sababu ya kushindwa,” bali “kelele za watu waimbao [“wimbo tofauti,” NW].” Huo ulikuwa muziki unaohusianishwa na ibada ya sanamu, jambo ambalo lilimkasirisha Mungu na kusababisha vifo vya watu wapatao 3,000 waliohusika katika muziki huo.—Kutoka 32:18, 25-28.

Ingawa wanadamu wanaweza kutunga, kupiga, na kufurahia muziki wa kila aina, hiyo haimaanishi kwamba muziki wa aina zote unamfurahisha Mungu. Kwa nini? Mtume Mkristo Paulo aeleza: “Wote wamefanya dhambi na hupungukiwa na utukufu wa Mungu.” (Waroma 3:23) Sherehe za kipagani zinazohusu mambo ya uzazi, fundisho la kutokufa kwa nafsi ya mwanadamu, na kutukuzwa kwa Maria kama “mama ya Mungu” ni habari zinazotumiwa mara nyingi kutunga aina fulani za muziki. Hata hivyo, itikadi hizo na mazoea hayo humvunjia heshima Mungu wa ile kweli, kwa kuwa ni kinyume cha yale ambayo yamefunuliwa katika Neno lake lililopuliziwa, Biblia.—Kumbukumbu la Torati 18:10-12; Ezekieli 18:4; Luka 1:35, 38.

Kuchagua Muziki kwa Hekima

Kuchagua muziki unaofaa ni jambo linalotatanisha sana. Vifuniko vya rekodi vinakusudiwa kuchochea wateja wanunue muziki wa aina zote. Lakini ikiwa mwabudu wa Mungu ataka kumfurahisha, atakuwa mwenye tahadhari na kuchagua kwa hekima ili kuepuka muziki wa kuimbwa na muziki wa ala ambao una itikadi za kidini zisizo za kweli au unaokazia ukosefu wa adili na ibada ya roho waovu.

Albert, ambaye wakati mmoja alitumikia akiwa mishonari hapa Afrika, anakiri kwamba hakuwa na fursa ya kupiga piano. Hata hivyo, alisikiliza tena na tena sahani za santuri ambazo alikuja nazo Afrika. Sasa Albert hutembelea makutaniko ya Kikristo akiwa mwangalizi asafiriye katika nchi ya kwao. Hana wakati mwingi wa kusikiliza muziki. “Mtungaji-nyimbo ninayempenda sana ni Beethoven,” asema. “Kwa miaka mingi, nimekusanya rekodi zake za simfoni, concertos, sonata, na zile za ala nne.” Kuusikiliza muziki huo kumemletea furaha nyingi. Bila shaka, kila mtu ana muziki aupendao, lakini tukiwa Wakristo tunakumbuka ushauri wa Paulo: “Kama mnakula au mnakunywa au mnafanya jambo jingine lolote, fanyeni mambo yote kwa utukufu wa Mungu.”—1 Wakorintho 10:31.

Muziki na Kujitoa Wakfu

Susie alipenda muziki sana. “Nilianza kupiga piano nikiwa na umri wa miaka 6, fidla nikiwa na umri wa miaka 10, na hatimaye kinubi nikiwa na umri wa miaka 12,” aeleza. Baadaye Susie alijiunga na chuo cha Royal College of Music jijini London, Uingereza, ili kujifunza kupiga kinubi. Alifundishwa kwa miaka minne na mpiga-kinubi mashuhuri wa Hispania, akajifunza kwa mwaka mwingine mmoja kwenye shule ya Paris Conservatoire, na kupata digrii ya daraja la juu katika muziki na vilevile diploma ya kupiga kinubi na diploma ya kufundisha kupiga piano.

Susie alijiunga na kutaniko la Mashahidi wa Yehova huko London. Katika kutaniko hilo alipata upendezi na upendo wa kweli miongoni mwa Mashahidi. Hatua kwa hatua, upendo wake kwa Yehova ukakua, na tamaa yake kwa ajili ya utumishi wake ikamsukuma kutafuta njia za kumtumikia. Jambo hilo lilifanya ajiweke wakfu na kubatizwa. “Kufanya muziki kuwa kazi-maisha ni sawa na kujitoa wakfu, hivyo maisha ya kujitoa wakfu hayakuwa mapya kwangu,” Susie asema. Wakati aliotumia kwa ajili ya maonyesho ya muziki ulipungua alipoanza kushiriki katika huduma ya Kikristo ya kuhubiri habari njema za Ufalme wa Mungu kwa kutii maagizo ya Yesu.—Mathayo 24:14; Marko 13:10.

Yeye anahisije kwa kuwa sasa anatumia wakati mchache katika maonyesho ya muziki? “Wakati mwingine ninavunjika moyo kwamba sina wakati mwingi wa kujizoeza,” yeye akiri, “lakini bado mimi hupiga ala zangu na kufurahia muziki. Muziki ni zawadi kutoka kwa Yehova. Sasa ninaufurahia zaidi kwa kuwa ninatanguliza utumishi wake maishani mwangu.”—Mathayo 6:33.

Muziki Unaomsifu Mungu

Kwa ukawaida, Albert na Susie, pamoja na Mashahidi wa Yehova wengine wapatao milioni sita, humsifu Yehova Mungu kwa muziki. Kwenye mikutano ya Kikristo ambayo hufanywa katika Majumba ya Ufalme katika nchi 234, mahali inapowezekana wao huanza na kumaliza mikutano yao kwa kumwimbia Yehova nyimbo. Nyimbo tamu za skeli kuu na skeli ya chini, zenye maneno yanayotokana na Maandiko, humsifu Yehova Mungu.

Wahudhuriaji wote huinua sauti zao kuimba kwa uchangamfu kwamba Yehova ni Mungu anayejali (Wimbo namba 44). Wao huimba wimbo wa sifa kwa Yehova (Wimbo namba 190). Nyimbo zao hutaja furaha na majukumu ya udugu wa Kikristo, maisha ya Kikristo, na sifa za Kikristo. Furaha yao huzidishwa na mitindo mbalimbali ya muziki iliyotumiwa na ndugu wa Asia, Australia, Ulaya, na Amerika Kaskazini na Kusini, kutunga nyimbo hizo. *

“Mwimbieni BWANA wimbo mpya. Mwimbieni BWANA, nchi yote. Mwimbieni BWANA, libarikini jina lake,” ndiyo maneno ya ufunguzi ya wimbo mtukufu wa kusifu ulioandikwa wakati wa mtunga-zaburi. “Tangazeni wokovu wake siku kwa siku. Wahubirini mataifa habari za utukufu wake, na watu wote habari za maajabu yake.” (Zaburi 96:1-3) Hivyo ndivyo Mashahidi wa Yehova wanavyofanya katika eneo unaloishi, nao wanakualika ushiriki kuimba sifa hiyo. Unakaribishwa kwenye Majumba yao ya Ufalme, ambako utajifunza jinsi ya kumsifu Yehova kwa muziki unaomfurahisha.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Imechapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

^ fu. 22 Nyimbo hizo zapatikana kwenye kitabu Mwimbieni Yehova Sifa, kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

[Picha katika ukurasa wa 28]

Kumwimbia Yehova Sifa