Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Enda Sambamba na Tengenezo la Yehova

Enda Sambamba na Tengenezo la Yehova

Enda Sambamba na Tengenezo la Yehova

“Mungu wa amani . . . na awape nyinyi vifaa kwa kila jambo jema ili kufanya mapenzi yake.”—WAEBRANIA 13:20, 21.

1. Kuna watu wangapi ulimwenguni, na kuna washiriki wangapi wa dini fulani-fulani?

KATIKA mwaka wa 1999, idadi ya watu duniani ilifikia bilioni sita! Kichapo The World Almanac chaonyesha kwamba kati ya watu hao 1,165,000,000 ni Waislamu; 1,030,000,000 ni Wakatoliki; 762,000,000 ni Wahindu; 354,000,000 ni Wabudha; 316,000,000 ni Waprotestanti; na 214,000,000 ni Waothodoksi.

2. Twaweza kusema nini kuhusu hali ya kidini iliyoko leo?

2 Kwa kuzingatia mgawanyiko na mchafuko wa kidini ulioko leo, je, mamilioni hao wanaweza kuwa wakitenda kupatana na mapenzi ya Mungu? La, “kwa maana Mungu ni Mungu, si wa kukosa utaratibu, bali wa amani.” (1 Wakorintho 14:33) Kwa upande mwingine, vipi juu ya udugu wa ulimwenguni pote wa watumishi wa Yehova? (1 Petro 2:17) Uchunguzi wa makini wathibitisha kwamba ‘Mungu wa amani huwapa vifaa kwa kila jambo jema ili kufanya mapenzi yake.’—Waebrania 13:20, 21.

3. Ni nini kilichotokea Yerusalemu katika Pentekoste 33 W.K., na kwa nini?

3 Bila shaka, si idadi ya watu wanaoshirikiana na Mashahidi wa Yehova inayoamua kama wana upendeleo wa Mungu, wala Mungu havutiwi na takwimu. Hakuchagua Waisraeli kwa sababu walikuwa “wengi” kuliko watu wote. Kwa kweli, walikuwa ndio “wachache” zaidi kati yao. (Kumbukumbu la Torati 7:7) Lakini kwa sababu Waisraeli walikosa kuwa waaminifu, katika Pentekoste 33 W.K., Yehova alielekeza upendeleo wake kwa kutaniko jipya lililofanyizwa na wafuasi wa Yesu Kristo. Walikuwa wametiwa mafuta kwa roho takatifu ya Yehova nao wakasonga mbele kwa bidii wakitangazia wengine kweli kuhusu Mungu na Kristo.—Matendo 2:41, 42.

Kusonga Mbele Daima

4. Kwa nini unaweza kusema kwamba kutaniko la Kikristo la mapema lilikuwa likisonga mbele daima?

4 Katika karne ya kwanza, kutaniko la Kikristo lilikuwa likisonga mbele daima, likihubiri maeneo mapya, likifanya wanafunzi, na kuelewa vizuri zaidi makusudi ya Mungu. Wakristo wa mapema walienda sambamba na nuru ya kiroho ambayo ilifunuliwa kupitia barua zilizopuliziwa na Mungu. Walitimiza huduma yao kwa kuchochewa na ziara za mitume na wengineo. Yote hayo yameandikwa katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo.—Matendo 10:21, 22; 13:46, 47; 2 Timotheo 1:13; 4:5; Waebrania 6:1-3; 2 Petro 3:17, 18.

5. Kwa nini tengenezo la Yehova linasonga mbele leo, na kwa nini twapaswa kwenda sambamba nalo?

5 Kama Wakristo wa mapema, Mashahidi wa Yehova wa siku hizi wamekua kutoka mwanzo mdogo. (Zekaria 4:8-10) Tangu mwisho-mwisho wa karne ya 19, imedhihirika wazi kwamba roho ya Mungu iko katika tengenezo lake. Kwa kuwa tumetegemea mwongozo wa roho takatifu, wala si nguvu za wanadamu, tumezidi kusonga mbele katika uelewevu wetu wa Maandiko na katika kufanya mapenzi ya Mungu. (Zekaria 4:6) Kwa kuwa sasa tuko katika “siku za mwisho,” ni muhimu twende sambamba na tengenezo la Yehova linalosonga mbele hatua kwa hatua. (2 Timotheo 3:1-5) Kufanya hivyo hutuwezesha tudumishe tumaini letu likiwa hai na kushiriki kutoa ushahidi kuhusu Ufalme wa Mungu uliosimamishwa kabla mwisho wa mfumo huu wa mambo haujafika.—Mathayo 24:3-14.

6, 7. Tutachunguza nyanja zipi tatu ambazo tengenezo la Yehova limesonga mbele?

6 Miongoni mwetu mna wale walioanza kushirikiana na tengenezo la Yehova katika miaka ya 1920, 1930, na 1940. Katika miaka hiyo ya mapema, ni nani miongoni mwetu ambaye angewazia ukuzi wenye kutokeza na maendeleo ya hatua kwa hatua ambayo tengenezo limefanya kufikia leo? Hebu fikiria matukio muhimu katika historia yetu ya leo! Kwa kweli, inathawabisha kiroho kutafakari mambo ambayo Yehova ametimiza kupitia watu wake waliopangwa kitheokrasi.

7 Daudi wa kale alivutiwa sana alipotafakari kazi za ajabu za Yehova. “Kama ningependa kuyatangaza na kuyahubiri,” akasema, “ni mengi sana hayahesabiki.” (Zaburi 40:5) Twakabili kizuizi hichohicho, kwa kuwa matendo ya Yehova yaliyo makuu na yenye kusifika katika siku zetu ni mengi sana kuweza kuyasimulia. Hata hivyo, acheni tuchunguze nyanja tatu ambazo tengenezo la Yehova limesonga mbele: (1) nuru ya kiroho inayoongezeka hatua kwa hatua, (2) huduma iliyoboreshwa na kupanuliwa, na (3) marekebisho ya wakati ufaao katika utaratibu mbalimbali wa kitengenezo.

Twashukuru kwa Nuru ya Kiroho

8. Kupatana na Mithali 4:18, nuru ya kiroho imetuwezesha kufahamu nini kuhusu Ufalme?

8 Kuhusu nuru ya kiroho inayoongezeka hatua kwa hatua, Mithali 4:18 imetimia. Yasema hivi: “Njia ya wenye haki ni kama nuru ing’aayo, ikizidi kung’aa hata mchana mkamilifu.” Tunashukuru kama nini kuipata nuru ya kiroho inayoongezeka hatua kwa hatua! Kwenye mkusanyiko wa mwaka wa 1919 huko Cedar Point, Ohio, Ufalme wa Mungu ulikaziwa. Yehova hutumia Ufalme kutakasa jina lake na kutetea enzi kuu yake. Kwa kweli, nuru ya kiroho imetuwezesha kufahamu kwamba kuanzia Mwanzo hadi Ufunuo, Biblia hushuhudia kusudi la Yehova la kutakasa jina lake kupitia Ufalme unaotawalwa na Mwana wake. Huo ndio tumaini kubwa zaidi la wapendao uadilifu.—Mathayo 12:18, 21.

9, 10. Katika miaka ya 1920, ni nini kilichojulikana kuhusu Ufalme na kuhusu matengenezo mawili yanayopingana, na hilo limesaidiaje?

9 Kwenye mkusanyiko wa mwaka wa 1922 huko Cedar Point, msemaji mkuu, J. F. Rutherford, aliwahimiza watu wa Mungu kwa kuwaambia “tangazeni, tangazeni, tangazeni, Mfalme na ufalme wake.” Makala yenye kichwa “Kuzaliwa kwa Taifa,” iliyochapishwa katika Mnara wa Mlinzi, Machi 1, 1925, ilikazia ufahamu wa kiroho kuhusu unabii mbalimbali uliorejezea kuanzishwa kwa Ufalme wa Mungu mwaka wa 1914. Pia katika miaka ya 1920, ilifahamika kwamba kuna matengenezo mawili tofauti yanayopingana, tengenezo la Yehova na tengenezo la Shetani. Pigano linaendelea kati ya matengenezo hayo, na tutakuwa upande unaoshinda ikiwa tu tutaenda sambamba na tengenezo la Yehova.

10 Nuru hiyo ya kiroho imetusaidiaje? Kwa kuwa Ufalme wa Mungu na Mfalme Yesu Kristo si sehemu ya ulimwengu, sisi nasi hatuwezi kuwa sehemu yake. Kwa kujitenga na ulimwengu, twaonyesha kwamba tuko upande wa ile kweli. (Yohana 17:16; 18:37) Tunapoona matatizo magumu yanayoukumba mfumo huu mwovu, twashukuru kama nini kwamba sisi si sehemu ya tengenezo la Shetani! Nasi tuna pendeleo lililoje la kupata usalama wa kiroho ndani ya tengenezo la Yehova!

11. Watu wa Mungu walikubali jina gani la Kimaandiko mwaka wa 1931?

11 Kwenye mkusanyiko wa mwaka wa 1931, huko Columbus, Ohio, matumizi yafaayo ya andiko la Isaya 43:10-12 yalionyeshwa. Wanafunzi wa Biblia walikubali jina la pekee Mashahidi wa Yehova. Ni pendeleo kubwa kama nini kuwajulisha wengine jina la Mungu ili waliitie kusudi wapate kuokolewa!—Zaburi 83:18; Waroma 10:13.

12. Ni nuru gani ya kiroho kuhusu umati mkubwa iliyotolewa mwaka wa 1935?

12 Kabla ya miaka ya 1930, wengi wa watu wa Mungu walikuwa na tashwishi kuhusu matumaini yao ya uhai wa wakati ujao. Baadhi yao walitamani kwa kiasi fulani uhai wa kimbingu huku wakivutiwa sana na mafundisho ya Biblia kuhusu dunia paradiso. Kwenye mkusanyiko wa mwaka wa 1935 huko Washington, D.C., kulikuwa na habari zenye kusisimua kwamba halaiki kubwa, au umati mkubwa, wa Ufunuo sura ya 7 ni jamii yenye matumaini ya kidunia. Kukusanywa kwa umati mkubwa kumesonga mbele kwa kupamba moto tangu wakati huo. Je, hatushukuru kwamba “umati mkubwa” si fumbo kwetu? Kukusanywa kwa watu wengi kutoka katika mataifa, makabila, na lugha zote, hutuchochea kuimarisha azimio letu na kuharakisha hatua zetu tuendapo sambamba na tengenezo la Yehova.

13. Ni suala gani kuu lililokaziwa mwaka wa 1941 kwenye mkusanyiko wa St. Louis?

13 Suala kuu ambalo wanadamu wanapaswa kuhangaikia lilikaziwa mwaka wa 1941 kwenye mkusanyiko wa St. Louis, Missouri. Ni utawala wa ulimwengu wote, au enzi kuu ya ulimwengu wote. Suala hilo halina budi kutatuliwa karibuni, nayo siku kuu na yenye kutia hofu itakayotatua suala hilo yaja mbio! Suala jingine lililozingatiwa pia mwaka wa 1941 linalohusiana na hilo, ni lile la uaminifu-maadili, ambao huwezesha kila mmoja wetu kuonyesha msimamo wake kuhusiana na enzi kuu ya Mungu.

14. Kwenye mkusanyiko wa kimataifa wa mwaka wa 1950, watu walijifunza nini kuhusu wakuu wanaotajwa katika Isaya 32:1, 2?

14 Kwenye mkusanyiko wa kimataifa wa mwaka wa 1950 huko New York City, wakuu kwenye Isaya 32:1, 2 walitambulishwa kwa usahihi. Ilikuwa pindi yenye kusisimua kwelikweli, Ndugu Frederick Franz alipoeleza kwamba wale ambao wangekuwa wakuu wa dunia mpya walikuwa miongoni mwetu. Kwenye mkusanyiko huo na mingine iliyofuata, kumekuwa na mimweko mingi ya nuru ya kiroho. (Zaburi 97:11) Tunashukuru kama nini kwamba njia yetu “ni kama nuru ing’aayo, ikizidi kung’aa”!

Kusonga Mbele Katika Huduma Yetu

15, 16. (a) Tulisonga mbele jinsi gani katika huduma yetu katika miaka ya 1920 na 1930? (b) Ni vichapo vipi ambavyo vimechochea huduma ya Kikristo katika miongo ya karibuni?

15 Nyanja ya pili ambayo tengenezo la Yehova limesonga mbele yahusu kazi yetu kuu ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi. (Mathayo 28:19, 20; Marko 13:10) Ili kutimiza kazi hiyo, tengenezo limekazia umuhimu wa kupanua huduma yetu. Mwaka wa 1922, Wakristo wote walihimizwa kushiriki katika utendaji wa kuhubiri. Kila mmoja angeamua kuacha nuru yake iangaze na hivyo ashiriki kibinafsi kutoa ushahidi juu ya ile kweli. (Mathayo 5:14-16) Mwaka wa 1927 hatua zilichukuliwa ili kutenga Jumapili iwe siku ya utumishi wa shambani. Kuanzia Februari 1940, ikawa kawaida kuwaona Mashahidi barabarani kwenye sehemu za biashara wakitoa The Watchtower na Consolation (ambalo sasa ni Amkeni!).

16 Kijitabu Model Study kilitolewa mwaka wa 1937, nacho kilikazia uhitaji wa kufanya ziara za kurudia ili kuwafundisha wengine kweli ya Biblia. Miaka iliyofuata, utendaji wa kuongoza mafunzo ya Biblia ulikaziwa sana. Sehemu hiyo ya huduma ilichochewa zaidi kitabu “Let God Be True” kilipotolewa mwaka wa 1946 na kitabu Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele mwaka wa 1968. Sasa, twatumia kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele. Kuchanganua habari hizo huweka msingi mzuri wa Kimaandiko wa kufanya wanafunzi.

Kusonga Mbele na Marekebisho ya Kitengenezo

17. Ili kwenda sambamba na unabii wa Isaya 60:17, tengenezo la Yehova limesongaje mbele?

17 Nyanja ya tatu ambayo tengenezo la Yehova limesonga mbele yahusu marekebisho ya kitengenezo. Kulingana na Isaya 60:17, Yehova aliahidi hivi: “Badala ya shaba nitaleta dhahabu, na badala; ya chuma nitaleta fedha, na badala ya mti, shaba, na badala ya mawe, chuma; tena nitawafanya wasimamizi wako wawe amani, na hao wakutozao fedha kuwa haki.” Ili kwenda sambamba na unabii huo, hatua zimechukuliwa kuboresha usimamizi wa kazi ya kuhubiri Ufalme na kulichunga kundi.

18, 19. Kumekuwa na marekebisho gani ya kitengenezo katika miaka ambayo imepita?

18 Mwaka wa 1919 mwelekezi wa utumishi aliwekwa katika kila kutaniko lililoomba kupangwa kwa ajili ya utumishi wa shambani. Mpango huo ulichochea huduma yetu ya shambani. Kupiga kura ili kuchagua wazee na mashemasi kulikomeshwa mwaka wa 1932, na huo ukawa mwisho wa kutumia njia za kidemokrasi. Hatua nyingine kuu ilipigwa mwaka wa 1938 wakati watumishi wote katika kutaniko walipoanza kuwekwa rasmi ili kupatanisha mambo zaidi na mpango uliokuwako katika kutaniko la Wakristo wa mapema wa kuwekwa rasmi kitheokrasi. (Matendo 14:23; 1 Timotheo 4:14) Mwaka wa 1972 waangalizi na watumishi wa huduma waliwekwa rasmi kutumikia, kama walivyowekwa wanaume miongoni mwa Wakristo wa mapema. Badala ya mtu mmoja tu kutumikia akiwa mwangalizi wa kutaniko, Wafilipi 1:1 na maandiko mengine yanaonyesha kwamba wale wanaotimiza matakwa ya Kimaandiko ya waangalizi hufanyiza baraza la wazee.—Matendo 20:28; Waefeso 4:11, 12.

19 Mwaka wa 1975, mpango fulani ulianzishwa ili halmashauri mbalimbali za Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova zisimamie utendaji mbalimbali wa ulimwenguni pote wa tengenezo la Mungu. Halmashauri za Tawi zikaanzishwa ili kusimamia kazi katika maeneo yake. Tangu wakati huo, kurahisishwa kwa kazi katika makao makuu na katika ofisi za tawi za Watch Tower Society kumezingatiwa ili “kuhakikisha mambo yaliyo ya maana zaidi.” (Wafilipi 1:9, 10) Madaraka ya wachungaji walio chini ya Kristo yatia ndani kuongoza katika kazi ya kueneza evanjeli, kufundisha katika kutaniko, na kuchunga kundi la Mungu ifaavyo.—1 Timotheo 4:16; Waebrania 13:7, 17; 1 Petro 5:2, 3.

Uongozi wa Yesu Wenye Bidii

20. Ili kwenda sambamba na tengenezo la Yehova twahitaji kutambua nini kuhusu wadhifa wa Yesu?

20 Ili kwenda sambamba na tengenezo la Yehova linalosonga mbele hatua kwa hatua hatuna budi kutambua mgawo ambao Yesu Kristo amepewa na Mungu wa kuwa “kichwa cha kutaniko.” (Waefeso 5:22, 23) Yafaa tuangalie pia yale tunayoambiwa katika Isaya 55:4: “Angalieni, [mimi Yehova] nimemweka kuwa shahidi kwa kabila za watu; kuwa kiongozi na jemadari kwa kabila za watu.” Bila shaka Yesu ni kiongozi stadi. Awajua kondoo zake na matendo yao. Kwa kweli, alipokagua yale makutaniko saba katika Asia Ndogo, alisema hivi mara tano: “Mimi navijua vitendo vyako.” (Ufunuo 2:2, 19; 3:1, 8, 15) Yesu pia ayajua mahitaji yetu, kama ayajuavyo Baba yake, Yehova. Kabla ya kutoa Sala ya Kigezo, Yesu alisema: “Mungu Baba yenu ajua ni vitu gani mnavyohitaji hata kabla nyinyi hamjamwomba.”—Mathayo 6:8-13.

21. Uongozi wa Yesu huonekanaje katika kutaniko la Kikristo?

21 Uongozi wa Yesu huonekanaje? Njia moja ni kupitia waangalizi Wakristo, ambao ni “zawadi zikiwa wanadamu.” (Waefeso 4:8) Andiko la Ufunuo 1:16 laonyesha kwamba waangalizi watiwa-mafuta wako kwenye mkono wa kuume wa Kristo, chini ya uongozi wake. Leo, Yesu huelekeza mpango wa kuwa na wazee, iwe wanaume hao wana tumaini la kimbingu au la kidunia. Kama ilivyoelezwa katika makala iliyotangulia, wanawekwa rasmi na roho takatifu kupatana na matakwa ya Kimaandiko. (1 Timotheo 3:1-7; Tito 1:5-9) Katika karne ya kwanza, kikundi cha wanaume wazee katika Yerusalemu kilifanyiza baraza linaloongoza lililosimamia makutaniko na kazi ya kuhubiri Ufalme kwa ujumla. Kiolezo hicho hufuatwa leo katika tengenezo la Yehova.

Nenda Sambamba!

22. Baraza Linaloongoza huandaa msaada gani?

22 Masilahi ya Ufalme duniani yamekabidhiwa “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” anayewakilishwa na Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova. (Mathayo 24:45-47) Baraza Linaloongoza linashughulika hasa na kuandaa maagizo na mwelekezo wa kiroho kwa ajili ya kutaniko la Kikristo. (Matendo 6:1-6) Hata hivyo, waabudu wenzetu wanapoathiriwa na misiba ya asili, Baraza Linaloongoza huomba shirika au mashirika fulani ya kisheria kutoa msaada na kurekebisha nyumba na Majumba ya Ufalme yaliyoharibika. Baadhi ya ndugu zetu wakitendewa kwa ukali au kunyanyaswa, hatua huchukuliwa kuwajenga kiroho. Na “katika majira yenye taabu,” jitihada nyingi hufanywa ili kazi ya kuhubiri izidi kusonga mbele.—2 Timotheo 4:1, 2.

23, 24. Hata watu wake wapatwe na hali gani, Yehova huandaa nini daima, nasi twapaswa kuazimia kufanya nini?

23 Haidhuru watu wake watapatwa na hali gani, Yehova huandaa daima chakula cha kiroho na mwelekezo unaohitajika. Mungu pia huwapa ndugu wenye madaraka ufahamu wa kufanya matayarisho kwa ajili ya maendeleo na marekebisho zaidi katika mipango ya kitheokrasi. (Kumbukumbu la Torati 34:9; Waefeso 1:16, 17) Bila kushindwa, Yehova hutuandalia tunachohitaji ili kutimiza utume wetu wa kufanya wanafunzi na kutimiza huduma yetu ulimwenguni pote.—2 Timotheo 4:5.

24 Tuna uhakika kabisa kwamba Yehova hatawaacha kamwe watu wake waaminifu; atawaokoa wapite “dhiki kubwa” inayokuja. (Ufunuo 7:9-14; Zaburi 94:14; 2 Petro 2:9) Tuna sababu nzuri za kudumisha uhakika tuliokuwa nao mwanzoni ukiwa imara hadi mwisho. (Waebrania 3:14) Kwa hiyo, acheni tuazimie kwenda sambamba na tengenezo la Yehova.

Ungejibuje?

• Kwa nini twaweza kusema kwamba tengenezo la Yehova linazidi kusonga mbele?

• Kuna uthibitisho gani kwamba watu wa Mungu wanafurahia nuru ya kiroho inayoongezeka hatua kwa hatua?

• Huduma ya Kikristo imeboreshwa jinsi gani?

• Ni marekebisho gani ya wakati ufaao ambayo yamefanywa kuhusu hatua za kitengenezo miongoni mwa watumishi wa Yehova?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 17]

Kama Daudi, hatuwezi kusimulia kazi zote za ajabu za Yehova

[Picha katika ukurasa wa 18]

Kundi la Mungu limenufaika na marekebisho ya wakati ufaao katika utaratibu mbalimbali wa kitengenezo