Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 10

Unawezaje Kuitambua Ibada ya Kweli?

Unawezaje Kuitambua Ibada ya Kweli?

1. Je, kuna dini moja tu ya kweli?

“Jihadharini na manabii wa uwongo.”​—MATHAYO 7:15.

Yesu aliwafundisha wafuasi wake dini moja tu, dini ya kweli. Dini hiyo ni kama barabara inayoelekea kwenye uzima wa milele. Yesu alisema hivi: “Ni wachache wanaoipata” barabara hiyo. (Mathayo 7:14) Mungu anakubali tu ibada inayotegemea Neno lake la kweli. Waabudu wote wa kweli wameunganishwa katika imani moja.​—Soma Yohana 4:23, 24; 14:6; Waefeso 4:4, 5.

Tazama video Je, Mungu Anakubali Aina Zote za Ibada?

2. Yesu alisema nini kuhusu Wakristo wa uwongo?

“Wao hutangaza hadharani kwamba wanamjua Mungu, lakini wanamkana kwa matendo yao.”​—TITO 1:16.

Yesu alionya kwamba manabii wa uwongo wangepotosha Ukristo. Kwa nje wanaonekana kama waabudu wa kweli. Makanisa yao yanadai kuwa ya Kikristo. Lakini unaweza kujua kwamba watu hao si Wakristo wa kweli. Jinsi gani? Ni ibada ya kweli tu inayotokeza Wakristo wa kweli wenye sifa na mwenendo unaowatambulisha wazi.​—Soma Mathayo 7:13-23.

3. Unaweza kuwatambuaje waabudu wa kweli?

Fikiria mambo haya matano yanayowatambulisha:

  • Waabudu wa kweli wanaiheshimu Biblia kuwa Neno la Mungu. Wanajitahidi kuishi kulingana na kanuni za Biblia. Hivyo, dini ya kweli ni tofauti sana na dini zinazotegemea maoni ya wanadamu. (Mathayo 15:7-9) Waabudu wa kweli wanaishi kulingana na mambo wanayofundisha.​—Soma Yohana 17:17; 2 Timotheo 3:16, 17.

  • Wafuasi wa kweli wa Yesu wanaliheshimu jina la Mungu, Yehova. Yesu aliliheshimu jina la Mungu kwa kuwajulisha watu jina hilo. Aliwasaidia watu kumjua Mungu na kuwafundisha wasali kwamba jina la Mungu litakaswe. (Mathayo 6:9) Katika eneo unaloishi, ni dini gani inayowajulisha watu jina la Mungu?​—Soma Yohana 17:26; Waroma 10:13, 14.

  • Wakristo wa kweli wanahubiri kuhusu Ufalme wa Mungu. Mungu alimtuma Yesu kuhubiri habari njema ya Ufalme. Ufalme wa Mungu ndilo tumaini pekee la wanadamu. Yesu aliendelea kuhubiri kuhusu Ufalme huo hadi siku aliyokufa. (Luka 4:43; 8:1; 23:42, 43) Alisema kwamba wafuasi wake wangehubiri kuhusu Ufalme huo. Ikiwa mtu fulani angekuja kwako kuzungumza nawe kuhusu Ufalme wa Mungu, wewe ungefikiria mtu huyo ni wa dini gani?​—Soma Mathayo 24:14.

  • Wafuasi wa Yesu si sehemu ya ulimwengu huu mwovu. Unaweza kuwatambua kwa sababu hawajihusishi na siasa wala migogoro ya kijamii. (Yohana 17:16; 18:36) Pia, hawaigi mitazamo na mazoea yenye kudhuru ya ulimwengu.​—Soma Yakobo 4:4.

  • Wakristo wa kweli wanapendana sana. Wamejifunza katika Neno la Mungu kuwaheshimu watu wa jamii zote. Ingawa mara nyingi dini za uwongo zimeunga mkono kwa dhati vita vya mataifa, waabudu wa kweli wamekataa kufanya hivyo. (Mika 4:1-3) Badala yake, Wakristo wa kweli hutumia bila choyo wakati na mali zao ili kuwasaidia na kuwatia moyo wengine.​—Soma Yohana 13:34, 35; 1 Yohana 4:20.

4. Je, unaweza kuitambua dini ya kweli?

Ni dini gani ambayo mafundisho yake yote yanategemea Neno la Mungu, inaheshimu jina la Mungu, na kutangaza kwamba Ufalme wa Mungu ndilo tumaini pekee la wanadamu? Ni dini gani ambayo washiriki wake wanapendana na hawaungi mkono vita? Una maoni gani?​—Soma 1 Yohana 3:10-12.