SOMO LA 13
Kuna Habari Gani Kuhusu Dini?
1. Je, dini zote ni nzuri?
Kuna watu wanyoofu katika dini zote. Ni habari njema kwamba Mungu anawaona watu hao na anawajali. Hata hivyo, ni jambo lenye kusikitisha kwamba dini imetumiwa kwa makusudi maovu. (2 Wakorintho 4:3, 4; 11:13-15) Kulingana na ripoti fulani ya habari, dini fulani zimejihusisha na ugaidi, mauaji ya halaiki, vita, na kuwatendea watoto vibaya. Jambo hilo linawahuzunisha sana waamini wa kweli wa Mungu!—Soma Mathayo 24:3-5, 11, 12.
Ingawa dini ya kweli inamtukuza Mungu, dini ya uwongo inamchukiza. Inafundisha mambo ambayo hayapatikani katika Biblia, kutia ndani mafundisho ya uwongo kumhusu Mungu na kuhusu hali ya wafu. Lakini Yehova anataka watu wajue ukweli kumhusu yeye.—Soma Ezekieli 18:4; 1 Timotheo 2:3-5.
2. Kuna habari gani kuhusu dini?
Habari njema ni kwamba, Mungu hadanganywi na dini zinazodai kwamba zinampenda lakini ambazo kwa kweli zinapenda ulimwengu wa Shetani. (Yakobo 4:4) Neno la Mungu linaziita dini zote za uwongo “Babiloni Mkubwa.” Babiloni lilikuwa jiji la kale, mahali ambapo dini ya uwongo ilianzia mara baada ya Gharika ya siku za Noa. Hivi karibuni, Mungu atazikomesha dini zote za uwongo ambazo zinawadanganya na kuwakandamiza wanadamu. —Soma Ufunuo 17:1, 2, 5, 16, 17; 18:8.
Kuna habari njema nyingine. Yehova hajawasahau watu wanyoofu ambao wametawanyika katika dini za uwongo ulimwenguni pote. Anawaunganisha watu hao kwa kuwafundisha kweli.—Soma Mika 4:2, 5.
3. Watu wanyoofu wanapaswa kufanya nini?
Dini ya kweli inawaunganisha watu
Yehova anawajali watu wanaopenda mema na kweli. Anawahimiza watoke katika dini ya uwongo. Watu wanaompenda Mungu wako tayari kufanya mabadiliko ili kumfurahisha.—Soma Ufunuo 18:4.
Watu wanyoofu walishangilia waliposikia habari njema kutoka kwa mitume katika karne ya kwanza. Walijifunza njia mpya ya maisha kutoka kwa Yehova, njia yenye furaha, kusudi, na tumaini. Walituwekea kielelezo kizuri leo kwa sababu waliitikia habari njema kwa kumtanguliza Yehova katika maisha yao.—Soma 1 Wathesalonike 1:8, 9; 2:13.
Yehova anawakaribisha wale wanaoiacha dini ya uwongo wajiunge na familia yake ya waabudu wa kweli. Ukikubali mwaliko huo mchangamfu wa Yehova, utakuwa rafiki yake, utafurahia ushirika wenye upendo wa waabudu wenzako, na kupata uzima wa milele.—Soma Marko 10:29, 30; 2 Wakorintho 6:17, 18.
4. Mungu ataletaje shangwe duniani pote?
Hukumu inayokuja dhidi ya dini ya uwongo ni habari njema. Italeta kitulizo kutokana na ukandamizaji ulimwenguni pote. Dini ya uwongo haitawapotosha na kuwagawanya wanadamu tena kamwe. Wanadamu wote wanaoishi wataungana katika ibada ya Mungu wa pekee wa kweli.—Soma Ufunuo 18:20, 21; 21:3, 4.