Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 5

Mungu Ana Kusudi Gani Kuelekea Dunia?

Mungu Ana Kusudi Gani Kuelekea Dunia?

1. Kwa nini Mungu aliiumba dunia?

Yehova aliwapa wanadamu dunia. Dunia ni makao yetu. Kwa hiyo, wanadamu wa kwanza, Adamu na Hawa, hawakuumbwa waijaze mbingu kwa kuwa tayari Mungu alikuwa amewaumba malaika waishi mbinguni. (Ayubu 38:4, 7) Badala yake, Mungu alimweka mwanadamu wa kwanza katika paradiso yenye kupendeza iliyoitwa bustani ya Edeni. (Mwanzo 2:15-17) Yehova alimpa Adamu na watoto ambao angepata tumaini la kufurahia maisha duniani milele.​—Soma Zaburi 37:29; 115:16.

Mwanzoni, bustani ya Edeni tu ndiyo iliyokuwa paradiso. Wanadamu hao wa kwanza walipaswa kuzaa na kuijaza dunia. Baada ya muda, wangeitiisha dunia nzima na kuifanya kuwa paradiso. (Mwanzo 1:28) Dunia haitaharibiwa kamwe. Itaendelea kuwa makao ya wanadamu sikuzote.​—Soma Zaburi 104:5.

Tazama video Kwa Nini Mungu Aliiumba Dunia?

2. Kwa nini dunia si paradiso leo?

Adamu na Hawa hawakumtii Mungu, hivyo Yehova akawafukuza kutoka katika bustani hiyo. Paradiso ikapotea, na hakuna mtu ambaye amefanikiwa kuirudisha. Biblia inasema: “Dunia imetiwa mikononi mwa mwovu.”—Ayubu 9:24.​—Soma Mwanzo 3:23, 24.

Je, Yehova ameshindwa kutimiza kusudi lake la awali kuelekea wanadamu? Hapana! Yeye ni mweza-yote. Hawezi kushindwa. (Isaya 45:18) Atawarudisha wanadamu katika hali ambayo alikusudia wawe nayo.​—Soma Zaburi 37:11, 34.

3. Paradiso itarudishwa jinsi gani?

Paradiso itarudishwa duniani Yesu atakapotawala akiwa Mfalme aliyewekwa na Mungu. Katika vita vinavyoitwa Har–Magedoni, Yesu atawaongoza malaika wa Mungu kuwaharibu wote wanaompinga Mungu. Kisha Yesu atamfunga Shetani kwa miaka 1,000. Watu wa Mungu wataokoka uharibifu huo kwa sababu Yesu atawalinda na kuwaongoza. Watafurahia uzima wa milele katika Paradiso duniani.​—Soma Ufunuo 20:1-3; 21:3, 4.

4. Kuteseka kutaisha lini?

Mungu ataondoa uovu duniani lini? Yesu alitoa “ishara” ya kuonyesha wakati ambapo mwisho ungekuwa karibu. Hali zilizo ulimwenguni leo zinahatarisha maisha ya watu na zinaonyesha kwamba tunaishi katika “umalizio wa mfumo wa mambo.”​—Soma Mathayo 24:3, 7-14, 21, 22.

Wakati wa utawala wa miaka 1,000 wa Yesu, atakapokuwa akiitawala dunia kutoka mbinguni, atakomesha kuteseka kote. (Isaya 9:6, 7; 11:9) Zaidi ya kutawala akiwa Mfalme, Yesu atatenda akiwa Kuhani Mkuu, naye atazifuta dhambi za wale wanaompenda Mungu. Hivyo, kupitia Yesu, Mungu ataondoa magonjwa, uzee, na kifo.​—Soma Isaya 25:8; 33:24.

5. Ni nani watakaoishi katika Paradiso?

Katika Jumba la Ufalme, utakutana na watu wanaompenda Mungu na wanaotaka kujifunza jinsi wanavyoweza kumpendeza

Watu wanaomtii Mungu wataishi katika Paradiso. (1 Yohana 2:17) Yesu aliwatuma wafuasi wake wawatafute watu wapole na kuwafundisha jinsi ya kuwa watu wenye kukubalika mbele za Mungu. Leo, Yehova anawatayarisha mamilioni ya watu kuishi katika Paradiso ijayo hapa duniani. (Sefania 2:3) Katika Majumba ya Ufalme ya Mashahidi wa Yehova, watu hujifunza jinsi ya kuwa waume na wake bora, na pia wazazi bora. Watoto na wazazi huabudu pamoja na kujifunza jinsi wanavyoweza kufaidika na habari njema.​—Soma Mika 4:1-4.