Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Thamini Ukarimu na Usawaziko wa Yehova

Thamini Ukarimu na Usawaziko wa Yehova

“Yehova ni mwema kwa wote, na rehema zake ziko juu ya kazi zake zote.”—ZAB. 145:9.

1, 2. Marafiki wa Yehova wana fursa gani?

“MIAKA 35 hivi imepita tangu niolewe,” anasema Mkristo anayeitwa Monika. “Mimi na mume wangu tunajuana vizuri sana. Hata hivyo, ingawa tumeishi pamoja miaka hiyo yote, kila mmoja wetu angali anajifunza mambo mapya kuhusu mwenzake, mambo ambayo hatukuyajua kamwe!” Bila shaka, ndivyo mambo yalivyo katika ndoa nyingi na kati ya marafiki wengi.

2 Tunafurahia kuwajua vizuri wale tunaowapenda. Hata hivyo, hakuna urafiki wowote tunaoweza kusitawisha ulio muhimu zaidi ya urafiki wetu pamoja na Yehova. Hatutawahi kamwe kujua kila kitu kumhusu. (Rom. 11:33) Kwa umilele wote, tutakuwa na fursa na shangwe ya kuthamini hata zaidi sifa za Yehova.—Mhu. 3:11.

3. Tutachunguza nini katika makala hii?

3 Makala iliyotangulia ilitusaidia kuthamini zaidi sifa ya Yehova ya kuwa mwenye urafiki na kutokuwa na ubaguzi. Acheni sasa tuchunguze sifa nyingine mbili za Yehova zenye kuvutia, yaani, ukarimu na usawaziko wake. Tukifanya hivyo, tutaelewa kikamili zaidi kwamba “Yehova ni mwema kwa wote, na rehema zake ziko juu ya kazi zake zote.”Zab. 145:9.

YEHOVA NI MKARIMU

4. Ni nini maana halisi ya ukarimu wa kweli?

4 Ni nini maana ya kuwa mkarimu? Yesu alijibu swali hilo katika andiko la Matendo 20:35: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.” Kwa maneno hayo rahisi, Yesu alifafanua vizuri maana halisi ya ukarimu wa kweli. Mtu mkarimu hutumia kwa hiari wakati, nguvu, na mali zake kwa faida ya wengine, akifanya hivyo kwa shangwe. Kwa kweli, ukarimu haupimwi na ukubwa wa zawadi inayotolewa, bali nia ya mtoaji.  (Soma 2 Wakorintho 9:7.) Hakuna mtu mkarimu zaidi ya ‘Mungu wetu mwenye furaha,’ Yehova.1 Tim. 1:11.

5. Yehova huonyesha ukarimu katika njia zipi?

5 Yehova huonyeshaje ukarimu? Yeye huwapa wanadamu wote mahitaji yao, kutia ndani wale ambao hawajaanza kumwabudu. Kwa kweli, “Yehova ni mwema kwa wote.” Yeye “hulichomoza jua lake juu ya watu waovu na wema na hunyesha mvua juu ya watu waadilifu na wasio waadilifu.” (Mt. 5:45) Ndiyo sababu mtume Paulo alipokuwa akiongea na watu wasio waamini aliwaambia kwamba Yehova ‘alitenda mema, akiwapa mvua kutoka mbinguni na majira yenye kuzaa matunda, akijaza mioyo yao kikamili kwa chakula na uchangamfu.’ (Mdo. 14:17) Ni wazi kwamba Yehova ni mkarimu kuwaelekea wanadamu wote.Luka 6:35.

6, 7. (a) Yehova hufurahia kuwaandalia nani hasa mahitaji yao? (b) Toa mfano unaoonyesha jinsi Yehova anavyowaandalia mahitaji waabudu wake waaminifu.

6 Yehova hufurahia hasa kuwaandalia waabudu wake waaminifu mahitaji yao. Mfalme Daudi alisema hivi: “Nilikuwa kijana, pia nimezeeka, na bado sijamwona mtu yeyote mwadilifu akiwa ameachwa kabisa, wala uzao wake ukitafuta mkate.” (Zab. 37:25) Wakristo wengi waaminifu wamejionea uthibitisho wa kwamba Yehova huwatunza watu wake. Fikiria mfano ufuatao.

7 Miaka kadhaa iliyopita, mtumishi mmoja wa wakati wote anayeitwa Nancy alijikuta katika hali ngumu. Nancy anakumbuka hivi: “Nilihitaji dola 66 za Marekani ili nilipe kodi yangu ya nyumba siku iliyofuata. Sikujua ningepata wapi pesa hizo. Nilisali kuhusu tatizo hilo, kisha nikaenda kazini ambako nilikuwa mhudumu wa mkahawa. Sikutarajia kupata bakshishi nyingi jioni hiyo kwa sababu kwa kawaida wateja si wengi siku hiyo. Jambo la kushangaza ni kwamba jioni hiyo wateja wengi walikuja kwenye mkahawa huo. Nilipomaliza zamu yangu na kuhesabu bakshishi nilizopata, nilikuwa na jumla ya dola 66.” Nancy anasadiki kwamba Yehova alimwandalia kwa ukarimu kile alichohitaji hasa.Mt. 6:33.

8. Ni zawadi gani kubwa zaidi inayoonyesha ukarimu wa Yehova?

8 Kila mtu anaweza kufaidika kutokana na zawadi kubwa zaidi inayoonyesha ukarimu wa Yehova. Ni zawadi gani hiyo? Dhabihu ya fidia ya Mwana wake. Yesu alisema hivi: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.” (Yoh. 3:16) Katika muktadha huo, neno “ulimwengu” linarejelea wanadamu. Naam, yeyote anayekubali zawadi hiyo kubwa zaidi inayoonyesha ukarimu wa Yehova anaweza kufaidika kutokana nayo. Wale wanaodhihirisha imani katika Yesu watapata uzima kwa wingi, naam, uzima wa milele! (Yoh. 10:10) Kwa kweli, huo ni uthibitisho wa kutosha kwamba Yehova ni mkarimu, sivyo?

 IGA UKARIMU WA YEHOVA

Waisraeli walitiwa moyo kuiga ukarimu wa Yehova (Tazama fungu la 9)

9. Tunawezaje kuiga ukarimu wa Yehova?

 9 Tunaweza kuiga jinsi gani ukarimu wa Yehova? Yehova “hutupa sisi vitu vyote kwa wingi ili tuvifurahie; kwa hiyo, tunapaswa kuwa “tayari kushiriki” pamoja na wengine, na hivyo kuchangia shangwe yao. (1 Tim. 6:17-19) Kwa furaha, tunatumia mali zetu kuwapa zawadi wapendwa wetu na kuwasaidia wale walio na uhitaji. (Soma Kumbukumbu la Torati 15:7.) Ni nini kinachoweza kutusaidia kukumbuka kuwa wakarimu? Wakristo fulani huchukua hatua hii inayofaa: Kila mara wanapopewa zawadi, wanatafuta fursa ya kumpa mtu mwingine zawadi. Kutaniko la Kikristo limebarikiwa kwa kuwa na ndugu na dada wengi wanaositawisha roho ya ukarimu.

10. Tunaweza kuonyesha ukarimu katika njia gani bora zaidi?

10 Njia moja bora zaidi ya kuonyesha ukarimu ni kujitoa kuwasaidia wengine kwa maneno na matendo. Tunawezaje kufanya hivyo? Kwa kutumia wakati na nguvu zetu kuwasaidia na kuwatia moyo wengine. (Gal. 6:10) Ili kujua ikiwa tunatimiza jambo hilo, tunaweza kujiuliza hivi: ‘Je, wengine wanahisi kwamba niko tayari kujitoa na kusikiliza mahangaiko yao? Mtu anaponiomba nimsaidie kufanya kazi fulani, je, mimi hukubali inapowezekana? Ni lini mara ya mwisho nilipompongeza kwa unyoofu mshiriki wa familia yangu au mwamini mwenzangu?’ Tukiwa na “mazoea ya kuwapa watu,” tuna hakika kwamba tutamkaribia zaidi Yehova na rafiki zetu.Luka 6:38; Met. 19:17.

11. Tunaweza kumwonyesha Yehova ukarimu kwa njia gani?

 11 Tunaweza pia kumwonyesha Yehova ukarimu. Maandiko yanatuhimiza hivi: ‘Mheshimuni Yehova kwa vitu vyenu vyenye thamani.’ (Met. 3:9) Vitu hivyo “vyenye thamani” vinatia ndani wakati, nguvu, na mali zetu tunazoweza kutumia kwa  hiari tunapomtumikia. Hata watoto wadogo wanaweza kujifunza kumwonyesha Yehova ukarimu. “Familia yetu inapotoa michango katika Jumba la Ufalme, tunawapa watoto pesa hizo ili wazitumbukize katika sanduku la michango,” asema baba yao anayeitwa Jason. “Wanafurahia jambo hilo kwa sababu wanapofanya hivyo, ‘wanampa Yehova kitu fulani.’” Inaelekea kwamba watoto wanaopata shangwe kwa kumpa Yehova kitu fulani wakiwa wachanga wataendelea kumwonyesha ukarimu hata watakapokuwa watu wazima.Met. 22:6.

YEHOVA NI MWENYE USAWAZIKO

12. Inamaanisha nini kuwa na usawaziko?

12 Usawaziko ni sifa nyingine ya Yehova yenye kuvutia sana. Inamaanisha nini kuwa na usawaziko? Neno la lugha ya awali ambalo kwa kawaida hutafsiriwa kuwa “usawaziko” katika Tafsiri ya Ulimwengu Mpya, kihalisi linamaanisha “kukubali maoni ya wengine.” (Tito 3:1, 2) Mtu mwenye usawaziko hasisitizi daima kufuata mambo madogo-madogo ya sheria, wala si mkali kupindukia, mgumu, au asiye na huruma. Badala yake, anajitahidi sana kuwatendea wengine kwa wororo, akijali hali zao. Yuko tayari kuwasikiliza wengine, na inapofaa, hukubali maoni yao na kubadili matakwa yake.

13, 14. (a) Yehova huonyeshaje usawaziko? (b) Tunajifunza nini kuhusu usawaziko kutokana na jinsi Yehova alivyoshughulika na Loti?

13 Yehova huonyeshaje usawaziko? Kwa fadhili, yeye hujali hisia za watumishi wake, na mara nyingi anakubali maombi yao. Kwa mfano, fikiria jinsi Yehova alivyoshughulika na Loti, yule mwanamume mwadilifu. Yehova alipoazimia kuyaangamiza majiji ya Sodoma na Gomora, alimpa Loti maagizo ya wazi kwamba akimbilie milimani. Hata hivyo, kwa sababu fulani Loti alimsihi Yehova amruhusu akimbilie eneo lingine. Hebu fikiria—kwa kweli Loti alimwomba Yehova abadili maagizo Yake!Soma Mwanzo 19:17-20.

14 Huenda ikawa rahisi kusema kwamba Loti alikuwa na imani dhaifu au hakuwa mtiifu. Kwa vyovyote vile, bila shaka Yehova angemwokoa Loti popote pale, kwa hiyo Loti hakuwa na sababu ya kuhofu. Hata hivyo, alihofu—hivyo ndivyo Loti alivyohisi, na Yehova alijali maoni yake. Alimruhusu Loti kukimbilia katika jiji ambalo Yehova alikusudia kuangamiza. (Soma Mwanzo 19:21, 22.) Ni wazi kwamba Yehova si mkali kupindukia wala hashikilii sana maoni yake. Yeye hukubali maoni ya wengine na ni mwenye usawaziko.

15, 16. Sheria ya Musa ilionyeshaje usawaziko wa Yehova? (Tazama picha kwenye ukurasa wa 12.)

15 Fikiria mfano mwingine katika Sheria ya Musa unaoonyesha usawaziko wa Yehova. Ikiwa Mwisraeli alikuwa maskini sana hivi kwamba hangeweza kutoa dhabihu ya mwana-kondoo au mbuzi, angeweza kutoa njiwa-tetere wawili au hua wawili. Lakini namna gani ikiwa Mwisraeli alikuwa maskini sana hivi kwamba hangeweza kupata hua wawili? Katika hali hiyo, Yehova alimruhusu Mwisraeli huyo maskini kutoa kiasi kidogo cha unga. Hata hivyo, kumbuka jambo hili muhimu: Ulipaswa kuwa unga anaoweza kuwatayarishia wageni waheshimiwa, yaani, “unga laini,” wala si unga wowote tu. (Mwa. 18:6) Kwa nini hilo ni jambo muhimu?Soma Mambo ya Walawi 5:7, 11.

16 Hebu jiwazie ukiwa Mwisraeli maskini sana. Unapofika kwenye maskani ukiwa na kiasi kidogo cha unga ili kutoa dhabihu, unawaona Waisraeli matajiri wakileta mifugo. Huenda ukaaibika kwa sababu ya dhabihu yako ya unga inayoonekana kuwa haina thamani. Kisha, unakumbuka kwamba machoni pa Yehova, dhabihu yako ina thamani sana. Kwa nini? Kwa sababu Yehova aliagiza kwamba unga huo ulipaswa kuwa bora kabisa. Ni kana kwamba Yehova alikuwa akiwaambia hivi Waisraeli maskini: ‘Ninaelewa kwamba huwezi kutoa kama wengine,  lakini ninajua pia kwamba unanipa kilicho bora zaidi.’ Kwa kweli, Yehova anaonyesha usawaziko kwa kutilia maanani upungufu wa watumishi wake na anaelewa hali zao.—Zab. 103:14.

17. Unaweza kuwa na hakika kwamba Yehova anakubali utumishi wa aina gani?

 17 Tunaweza kufarijiwa tunapojua kwamba Yehova hukubali utumishi wetu wa nafsi yote kwa sababu ya sifa yake ya usawaziko. (Kol. 3:23) Dada mmoja Mwitaliano aliyezeeka aitwaye Constance alisema hivi: “Hakuna jambo ninalopenda zaidi kuliko kuzungumza na wengine kuhusu Muumba wangu. Ndiyo sababu ninaendelea kuhubiri na kuongoza mafunzo ya Biblia. Nyakati nyingine ninasikitika kwamba siwezi kufanya mengi zaidi kwa sababu ya afya yangu. Lakini ninatambua kwamba Yehova anajua upungufu wangu na ananipenda na kuthamini kile ninachotimiza.”

IGA USAWAZIKO WA YEHOVA

18. Wazazi wanaweza kuiga mfano wa Yehova katika njia gani?

18 Tunawezaje kuiga usawaziko wa Yehova? Fikiria tena jinsi Yehova alivyoshughulika na Loti. Yehova ndiye aliyekuwa na mamlaka; hata hivyo, alimsikiliza Loti kwa fadhili alipokuwa akieleza jinsi anavyohisi. Na Mungu alikubali ombi la Loti. Ikiwa wewe ni mzazi, je, unaweza kuiga mfano wa Yehova? Je, unaweza kusikiliza maombi ya watoto wako, na inapofaa, kukubali maombi yao? Kuhusiana na hilo, gazeti la Mnara wa Mlinzi la Septemba 1, 2007, lilitaja kwamba huenda wazazi fulani wakazungumza na watoto wao wanapoweka sheria za nyumbani. Kwa mfano, wazazi huamua kuweka wakati hususa wa kurudi nyumbani, na kwa kweli wana haki ya kuchagua saa hususa wanayotaka watoto wafike nyumbani. Hata hivyo, huenda wazazi Wakristo wakasikiliza maoni ya watoto wao kuhusu saa iliyowekwa. Katika visa fulani, wazazi wanaweza kuamua kubadili saa waliyowawekea watoto wao ikiwa kufanya hivyo hakuvunji kanuni za Biblia. Wazazi wanaweza kugundua kwamba wanapotilia maanani maoni ya watoto wao wanapoweka sheria za nyumbani, watoto wataelewa sheria hizo na kuzitii kwa utayari zaidi.

19. Wazee wanawezaje kujitahidi kuiga usawaziko wa Yehova?

19 Wazee wa kutaniko hujitahidi kuiga usawaziko wa Yehova kwa kutilia maanani hali za waamini wenzao. Kumbuka kwamba Yehova alithamini pia dhabihu zilizotolewa na Waisraeli maskini. Vivyo hivyo, baadhi ya ndugu na dada hawawezi kufanya mengi katika utumishi, labda kwa sababu ya matatizo ya kiafya au kuzeeka. Namna gani ikiwa wapendwa hao wanavunjika moyo kwa sababu hawawezi kufanya mengi katika huduma? Wazee wanaweza kuwahakikishia kwa fadhili kwamba Yehova anawapenda kwa sababu wanampa kilicho bora.Marko 12:41-44.

20. Je, kuwa na usawaziko kunamaanisha kutomtumikia Mungu kwa moyo wote? Eleza.

20 Bila shaka, hatupaswi kamwe kufikiri kimakosa kwamba tunaonyesha usawaziko kwa kutomtumikia Mungu kwa moyo wote kwa sababu tu tunataka kujitendea kwa fadhili. (Mt. 16:22) Hatutaki kufanya machache tu na kisha kutetea mtazamo huo tukisema kwamba tuna usawaziko. Badala yake, sote tunahitaji ‘kujitahidi sana’ kuunga mkono kazi ya Ufalme. (Luka 13:24) Kwa kweli, tunajitahidi kusawazisha kanuni mbili. Kwa upande mmoja, tunajitahidi sana kutofanya machache katika utumishi wetu. Kwa upande mwingine, tunakumbuka kwamba Yehova hatazamii tutimize mengi zaidi ya uwezo wetu. Tunapompa kilicho bora, tuna hakika kwamba anafurahi. Je, hatufurahi kumtumikia Bwana huyo mwenye uthamini na usawaziko? Katika makala inayofuata, tutachunguza sifa nyingine mbili zinazovutia za utu wa Yehova.Zab. 73:28.

“Mheshimu Yehova kwa vitu vyako vyenye thamani.”—Met. 3:9 (Tazama fungu la 11)

“Lolote mnalofanya, lifanyeni kwa nafsi yote.”—Kol. 3:23 (Tazama fungu la 17)