Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

“Wana wa Mungu wa kweli” wanaotajwa katika Mwanzo 6:2 na 4 walioishi kabla ya Gharika ni nani?

Uthibitisho unaonyesha kwamba maneno hayo yanarejelea wana wa roho wa Mungu. Uthibitisho gani?

Mstari wa pili unasomeka hivi: “Wana wa Mungu wa kweli wakaanza kuwaona mabinti wa wanadamu, kwamba ni wenye sura ya kupendeza; nao wakajichukulia wake, yaani, wote waliowachagua.”—Mwa. 6:2.

Katika Maandiko ya Kiebrania, maneno “wana wa Mungu wa kweli” na “wana wa Mungu” yanapatikana katika Mwanzo 6:2, 4; Ayubu 1:6; 2:1; 38:7; na Zaburi 89:6. Maandiko hayo yanaonyesha nini kuhusu “wana [hao] wa Mungu”?

Ni wazi kwamba “wana wa Mungu wa kweli” tunaosoma kuwahusu katika Ayubu 1:6 walikuwa viumbe wa roho waliokusanyika mbele za Mungu. Shetani aliyetoka “kuzurura huku na huku duniani,” alikuwa miongoni mwa viumbe hao wa roho. (Ayu. 1:7; 2:1, 2) Vivyo hivyo, katika Ayubu 38:4-7, tunasoma kuhusu ‘wana wa Mungu’ ‘waliopaaza sauti kwa kushangilia’ Mungu ‘alipoweka jiwe la pembeni’ la dunia. Kwa sababu wanadamu hawakuwa wameumbwa, ni lazima wana hao walikuwa wana wa kimalaika wa Mungu. “Wana wa Mungu” wanaotajwa katika Zaburi 89:6 lazima wawe ni viumbe wa kimbingu walio pamoja na Mungu, wala si wanadamu.

Basi, “wana wa Mungu wa kweli” wanaotajwa katika Mwanzo 6:2 na 4 ni nani? Kulingana na ushahidi wa Biblia tuliozungumzia, ni jambo linalopatana na akili kusema kwamba simulizi hilo linarejelea wana wa roho wa Mungu waliokuja duniani.

Ni vigumu kwa wengine kukubali kwamba malaika wanaweza kutamani kuwa na mahusiano ya kingono. Maneno ya Yesu katika Mathayo 22:30 yanaonyesha kwamba mbinguni hakuna ndoa wala mahusiano ya kingono. Hata hivyo, katika pindi fulani malaika walivaa miili ya kibinadamu, na hata kula na kunywa pamoja na wanadamu. (Mwa. 18:1-8; 19:1-3) Hivyo, ni jambo linalopatana na akili kufikia mkataa kwamba wakiwa wamejivika miili ya kibinadamu, wangeweza kufanya ngono na wanawake.

Kuna sababu zinazotegemea Biblia za kuamini kwamba malaika fulani walifanya hivyo. Andiko la Yuda 6, 7 linalinganisha dhambi ya watu wa Sodoma, waliofuatilia mwili kwa ajili ya matumizi yasiyo ya asili, na dhambi ya ‘malaika ambao hawakubaki mahali pao pa kwanza bali waliyaacha makao yao wenyewe yanayofaa.’ Malaika hao walikuwa kama watu wa Sodoma kwa sababu ‘walifanya uasherati kwa kuzidi mno na kwenda kufuatilia mwili kwa ajili ya matumizi yasiyo ya asili.’ Andiko la 1 Petro 3:19, 20 linalozungumzia habari hiyo linahusianisha malaika hao wasiotii na “siku za Noa.” (2 Pet. 2:4, 5) Hivyo, mwelekeo wa kutotii walioonyesha malaika katika siku za Noa unaweza kulinganishwa na dhambi ya Sodoma na Gomora.

Mkataa huo unapatana na akili hasa tunapotambua kwamba “wana wa Mungu wa kweli” wanaotajwa katika Mwanzo 6:2 na 4 ni malaika waliojivika miili ya kibinadamu na kufanya uasherati na wanawake.

 Biblia inasema kwamba Yesu ‘aliwahubiria roho walio gerezani.’ (1 Pet. 3:19) Hilo linamaanisha nini?

Mtume Petro anasema kwamba roho hao ni wale ambao “wakati fulani hawakuwa watiifu wakati subira ya Mungu ilipokuwa ikingoja katika siku za Noa.” (1 Pet. 3:20) Ni wazi kwamba Petro alikuwa akirejelea viumbe wa roho waliochagua kuunga mkono uasi wa Shetani. Yuda anataja malaika ambao “hawakubaki mahali pao pa kwanza bali wakayaacha makao yao wenyewe yanayofaa,” akisema kwamba Mungu “amewaweka akiba wakiwa na vifungo vya milele chini ya giza zito kwa ajili ya hukumu ya ile siku kuu.”—Yuda 6.

Viumbe wa roho walikosa kutii katika siku za Noa kwa njia gani? Kabla ya Gharika, roho hao waovu walijivika miili ya kibinadamu—jambo ambalo Mungu hakuwa amekusudia malaika wafanye. (Mwa. 6:2, 4) Isitoshe, malaika hao waliofanya ngono na wanawake walikuwa wakifanya jambo lisilo la asili. Mungu hakuwaumba viumbe wa roho wafanye ngono na wanawake. (Mwa. 5:2) Mungu atawaharibu malaika hao waovu na wasiotii wakati wake utakapofika. Kwa sasa, kama Yuda anavyosema, ni kama wako chini ya “giza zito,” yaani, gereza la kiroho la mfano.

Yesu aliwahubiria lini na jinsi gani “roho walio gerezani”? Petro anaandika kwamba jambo hilo lilitukia baada ya Yesu ‘kufanywa kuwa hai katika roho.’ (1 Pet. 3:18, 19) Ona pia kwamba Petro anasema kuwa Yesu ‘aliwahubiria.’ Petro anatumia neno linaloonyesha tendo la wakati uliopita kudokeza kwamba Yesu aliwahubiria roho hao kabla Petro hajaandika barua yake ya kwanza. Hivyo basi, inaonekana kwamba muda fulani baada ya kufufuliwa, Yesu aliwatangazia roho hao waovu habari kuhusu hukumu waliyostahili kabisa ambayo watapata. Hayakuwa mahubiri yaliyowapa tumaini lolote. Yalikuwa mahubiri ya kihukumu. (Yona 1:1, 2) Mara tu Yesu alipokuwa amedhihirisha imani na ushikamanifu wake hadi kifo na kufufuliwa na hivyo kuthibitisha wazi kwamba Ibilisi hakuwa na uwezo juu yake, Yesu alikuwa na msingi wa kutangaza ujumbe huo wa kihukumu.—Yoh. 14:30; 16:8-11.

Wakati ujao, Yesu atamfunga Shetani pamoja na malaika hao na kuwatupa ndani ya abiso. (Luka 8:30, 31; Ufu. 20:1-3) Kabla ya wakati huo, roho hao wasiotii wako katika hali ya giza zito la kiroho, na bila shaka wataharibiwa kabisa hatimaye.Ufu. 20:7-10.