Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Biblia inasema nini kuhusu kutoa kiapo?

Kiapo kinaweza kufafanuliwa kuwa “tangazo au ahadi rasmi iliyo nzito ya kutimiza jambo fulani, na mara nyingi Mungu anatajwa . . . kuwa shahidi.” Mtu anaweza kutoa kiapo kupitia maneno au maandishi.

Huenda baadhi ya watu wakafikiri kwamba ni kosa kutoa kiapo kwa sababu Yesu alisema: “Msiape kamwe . . . Acheni ‘Ndiyo’ yenu imaanishe ndiyo, na ‘Siyo’ yenu, siyo, kwa maana linalozidi hayo linatoka kwa yule mwovu.” (Mt. 5:33-37) Bila shaka, Yesu alijua kwamba Sheria ya Musa ilihusisha kuapa na kwamba pindi mbalimbali watumishi waaminifu wa Mungu waliapa. (Mwa. 14:22, 23; Kut. 22:10, 11) Pia, alijua kwamba hata Yehova mwenyewe alikuwa ameapa pindi mbalimbali. (Ebr. 6:13-17) Basi, Yesu hakumaanisha kwamba hatupaswi kamwe kuapa. Badala yake, alikuwa akionya dhidi ya kuapa kuhusu mambo madogo-madogo au yasiyo muhimu. Tunapaswa kuona kwamba kutimiza ahadi yetu ni wajibu mtakatifu. Tunapaswa kutimiza ahadi tunazotoa.

Basi, unapaswa kufanya nini unapoombwa kutoa kiapo? Kwanza, hakikisha kwamba unaweza kutimiza jambo unaloapa kufanya. Ikiwa huna uhakika, ni jambo la busara kuepuka kutoa kiapo. Neno la Mungu linatuonya hivi: “Ni afadhali usiweke nadhiri kuliko kuweka nadhiri na kukosa kuitimiza.” (Mhu. 5:5) Kisha, chunguza kanuni za Kimaandiko zinazohusiana na kiapo hicho, halafu tenda kulingana na dhamiri yako iliyozoezwa. Unaweza kuchunguza kanuni gani za Kimaandiko?

Baadhi ya viapo havipingani na mapenzi ya Mungu. Kwa mfano, Mashahidi wa Yehova hutoa nadhiri wanapofunga ndoa. Nadhiri hizo ni aina ya kiapo. Mbele za Mungu na mashahidi, bwana na bibi harusi hutoa ahadi kwamba watapendana, watatunzana, na kuheshimiana na kwamba watafanya hivyo “kwa muda wote ambao [wote wawili wataishi].” (Huenda wenzi wengine wasiseme maneno hayohayo wanapofunga ndoa, lakini bado wanatoa nadhiri mbele za Mungu.) Kisha wanatangazwa kuwa mume na mke, na wanapaswa kuendelea kuwa mume na mke kwa maisha yao yote. (Mwa. 2:24; 1 Kor. 7:39) Mpango huo unafaa kabisa, na unapatana na mapenzi ya Mungu.

Baadhi ya viapo vinapingana na mapenzi ya Mungu. Mkristo wa kweli hatatoa kiapo cha aina hiyo, kama vile kiapo cha kutetea nchi yake kwa kutumia silaha au kukana imani yake katika Mungu. Kufanya hivyo ni kuvunja amri za Mungu. Wakristo hawapaswi kuwa “sehemu ya ulimwengu,” basi hatujihusishi katika mizozo na mapambano ya ulimwengu.—Yoh. 15:19; Isa. 2:4; Yak. 1:27.

Baadhi ya viapo vinahusisha dhamiri yetu. Nyakati nyingine, huenda tukahitaji kuchanganua kiapo kwa kutegemea shauri hili la Yesu: “Mlipeni Kaisari vitu vya Kaisari, na Mungu vitu vya Mungu.”​—Luka 20:25.

Kwa mfano, tuseme kwamba Mkristo ametuma ombi la kupata uraia au pasipoti na anatambua kwamba anapaswa kutoa kiapo cha utii. Ikiwa katika nchi hiyo kiapo hicho kinamaanisha kuapa kwamba atatenda kwa njia iliyo kinyume na sheria ya Mungu, basi dhamiri yake iliyozoezwa na Biblia haitamruhusu kutoa kiapo hicho. Hata hivyo, huenda serikali hiyo ikamruhusu kurekebisha maneno ya kiapo hicho ili yapatane na dhamiri yake.

Huenda kutoa kiapo cha utii kilichorekebishwa kukapatana na kanuni ya Waroma 13:1, inayosema: “Kila mtu na ajitiishe kwa mamlaka zilizo kubwa.” Basi, Mkristo anaweza kuamua kwamba si kosa kuapa kufanya jambo ambalo tayari Mungu amemwagiza afanye.

Dhamiri pia inahusika unapoombwa kutumia kitu fulani au kutumia ishara ya mwili unapotoa kiapo. Waroma na Wasikithe wa kale waliapa kwa kutumia upanga wao, ishara ya mungu wa vita, ili kutoa uhakikisho kwamba wangekuwa waaminifu. Wagiriki walinyoosha mkono kuelekea mbinguni walipotoa kiapo. Hivyo walionyesha kwamba wanatambua kuna mungu ambaye aliona kile kilichosemwa na kufanywa na kwamba wanadamu waliwajibika kwake.

Bila shaka, mtumishi wa Yehova hawezi kamwe kuapa kwa kutumia nembo yoyote ya kitaifa inayohusiana na ibada ya uwongo. Lakini vipi ukiagizwa mahakamani uweke mkono juu ya Biblia na kuapa kwamba utatoa ushahidi wa kweli? Katika kisa hicho, huenda ukakubali kufanya hivyo, kwa kuwa Maandiko yanawataja watumishi waaminifu waliofanya ishara fulani walipokuwa wakitoa kiapo. (Mwa. 24:2, 3, 9; 47:29-31) Ni muhimu kukumbuka kwamba ukitoa kiapo kama hicho, unaapa mbele za Mungu kwamba utasema ukweli. Unapaswa kuwa tayari kusema ukweli unapojibu swali lolote ambalo utaulizwa.

Kwa kuwa tunathamini uhusiano wetu pamoja na Yehova, tunapaswa kusali na kufikiria kwa makini kuhusu kiapo chochote tunachoombwa kutoa, na kuhakikisha kwamba hakipingani na dhamiri yetu au kanuni za Biblia. Ukiamua kutoa kiapo unapaswa kuhakikisha kwamba unatimiza kiapo hicho.​—1 Pet. 2:12.