Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 SIMULIZI LA MAISHA

Kumtii Yehova Kumeleta Baraka Nyingi

Kumtii Yehova Kumeleta Baraka Nyingi

“Tunajifunza somo zuri kama nini kutoka kwa Noa!” akasema baba yangu. “Noa alimtii Yehova na kuipenda familia yake, na wote waliokoka Gharika kwa sababu familia yote iliingia ndani ya safina.”

HILO ni mojawapo ya mambo ya zamani zaidi ninayokumbuka kumhusu baba yangu, mwanamume mnyenyekevu na mwenye bidii ya kazi. Alipenda sana haki, kwa hiyo alivutiwa mara moja na ujumbe wa Biblia alipousikia katika mwaka wa 1953. Tangu wakati huo na kuendelea, alifanya yote aliyoweza ili kutufundisha tukiwa watoto mambo aliyokuwa akijifunza. Mwanzoni mama yangu alisita kuacha desturi za dini ya Katoliki. Hata hivyo, baada ya muda yeye pia akaanza kuthamini mafundisho ya Biblia.

Ilikuwa vigumu kwa wazazi wetu kutufundisha Biblia kwa kuwa Mama hakujua kusoma wala kuandika vizuri, naye Baba alifanya kazi ngumu kwa saa nyingi shambani. Pindi nyingine alichoka sana hivi kwamba alisinzia wakati wa funzo. Hata hivyo, jitihada zake hazikuwa za bure. Nilikuwa mtoto wa kwanza katika familia yetu, hivyo, niliwasaidia wazazi wangu kumfundisha dada yangu na ndugu zangu wawili. Hilo lilitia ndani jambo fulani alilotaja Baba mara nyingi, yaani, upendo wa Noa kwa familia yake, aliouonyesha kwa kumtii Mungu. Nilipenda sana simulizi hilo la Biblia! Baada ya muda mfupi, sote tulikuwa tukihudhuria mikutano katika Jumba la Ufalme huko Roseto degli Abruzzi, mji ulio kwenye pwani ya Adriatiki nchini Italia.

Nilikuwa na umri wa miaka 11 tu katika mwaka 1955 nilipovuka na mama yangu milima iliyo magharibi mwa nchi ili kuhudhuria kusanyiko letu la kwanza la wilaya huko Rome. Tangu wakati huo, nimeyaona makusanyiko hayo makubwa kuwa mojawapo ya sehemu zinazopendeza zaidi za maisha ya Mkristo.

Mwaka uliofuata nilibatizwa, na baada ya muda mfupi nikaanza utumishi wa wakati wote. Nilipokuwa na umri wa miaka 17, niliwekwa rasmi kuwa painia wa pekee katika jiji la Latina, upande wa kusini wa jiji la Rome, kilomita 300 hivi kutoka nyumbani. Lilikuwa jiji jipya, hivyo hakuna yeyote aliyehofu sana maoni ya jirani zake. Mimi na painia mwenzangu tulifurahia sana kuwaachia watu machapisho mengi ya Biblia, hata hivyo, kwa kuwa nilikuwa na umri mdogo, nilitamani sana kurudi nyumbani! Lakini, niliazimia kutii agizo nililopewa.

Siku yetu ya harusi

 Baadaye nilipewa mgawo wa kusaidia kufanya matayarisho ya Kusanyiko la Kimataifa la mwaka 1963 lenye kichwa “Habari Njema za Milele,” lililofanywa katika jiji la Milan. Katika kusanyiko hilo, nilifanya kazi nikiwa mjitoleaji pamoja na wengine wengi, kutia ndani Paolo Piccioli, ndugu kijana kutoka Florence. Siku ya pili ya kusanyiko, alitoa hotuba yenye kuchochea sana kuhusu useja. Ninakumbuka nikiwaza hivi, ‘Bila shaka ndugu huyu hataoa kamwe.’ Hata hivyo, tulianza kuandikiana barua na baada ya muda ikawa wazi kwamba mapendezi yetu mengi yalifanana, yaani, tulikuwa na miradi ileile, sote tulimpenda Yehova, na tulitaka sana kumtii. Nilifunga ndoa na Paolo mwaka wa 1965.

KUPAMBANA NA MAKASISI

Nilitumikia kwa miaka kumi nikiwa painia wa kawaida katika jiji la Florence. Lilikuwa jambo lenye kusisimua kuona ongezeko katika makutaniko na hasa kuona vijana wakifanya maendeleo. Mimi na Paolo tulifurahia kutumia wakati wetu pamoja nao kuzungumzia mambo ya kiroho na kufurahia tafrija, na katika pindi hizo Paolo alicheza mpira wa miguu. Ni kweli kwamba nilithamini kutumia wakati pamoja na mume wangu, lakini niliona wazi kwamba vijana hao na familia katika kutaniko zilihitaji na zilifaidika Paolo alipotumia wakati wake kuwa nao na kupendezwa nao kwa fadhili.

Bado mimi hupata shangwe ninapokumbuka mafunzo mengi ya Biblia tuliyoongoza. Nilijifunza na Adriana, aliyezungumza na familia mbili kuhusu mambo aliyokuwa akijifunza. Familia hizo zikapanga tuwe na mkutano na kasisi ili kuzungumzia mafundisho ya kanisa kama vile Utatu na kutokufa kwa nafsi. Makasisi watatu walifika katika mkutano huo. Maelezo yao kuhusu mafundisho hayo hayakueleweka na yalipingana, jambo lililogunduliwa kwa urahisi na wanafunzi wetu wa Biblia walipolinganisha maelezo hayo na mafundisho ya Biblia yaliyo wazi. Kwa kweli, mkutano huo ulileta mabadiliko makubwa. Baada ya muda, washiriki 15 hivi wa familia hizo wakawa Mashahidi.

Ni kweli kwamba siku hizi tunatumia njia tofauti kabisa za kuhubiri. Wakati huo, Paolo alikuwa “mtaalamu” wa kupambana na makasisi, naye alipambana nao mara kadhaa. Ninakumbuka mkutano mmoja uliofanywa mbele ya wasikilizaji wasio Mashahidi. Yaonekana kwamba wapinzani walipanga mapema wasikilizaji fulani waulize maswali ya ubishi. Hata hivyo, mambo hayakuwa hivyo. Mtu mmoja aliuliza ikiwa ni jambo linalofaa kwa kanisa kujihusisha na siasa kama lilivyofanya kwa karne nyingi. Wakati huo, ilikuwa wazi kwamba makasisi walikuwa mashakani. Kwa ghafla, taa zikazima na mkutano ukavunjwa. Miaka mingi baadaye tukajua kwamba makasisi ndio waliopanga kuzima taa ikiwa mazungumzo hayangeenda kama walivyopanga.

 MAPENDELEO MAPYA YA UTUMISHI

Miaka kumi baada ya kufunga ndoa na Paolo, tulipewa mgawo wa kuzungukia makutaniko. Paolo alikuwa na kazi nzuri hivyo haikuwa rahisi kukubali mgawo huo. Hata hivyo, baada ya kutafakari na kusali kuhusu jambo hilo, tulikubali mgawo huo mpya wa utumishi. Tulifurahia kukaa pamoja na familia zilizotukaribisha. Mara nyingi tulijifunza jioni tukiwa kikundi, kisha Paolo aliwasaidia watoto kufanya kazi za shule hasa hesabu. Zaidi ya hayo, Paolo alikuwa msomaji mwenye bidii na aliwaambia wengine kwa msisimko mambo yenye kuvutia na yenye kujenga aliyosoma. Mara nyingi tulienda kuhubiri katika miji isiyo na Mashahidi kila Jumatatu, tukiwaalika watu ili waje kusikiliza hotuba jioni.

Tulifurahia sana kutumia wakati wetu pamoja na vijana, na katika pindi hizo Paolo alicheza mpira wa miguu

Baada ya miaka miwili tu katika kazi ya mzunguko, tulialikwa kutumikia Betheli katika jiji la Rome. Paolo alipewa mgawo katika idara ya sheria, na mimi nilipewa mgawo katika Idara ya Magazeti. Badiliko hilo halikuwa rahisi, lakini tuliazimia kuwa watiifu. Ilisisimua kuona upanuzi wa hatua kwa hatua wa ofisi ya tawi na ongezeko kubwa la ndugu zetu nchini Italia. Wakati huo ndipo Mashahidi wa Yehova walipotambuliwa kisheria nchini Italia. Bila shaka, tulifurahia utumishi huo.

Paolo alipenda kazi yake Betheli Paolo loved his work at Bethel

Tulipokuwa tukitumikia Betheli, msimamo wetu unaotegemea Biblia kuhusu damu ulijaribiwa Italia. Mwanzoni mwa miaka ya 1980, kulikuwa na kesi kuhusu suala hilo iliyosababisha upinzani mkubwa sana. Wenzi fulani wa ndoa waliokuwa Mashahidi, walishtakiwa kwa uwongo kwamba walisababisha kifo cha binti yao, ingawa alikufa kutokana na ugonjwa fulani mbaya wa damu unaorithiwa na watu wengi wanaoishi katika eneo la Mediterania. Ndugu na dada wa familia ya Betheli waliwasaidia mawakili waliowatetea wazazi hao Wakristo. Trakti na toleo maalumu la Amkeni! liliwasaidia watu kujua ukweli wa mambo na kuelewa kwa usahihi maoni ya Neno la Mungu kuhusu damu. Katika miezi hiyo, mara nyingi Paolo alifanya kazi kwa saa 16 hivi kwa siku bila kupumzika. Nilifanya yote niwezayo kuunga mkono jitihada zake muhimu.

BADILIKO LINGINE MAISHANI

Tulikuwa tumeoana kwa miaka 20 wakati mambo yalipobadilika kwa ghafla. Nilikuwa na umri wa miaka 41 naye Paolo alikuwa na miaka 49 nilipomwambia ninahisi kwamba nina mimba. Aliandika hivi katika kitabu chake cha kumbukumbu siku niliyomwambia kuhusu hali yangu: “Sala: Ikiwa ni kweli, tusaidie tubaki katika utumishi wa wakati wote, tusipunguze bidii yetu ya kiroho, na tuwe wazazi wazuri kupitia mfano wetu. Zaidi ya yote, nisaidie nitende angalau asilimia 1 ya yote niliyosema jukwaani katika kipindi cha miaka 30 hivi iliyopita.” Ninapoangalia maisha yetu, ni wazi kwamba Yehova alijibu sala yake na yangu.

 Maisha yetu yalibadilika sana baada ya kumzaa Ilaria. Kwa kweli, pindi nyingine tulivunjika moyo kama Methali 24:10 inavyosema: “Je, umejionyesha kuwa umevunjika moyo siku ya taabu? Nguvu zako zitakuwa chache.” Hata hivyo tulitegemezana huku tukikumbuka umuhimu wa kutiana moyo.

Ilaria husema bila kusita jinsi anavyofurahi kuwa na wazazi wawili Mashahidi waliokuwa na mengi ya kufanya katika utumishi wa wakati wote. Hajawahi kamwe kuhisi kwamba anapuuzwa, badala yake alikua katika familia yenye hali za kawaida kabisa. Nilikaa naye wakati wa mchana. Paolo aliporudi nyumbani jioni, mara nyingi alihitaji kumalizia kazi fulani; hata hivyo, alitumia wakati wake pamoja na Ilaria, akicheza naye na kumsaidia kazi za shule. Alifanya hivyo hata kama ingemaanisha kwamba angehitaji kuendelea na kazi yake hadi saa nane au saa tisa usiku. Mara nyingi Ilaria alisema, “Baba ndiye rafiki yangu bora zaidi.”

Kama ujuavyo, tulihitaji kuwa na msimamo thabiti ili kumsaidia Ilaria kubaki katika njia ya Kikristo. Nakumbuka pindi moja alitenda isivyofaa alipokuwa akicheza na rafiki yake. Tulitumia Biblia kumweleza kwa nini hapaswi kutenda hivyo. Pia tukamwambia amwombe msamaha rafiki yake mbele yetu.

Ilaria husema wazi jinsi anavyothamini sana upendo ambao wazazi wake walionyesha kwa ajili ya huduma. Kwa kuwa sasa ameolewa, anaelewa vizuri hata zaidi umuhimu wa kutii na kufuata mwongozo wa Yehova.

TULITII HATA NYAKATI ZA HUZUNI

Mwaka wa 2008, Paolo alijua kwamba ana ugonjwa wa kansa. Mwanzoni ilionekana kwamba angepona ugonjwa huo, naye alinitia moyo sana. Mbali na kutafuta matibabu bora zaidi, mimi na Ilaria tulitoa sala nyingi ndefu kwa Yehova, tukimwomba atusaidie kukabiliana na hali hiyo. Hata hivyo, nilishuhudia mwanamume huyo ambaye wakati mmoja alikuwa mwenye nguvu na afya njema, akidhoofika polepole. Kifo chake katika mwaka wa 2010 kilikuwa pigo kubwa sana. Hata hivyo, ninafarijiwa sana na tuliyotimiza kwa miaka 45 tuliyokuwa pamoja. Tulimpa Yehova kilicho bora kabisa. Ninajua kwamba kazi yetu ina thamani ya kudumu. Nina hamu kubwa ya kumwona Paolo akifufuliwa kama alivyosema Yesu katika Yohana 5:28, 29.

“Moyoni, mimi bado ni yule msichana mdogo anayependa sana simulizi la Noa. Azimio langu halijabadilika”

Moyoni, mimi bado ni yule msichana mdogo anayependa sana simulizi la Noa. Azimio langu halijabadilika. Ninataka kumtii Yehova katika kila jambo. Nina uhakika kwamba vikwazo, kujidhabihu, au misiba ya aina yoyote ni mambo madogo sana yanapolinganishwa na baraka nzuri ajabu tunazopewa na Mungu wetu mwenye upendo. Mimi binafsi nimejionea jambo hilo na ninakuhakikishia kwamba ni muhimu kuwa na uhakika huo.