Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Usichoke Kabisa’

‘Usichoke Kabisa’

“Tusife moyo katika kufanya yaliyo mema.”—GAL. 6:9.

1, 2. Uhakika wetu unaimarishwaje tunapotafakari kuhusu tengenezo la Yehova la ulimwenguni pote?

NI JAMBO linalostaajabisha sana kujua kwamba sisi ni sehemu ya tengenezo kubwa la ulimwenguni pote. Maono yaliyoandikwa katika Ezekieli sura ya 1 na Danieli sura ya 7 yanaonyesha waziwazi jinsi Yehova anavyoongoza mambo mpaka yatakapotimia. Yesu anaongoza katika kuielekeza sehemu ya kidunia ya tengenezo la Yehova ili ikazie fikira kazi ya kuhubiri habari njema, iwatunze kiroho wale wanaofanya kazi hiyo, na kuiendeleza ibada ya kweli ya Yehova. Hilo linatusaidia kuwa na uhakika kabisa katika tengenezo la Yehova.—Mt. 24:45.

2 Je, sisi binafsi tunasonga pamoja na tengenezo hilo zuri ajabu? Je, bidii yetu kwa ajili ya kweli inazidi kuongezeka au inapungua? Tunapofikiria maswali hayo, huenda tukagundua kwamba tumeanza kuchoka au labda bidii yetu imepungua. Inaweza kuwa hivyo. Katika karne ya kwanza, mtume Paulo alilazimika kuwahimiza Wakristo wenzake wafikirie kielelezo ambacho Yesu aliweka katika kuonyesha bidii. Paulo alisema kwamba kufanya hivyo kungewasaidia ‘kutochoka na kutozimia katika nafsi zao.’ (Ebr. 12:3) Vivyo hivyo, kuchunguza kwa makini makala iliyotangulia iliyoonyesha mambo yanayotimizwa na tengenezo la Yehova, kulipaswa kutusaidia sana kuendelea kuwa na bidii na uvumilivu.

3. Tunahitaji kufanya nini ili tusichoke kabisa, na tutachunguza nini katika makala hii?

3 Hata hivyo, Paulo alionyesha kwamba tunahitaji kufanya mengi zaidi ili tusichoke kabisa. Alisema kwamba tunahitaji kujitahidi “kufanya yaliyo mema.” (Gal. 6:9) Kwa hiyo, tunahitaji kuchukua hatua. Acheni tuchunguze mambo matano yanayoweza kutusaidia kuendelea kuwa imara na kusonga pamoja na tengenezo la Yehova. Kisha tunaweza kuamua kibinafsi ikiwa kuna mambo fulani tunayohitaji kukazia fikira zaidi tukiwa familia au mtu mmoja-mmoja.

 HUDHURIA MIKUTANO ILI KUTIANA MOYO NA KUABUDU

4. Kwa nini tunaweza kusema kwamba kukusanyika pamoja ni sehemu muhimu ya ibada ya kweli?

4 Sikuzote kukusanyika pamoja kumekuwa sehemu muhimu ya utendaji wa watumishi wa Yehova. Katika makao ya kimbingu, viumbe wa roho hualikwa kukusanyika pamoja mbele za Yehova katika pindi zinazofaa. (1 Fal. 22:19; Ayu. 1:6; 2:1; Dan. 7:10) Taifa la kale la Israeli lilipaswa kukusanyika ‘ili kusikiliza na ili kujifunza.’ (Kum. 31:10-12) Wayahudi wa karne ya kwanza walikuwa na desturi ya kwenda katika sinagogi kusoma Maandiko. (Luka 4:16; Mdo. 15:21) Kutaniko la Kikristo lilipoanzishwa, agizo hilo la kukusanyika pamoja liliendelea kukaziwa, na bado ni sehemu muhimu ya ibada yetu. Wakristo wa kweli ‘hufikiriana ili kuchocheana katika upendo na matendo mazuri.’ Tunahitaji kuendelea ‘kutiana moyo, na kufanya hivyo zaidi kwa kadiri tunavyoona siku ya Yehova kuwa inakaribia.’—Ebr. 10:24, 25.

5. Tunaweza kutiana moyo jinsi gani katika mikutano yetu?

5 Njia moja muhimu ya kutiana moyo ni kushiriki katika mikutano yetu. Tunaweza kutangaza hadharani imani yetu kwa kujibu swali, kueleza matumizi ya andiko, kusimulia jambo fupi lililoonwa linaloonyesha hekima ya kufuata kanuni za Biblia, au kwa njia nyinginezo. (Zab. 22:22; 40:9) Bila shaka, utakubali kwamba hata kama tumekuwa tukihudhuria mikutano kwa miaka mingapi, bado tunatiwa moyo tunaposikiliza maelezo yanayotoka moyoni ya ndugu na dada zetu, wazee kwa vijana.

6. Mikutano yetu inatusaidiaje kuendelea kuwa na bidii kiroho?

6 Ni sababu gani nyingine zinazomfanya Mungu wetu akazie umuhimu wa sisi kukusanyika pamoja kwa ukawaida? Mikutano na makusanyiko yetu hutusaidia kuwa hodari na kuhubiri kwa ujasiri na pia kukabiliana na upinzani au hali ya watu kutopendezwa na ujumbe wetu katika maeneo yetu. (Mdo. 4:23, 31) Mazungumzo ya Kimaandiko yanatuimarisha na kututia nguvu katika imani. (Mdo. 15:32; Rom. 1:11, 12) Mafundisho na pia ubadilishanaji wa kitia-moyo tunaopata katika mikutano yetu ya ibada hutusaidia kuwa na shangwe ya kweli na “utulivu kutokana na siku za msiba.” (Zab. 94:12, 13) Halmashauri ya Ufundishaji ya Baraza Linaloongoza husimamia kazi ya kutayarisha programu zote za kiroho za kuwaelimisha watu wa Yehova duniani pote. Tunapaswa kushukuru sana kwa sababu ya mafundisho yenye kujenga tunayoandaliwa katika mikutano yetu ya kila juma, kwa mwaka mzima.

7, 8. (a) Kusudi kuu la mikutano yetu ya kutaniko ni nini? (b) Mikutano inakusaidiaje kiroho?

7 Hata hivyo, kuna jambo muhimu zaidi kuliko manufaa ya kibinafsi tunayopata katika mikutano yetu. Kusudi kuu linalotufanya tukusanyike pamoja ni kumwabudu Yehova. (Soma Zaburi 95:6.) Ni pendeleo kubwa kama nini kumsifu Mungu wetu mzuri ajabu! (Kol. 3:16) Yehova anastahili ibada tunayotoa kwa ukawaida tunapohudhuria na kushiriki katika mikutano yetu ya kitheokrasi. (Ufu. 4:11) Basi haishangazi kwamba tunahimizwa ‘kutoacha kukusanyika pamoja sisi wenyewe, kama vile wengine walivyo na desturi.’—Ebr. 10:25.

8 Je, tunaiona mikutano yetu ya Kikristo kuwa uandalizi wa kutusaidia kuvumilia mpaka Yehova atakapouharibu mfumo huu mwovu wa mambo? Ikiwa ndivyo, mikutano yetu itakuwa kati ya “mambo yaliyo ya maana zaidi,” ambayo tunatanguliza katika maisha yetu yenye shughuli nyingi. (Flp. 1:10) Hatupaswi kamwe kukosa fursa ya kuungana na ndugu zetu katika kumwabudu Yehova isipokuwa tuwe na sababu kubwa sana ya kutohudhuria.

 TAFUTA WATU WENYE MIOYO MINYOOFU

9. Tunajuaje kwamba kazi ya kuhubiri ni muhimu?

9 Kushiriki kikamili katika kazi ya kuhubiri hutusaidia pia kusonga pamoja na tengenezo la Yehova. Yesu alianzisha kazi hiyo alipokuwa hapa duniani. (Mt. 28:19, 20) Tangu wakati huo, kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme na kufanya wanafunzi imekuwa kazi kuu ya tengenezo lote la Yehova. Mambo mengi yaliyoonwa yanathibitisha kwamba malaika wanaunga mkono kazi yetu na kutuelekeza kwa watu ‘wenye mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uzima wa milele.’ (Mdo. 13:48; Ufu. 14:6, 7) Leo pia kuna sehemu ya kidunia ya tengenezo la Yehova iliyopangwa ili kuitegemeza kazi hii muhimu sana. Je, tunatanguliza huduma hiyo maishani mwetu?

10. (a) Ukitumia jambo lililoonwa, eleza jinsi tunavyoweza kudumisha shauku yetu kwa ajili ya kweli. (b) Huduma imekusaidiaje kutochoka kabisa?

10 Kuwa na bidii katika huduma hutusaidia kudumisha shauku yetu kuelekea kweli. Fikiria maelezo ya Mitchel, mzee wa muda mrefu na painia wa kawaida. Anasema hivi: “Ninapenda kuwaambia watu kuhusu kweli. Ninapofikiria makala mpya katika Mnara wa Mlinzi au Amkeni! mimi hustaajabishwa na usawaziko, ufahamu, na hekima iliyo katika kila toleo. Ninakuwa na hamu ya kuhubiri ili nione jinsi watu watakavyoitikia na jinsi ninavyoweza kuchochea upendezi wao. Huduma yangu inaniimarisha. Ninahakikisha kwamba hakuna  jambo lingine lolote litakalochukua wakati niliotenga kwa ajili ya huduma.” Kuwa na mengi ya kufanya katika utumishi wetu mtakatifu kunaweza pia kutusaidia kuendelea kuwa imara katika siku hizi za mwisho.—Soma 1 Wakorintho 15:58.

KULA CHAKULA CHA KIROHO

11. Kwa nini tunapaswa kula chakula chote cha kiroho tunachopokea kutoka kwa Yehova?

11 Ili kututia nguvu, Yehova ameandaa chakula kingi sana cha kiroho katika machapisho. Bila shaka, unakumbuka pindi ambazo ulijiambia hivi baada ya kusoma chapisho fulani: ‘Kwa kweli nilihitaji kabisa habari hii! Ni kana kwamba Yehova aliandika habari hii kwa ajili yangu tu!’ Hilo halitukii kivivi hivi tu. Yehova hutufundisha na kutuongoza kupitia maandalizi hayo. Alisema hivi: “Nitakufanya uwe na ufahamu na kukufundisha katika njia unayopaswa kuiendea.” (Zab. 32:8) Je, tunajitahidi sana kula chakula chote cha kiroho tunachopokea na kutafakari juu yake? Kufanya hivyo kutatusaidia kuendelea kuzaa matunda na kutonyauka kiroho katika siku hizi za mwisho zenye matatizo.—Soma Zaburi 1:1-3; 35:28; 119:97.

12. Ni nini kinachoweza kutusaidia kutopuuza maandalizi yetu ya kiroho?

12 Ni vizuri tufikirie kazi inayofanywa ili kuhakikisha kwamba tunapata kwa ukawaida maandalizi hayo yanayoboresha afya yetu ya kiroho. Halmashauri ya Uandikaji ya Baraza Linaloongoza husimamia kazi ya kufanya utafiti, kuandika, kusahihisha, kutayarisha picha na michoro, na kutafsiriwa kwa machapisho yetu na pia habari zinazowekwa kwenye Tovuti yetu. Ofisi za tawi zinazofanya kazi ya uchapishaji husafirisha machapisho yetu kwa makutaniko yaliyo nchini mwao na katika nchi za mbali. Kwa nini kazi hiyo yote inafanywa? Ili watu wa Yehova walishwe vyema kiroho. (Isa. 65:13) Acheni tujitahidi kula chakula chote cha kiroho tunachopokea kupitia tengenezo la Yehova.—Zab. 119:27.

UNGA MKONO MIPANGO YA TENGENEZO

13, 14. Ni nani wanaounga mkono mipango ya Yehova mbinguni, na tunawezaje kufanya hivyo hapa duniani?

13 Katika maono aliyopewa mtume Yohana, Yesu anaonekana akiwa amepanda farasi mweupe ili kuwashinda wale wanaomwasi Yehova. (Ufu. 19:11-15) Imani yetu inaimarishwa kama nini tunapojua kwamba Yesu anaandamana na malaika waaminifu pamoja na watiwa-mafuta washindi kutoka duniani, ambao tayari wamepokea thawabu yao mbinguni! (Ufu. 2:26, 27) Wanaweka mfano bora kama nini katika kuunga mkono mipango ya Yehova!

14 Vivyo hivyo, umati mkubwa unaunga mkono kikamili kazi ya ndugu watiwa-mafuta wa Kristo ambao wangali duniani, na ambao wanaongoza katika tengenezo leo. (Soma Zekaria 8:23.) Kila mmoja wetu anaweza kuonyeshaje kwamba anaunga mkono mipango ya Yehova? Njia moja ni kwa kujitiisha chini ya wale wanaoongoza. (Ebr. 13:7, 17) Tunajitiisha kuanzia kutanikoni. Je, mambo tunayosema kuhusu wazee yanawafanya wengine wawaheshimu na kuheshimu pendeleo lao wakiwa waangalizi? Je, tunawahimiza watoto wetu wawaheshimu wanaume hao waaminifu na kuwaomba mashauri ya Kimaandiko? Kwa kuongezea, je, tukiwa familia tunazungumzia jinsi tunavyoweza kutumia pesa zetu kutoa michango ili kutegemeza kazi ya ulimwenguni pote? (Met. 3:9; 1 Kor. 16:2; 2 Kor. 8:12) Je, tunaona pendeleo la kushiriki kutunza Jumba la Ufalme kuwa muhimu? Roho ya Yehova inafanya kazi kwa uhuru mahali palipo na heshima na umoja wa aina hiyo. Kupitia roho hiyo, Yehova anaendelea kutusaidia ili tusichoke kabisa katika siku hizi za mwisho.—Isa. 40:29-31.

 ISHI KULINGANA NA UJUMBE WETU

15. Kwa nini ni lazima tupambane daima ili kuishi kulingana na kusudi la Yehova lililo bora?

15 Mwishowe, ili tuvumilie na kusonga pamoja na tengenezo la Yehova, ni lazima sisi binafsi tuishi kulingana na ujumbe tunaohubiri kwa “kuhakikisha lile linalokubalika kwa Bwana.” (Efe. 5:10, 11) Kwa sababu ya mwili wetu usio mkamilifu, jitihada za Shetani na ulimwengu wake mwovu, tunapambana daima na uvutano usiofaa maishani mwetu. Baadhi yenu ndugu na dada mnakabili vita vikali kila siku ili kudumisha uhusiano wenu pamoja na Yehova. Hilo linamfanya awapende sana. Msife moyo! Tukiishi kulingana na kusudi la Yehova tutapata uradhi mkubwa na uhakikisho wa kwamba ibada yetu si ya bure.—1 Kor. 9:24-27.

Wasaidie wengine kwa bidii kuona kwamba wao pia wanaweza kuwa sehemu ya tengenezo kubwa sana la Yehova

16, 17. (a) Tunapaswa kufanya nini tukitenda dhambi nzito? (b) Tunaweza kunufaikaje kutokana na mfano wa Anne?

16 Hata hivyo, tukitenda dhambi nzito, tunapaswa kufanya nini? Tunapaswa kutafuta msaada haraka iwezekanavyo. Kuficha dhambi hiyo kutafanya tu hali iwe mbaya zaidi. Kumbuka Daudi alisema kwamba alipokaa kimya kuhusu dhambi zake, ‘mifupa yake ilichakaa kwa sababu ya kuugua kwake mchana kutwa.’ (Zab. 32:3) Naam, kuficha dhambi za siri kutatufanya tuchoke kabisa kihisia na kiroho, lakini yule ‘anayeziungama na kuziacha ataonyeshwa rehema.’—Met. 28:13.

17 Fikiria mfano wa Anne. * Anne alipokuwa katika miaka ya mwisho ya utineja, alitumikia akiwa painia wa kawaida. Hata hivyo, alianza kuishi maisha ya kinafiki. Jambo hilo lilimwathiri sana. Anasema hivi: “Dhamiri yangu ilinisumbua licha ya kwamba ilikuwa imekufa ganzi. Mara nyingi nilishuka moyo na kukosa furaha.” Alifanya nini? Anasema kwamba siku moja andiko la Yakobo 5:14, 15 lilizungumziwa katika mikutano. Anne akatambua kwamba alihitaji msaada, hivyo akawaomba wazee wamsaidie. Anasema hivi anapokumbuka wakati huo: “Maandiko ni kama dawa ambayo Yehova ametuagiza tutumie ili kupona kiroho. Si rahisi kumeza dawa hiyo, lakini inaponya. Nilifuata mashauri yaliyo katika maandiko, nayo yalifanya kazi.” Miaka kadhaa imepita, sasa Anne anamtumikia tena Yehova kwa bidii akiwa na dhamiri njema.

18. Tunapaswa kuazimia nini?

18 Ni pendeleo kubwa kama nini kuishi katika siku hizi za mwisho na kuwa sehemu ya tengenezo la Yehova lenye kustaajabisha sana! Acheni tuazimie kutopuuza kamwe pendeleo letu. Badala yake, acheni tushirikiane kama familia kuhudhuria kwa ukawaida mikutano ya ibada katika kutaniko letu, kuwatafuta kwa bidii watu wenye mioyo minyoofu katika eneo letu, na kuthamini chakula cha kiroho tunachopokea kwa ukawaida. Acheni pia tuwaunge mkono wale wanaoongoza na tuishi kulingana na ujumbe tunaohubiri. Tukifanya hivyo, tutasonga pamoja na tengenezo la Yehova na kamwe hatutachoka kabisa katika kufanya yaliyo mema!

^ fu. 17 Jina limebadilishwa.