Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Mhakikishe Mambo Yaliyo ya Maana Zaidi”

“Mhakikishe Mambo Yaliyo ya Maana Zaidi”

“Mhakikishe mambo yaliyo ya maana zaidi.”—FLP. 1:10.

1, 2. Ni unabii gani kuhusu siku za mwisho ambao bila shaka uliwashangaza wanafunzi wa Yesu, na kwa nini?

MWISHOWE, Petro, Yakobo, Yohana, na Andrea walibaki na Bwana wao. Walikuwa wakifikiria sana maneno ambayo Yesu alisema awali kuhusu uharibifu wa hekalu. (Marko 13:1-4) Basi wakamuuliza hivi: “Tuambie, Mambo haya yatakuwa wakati gani, na ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?” (Mt. 24:1-3) Yesu akaanza kuwaambia kuhusu hali au matukio ambayo hayangebadili tu maisha wakati huo, bali pia yangetambulisha siku za mwisho za mfumo mwovu wa mambo wa Shetani. Bila shaka wanafunzi wa Yesu walishangazwa sana na tukio moja hususa. Baada ya kutaja matukio yenye kuhuzunisha kama vile vita, upungufu wa chakula, na kuongezeka kwa uasi-sheria, Yesu alitabiri kwamba jambo fulani zuri lingetukia katika siku za mwisho. Alisema hivi: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.”—Mt. 24:7-14.

2 Wanafunzi wa Yesu walifurahia kuhubiri habari njema ya Ufalme pamoja na Kristo. (Luka 8:1; 9:1, 2) Huenda walikumbuka maneno haya aliyosema: “Kwa kweli, mavuno ni mengi, lakini wafanyakazi ni wachache. Kwa hiyo mwombeni Bwana wa mavuno atume wafanyakazi katika mavuno yake.” (Luka 10:2) Lakini wangehubirije “katika dunia yote inayokaliwa” na kutoa “ushahidi kwa mataifa yote”? Wafanyakazi hao wangetoka wapi? Ikiwa wanafunzi walioketi na Yesu siku hiyo wangeweza kuona matukio ya wakati ujao, bila shaka wangeshangazwa sana na utimizo wa maneno hayo machache tunayosoma katika Mathayo 24:14.

3. Andiko la Luka 21:34 linatimizwaje leo, na tunapaswa kujichunguza jinsi gani?

 3 Tunaishi wakati ambapo unabii wa Yesu unatimizwa. Mamilioni wameungana ili kuhubiri habari njema ya Ufalme duniani pote. (Isa. 60:22) Hata hivyo, Yesu alisema kwamba ingekuwa vigumu kwa baadhi ya watu kuendelea kuikazia fikira kazi hiyo katika siku hizi za mwisho. Wangekengeushwa na ‘kulemewa.’ (Soma Luka 21:34.) Tunaona maneno hayo yakitimizwa pia. Baadhi ya watu wa Mungu wanakengeushwa fikira. Hilo linaonekana katika maamuzi wanayofanya kuhusu kazi ya kimwili, elimu ya juu, kupata vitu vya kimwili, na muda wanaotumia katika michezo na burudani. Wengine wanachoka kwa sababu ya mikazo na mahangaiko ya maisha ya kila siku. Jiulize: ‘Ninatendaje? Maamuzi yangu yanaonyesha nini kuhusu mambo ninayotanguliza maishani?’

4. (a) Paulo alisali ili Wakristo walioishi Filipi wafanye nini, na kwa nini? (b) Tutachunguza nini katika makala hii na inayofuata, tukiwa na lengo gani?

4 Wakristo walioishi katika karne ya kwanza walihitaji kujitahidi kuendelea kutanguliza mambo ya kiroho. Mtume Paulo aliona uhitaji wa kusali ili Wakristo walioishi Filipi ‘wahakikishe mambo yaliyo ya maana zaidi.’ (Soma Wafilipi 1:9-11.) Kama mtume Paulo, wengi katika siku hizo ‘walionyesha uhodari hata zaidi katika kulisema neno la Mungu bila woga.’ (Flp. 1:12-14) Vivyo hivyo leo, wengi wetu tunahubiri kwa uhodari Neno la Mungu. Hata hivyo, je, kuchunguza mambo yanayotimizwa sasa katika tengenezo la Yehova kunaweza kutusaidia kukazia fikira zaidi kazi muhimu sana ya kuhubiri? Bila shaka! Katika makala hii, acheni tuchunguze kwa undani mpango au utaratibu ambao Yehova ameweka ili kutimiza andiko la Mathayo 24:14. Tengenezo lake linakazia nini, na kujua hilo kunawezaje kutuchochea na kuchochea familia zetu? Katika makala inayofuata, tutachunguza mambo yanayoweza kutusaidia kuvumilia na kuendelea kusonga mbele pamoja na tengenezo la Yehova.

SEHEMU YA KIMBINGU YA TENGENEZO LA YEHOVA IKO MWENDONI

5, 6. (a) Kwa nini Yehova alitumia maono kuonyesha sehemu ya kimbingu ya tengenezo lake? (b) Ezekieli aliona nini katika maono?

5 Kuna mambo mengi ambayo Yehova aliamua kutoweka katika Neno lake lililoandikwa. Kwa mfano, hakueleza kwa undani kuhusu ulimwengu au jinsi ubongo unavyofanya kazi, hata ingawa habari hizo zingetustaajabisha sana! Badala yake, Yehova alitupa habari tunazohitaji ili kuelewa makusudi yake na kuishi kupatana nayo. (2 Tim. 3:16, 17) Basi inapendeza kama nini kwamba Biblia inatueleza habari fulani kuhusu sehemu isiyoonekana ya tengenezo la Yehova! Tunasisimka tunaposoma maelezo yaliyoandikwa na Isaya, Ezekieli, Danieli, na pia masimulizi ya Yohana katika Ufunuo kuhusu utaratibu wa kimbingu wa Yehova. (Isa. 6:1-4; Eze. 1:4-14, 22-24; Dan. 7:9-14; Ufu. 4:1-11) Ni kana kwamba Yehova alifungua pazia na kuturuhusu kuona mbinguni. Kwa nini aliandaa habari hizo?

6 Yehova hakutaka tusahau kamwe kwamba sisi ni sehemu ya tengenezo la ulimwenguni pote. Ili kutimiza makusudi ya Yehova, kuna mengi zaidi yanayofanywa kuliko yale tunayoweza kuona. Kwa mfano, Ezekieli aliona sehemu ya tengenezo la Yehova isiyoonekana inayofananishwa na gari kubwa sana la kimbingu. Gari hilo lingeweza kusonga upesi sana na kubadili mwelekeo kwa ghafla. (Eze. 1:15-21) Kila mara magurudumu yalipozunguka, gari hilo lilisafiri mbali sana. Katika maono, Ezekieli alimwona pia  Mwendeshaji wa gari hilo. Ezekieli alisema hivi: “Nikaona kitu kama mng’ao wa mchanganyiko wa dhahabu na fedha, kinachoonekana kama moto kuzunguka pande zote . . . Kulikuwa ni kuonekana kwa mfano wa utukufu wa Yehova.” (Eze. 1:25-28) Lazima Ezekieli aliogopa na kustaajabu sana alipoona maono hayo. Alimwona Yehova akiliongoza kikamili tengenezo lake, na kulielekeza kupitia roho yake takatifu. Huo ni wonyesho wenye kustaajabisha kama nini wa sehemu ya kimbingu ya tengenezo la Yehova lililo mwendoni!

7. Maono ambayo Danieli alionyeshwa yanatusaidiaje kuwa na uhakika?

7 Danieli pia aliona mambo mengi yanayotupa uhakika. Aliruhusiwa kumwona Yehova akiwa kama “Mzee wa Siku” aliyeketi kwenye kiti cha ufalme chenye miali ya moto. Kiti hicho cha ufalme kilikuwa na magurudumu. (Dan. 7:9) Yehova alitaka Danieli aone kwamba tengenezo Lake liko mwendoni, likitimiza kusudi Lake. Danieli aliona pia “mtu fulani kama mwana wa binadamu,” yaani, Yesu, akipewa mamlaka ya kusimamia sehemu ya kidunia ya tengenezo la Yehova. Utawala mkamilifu wa Kristo haudumu kwa miaka michache tu. Badala yake, ni “utawala unaodumu mpaka wakati usio na kipimo ambao hautapitilia mbali, na ufalme wake ni ufalme ambao hautaharibiwa.” (Dan. 7:13, 14) Tunachochewa kuwa na imani katika Yehova na kutambua yale anayotimiza. Alimpa “utawala na heshima na ufalme,” Yesu, Mwana wake aliyejaribiwa na kuthibitika kuwa mwaminifu. Yehova anamwamini Mwana wake. Hivyo, sisi pia tunaweza kuwa na uhakika katika uongozi wa Yesu.

8. Ezekieli na Isaya walichochewaje na maono waliyoonyeshwa na Yehova, nayo yanapaswa kutuchocheaje?

 8 Maono hayo kuhusu sehemu isiyoonekana ya tengenezo la Yehova yanapaswa kutuchocheaje? Kama Ezekieli, bila shaka tunastaajabishwa na kunyenyekezwa na mambo ambayo Yehova anatimiza. (Eze. 1:28) Kutafakari kuhusu tengenezo la Yehova kunaweza kutuchochea kutenda kama Isaya. Alipopata fursa ya kuwaambia wengine kuhusu mambo ambayo Yehova anatimiza, alikubali bila kusitasita. (Soma Isaya 6:5, 8.) Isaya alikuwa na hakika kwamba kwa msaada wa Yehova, angeweza kukabiliana na tatizo lolote na kulishinda. Vivyo hivyo, maono hayo yanayoonyesha mambo fulani kuhusu sehemu isiyoonekana ya tengenezo la Yehova yanapaswa kutufanya tumhofu na kumheshimu, na kutuchochea kutenda. Tunaguswa moyo kama nini tunapotafakari kuhusu tengenezo hilo lililo mwendoni daima na linalojitahidi kabisa kutimiza makusudi ya Yehova!

SEHEMU YA KIDUNIA YA TENGENEZO LA YEHOVA

9, 10. Kwa nini sehemu inayoonekana ya tengenezo la Yehova inahitajiwa?

9 Kupitia Mwana wake, Yehova alianzisha utaratibu hapa duniani ambao unatenda kupatana na sehemu isiyoonekana ya tengenezo Lake. Kwa nini utaratibu unaoonekana unahitajiwa ili kutimiza kazi inayotajwa katika Mathayo 24:14? Fikiria sababu tatu.

10 Kwanza, Yesu alisema kwamba wanafunzi wake wangefanya kazi hiyo ya kuhubiri “mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Mdo. 1:8) Pili, mipango ingehitajiwa ili kuandaa chakula cha kiroho na kuwatunza kiroho wale wanaoshiriki katika kazi hiyo. (Yoh. 21:15-17) Tatu, mipango ingehitaji kufanywa ili wale wanaohubiri habari njema wakutanike pamoja kumwabudu Yehova na kufundishwa jinsi ya kufanya kazi hiyo. (Ebr. 10:24, 25) Hawangeweza kutimiza mambo hayo bila utaratibu wowote. Ili wafuasi wa Kristo wafanikiwe, kazi hiyo ingehitaji kupangwa vizuri.

11. Tunaonyeshaje kwamba tunaunga mkono mipango inayofanywa na tengenezo la Yehova?

11 Tunaonyeshaje kwamba tunaunga mkono mipango inayofanywa na tengenezo la Yehova? Njia moja muhimu ni kuwaamini siku zote wale ambao Yehova na Yesu wamewakabidhi daraka la kutuongoza katika kazi ya kuhubiri. Leo, kuna mambo au shughuli nyingi katika ulimwengu ambazo wale wanaoongoza kati yetu wanaweza kukazia fikira. Hata hivyo, sehemu inayoonekana ya tengenezo la Yehova imekuwa ikikazia fikira nini?

WANAKAZIA FIKIRA “MAMBO YALIYO YA MAANA ZAIDI”

12, 13. Wazee Wakristo wanatimizaje mgawo wao, na kwa nini hilo linakutia moyo?

12 Wazee Wakristo wenye uzoefu ulimwenguni pote wamewekwa rasmi kuongoza katika kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme katika nchi zao na kuwachochea wengine kushiriki. Ndugu hao wanapofanya maamuzi, wanatafuta mwongozo katika Neno la Mungu, wakilifanya liwe ‘taa ya miguu yao na nuru kwa barabara yao,’ nao wanasali kwa bidii ili Yehova awaongoze.—Zab. 119:105; Mt. 7:7, 8.

13 Kama wale walioongoza katika karne ya kwanza, wazee Wakristo wanaoongoza katika kazi ya kuhubiri leo wamejitoa “kwa huduma ya neno.” (Mdo. 6:4) Wanashangilia sana kuona maendeleo yanayofanywa katika kazi ya kuhubiri habari njema katika eneo lao na ulimwenguni pote. (Mdo. 21:19, 20) Hawatungi sheria nyingi sana na kutoa maagizo mengi  ya kufuatwa. Badala yake, wanafuata Maandiko na mwongozo wa roho takatifu ya Mungu wanapofanya mipango inayohitajiwa ili kazi ya kuhubiri isonge mbele. (Soma Matendo 15:28.) Kwa kufanya hivyo, ndugu hao wenye madaraka wanawawekea mfano mzuri wote walio katika makutaniko.—Efe. 4:11, 12.

14, 15. (a) Ni mipango gani inayofanywa ili kuhakikisha kwamba kazi ya kuhubiri inaenezwa duniani pote? (b) Unahisije kuhusu sehemu unayotimiza katika kazi ya kuhubiri habari njema ya Ufalme?

14 Wengi hawajui jitihada zinazofanywa daima za kutayarisha chakula cha kiroho kinachotolewa kupitia machapisho, mikutano, na makusanyiko yetu. Maelfu ya wajitoleaji wenye bidii hufanya kazi ya kutafsiri chakula hicho cha kiroho katika lugha 600 hivi ili watu wengi iwezekanavyo wajifunze “mambo makuu ya Mungu” katika lugha yao wenyewe. (Mdo. 2:7-11) Ndugu na dada vijana huchapisha na kujalidi machapisho yetu kwa matbaa zenye mwendo wa kasi. Kisha, machapisho hayo husambazwa katika makutaniko yote hata yale yaliyo sehemu za mbali zaidi duniani.

15 Mipango mingi imefanywa ili kutusaidia kukazia fikira kazi ya kuhubiri habari njema tukishirikiana na kutaniko letu. Kwa mfano, maelfu hujitolea kusaidia katika ujenzi wa Majumba ya Ufalme na Majumba ya Kusanyiko, kuwasaidia wale walioathiriwa na misiba ya asili au wale wanaohitaji matibabu ya dharura, kupanga makusanyiko yetu, kufundisha shule za kitheokrasi, na kufanya mambo mengine mengi ambayo hayaonekani waziwazi. Kazi hiyo yote inafanywa kwa kusudi gani? Ili kueneza habari njema, kuboresha hali ya kiroho ya wale wanaofanya kazi hiyo, na kuendeleza ibada ya kweli. Je, sehemu ya kidunia ya tengenezo la Yehova imeendelea kukazia fikira mambo yaliyo ya maana zaidi? Bila shaka!

IGA MFANO WA TENGENEZO LA YEHOVA

16. Mnaweza kufanya utafiti kuhusu nini katika ibada ya familia au katika funzo la kibinafsi la Biblia?

16 Je, mara kwa mara tunatumia wakati kutafakari kuhusu utendaji wa tengenezo la Yehova? Baadhi ya watu wameamua kutia ndani ya ibada yao ya familia au funzo lao la kibinafsi wakati wa kufanya utafiti na kutafakari mambo hayo. Kujifunza maono ambayo Isaya, Ezekieli, Danieli, na Yohana walionyeshwa kunasisimua sana. Kitabu Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu na machapisho mengine au DVD zinazopatikana katika lugha yenu zina habari za kina zenye kupendeza sana kuhusu tengenezo.

17, 18. (a) Mazungumzo haya yamekunufaishaje? (b) Ni maswali gani tunayopaswa kufikiria?

17 Ni vizuri kwetu kutafakari kuhusu mambo ambayo Yehova anatimiza kupitia tengenezo lake. Acheni tuazimie kuendelea kukazia fikira mambo yaliyo ya maana zaidi pamoja na tengenezo hili zuri ajabu. Kufanya hivyo kutatuimarisha na hivyo tutaazimia kama Paulo aliyeandika hivi: “Kwa kuwa sisi tuna huduma hii kulingana na rehema tuliyoonyeshwa, hatufi moyo.” (2 Kor. 4:1) Pia, aliwatia moyo hivi wafanyakazi wenzake: “Na tusife moyo katika kufanya yaliyo mema, kwa maana katika majira yanayofaa tutavuna ikiwa hatuchoki kabisa.”—Gal. 6:9.

18 Je, kuna mabadiliko tunayohitaji kufanya tukiwa mtu mmoja-mmoja au familia ili kuhakikisha kwamba tunakazia fikira mambo yaliyo ya maana zaidi katika maisha yetu ya kila siku? Je, tunaweza kurahisisha maisha yetu au kupunguza mambo yanayokengeusha ili tukazie fikira zaidi kazi muhimu sana ya kuhubiri? Katika makala inayofuata, tutachunguza mambo matano yatakayotusaidia kuendelea kusonga pamoja na tengenezo la Yehova.