Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Mlipokea Bure, Toeni Bure”

“Mlipokea Bure, Toeni Bure”

“Mlipokea Bure, Toeni Bure”

“MLIPOKEA bure, toeni bure.” (Mathayo 10:8) Yesu alitoa agizo hilo kwa mitume wake alipowatuma kuhubiri habari njema. Je, mitume walitii agizo hilo? Ndiyo, nao waliendelea kufanya hivyo hata baada ya Yesu kuondoka duniani.

Kwa mfano, Simoni, ambaye hapo kwanza alikuwa mchawi, alipoona nguvu za kufanya miujiza za mitume Petro na Yohana, alitaka kuwalipa ili wamgawie nguvu hizo. Lakini Petro alimkemea Simoni, akamwambia: “Fedha yako na iangamie pamoja nawe, kwa sababu kupitia fedha ulifikiri kupata umiliki wa zawadi ya bure ya Mungu.”—Matendo 8:18-20.

Mtume Paulo alikuwa na mtazamo kama wa Petro. Paulo angejiruhusu kuwatwika mzigo wa fedha ndugu zake Wakristo kule Korintho. Lakini alifanya kazi kwa mikono yake mwenyewe ili kujitegemeza. (Matendo 18:1-3) Kwa hiyo, angeweza kusema kwa uhakika kwamba aliwahubiria Wakorintho habari njema “bila gharama.”—1 Wakorintho 4:12; 9:18.

Kwa kusikitisha, wengi wanaodai kuwa wafuasi wa Kristo hawajaonyesha nia hiyo ya ‘kutoa bure.’ Kwa kweli, viongozi wengi wa kidini katika Jumuiya ya Wakristo “hufundisha kwa malipo.” (Mika 3:11, Biblia Habari Njema) Hata viongozi fulani wa kidini wamejitajirisha kwa michango ya wafuasi wao. Katika mwaka wa 1989, mwinjilisti mmoja Mmarekani alifungwa jela miaka 45. Kwa nini? Alikuwa “akiwapunja wafuasi wake mamilioni ya dola na kutumia baadhi ya pesa hizo kununua nyumba, magari, kwenda likizo na hata kujengea mbwa wake nyumba yenye mfumo wa kusafisha hewa.”—People’s Daily Graphic, Oktoba 7, 1989.

Kulingana na gazeti la Ghanaian Times la Machi 31, 1990, huko Ghana, kasisi mmoja Mkatoliki alichukua pesa zilizokusanywa wakati wa ibada na kuwatupia washiriki wa kanisa. “Kisa na maana,” lasema gazeti hilo, “ni kwamba, watu wazima walitarajiwa kutoa mchango wa noti kubwa-kubwa.” Kwa hiyo haishangazi kwamba makanisa mengi hata hujaribu kuwachochea wafuasi wake wawe na pupa kwa kuanzisha michezo mbalimbali ya kamari na miradi mingine ya kuchangisha pesa.

Tofauti na makanisa hayo, Mashahidi wa Yehova hujitahidi kumwiga Yesu na wanafunzi wake wa karne ya kwanza. Hawana makasisi wanaolipwa. Kila Shahidi ni mhudumu ambaye ana daraka la kuwahubiria wengine ‘habari njema ya ufalme.’ (Mathayo 24:14) Kwa hiyo, zaidi ya Mashahidi milioni sita ulimwenguni pote hushiriki katika kazi ya kuwapelekea watu “maji ya uhai” bure. (Ufunuo 22:17) Kwa kufanya hivyo, hata wale ‘wasio na fedha’ wanaweza kufaidika na ujumbe wa Biblia. (Isaya 55:1) Ingawa kazi yao ya ulimwenguni pote inategemezwa kwa michango ya hiari, wao hawaombi-ombi pesa kamwe. Wakiwa wahudumu wa kweli wa Mungu, wao si “wachuuzi wa neno la Mungu,” bali husema ‘kwa weupe wa moyo, ndiyo, wakiwa waliotumwa kutoka kwa Mungu.’—2 Wakorintho 2:17.

Hata hivyo, kwa nini Mashahidi wa Yehova wana nia ya kuwasaidia wengine, kwa gharama yao wenyewe? Ni nini kinachowachochea? Je, hii inamaanisha kwamba bidii yao ya kutoa bure haitathawabishwa?

Kujibu Dai la Shetani

Wakristo wa kweli leo huchochewa hasa na tamaa ya kumpendeza Yehova, si kujitajirisha wenyewe. Kwa hiyo, wanaweza kutoa jibu kwa dai ambalo Shetani Ibilisi alitokeza karne nyingi zilizopita. Shetani alimwuliza Yehova swali hili kuhusiana na mtu mwadilifu aliyeitwa Ayubu: “Je! huyo Ayubu yuamcha BWANA bure?” Shetani alidai kwamba Ayubu alimtumikia Mungu kwa sababu tu Mungu alikuwa amemlinda pande zote. Shetani alidai kwamba ikiwa Ayubu angenyang’anywa mali yake, Ayubu angemkufuru Mungu mbele za uso wake!—Ayubu 1:7-11.

Ili kujibu dai hilo, Mungu alimruhusu Shetani amjaribu Ayubu, akisema: “Yote aliyo nayo yamo katika uwezo wako.” (Ayubu 1:12) Matokeo yalikuwaje? Ayubu alimthibitisha Shetani kuwa mwongo. Ayubu aliendelea kuwa mwaminifu licha ya majanga yaliyompata. Alisema: “Hata nitakapokufa sitajiondolea uelekevu wangu.”—Ayubu 27:5, 6.

Waabudu wa kweli leo wana mtazamo kama wa Ayubu. Hawamtumikii Mungu kwa sababu ya vitu vya kimwili.

Zawadi ya Mungu ya Bure ya Fadhili Isiyostahiliwa

Sababu nyingine inayofanya Wakristo wa kweli wawe na nia ya ‘kutoa bure’ ni kwamba wao wenyewe ‘wamepokea bure’ kutoka kwa Mungu. Mwanadamu yuko katika utumwa wa dhambi na kifo kwa sababu ya dhambi ya babu yetu Adamu. (Waroma 5:12) Kwa upendo, Yehova alifanya mpango ili Mwana wake afe kifo cha kidhabihu, jambo ambalo lilimgharimu Mungu sana. Mwanadamu hastahili hata kidogo mpango huo. Huo ni zawadi kutoka kwa Mungu.—Waroma 4:4; 5:8; 6:23.

Kama ilivyoandikwa katika Waroma 3:23, 24, Paulo aliwaambia hivi Wakristo watiwa-mafuta: “Wote wamefanya dhambi na hupungukiwa na utukufu wa Mungu, nayo ni kama zawadi ya bure kwamba wao wanatangazwa kuwa waadilifu kwa fadhili yake isiyostahiliwa kupitia kuachiliwa kwa njia ya fidia iliyolipwa na Kristo Yesu.” Wale walio na tumaini la kuishi milele duniani pia hupokea “zawadi ya bure.” Zawadi hiyo hutia ndani pendeleo la kutangazwa kuwa waadilifu wakiwa rafiki za Yehova.—Yakobo 2:23; Ufunuo 7:14.

Dhabihu ya fidia ya Kristo pia huwawezesha Wakristo wote kuwa wahudumu wa Mungu. Mtume Paulo aliandika: “Mimi nikapata kuwa mhudumu wa hilo [yaani, siri takatifu] kulingana na zawadi ya bure ya fadhili isiyostahiliwa ya Mungu.” (Waefeso 3:4-7) Kwa kuwa walipewa huduma hii kupitia zawadi ambayo hawakustahili au ambayo hawangeweza kununua, wahudumu wa kweli wa Mungu hawangeweza kutarajia kulipwa kwa kuwaeleza wengine kuhusu zawadi hiyo.

Je, Zawadi ya Uhai wa Milele Hutuchochea Kuwa na Ubinafsi?

Basi, je, hiyo inamaanisha kwamba Mungu anawatarajia Wakristo wamtumikie bila tumaini lolote la kupata thawabu? La, kwa kuwa mtume Paulo aliwaambia waamini wenzake hivi: “Mungu si asiye mwadilifu ili asahau kazi yenu na upendo mlioonyesha kwa ajili ya jina lake.” (Waebrania 6:10) Yehova pia ni mwenye haki. (Kumbukumbu la Torati 32:4) Naye Yehova huwa “mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.” (Waebrania 11:6) Lakini je, ahadi ya uhai wa milele katika Paradiso haituchochei tuwe na ubinafsi?—Luka 23:43.

Sivyo hata kidogo. Sababu moja ni kwamba tamaa ya kuishi milele katika Paradiso duniani hutoka kwa Mungu mwenyewe. Yeye ndiye aliyewapa wanadamu wa kwanza wawili tumaini hilo. (Mwanzo 1:28; 2:15-17) Pia alifanya iwezekane tena kwa wazao wa Adamu na Hawa kuwa na tumaini hilo baada ya wazazi wao kulipoteza. Kwa hiyo, Mungu anaahidi hivi katikaNeno lake: “Viumbe vyenyewe pia vitawekwa huru kutoka katika utumwa wa uharibifu na kuwa na uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.” (Waroma 8:21) Kwa hiyo, kama Musa wa kale, ni sawa kabisa kwa Wakristo leo ‘kukaza macho kuelekea malipo ya thawabu.’ (Waebrania 11:26) Mungu hatoi zawadi hiyo kama rushwa. Anaitoa kwa sababu anawapenda kikweli wale wanaomtumikia. (2 Wathesalonike 2:16, 17) Kwa hiyo, “twapenda, kwa sababu yeye alitupenda sisi kwanza.”—1 Yohana 4:19.

Kusudi Linalofaa la Kumtumikia Mungu

Hata hivyo, Wakristo leo wanapaswa kujichunguza wenyewe daima na kuona sababu zinazofanya wamtumikie Mungu. Katika Yohana 6:10-13, tunasoma kwamba Yesu alilisha kimuujiza umati wa watu zaidi ya elfu tano. Baada ya hapo, baadhi yao walianza kumfuata Yesu kwa sababu tu za ubinafsi. Yesu aliwaambia: “Mnanitafuta, . . . kwa sababu mlikula kutokana na mikate mkashiba.” (Yohana 6:26) Vivyo hivyo, miaka mingi baadaye Wakristo fulani waliojiweka wakfu walimtumikia Mungu, lakini “si kwa madhumuni safi.” (Wafilipi 1:17) Wengine ambao ‘hawakukubaliana na maneno yenye afya ya Yesu Kristo’ hata walitafuta njia za kujipatia faida kutoka kwa Wakristo walioshirikiana nao.—1 Timotheo 6:3-5.

Leo, Mkristo ambaye hutumikia kwa sababu tu anataka kuishi milele katika Paradiso anaweza kuwa pia akitumikia akiwa na kusudi la ubinafsi. Hatimaye, hilo laweza kufanya aanguke kiroho. Kwa sababu mfumo huu wa Shetani unaonekana kwamba unachukua muda mrefu kuliko alivyotazamia, mtu huyo anaweza ‘kuchoka kabisa,’ na kuhisi kwamba mwisho unakawia. (Wagalatia 6:9) Hata huenda akawa na uchungu kwa sababu ya vitu vya kimwili ambavyo amejinyima. Yesu anatukumbusha: “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote.” (Mathayo 22:37) Naam, mtu ambaye anachochewa kumtumikia Mungu hasa kwa sababu ya upendo, haweki mpaka wa muda atakaomtumikia. Ameazimia kumtumikia Yehova milele! (Mika 4:5) Hajuti kamwe kwamba alijinyima mambo fulani ili amtumikie Mungu. (Waebrania 13:15, 16) Upendo wake kwa Mungu humchochea kutanguliza utumishi wa Mungu maishani.—Mathayo 6:33.

Leo, waabudu wa kweli zaidi ya milioni sita “wanajitoa kwa hiari” kumtumikia Yehova. (Zaburi 110:3) Je, wewe ni mmoja wao? Ikiwa sivyo, tafakari yale ambayo Mungu amekupa: ujuzi safi wa ukweli; (Yohana 17:3) uhuru kutoka katika utumwa wa mafundisho ya dini ya uwongo; (Yohana 8:32) tumaini la kuishi milele. (Ufunuo 21:3, 4) Mashahidi wa Yehova wanaweza kukusaidia ujifunze jinsi unavyoweza kupata mambo hayo yote kutoka kwa Mungu—bila malipo.

[Blabu katika ukurasa wa 22]

Wakristo wa kweli leo huchochewa hasa na tamaa ya kumpendeza Yehova, si kujitajirisha wenyewe

[Picha katika ukurasa wa 21]

Zawadi ya Mungu ya bure ya fidia huwachochea Wakristo kuwaeleza wengine habari njema bila malipo