Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kumwiga Mungu wa Ukweli

Kumwiga Mungu wa Ukweli

Kumwiga Mungu wa Ukweli

“Iweni waigaji wa Mungu, mkiwa watoto wapendwa.”—WAEFESO 5:1.

1. Watu wengine huamini nini kuhusu ukweli, na kwa nini maoni yao yana kasoro?

“KWELI ni nini?” (Yohana 18:38) Swali hilo ambalo Pontio Pilato aliuliza kwa dhihaka karibu miaka 2,000 iliyopita linadokeza kwamba ukweli haupatikani kwa urahisi. Wengi leo watakubaliana na maoni hayo. Maana halisi ya ukweli inapingwa. Huenda umesikia ikisemwa kwamba kila mtu hujiamulia ukweli wake mwenyewe, au hakuna ukweli kamili, au ukweli hubadilika daima. Maoni hayo yana kasoro. Lengo hasa la utafiti na elimu ni kujifunza mambo hakika na ukweli kuhusu ulimwengu tunamoishi. Ukweli hautegemei maoni ya mtu binafsi. Kwa mfano, ama nafsi ya mwanadamu hufa au haifi. Ama Shetani yuko au hayuko. Ama maisha yana kusudi au hayana. Katika mambo hayo yote kuna jibu moja tu lililo sahihi. Majibu yote mawili hayawezi kuwa sahihi; lazima moja liwe la kweli na lingine liwe la uwongo.

2. Yehova ni Mungu wa ukweli kwa njia gani, na ni maswali gani yatakayozungumziwa sasa?

2 Katika makala iliyotangulia, tulijifunza kwamba Yehova ni Mungu wa ukweli. Anajua ukweli kuhusu vitu vyote. Kinyume kabisa na adui wake mdanganyifu Shetani Ibilisi, Yehova husema ukweli sikuzote. Isitoshe, Yehova huwafunulia wengine ukweli kwa wingi. Mtume Paulo aliwahimiza Wakristo wenzake hivi: “Iweni waigaji wa Mungu, mkiwa watoto wapendwa.” (Waefeso 5:1) Tukiwa Mashahidi wa Yehova, tunawezaje kumwiga katika kusema na kuishi kupatana na ukweli? Kwa nini ni muhimu kufanya hivyo? Na tuna uhakika gani kwamba Yehova huwakubali wale ambao hufuata njia ya ukweli? Hebu tuone.

3, 4. Mitume Paulo na Petro walielezaje mambo yatakayotukia katika “siku za mwisho”?

3 Tunaishi katika wakati ambapo kuna uwongo mwingi wa kidini. Kama vile mtume Paulo alivyoongozwa na roho ya Mungu kutabiri, watu wengi katika hizi “siku za mwisho” wana namna ya ujitoaji-kimungu lakini wanakana nguvu zake. Wengine hupinga ukweli, wakiwa ‘wamefisidika kabisa katika akili.’ Zaidi ya hayo, ‘watu waovu na walaghai wanaendelea kutoka ubaya hadi ubaya zaidi, wakiongoza vibaya na kuwa wenye kuongozwa vibaya.’ Ingawa watu hao hujifunza sikuzote, hawapati kamwe “ujuzi sahihi juu ya kweli.”—2 Timotheo 3:1, 5, 7, 8, 13.

4 Mtume Petro pia aliongozwa na roho ya Mungu kuandika kuhusu siku za mwisho. Sawa na alivyotabiri, watu wanaukataa ukweli na pia hudhihaki Neno la Mungu na wale wanaotangaza ukweli uliomo katika neno hilo. “Kulingana na kutaka kwao,” wadhihaki hao hupuuza ukweli wa kwamba ulimwengu wa siku za Noa uliharibiwa kwa gharika, jambo linaloonyesha yatakayotokea katika hukumu ya wakati ujao. Mawazo yao mabaya yatafanya waharibiwe Mungu atakapowaharibu watu wasiomwogopa.—2 Petro 3:3-7.

Watumishi wa Yehova Wanajua Ukweli

5. Kulingana na nabii Danieli, ni nini kingetukia “wakati wa mwisho,” na unabii huo umetimizwaje?

5 Katika ufafanuzi wake kuhusu “wakati wa mwisho,” nabii Danieli alitabiri jambo tofauti kabisa ambalo lingetukia miongoni mwa watu wa Mungu—kurudishwa kwa ukweli wa kidini. Aliandika hivi: “Wengi wataenda mbio huko na huko, na maarifa yataongezeka.” (Danieli 12:4) Watu wa Yehova hawatatanishwi au kupofushwa na yule Mdanganyifu mkuu. Wamepata ujuzi sahihi kwa kuenda huko na huko katika Biblia. Katika karne ya kwanza, Yesu aliwaelimisha wanafunzi wake. ‘Alifungua kabisa akili zao ili wafahamu maana ya Maandiko.’ (Luka 24:45) Yehova ametuelimisha pia katika siku zetu. Kupitia Neno lake, roho yake, na tengenezo lake, amewezesha mamilioni ya watu ulimwenguni pote kuelewa kile ambacho yeye tayari anakijua, yaani, ukweli.

6. Watu wa Mungu leo wanaelewa kweli gani za Biblia?

6 Tukiwa watu wa Mungu, tunaelewa mambo mengi ambayo hatungeweza kuelewa. Tunajua majibu ya maswali ambayo yamewasumbua watu wenye hekima ya kilimwengu kwa maelfu ya miaka. Kwa mfano, tunajua kwa nini watu wanateseka, wanakufa, na kwa nini wanadamu hawawezi kuleta amani na umoja ulimwenguni. Pia tuna pendeleo la kujua yale yatakayotukia wakati ujao—Ufalme wa Mungu, dunia paradiso, na uzima mkamilifu usio na mwisho. Tumemjua Yehova, Aliye Mkuu Zaidi. Tumejifunza kuhusu utu wake wenye kuvutia, na pia mambo tunayopaswa kufanya ili kupata baraka zake. Kujua ukweli hutuwezesha kutambua mambo yasiyo ya kweli. Kuishi kupatana na ukweli hutusaidia tuepuke kufuatia mambo yasiyo na faida, hutuwezesha kuishi maisha bora zaidi, na hutupa tumaini zuri la wakati ujao.

7. Ni nani ambao wanaruhusiwa kuelewa kweli za Biblia, na ni nani wasioruhusiwa?

7 Je, unaelewa ukweli wa Biblia? Ikiwa ndivyo, wewe umebarikiwa kwelikweli. Mtungaji anapoandika kitabu, kwa kawaida yeye hukiandika kwa njia itakayowavutia watu wa kikundi fulani hususa. Vitabu fulani huandikwa kwa ajili ya wale wenye elimu ya juu, vingine kwa ajili ya watoto, na vingine kwa ajili ya wataalamu katika nyanja mbalimbali. Ingawa Biblia hupatikana kwa urahisi kwa watu wote, ni watu wa kikundi fulani hususa ambao wamekusudiwa kuielewa na kuifurahia. Yehova aliitunga kwa ajili ya wanyenyekevu na wapole wa dunia. Watu hao wanaweza kuielewa Biblia bila kujali elimu, utamaduni, hadhi, au kabila lao. (1 Timotheo 2:3, 4) Kwa upande mwingine, wale wasio na mwelekeo unaofaa, hata wawe ni werevu au wawe na elimu ya juu kadiri gani, hawaruhusiwi kuelewa ukweli wa Biblia. Watu wenye majivuno na wenye kiburi hawawezi kuzielewa kweli zenye thamani za Neno la Mungu. (Mathayo 13:11-15; Luka 10:21; Matendo 13:48) Ni Mungu tu ambaye angeweza kutunga kitabu kama hicho.

Watumishi wa Yehova Husema Ukweli

8. Kwa nini Yesu mwenyewe alikuwa ukweli?

8 Kama Yehova, Mashahidi wake waaminifu husema ukweli. Yesu Kristo ambaye ni Shahidi mkuu wa Yehova, alithibitisha ukweli kupitia yale aliyofundisha na jinsi alivyoishi na kufa. Alitetea ukweli wa neno la Yehova na ahadi zake. Kwa hiyo, kama Yesu alivyosema, yeye mwenyewe alikuwa ukweli.—Yohana 14:6; Ufunuo 3:14; 19:10.

9. Maandiko husema nini kuhusu kusema ukweli?

9 Yesu alikuwa “mwenye kujaa fadhili isiyostahiliwa na kweli” na “hapakuwa na hila kinywani mwake.” (Yohana 1:14; Isaya 53:9) Wakristo wa kweli hufuata mfano wa Yesu kwa kusema ukweli. Paulo aliwashauri waamini wenzake hivi: “Semeni kweli kila mmoja wenu pamoja na jirani yake, kwa sababu sisi ni viungo vya mtu na mwenzake.” (Waefeso 4:25) Hapo mapema, nabii Zekaria aliandika: “Kila mtu na aseme kweli na jirani yake.” (Zekaria 8:16) Wakristo husema ukweli kwa sababu wanataka kumpendeza Mungu. Yehova husema ukweli na anajua matokeo mabaya ya kusema uwongo. Kwa hiyo, ana haki ya kutarajia watumishi wake waseme ukweli.

10. Kwa nini watu husema uwongo, na uwongo huo huwa na matokeo gani mabaya?

10 Watu wengi huona kusema uwongo kuwa njia rahisi ya kupata faida fulani. Watu husema uwongo ili waepuke adhabu, wafaidike kwa njia fulani, au wasifiwe na wengine. Ingawa hivyo, kusema uwongo ni mazoea mabaya. Zaidi ya hayo, mwongo hawezi kupata kibali cha Mungu. (Ufunuo 21:8, 27; 22:15) Tunapojulikana kuwa wasema ukweli, wengine wataamini yale tunayosema na watatutumaini. Hata hivyo, tukisema uwongo hata mara moja, wengine watakuwa wakitilia shaka ukweli wa yale tunayowaambia. Methali moja ya Kiafrika husema: “Uwongo mmoja huharibu kweli elfu.” Methali nyingine husema: “Mwongo hataaminiwa ajaposema ukweli.”

11. Ni katika njia gani ukweli unahusisha mengi zaidi ya kusema ukweli?

11 Ukweli unahusisha mengi zaidi ya kusema ukweli. Ukweli ni njia ya maisha. Huo hututambulisha sisi ni watu wa aina gani. Tunawajulisha wengine ukweli kupitia yale tunayosema na pia kutenda. Mtume Paulo aliuliza hivi: “Je, wewe unayemfundisha mtu mwingine, hujifundishi mwenyewe? Wewe, unayehubiri ‘Usiibe,’ je, wewe huiba? Wewe, unayesema ‘Usifanye uzinzi,’ je, wewe hufanya uzinzi?” (Waroma 2:21, 22) Tukitaka kuwaeleza wengine ukweli, ni lazima tufuate ukweli katika njia zetu zote. Tunapojulikana kuwa sisi husema ukweli na ni wanyofu, itakuwa rahisi kwa watu kusikiliza yale tunayowafundisha.

12, 13. Kijana mmoja aliandika nini kuhusu ukweli, na kwa nini alifuata viwango vya juu vya maadili?

12 Vijana walio miongoni mwa watumishi wa Yehova pia wanaelewa umuhimu wa kusema ukweli. Jenny, aliyekuwa na umri wa miaka 13, aliandika hivi katika insha yake shuleni: “Ninathamini sana sifa ya unyofu. Kwa kusikitisha, watu wengi leo si wanyofu hata kidogo. Nimeazimia kwamba nitakuwa mnyofu sikuzote za maisha yangu. Pia nitakuwa mnyofu hata ikiwa kusema ukweli hakutanifaidi mimi au marafiki wangu. Mimi huhakikisha kwamba marafiki wangu ni watu ambao husema ukweli na ni wanyofu.”

13 Mwalimu wa Jenny alisema hivi kuhusu insha hiyo: “Ingawa wewe ni mchanga sana, umesitawisha tabia na maadili mazuri. Ninajua kwamba utadumisha tabia hizo kwa sababu una maadili mazuri.” Ni nini kilichomsaidia msichana huyo kuwa na msimamo imara wa kimaadili? Katika utangulizi wa insha yake, Jenny alisema kwamba dini yake humwekea “viwango vya kufuata maishani.” Sasa imepita miaka saba tangu Jenny aandike insha hiyo. Kama mwalimu wake alivyosema, Jenny bado anaendelea kufuata viwango vya juu vya maadili akiwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova.

Watumishi wa Yehova Hufunua Ukweli

14. Kwa nini watumishi wa Mungu hasa ndio wenye daraka kubwa la kutetea ukweli?

14 Ni kweli kwamba huenda watu wengine wasio Mashahidi wa Yehova wakasema ukweli na kujaribu kuwa wanyofu. Lakini tukiwa Mashahidi wa Yehova, tuna jukumu kubwa la kutetea ukweli. Tumekabidhiwa kweli za Biblia—kweli ambazo zinaweza kumwongoza mtu kwenye uhai wa milele. Hivyo, tuna daraka la kuwaambia wengine ukweli huo. Yesu alisema kwamba “kila mtu ambaye alipewa mengi, mengi yatadaiwa kutoka kwake.” (Luka 12:48) Bila shaka, ‘mengi yanadaiwa’ kutoka kwa wale ambao wamebarikiwa kuwa na ujuzi wenye thamani wa Mungu.

15. Unapata furaha gani unapowaeleza wengine ukweli wa Biblia?

15 Tunapata furaha tunapowaeleza wengine ukweli wa Biblia. Kama vile wanafunzi wa Yesu wa karne ya kwanza, tunatangaza habari njema—ujumbe wa tumaini unaochangamsha moyo—kwa wale ‘waliochunwa ngozi na kutupwa huku na huku kama kondoo wasio na mchungaji’ na kwa wale waliopofushwa na kutatanishwa na “mafundisho ya roho waovu.” (Mathayo 9:36; 1 Timotheo 4:1) Mtume Yohana aliandika hivi: “Sina kisababishi cha shukrani kilicho kikubwa zaidi kuliko mambo haya, kwamba niwe nikisikia kwamba watoto wangu waendelea kutembea katika kweli.” (3 Yohana 4) Yohana alifurahi sana kwa sababu ya uaminifu wa “watoto” wake ambao labda ni watu aliowahubiria ukweli. Tunafurahi kuona watu wakikubali na kulithamini Neno la Mungu.

16, 17. (a) Kwa nini si wote wanaokubali ukweli? (b) Unaweza kupata furaha gani unapotangaza ukweli wa Biblia?

16 Ni kweli kwamba si wote watakaokubali ukweli. Yesu alisema ukweli kumhusu Mungu hata kama watu wengi hawakuupenda. Aliwaambia wapinzani wake Wayahudi hivi: “Kwa nini hamniamini? Yeye atokaye kwa Mungu husikiliza semi za Mungu. Hii ndiyo sababu hamsikilizi, kwa sababu nyinyi hamtoki kwa Mungu.”—Yohana 8:46, 47.

17 Sisi, kama vile Yesu, hatusiti kuwaeleza wengine kweli zenye thamani kumhusu Yehova. Hatutazamii kila mtu akubali yale tunayomwambia, kwa kuwa si wote waliokubali yale ambayo Yesu alisema. Hata hivyo, tunafurahi kujua kwamba tunafanya lililo jema. Kwa sababu ya fadhili zake zenye upendo, Yehova anataka wanadamu wafunuliwe ukweli. Kwa kuwa Wakristo wana ukweli, wao ni wachukuaji-nuru katika ulimwengu wenye giza. Kwa kuacha nuru ya ukweli iangaze kupitia maneno na matendo yetu, tunaweza kuwasaidia wengine wampe utukufu Baba yetu wa mbinguni. (Mathayo 5:14, 16) Tunajulisha hadharani kwamba tunakataa kweli bandia ya Shetani na kulitetea Neno la Mungu lililo safi na lisiloghushiwa. Kweli tunayojua na kuwaeleza wengine inaweza kuwapa uhuru wale wanaoikubali.—Yohana 8:32.

Fuatia Njia ya Ukweli

18. Kwa nini Yesu alimkubali Nathanaeli, na alionyeshaje hivyo?

18 Yesu aliupenda ukweli na alisema ukweli. Wakati wa huduma yake hapa duniani, aliwakubali wale waliosema ukweli. Yesu alisema hivi kumhusu Nathanaeli: “Ona, Mwisraeli kwa uhakika, ambaye katika yeye hamna udanganyi.” (Yohana 1:47) Hatimaye, Nathanaeli, ambaye yaelekea aliitwa pia Bartholomayo, alichaguliwa kuwa mmoja wa wale mitume 12. (Mathayo 10:2-4) Hilo lilikuwa pendeleo lililoje!

19-21. Mtu mmoja aliyekuwa kipofu alibarikiwaje kwa sababu ya kusema ukweli kwa ujasiri?

19 Sura nzima ya kitabu cha Biblia cha Yohana inasimulia kisa cha mtu mwingine mnyofu aliyebarikiwa na Yesu. Hatujui jina la mtu huyo. Lakini tunajua kwamba mtu huyo alikuwa mwombaji aliyezaliwa akiwa kipofu. Watu walishangaa Yesu alipomponya. Habari kuhusu muujiza huo ziliwafikia baadhi ya Mafarisayo, waliouchukia ukweli, na ambao walikuwa wamekubaliana kwamba yeyote atakayemwamini Yesu atafukuzwa kutoka katika sinagogi. Walipojua njama yao, wazazi wa mtu huyo aliyekuwa kipofu waliogopa na hivyo wakawadanganya Mafarisayo, wakisema kwamba hawakujua jinsi mwana wao alivyopata kuona au ni nani aliyemponya.—Yohana 9:1-23.

20 Mtu huyo aliyeponywa aliitwa tena mbele ya Mafarisayo. Bila kujali mambo ambayo yangempata, alisema ukweli kwa ujasiri. Alieleza jinsi alivyoponywa na kwamba Yesu ndiye aliyemponya. Kwa kushangaa kwamba watu hao mashuhuri na wenye elimu hawakuamini kwamba Yesu alitoka kwa Mungu, mtu huyo aliyeponywa aliwasihi bila woga wakubali ukweli wa mambo: “Kama mtu huyu hangekuwa atoka kwa Mungu, hangeweza kufanya lolote hata kidogo.” Kwa kuwa walishindwa kumpinga, Mafarisayo walisema kwamba mtu huyo alikuwa mjeuri, nao wakamtupa nje.—Yohana 9:24-34.

21 Aliposikia habari hizo, kwa upendo Yesu alimtafuta mtu huyo. Alipompata, aliimarisha imani ya mtu huyo. Yesu alijitambulisha waziwazi kuwa ndiye Mesiya. Mtu huyo alibarikiwa sana kwa kusema ukweli. Bila shaka, wale wanaosema ukweli hupata kibali cha Mungu.—Yohana 9:35-37.

22. Kwa nini tunapaswa kufuatia njia ya ukweli?

22 Kuishi kupatana na ukweli ni jambo tunalopaswa kuchukua kwa uzito. Kufanya hivyo ni muhimu ili kusitawisha na kudumisha uhusiano mzuri pamoja na wanadamu na Mungu. Kusema ukweli kunamaanisha kusema mambo waziwazi, kuwa mnyofu, mwenye kufikika, na mwenye kutumainika, na huleta kibali cha Yehova. (Zaburi 15:1, 2) Kuwa mwongo ni kuwa mdanganyifu na asiyetegemeka, na hufanya mtu akose kibali cha Yehova. (Mithali 6:16-19) Hivyo basi na tuazimie kabisa kufuatia njia ya ukweli. Kwa hakika, ili kumwiga Mungu wa ukweli, ni lazima tujue ukweli, tuseme ukweli, na tuishi kupatana na ukweli.

Ungejibuje?

• Kwa nini tunapaswa kushukuru kwamba tunajua ukweli?

• Tunawezaje kumwiga Yehova kwa kusema ukweli?

• Tunapata faida gani kwa kuwaeleza wengine kweli ya Biblia?

• Kwa nini ni muhimu kufuatia njia ya ukweli?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 17]

Kwa kuwa Wakristo wamekabidhiwa kweli ya Biblia, wao huwaeleza wengine kweli hiyo kwa bidii

[Picha katika ukurasa wa 18]

Yule kipofu aliyeponywa na Yesu alibarikiwa sana kwa kusema ukweli