Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kujifunza Ustadi wa Kuwa na Busara

Kujifunza Ustadi wa Kuwa na Busara

Kujifunza Ustadi wa Kuwa na Busara

PEGGY alimwona mwana wake akisema na ndugu yake mdogo kwa ukali. Alimwuliza: “Je, unafikiri hiyo ndiyo njia nzuri zaidi ya kuongea na ndugu yako? Ona jinsi ambavyo amehuzunika!” Kwa nini alisema hivyo? Alikuwa akijaribu kumfundisha mwana wake ustadi wa kuwa na busara na kujali hisia za wengine.

Mtume Paulo alimtia moyo mwandamani wake, kijana Timotheo, kuwa “mwanana [au “mwenye busara”] kuelekea wote.” Kwa kufanya hivyo, Timotheo hangeumiza hisia za wengine. (2 Timotheo 2:24) Busara ni nini? Unawezaje kuboresha sifa hiyo? Na unawezaje kuwasaidia wengine wasitawishe sifa hiyo?

Busara Ni Nini?

Busara ni uwezo wa kutambua unyeti wa hali na kufanya au kusema jambo lenye fadhili zaidi au linalofaa zaidi. Mtu mwenye busara anaweza kutambua hisia za wengine na kujua jinsi maneno au matendo yake yatakavyowaathiri. Lakini kuwa na busara si ustadi tu; kunahusisha tamaa ya kweli ya kuepuka kuwaumiza wengine.

Simulizi la Biblia kuhusu Gehazi, mtumishi wa Elisha, ni mfano mmoja wa mtu ambaye hakuwa na busara. Mwanamke mmoja Mshunami ambaye mwana wake alikufa mikononi mwake alienda kumwona Elisha ili afarijiwe. Alipoulizwa kama watu wake hawajambo, alijibu: “Hawajambo.” Lakini alipomkaribia yule nabii, ‘Gehazi alikaribia amwondoe.’ Kisha Elisha akasema: “Mwache; maana roho yake ndani yake ina uchungu.”—2 Wafalme 4:17-20, 25-27.

Gehazi alitenda bila kufikiri na hakuwa na busara hata kidogo. Ni kweli kwamba mwanamke huyo hakufunua hisia zake alipoulizwa habari zake. Lakini watu wengi hawafunui hisia zao kwa mtu yeyote tu. Hata hivyo, ni lazima iwe mwanamke huyo alionyesha hisia zake kwa njia fulani. Yaonekana Elisha alitambua jambo hilo, lakini Gehazi hakulitambua, au aliamua kulipuuza. Mfano huo unaonyesha wazi sababu moja inayofanya watu watende bila busara. Mtu anapojali sana umuhimu wa kazi yake, huenda akakosa kutambua au kujali mahitaji ya wale anaoshughulika nao. Anakuwa kama dereva wa basi ambaye anahangaikia sana kufika kwa wakati hivi kwamba hasimami kubeba abiria.

Ili kuepuka kuwa watu wasio na busara kama Gehazi, tunapaswa kujitahidi kuwatendea wengine kwa fadhili kwa kuwa hatujui jinsi wanavyohisi kikweli. Tunapaswa kuwa macho kutambua dalili zinazoonyesha hisia za mtu na kumtendea au kusema naye kwa fadhili. Unawezaje kuboresha ustadi wako wa kuonyesha busara?

Kuelewa Hisia za Wengine

Yesu alikuwa stadi katika kutambua hisia za wengine na alijua jinsi ya kuwatendea kwa fadhili. Wakati mmoja alipokuwa akila katika nyumba ya Farisayo aliyeitwa Simoni, mwanamke “aliyejulikana katika jiji kuwa mtenda-dhambi” alimkaribia. Katika kisa hiki pia, mwanamke huyo hakusema lolote, lakini kwa matendo yake, mtu angeweza kutambua alivyohisi. ‘Alileta chupa ya alabasta iliyo na mafuta yenye marashi, na, akichukua kikao nyuma kwenye miguu ya Yesu, alitoa machozi na kuanza kulowesha miguu yake kwa machozi yake naye akawa akiyafuta kwa nywele za kichwa chake. Pia, alibusu miguu yake kwa wororo na kuipaka mafuta yenye marashi.’ Yesu alitambua sababu iliyofanya mwanamke huyo atende hivyo. Na hata ingawa Simoni hakusema lolote, Yesu alitambua aliyokuwa akiwaza moyoni mwake: “Mtu huyu, kama angekuwa ni nabii, angejua ni nani na ni wa aina gani mwanamke anayemgusa, kwamba ni mtenda-dhambi.”—Luka 7:37-39.

Je, unaweza kuwazia madhara ambayo yangetokea ikiwa Yesu angemsukuma mwanamke huyo kando, au ikiwa angemwambia Simoni: “Mpuuzi wewe! Huoni kwamba mwanamke huyu ametubu?” Badala ya kufanya hivyo, kwa busara Yesu alimweleza Simoni mfano wa mtu aliyemsamehe mtu mmoja deni kubwa na kumsamehe mwingine deni dogo zaidi. “Ni yupi kati yao atampenda zaidi?” Yesu akauliza. Kwa hiyo, badala ya Yesu kuonekana kwamba anamshutumu Simoni, alimpongeza kwa jibu lake sahihi. Kisha kwa fadhili, alimsaidia Simoni kutambua dalili nyingi zilizoonyesha hisia za mwanamke huyo na ishara za toba yake. Yesu alimgeukia mwanamke huyo na kwa fadhili akamwonyesha kwamba alielewa hisia zake. Alimwambia kwamba dhambi zake zimesamehewa, kisha akasema: “Imani yako imekuokoa; shika njia yako uende kwa amani.” Bila shaka inaonekana kwamba maneno hayo ya busara yaliimarisha azimio la mwanamke huyo la kutenda mema. (Luka 7:40-50) Yesu alifanikiwa kuwa mwenye busara kwa sababu alitambua hisia za wengine na kuwatendea kwa huruma.

Kama vile Yesu alivyomsaidia Simoni, sisi pia tunaweza kujifunza, kisha tuwasaidie wengine kutambua dalili zinazoonyesha hisia za wengine. Wahudumu wenye uzoefu wanaweza kuwafundisha wapya ustadi huo wanapokuwa katika huduma ya Kikristo. Baada ya kumhubiria mtu habari njema, wanaweza kuzungumzia dalili zilizoonyesha hisia za mtu huyo. Je, mtu huyo alikuwa mwenye haya, mwenye shaka, amekasirika, au mwenye shughuli nyingi? Ni njia gani yenye fadhili zaidi ambayo tungetumia kumsaidia? Wazee pia wanaweza kuwasaidia ndugu na dada ambao wamekosana kwa sababu ya kutokuwa na busara. Msaidie kila mmoja aelewe hisia za mwenzake. Je, anahisi kwamba ametukanwa, amepuuzwa, au ameeleweka vibaya? Je, kumtendea kwa fadhili kutamsaidia ahisi vizuri?

Wazazi wanapaswa kuwasaidia watoto wao wasitawishe huruma, kwa kuwa sifa hiyo itawachochea kutenda kwa busara. Mwana wa Peggy aliyetajwa mwanzoni mwa makala hii, alitambua jinsi alivyomwumiza ndugu yake alipoona uso wake umebadilika, amenuna, na kulengwa-lengwa na machozi. Kama vile mama yake alivyotazamia, mwana huyo alijuta na akaamua kubadilika. Wana hao wawili wa Peggy walitumia ustadi waliojifunza utotoni, na baadaye wakawa walimu wa habari njema na wachungaji wenye matokeo katika kutaniko la Kikristo.

Onyesha Kwamba Unaelewa

Busara inahitajiwa hasa unapohisi kwamba mtu fulani amekukosea. Usipojihadhari, unaweza kumvunjia heshima kwa urahisi. Kwanza, tunaweza kumpongeza kwa jambo fulani hususa. Badala ya kumchambua, jaribu kutatua tatizo hilo. Mweleze jinsi jambo alilofanya linavyokuathiri, na mabadiliko ambayo ungependa afanye. Kisha uwe tayari kumsikiliza. Labda umemwelewa vibaya.

Watu hutaka uelewe maoni yao hata kama hukubaliani nayo. Yesu alizungumza kwa busara na kuonyesha kwamba anaelewa mahangaiko ya Martha. Alisema hivi: “Martha, Martha, wewe wahangaika na kusumbuka juu ya mambo mengi.” (Luka 10:41) Vivyo hivyo, mtu anapokueleza tatizo lake, badala ya kumpa suluhisho kabla hujamsikiliza, njia ya busara ya kuonyesha kwamba unaelewa tatizo au malalamishi yake ni kurudia yale ambayo amekueleza kwa maneno yako mwenyewe. Hiyo ni njia ya fadhili ya kuonyesha kwamba unamwelewa.

Tambua Mambo Usiyopaswa Kusema

Malkia Esta alipotaka kumwomba mume wake atangue njama ya Hamani ya kuwaangamiza Wayahudi, alipanga kwa busara mume wake awe na furaha ndipo amweleze jambo hilo. Kisha akataja suala hilo gumu. Lakini inafaa kukumbuka mambo ambayo hakusema. Aliepuka kwa busara kutaja kwamba mume wake alihusika katika njama hiyo mbaya.—Esta 5:1-8; 7:1, 2; 8:5.

Vivyo hivyo, unapomtembelea mume asiyeamini wa dada Mkristo, badala ya kumsomea Biblia mara moja, mbona usimwulize kwa busara mambo anayopenda? Mgeni akija kwenye Jumba la Ufalme akiwa amevalia isivyofaa, badala ya kumwuliza kuhusu mavazi yake, mkaribishe kwa uchangamfu. Au mtu akihudhuria mikutano baada ya kutoonekana kwa muda mrefu, badala ya kumwuliza amepotelea wapi, mkaribishe pia kwa uchangamfu. Na unapoona kwamba mtu ambaye amependezwa hivi karibuni ana maoni yasiyofaa, huenda isifae kumrekebisha mara moja. (Yohana 16:12) Busara inahusisha kuwa na fadhili na kutambua mambo usiyopaswa kusema.

Maneno Ambayo Huponya

Kujifunza ustadi wa kusema kwa busara kutakusaidia uwe na uhusiano mzuri na wengine hata kama mtu fulani ameelewa vibaya kusudi lako, naye amekasirika na kuweka kinyongo. Kwa mfano, watu wa Efraimu ‘walipoteta sana’ na Gideoni, aliwajibu kwa busara na kuwaeleza waziwazi mambo yaliyokuwa yametendeka, naye akawasifu kwa unyofu watu wa Efraimu kwa yale waliyokuwa wametimiza. Hilo lilikuwa jambo la busara kwa sababu Gideoni alitambua kilichowakasirisha na unyenyekevu wake uliwatuliza.—Waamuzi 8:1-3; Mithali 16:24.

Sikuzote jaribu kufikiria jinsi maneno yako yatakavyowaathiri wengine. Kujitahidi kuwa na busara kutakusaidia upate furaha inayofafanuliwa katika Mithali 15:23: “Mtu hulifurahia jibu la kinywa chake; na neno linenwalo wakati wa kufaa ni jema kama nini!”

[Picha katika ukurasa wa 31]

Wahudumu Wakristo wenye uzoefu wanaweza kuwafundisha wapya kuwa na busara

[Picha katika ukurasa wa 31]

Wazazi wanaweza kuwafundisha watoto wao kujali hisia za wengine