Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ndoa​—Chanzo na Kusudi Lake

Ndoa​—Chanzo na Kusudi Lake

“Yehova Mungu akaendelea kusema: ‘Si vema huyo mwanamume aendelee kuwa peke yake. Nitamfanyia msaidizi.’”—MWA. 2:18.

NYIMBO: 36, 11

1, 2. (a) Ndoa ilianzaje? (b) Yaelekea mwanamume na mwanamke wa kwanza walitambua nini kuhusu ndoa? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

NDOA ni sehemu ya kawaida maishani. Kuchunguza jinsi ilivyoanzishwa na kusudi lake kunaweza kutusaidia kuwa na mtazamo mzuri kuelekea uhusiano huo na kufurahia zaidi baraka zake. Baada ya Mungu kumuumba mwanadamu wa kwanza, Adamu, wanyama waliletwa kwake ili awape majina. Lakini “kwa ajili ya huyo mwanamume hakupatikana msaidizi wa kuwa kikamilisho chake.” Kwa hiyo, Mungu akamletea Adamu usingizi mzito, akachukua ubavu wake mmoja na kuufanya kuwa mwanamke, na kisha akamleta kwa huyo mwanamume. (Soma Mwanzo 2:20-24.) Hivyo, Yehova ndiye Mwanzilishi wa ndoa.

2 Miaka mingi baadaye, Yesu alithibitisha kwamba Yehova ndiye aliyesema maneno haya: “Mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye atashikamana na mke wake, na hao wawili watakuwa mwili mmoja.” (Mt. 19:4, 5) Adamu na Hawa walitambua kwamba wana uhusiano wa karibu sana kwa sababu Mungu alitumia ubavu wa Adamu kumuumba mwanamke wa kwanza. Yehova hakukusudia kuwe na mpango wa talaka au mtu kuwa na mwenzi zaidi ya mmoja.

JINSI NDOA INAVYOTIMIZA KUSUDI LA YEHOVA

3. Kusudi muhimu la ndoa lilikuwa nini?

3 Adamu alifurahia kuwa na mke mrembo na baadaye alimwita Hawa. Akiwa “kikamilisho chake,” angekuwa “msaidizi,” nao wangefurahia kuwa pamoja kila siku na kutimiza majukumu yao wakiwa mume na mke. (Mwa. 2:18) Kusudi muhimu la ndoa lilikuwa kujaza dunia. (Mwa. 1:28) Ingawa waliwapenda wazazi wao, wana na mabinti wangewaacha ili kufunga ndoa na kuanzisha familia zao. Wanadamu wangeijaza dunia na kuifanya iwe paradiso.

4. Ndoa ya kwanza ilipatwa na nini?

4 Ndoa ya kwanza ilipatwa na matatizo makubwa Adamu na Hawa walipokosa kumtii Yehova. “Yule nyoka wa zamani,” Shetani Ibilisi, alimdanganya Hawa kwa kumfanya aamini kwamba ikiwa angekula tunda la “mti wa ujuzi wa mema na mabaya,” angepata ujuzi wa pekee ambao ungemwezesha kuamua mema na mabaya. Hawa hakuheshimu ukichwa wa mume wake kwa kumwuliza maoni yake kuhusu jambo hilo. Kwa upande mwingine, badala ya kumtii Mungu, Adamu alikubali tunda ambalo Hawa alimpa.—Ufu. 12:9; Mwa. 2:9, 16, 17; 3:1-6.

5. Tunaweza kujifunza nini kutokana na jinsi Adamu na Hawa walivyomjibu Yehova?

5 Mungu alipowauliza kuhusu jambo hilo, Adamu alimlaumu mke wake kwa kusema hivi: “Mwanamke uliyenipa awe pamoja nami, alinipa tunda kutoka katika ule mti nami nikala.” Naye Hawa alimlaumu nyoka kwa kumdanganya. (Mwa. 3:12, 13) Walitoa visingizio visivyo na msingi! Kwa kuwa wenzi hao wa kwanza walikosa kutii, Yehova aliwahukumu kuwa waasi. Hilo ni onyo kubwa kwetu! Ili ndoa ifanikiwe, wenzi wote wawili wanapaswa kuwajibika na kumtii Yehova.

6. Ungeelezaje andiko la Mwanzo 3:15?

6 Licha ya mambo ambayo Shetani alifanya katika Edeni, Yehova aliwapa wanadamu tumaini alipotoa unabii wa kwanza wa Biblia. (Soma Mwanzo 3:15.) Unabii huo ulionyesha kwamba kiumbe huyo wa roho aliyekuwa mwasi wa kwanza, angepondwa na “uzao” wa “mwanamke.” Hivyo, Yehova aliwasaidia wanadamu waone uhusiano wa pekee kati yake na viumbe wa roho waadilifu wanaomtumikia mbinguni. Baadaye, Maandiko yalifunua kwamba Mungu angemtuma mmoja kutoka katika tengenezo lake, ambalo ni kama mke wake, ili ‘amponde’ Ibilisi na kuandaa njia ya wanadamu watiifu kufurahia kile ambacho wenzi wa kwanza walipoteza, yaani, tumaini la kuishi milele duniani kulingana na kusudi la awali la Yehova.—Yoh. 3:16.

7. (a) Ndoa zimepatwa na nini tangu uasi wa Adamu na Hawa? (b) Biblia inawaamuru waume na wake wafanye nini?

7 Uasi wa Adamu na Hawa uliathiri ndoa yao na ndoa nyingine zote. Kwa mfano, Hawa na wazao wake wa kike wangepata maumivu mengi wakati wa ujauzito na wakati wa kuzaa. Wanawake wangekuwa na tamaa kuelekea waume zao, lakini wanaume wangewatawala wake zao, nyakati nyingine kimabavu, kama tunavyoona katika ndoa nyingi leo. (Mwa. 3:16) Biblia inawaamuru waume watumie ukichwa wao kwa upendo. Kwa upande mwingine, wake wanapaswa kujitiisha chini ya ukichwa wa waume zao. (Efe. 5:33) Wenzi wanaomwogopa Mungu wanaposhirikiana, hali zinazoweza kusababisha kutoelewana hupungua au kutoweka kabisa.

NDOA—KUANZIA WAKATI WA ADAMU HADI GHARIKA

8. Ni nini kilichoupata mpango wa ndoa tangu wakati wa Adamu hadi wakati wa Gharika?

8 Kabla ya kufa kwa sababu ya dhambi na kutokamilika, Adamu na Hawa walizaa wana na mabinti. (Mwa. 5:4) Mwana wao wa kwanza, Kaini, alioa mke kutoka kati ya watu wake wa ukoo. Lameki, mzao wa Kaini, ndiye mwanamume wa kwanza anayetajwa kuwa na wake wawili. (Mwa. 4:17, 19) Ni watu wachache tu wanaotajwa kuwa waabudu wa Yehova katika vizazi vilivyokuwapo tangu wakati wa Adamu hadi Gharika ya siku za Noa. Baadhi yao walikuwa Abeli, Enoko, na Noa pamoja na familia yake. Biblia inasema hivi kuhusu siku za Noa: “Wana wa Mungu wa kweli wakaanza kuwaona mabinti wa wanadamu, kwamba ni wenye sura ya kupendeza; nao wakajichukulia wake, yaani, wote waliowachagua.” Muungano huo usio wa kawaida kati ya malaika waliojivika miili ya kibinadamu na wanawake ulitokeza majitu yenye jeuri yaliyoitwa Wanefili. Isitoshe, “ubaya wa mwanadamu ulikuwa mwingi duniani na kila mwelekeo wa fikira za moyo wake ulikuwa mbaya tu wakati wote.”—Mwa. 6:1-5.

9. Yehova alifanya nini kuhusu watu waovu wa siku za Noa, na tunapaswa kujifunza nini kutokana na mambo yaliyofanyika wakati huo?

9 Yehova alileta Gharika ya siku za Noa ili kuharibu waovu. Wakati huo, watu walijishughulisha sana na shughuli za kila siku za maisha, kutia ndani ndoa, hivi kwamba hawakuchukua kwa uzito kile ambacho “Noa, mhubiri wa uadilifu,” alisema kuhusu uharibifu uliokuwa ukikaribia. (2 Pet. 2:5) Yesu alilinganisha hali hizo na hali ambazo tungeona leo. (Soma Mathayo 24:37-39.) Leo, watu wengi wanakataa kusikiliza habari njema ya Ufalme wa Mungu inayohubiriwa katika dunia yote ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote kabla ya mwisho wa mfumo huu mwovu. Tunajifunza kwamba hata majukumu ya familia, kama vile ndoa na kulea watoto, hayapaswi kutukengeusha tukose kutambua kwamba siku ya Yehova inakaribia.

NDOA—KUANZIA WAKATI WA GHARIKA HADI SIKU ZA YESU

10. (a) Ni mazoea gani ya kingono yaliyokuwa sehemu ya kawaida ya maisha katika tamaduni nyingi? (b) Abrahamu na Sara waliwekaje mfano mzuri katika ndoa yao?

10 Ingawa Noa na wana wake watatu hawakuoa mke zaidi ya mmoja, ilikuwa kawaida kwa watu kuoa wake wengi katika nyakati za kale. Katika tamaduni nyingi, upotovu wa maadili katika ngono ulikuwa sehemu ya kawaida ya maisha, na hata ulihusishwa katika ibada. Abramu (Abrahamu) na mke wake, Sarai (Sara), walimtii Mungu kwa kuhamia nchi ya Kanaani, nchi iliyojaa watu ambao hawakuiheshimu ndoa. Hivyo, Yehova aliamuru Sodoma na Gomora ziharibiwe kwa sababu wakazi wake walijihusisha au kuunga mkono upotovu mbaya sana wa maadili katika ngono. Abrahamu aliongoza familia yake kwa njia nzuri, na Sara aliweka mfano mzuri kwa kujitiisha chini ya ukichwa wa mume wake. (Soma 1 Petro 3:3-6.) Abrahamu alihakikisha kwamba mwana wake Isaka alioa mwabudu wa Yehova. Kwa njia hiyohiyo pia, Yakobo mwana wa Isaka, alihangaikia ibada ya kweli, na hivyo wanawe wakawa mababu wa makabila 12 ya Israeli.

11. Sheria ya Musa iliwalindaje Waisraeli?

11 Baadaye, Yehova alifanya agano pamoja na wazao wa Yakobo (Israeli). Sheria ya Musa ilidhibiti mambo ya msingi kuhusu ndoa katika nyakati za kale, kutia ndani ndoa za wake wengi. Iliwalinda Waisraeli kiroho kwa kuwakataza kuoa waabudu wa uwongo. (Soma Kumbukumbu la Torati 7:3, 4.) Matatizo makubwa ya ndoa yalipotokea, wazee waliandaa msaada. Kulikuwa na sheria dhidi ya wenzi waliokosa uaminifu, waliokuwa na wivu, na waliowashuku wenzi wao. Talaka iliruhusiwa, lakini ilidhibitiwa pia. Mwanamume angeweza kumtaliki mke wake kwa sababu ya “kitu fulani kisichofaa.” (Kum. 24:1) “Kitu fulani kisichofaa” hakikufafanuliwa lakini inaonekana kwamba hakikuhusisha mambo madogo-madogo.—Law. 19:18.

USIMTENDEE KAMWE MWENZI WAKO KWA HILA

12, 13. (a) Wanaume fulani katika siku za Malaki waliwatendeaje wake zao? (b) Leo, mtu aliyebatizwa akitoroka na mwenzi wa mtu mwingine, matokeo yatakuwa nini?

12 Katika siku za nabii Malaki, waume wengi Wayahudi waliwatendea wake zao kwa hila kwa kuwataliki bila sababu za msingi. Inawezekana wanaume hao waliwaacha wake wa ujanani ili waoe wanawake vijana au hata wanawake wa kipagani. Wanaume Wayahudi waliendelea kuwataliki wake zao “kwa kila sababu” hata Yesu alipokuwa duniani. (Mt. 19:3) Yehova Mungu alichukia talaka za aina hiyo.—Soma Malaki 2:13-16.

13 Leo, ni kosa kwa watu wa Yehova kutendeana kwa hila katika ndoa. Lakini tuseme kwamba mwanamume au mwanamke aliyebatizwa anatoroka na mwenzi wa mtu mwingine na kumwoa baada ya kupewa talaka. Mkosaji huyo asipotubu, atatengwa na ushirika ili kudumisha usafi wa kiroho wa kutaniko. (1 Kor. 5:11-13) Lazima mtu huyo ‘azae matunda yanayofaa toba’ kabla ya kurudishwa kutanikoni. (Luka 3:8; 2 Kor. 2:5-10) Ingawa hakuna muda hususa unaopaswa kupita kabla hajarudishwa, tendo hilo la hila, ambalo halitukii mara nyingi kati ya watu wa Mungu, halipaswi kupuuzwa. Huenda muda mrefu ukapita, labda mwaka mmoja au zaidi, ili mkosaji athibitishe kwamba ametubu kikweli. Hata mtu huyo akirudishwa kutanikoni, bado atatoa hesabu “mbele ya kiti cha hukumu cha Mungu.”—Rom. 14:10-12; w81 4/1, uku. 22, au w79-E 11/15 uku. 31-32.

NDOA YA KIKRISTO

14. Sheria ilitimiza kusudi gani la msingi?

14 Sheria ya Musa iliwaongoza Waisraeli kwa miaka zaidi ya 1,500. Iliwasaidia watu wa Mungu wazingatie kanuni za uadilifu waliposhughulikia mambo katika familia na mambo mengine, na wakati uleule ilikuwa mtunzaji aliyewaongoza kwa Masihi. (Gal. 3:23, 24) Sheria ilifutwa Yesu alipokufa na Mungu akaanzisha mpango mpya. (Ebr. 8:6) Chini ya mpango huo, Wakristo walikatazwa mambo fulani ambayo Sheria ilikuwa imeruhusu.

15. (a) Ni kielelezo gani cha ndoa ambacho kingefuatwa katika kutaniko la Kikristo? (b) Mkristo anapaswa kuzingatia mambo gani anapofikiria talaka?

15 Alipokuwa akijibu swali la Mafarisayo fulani, Yesu alisema kwamba Musa aliwapa ruhusa ya kuwataliki wenzi wao, lakini “haikuwa hivyo kutoka mwanzo.” (Mt. 19:6-8) Hivyo, jibu la Yesu lilionyesha kwamba kielelezo ambacho Mungu aliweka tangu mwanzo kuhusu ndoa, ndicho kingetumiwa katika ndoa za Kikristo. (1 Tim. 3:2, 12) Kwa kuwa wenzi wa ndoa ni “mwili mmoja,” wanapaswa kushikamana na kuimarisha kifungo chao kwa kumpenda Mungu na mwenzi wao. Hata hivyo, mtu akimtaliki mwenzi wake kisheria, na si kwa msingi wa uasherati, hapaswi kuoa au kuolewa tena. (Mt. 19:9) Bila shaka, mtu anaweza kumsamehe mwenzi ambaye alifanya uzinzi lakini akatubu, kama nabii Hosea alivyomsamehe mke wake Gomeri, aliyekuwa mwasherati. Vivyo hivyo, Yehova aliwaonyesha Waisraeli rehema walipotubu baada ya taifa hilo kufanya uzinzi wa kiroho. (Hos. 3:1-5) Pia, mtu akijua kwamba mwenzi wake amefanya uzinzi na aamue kufanya ngono naye, hilo lingeonyesha kwamba amemsamehe na hivyo kuondoa msingi wa Kimaandiko wa kumtaliki.

16. Yesu alisema nini kuhusu useja?

16 Baada ya kuonyesha kwamba msingi pekee wa Wakristo wa kweli kupata talaka ni uasherati, Yesu alizungumzia “wale walio na . . . zawadi” ya kubaki waseja. Aliongeza hivi: “Yule anayeweza kulipa nafasi na alipe nafasi.” (Mt. 19:10-12) Watu wengi wameamua kubaki waseja ili wamtumikie Yehova bila kukengeuka. Wanastahili pongezi kwa kufanya hivyo.

17. Ni nini kinachoweza kumsaidia Mkristo aamue ikiwa atafunga ndoa au la?

17 Uamuzi wa kubaki mseja au kufunga ndoa ni wa mtu binafsi ikitegemea kama anaweza kusitawisha zawadi ya useja kutoka moyoni au la. Mtume Paulo alipendekeza useja, hata hivyo, alisema hivi: “Kwa sababu ya kuenea kwa uasherati, kila mwanamume na awe na mke wake mwenyewe na kila mwanamke awe na mume wake mwenyewe.” Paulo aliongeza hivi: “Ikiwa hawawezi kujizuia, acheni wafunge ndoa, kwa maana ni bora kufunga ndoa kuliko kuwaka tamaa.” Kufunga ndoa kunaweza kumzuia mtu asiongozwe na tamaa kuingia kwenye mazoea kama vile kupiga punyeto au upotovu wa maadili katika ngono. Zaidi ya hilo, mtu anahitaji kuzingatia umri wake anapofikiria kufunga ndoa kwa sababu Paulo alisema hivi: “Kama yeyote akiona kwamba anajiendesha isivyofaa kuelekea ubikira wake, ikiwa huo umepita upeo wa ujana, na hivyo ndivyo inavyopaswa kutendeka, acheni afanye lile analotaka; hafanyi dhambi. Acheni afunge ndoa.” (1 Kor. 7:2, 9, 36; 1 Tim. 4:1-3) Hata hivyo, mtu hapaswi kufunga ndoa kwa sababu ya tamaa zenye nguvu za ngono ambazo zinaweza kutokea ujanani. Huenda asiwe na ukomavu wa kutosha kutimiza majukumu ya ndoa.

18, 19. (a) Ndoa ya Kikristo inapaswa kuanzishwaje? (b) Makala inayofuata itazungumzia nini?

18 Ndoa ya Kikristo inapaswa kuanzishwa na mwanamume na mwanamke waliojiweka wakfu kwa Yehova na wanaompenda kwa moyo wote. Pia, wanapaswa kuwa wanapendana sana hivi kwamba wangependa kuunganisha maisha yao katika kifungo cha ndoa. Bila shaka, watabarikiwa kwa kufuata ushauri wa kuoa “katika Bwana tu.” (1 Kor. 7:39) Baada ya kuoana, wenzi wa ndoa watatambua kwamba Biblia inatoa ushauri bora sana wa kufanikisha ndoa yao.

19 Makala inayofuata itazungumzia Maandiko yanayoweza kuwasaidia wenzi wa ndoa wakabiliane na changamoto za kuishi mwishoni mwa kipindi cha “siku za mwisho,” kipindi ambacho wanaume na wanawake wengi sana wana tabia zinazofanya ndoa zisifanikiwe. (2 Tim. 3:1-5) Katika Neno lake lenye thamani, Yehova ametupatia kile tunachohitaji ili ndoa zetu zifanikiwe na ziwe na furaha tunapoendelea kutembea katika barabara inayoongoza kwenye uzima wa milele.—Mt. 7:13, 14.