Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unaona Uhitaji wa Kufanya Maendeleo ya Kiroho?

Je, Unaona Uhitaji wa Kufanya Maendeleo ya Kiroho?

“Endelea kufanya bidii katika kusoma mbele ya watu wote, katika kuhimiza, katika kufundisha.”​—1 TIM. 4:13.

NYIMBO: 45, 70

1, 2. (a) Andiko la Isaya 60:22 limetimiaje katika siku hizi za mwisho? (b) Kuna uhitaji gani sasa katika sehemu ya kidunia ya tengenezo la Yehova?

“MDOGO atakuwa elfu, na mnyonge atakuwa taifa lenye nguvu.” (Isa. 60:22) Unabii huo unatimia katika siku hizi za mwisho. Katika mwaka wa utumishi wa 2015, kumekuwa na wahubiri wa Ufalme 8,220,105 ulimwenguni pote! Sehemu ya mwisho ya unabii huo inamhusu kila Mkristo, kwa kuwa Baba yetu wa mbinguni anasema hivi: “Mimi mwenyewe, Yehova, nitaharakisha jambo hilo kwa wakati wake.” Kama wasafiri kwenye gari linaloongeza mwendo, sote tunaona jinsi bidii katika kazi ya kufanya wanafunzi inavyoongezeka. Tukiwa mtu mmoja-mmoja tunaitikiaje ongezeko hilo? Je, tunafanya yote tuwezayo ili tuwe wahubiri wenye bidii wa Ufalme? Ndugu na dada wengi wanajitolea kuwa mapainia wa kawaida au mapainia wasaidizi. Pia, tunafurahi sana kuona wengi wakikubali kutumikia katika maeneo yenye uhitaji mkubwa wa wahubiri au wakijitolea kushiriki katika utendaji mwingine wa kitheokrasi.

2 Wakati huohuo, tunaona uhitaji mkubwa wa wafanyakazi wengi zaidi. Kila mwaka, makutaniko 2,000 hivi huanzishwa. Ikiwa kila kutaniko jipya linahitaji wazee 5, basi kila mwaka watumishi wa huduma 10,000 wanahitaji kustahili kuwa waangalizi. Hilo linamaanisha kwamba ndugu wengi zaidi wanahitaji kuwa na sifa za kustahili kutumikia wakiwa watumishi wa huduma. Isitoshe, iwe sisi ni ndugu au dada, bila shaka tuna “mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana.”—1 Kor. 15:58.

KUFANYA MAENDELEO YA KIROHO KUNAMAANISHA NINI?

3, 4. Unaweza kujiwekea malengo gani ya kiroho?

3 Soma 1 Timotheo 3:1. Kitenzi cha Kigiriki kinachotafsiriwa ‘kujitahidi kufikia,’ kinamaanisha kujinyoosha ili kushika kitu fulani ambacho huenda huwezi kukifikia kwa urahisi. Kwa kutumia neno hilo, mtume Paulo alikazia kwamba kufanya maendeleo ya kiroho kunahitaji jitihada. Wazia ndugu anayefikiria malengo anayoweza kufikia kutanikoni. Huenda kwa sasa hatumikii akiwa mtumishi wa huduma, lakini anatambua kwamba anahitaji kusitawisha sifa za kiroho. Kwanza, anajitahidi kustahili kuwa mtumishi wa huduma. Baadaye, anatumaini kuwa na sifa za kiroho zitakazomstahilisha kuwa mwangalizi. Katika visa vyote viwili, anajitahidi kufikia sifa zinazohitajiwa ili atimize majukumu mengi zaidi kutanikoni.

4 Vivyo hivyo, ndugu na dada wanaotamani kutumikia wakiwa mapainia, Wanabetheli, au wajitoleaji wa ujenzi wa Majumba ya Ufalme, wanahitaji kujitahidi ili wafikie malengo yao. Acheni tufikirie jinsi Neno la Mungu linavyowatia moyo watu wote wafanye maendeleo katika ibada ya kweli.

JITAHIDI KUFANYA MAENDELEO MAKUBWA YA KIROHO

5. Vijana wanaweza kutumiaje nguvu zao katika utumishi wa Ufalme?

5 Vijana wana nguvu zinazohitajiwa kutimiza mengi katika utumishi wa Yehova. (Soma Methali 20:29.) Baadhi ya vijana wanaotumikia Betheli wanashiriki kuchapisha na kujalidi Biblia na machapisho ya Biblia. Ndugu na dada wengi vijana wanashiriki katika kazi ya kujenga na kudumisha Majumba ya Ufalme. Misiba ya asili inapotokea, vijana wanawaunga mkono Mashahidi wenye uzoefu kutoa misaada. Na mapainia wengi vijana wanasaidia kuhubiri habari njema katika lugha za asili na lugha za kigeni.

6-8. (a) Kijana mmoja alibadili maoni yake jinsi gani kuelekea utumishi wake kwa Mungu, naye alipata matokeo gani? (b) Tunawezaje ‘kuonja na kuona ya kuwa Yehova ni mwema’?

6 Bila shaka unathamini umuhimu wa kujitoa kwa moyo wote katika utumishi wa Mungu. Namna gani ikiwa unahisi kama alivyohisi ndugu anayeitwa Aaron? Ingawa alilelewa katika familia ya Kikristo, anakiri hivi: “Niliona mikutano na utumishi wa shambani kuwa yenye kuchosha.” Alitaka kumtumikia Mungu kwa shangwe lakini hakuelewa ni kwa nini alikosa furaha. Alifanya nini?

7 Aaron alipanga ratiba ya kiroho iliyohusisha usomaji wa Biblia na kutayarisha na kutoa maelezo mikutanoni. Lakini zaidi ya yote, alianza kusali kwa ukawaida. Upendo wake kwa Yehova ulipoongezeka, alianza kufanya maendeleo makubwa ya kiroho. Tangu wakati huo, Aaron alifurahia kuwa painia, kushirikiana na wengine kutoa misaada wakati wa misiba, na kuhubiri katika nchi ya kigeni. Sasa Aaron anatumikia Betheli na ni mzee wa kutaniko. Ana maoni gani kuhusu maamuzi ambayo amefanya maishani? “‘Nimeonja na kuona ya kuwa Yehova ni mwema.’ Kwa kuwa Yehova amenibariki, ninahisi nikiwa na deni kwake na ninachochewa kufanya mengi zaidi katika utumishi wake, jambo ambalo limenipatia baraka nyingi hata zaidi.”

8 Mtunga-zaburi aliimba hivi: “Wale wanaomtafuta Yehova, hawatakosa chochote chema.” (Soma Zaburi 34:8-10.) Kwa kweli, Yehova hawatamaushi kamwe wale wanaomtumikia kwa bidii. Tunapofanya yote tuwezayo katika utumishi wake, kila mmoja wetu ‘anaonja na kuona ya kuwa Yehova ni mwema.’ Na tunapomtolea Mungu ibada ya nafsi yote, tunakuwa na furaha isiyo na kifani.

VUMILIA NA USICHOKE

9, 10. Kwa nini ni muhimu uwe na ‘mtazamo wa kungoja’?

9 Unapojitahidi kufikia malengo yako, onyesha “mtazamo wa [kungoja].” (Mika 7:7) Sikuzote Yehova huwategemeza watumishi wake waaminifu, ingawa huenda akaruhusu wakati upite kabla hawajapata mapendeleo au hali zao ziwe nzuri. Aliahidi kumpatia Abrahamu mwana, lakini mzee huyo wa ukoo alihitaji kuwa na imani na subira. (Ebr. 6:12-15) Ingawa alingoja kwa miaka mingi kabla ya kuzaliwa kwa Isaka, Abrahamu hakuvunjika moyo, na Yehova hakumkatisha tamaa.​—Mwa. 15:3, 4; 21:5.

10 Si rahisi kungoja. (Met. 13:12) Tukikazia fikira sana hali zenye kukatisha tamaa, tunaweza kuvunjika moyo. Badala yake, ni jambo la hekima kutumia muda wetu kuboresha sifa zetu za kiroho. Acheni tuone njia tatu za kufanya hivyo.

11. Tunaweza kujitahidi kusitawisha sifa zipi za kiroho, na kwa nini sifa hizo ni muhimu?

11 Sitawisha sifa za kiroho. Tunaposoma Neno la Mungu na kulitafakari, tunasitawisha hekima, ufahamu, uwezo wa kufanya maamuzi mazuri, ujuzi, uwezo wa kufikiri, na utimamu wa akili. Sifa kama hizo ni muhimu kwa wale wanaoongoza katika ibada ya kweli. (Met. 1:1-4; Tito 1:7-9) Tunaposoma machapisho yetu yanayotegemea Biblia, tunaweza kutambua maoni ya Mungu kuhusu mambo mbalimbali. Kila siku tunakabili mambo yanayohusiana na burudani, mavazi na mapambo, matumizi ya pesa, na jinsi ya kuishi kwa amani na wengine. Tukitumia mambo tunayojifunza katika Biblia, tunaweza kufanya maamuzi yanayomfurahisha Yehova.

12. Washiriki wa kutaniko wanaweza kuonyeshaje kwamba wanategemeka?

12 Onyesha kwamba unategemeka. Iwe sisi ni ndugu au dada, tunahitaji kufanya yote tuwezayo kutimiza migawo yoyote tunayopokea. Akiwa gavana, Nehemia alihitaji kuchagua wanaume watimize majukumu mbalimbali kati ya watu wa Mungu. Alichagua nani? Alichagua watu wanaomwogopa Mungu, wanaotumainika, na kutegemeka. (Neh. 7:2; 13:12, 13) Leo pia, “kinachoangaliwa katika wasimamizi-nyumba ni mtu kupatwa akiwa mwaminifu.” (1 Kor. 4:2) Matendo mazuri hayakosi kutambuliwa.​—Soma 1 Timotheo 5:25.

13. Unaweza kuigaje mfano wa Yosefu wengine wanapokutendea isivyo haki?

13 Mruhusu Yehova akusafishe. Unaweza kufanya nini wengine wakikutendea isivyo haki? Labda unaweza kurekebisha hali hiyo haraka. Lakini nyakati nyingine ukijaribu kujitetea sana, unaweza kufanya hali iwe mbaya hata zaidi. Ndugu za Yosefu walimtendea isivyofaa, hata hivyo, hakuwa na kinyongo kuwaelekea. Baadaye, Yosefu alishtakiwa kwa uwongo na kufungwa gerezani isivyo haki. Hata hivyo, alimruhusu Yehova amwongoze katika nyakati ngumu. Matokeo yalikuwa nini? “Maneno ya Yehova mwenyewe [yalimsafisha].” (Zab. 105:19) Majaribu hayo yalipoisha, Yosefu alistahili kutumikia katika mgawo wa pekee. (Mwa. 41: 37-44; 45:4-8) Unaposhughulika na matatizo yaliyo kama mwiba, sali upate hekima, utende na uzungumze kwa upole, na umtegemee Mungu akupe nguvu. Yehova atakusaidia.​—Soma 1 Petro 5:10.

FANYA MAENDELEO KATIKA HUDUMA YA SHAMBANI

14, 15. (a) Kwa nini tunapaswa ‘kuangalia daima’ jinsi tunavyohubiri? (b) Unawezaje kubadili njia yako ya kuhubiri ili ifaane na hali mbalimbali? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii na sanduku lenye kichwa, “ Je, Uko Tayari Kutumia Njia Tofauti ya Kuhubiri?”)

14 Paulo alimhimiza hivi Timotheo: “Endelea kufanya bidii katika kusoma mbele ya watu wote, katika kuhimiza, katika kufundisha. Jiangalie daima wewe mwenyewe na kufundisha kwako.” (1 Tim. 4:13, 16) Tayari Timotheo alikuwa mhubiri wa Ufalme mwenye uzoefu. Hata hivyo, huduma yake ingekuwa na matokeo mazuri ikiwa “[angeangalia] daima” kufundisha kwake. Hakufikiri tu kwamba watu wangeikubali habari njema ikiwa angeendelea kutumia njia yake ya kawaida ya kuhubiri. Ili aendelee kufikia mioyo, alihitaji kuboresha njia yake ya kufundisha ipatane na mahitaji yao. Tukiwa wahubiri wa Ufalme, tunahitaji kufanya vivyo hivyo.

15 Mara nyingi tunawakosa watu nyumbani tunapohubiri nyumba kwa nyumba. Katika maeneo mengine, haturuhusiwi kuingia kwenye nyumba au eneo lenye ulinzi mkali. Ikiwa eneo lenu liko hivyo, kwa nini usijaribu njia tofauti za kuhubiri habari njema?

16. Mahubiri ya hadharani yanaweza kutusaidiaje kuwa na matokeo mazuri?

16 Mahubiri ya hadharani ni njia bora sana ya kueneza habari njema. Mashahidi wengi wanapata matokeo mazuri na wanafurahia sana kazi hiyo. Wanatenga wakati ili wawahubirie watu katika vituo vya mabasi, vya garimoshi, sokoni, kwenye bustani, na katika maeneo mengine ya umma. Shahidi anaweza kutumia utambuzi kuanzisha mazungumzo pamoja na mtu kwa kutaja jambo fulani kutoka katika vyombo vya habari, kusema jambo fulani zuri kuhusu watoto wake, au kumwuliza swali kuhusu kazi yake. Kadiri mazungumzo yanavyoendelea, mhubiri anataja wazo la Kimaandiko linaloweza kumchochea ajieleze. Mara nyingi maelezo yake hutokeza mazungumzo zaidi ya Biblia.

17, 18. (a) Unaweza kupataje ujasiri zaidi wa kushiriki katika mahubiri ya hadharani? (b) Kwa nini kuwa na mtazamo kama wa Daudi wa kumsifu Yehova ni jambo lenye thamani unaposhiriki katika huduma?

17 Ikiwa unaona ni vigumu kushiriki mahubiri ya hadharani, usikate tamaa. Eddie, painia katika jiji la New York City, alisita kuanzisha mazungumzo na watu hadharani. Hata hivyo, baada ya muda alipata ujasiri. Ni nini kilichomsaidia? Anasema hivi: “Wakati wa ibada ya familia, mimi na mke wangu hufanya utafiti ili kujua jinsi ya kushughulika na vizuia-mazungumzo na maoni ya watu. Pia, tunauliza mapendekezo kutoka kwa Mashahidi wengine.” Sasa, Eddie anatazamia kwa hamu kuhubiri hadharani.

18 Kadiri unavyoendelea kupata ustadi na ujasiri katika kuhubiri habari njema, maendeleo yako ya kiroho yataonekana wazi. (Soma 1 Timotheo 4:15.) Zaidi ya hilo, utamsifu Baba yetu wa mbinguni kama alivyofanya Daudi, aliyeimba hivi: “Nitambariki Yehova nyakati zote; daima sifa yake itakuwa katika kinywa changu. Nafsi yangu itajisifu katika Yehova; wapole watasikia na kushangilia.” (Zab. 34:1, 2) Na labda kwa sababu ya huduma yako, wapole watajiunga nawe kwa shangwe katika ibada ya kweli.

MTUKUZE MUNGU KWA KUFANYA MAENDELEO YA KIROHO

19. Kwa nini mtumishi mshikamanifu wa Yehova anapaswa kuwa mwenye furaha hata ikiwa anakabili hali ngumu?

19 Daudi aliimba hivi: “Kazi zako zote zitakusifu, Ee Yehova, na washikamanifu wako watakusifu. Wataongea juu ya utukufu wa ufalme wako, nao watasema juu ya nguvu zako, kuwajulisha wana wa binadamu matendo yake yenye nguvu na utukufu wa fahari ya ufalme wake.” (Zab. 145:10-12) Bila shaka, maneno hayo yanaeleza hisia za Mashahidi wote washikamanifu wa Yehova. Lakini namna gani ikiwa ugonjwa au umri unakuzuia kutimiza mengi katika huduma? Sikuzote, kumbuka kwamba unapowahubiria habari njema wale wanaokuuguza na wengine, utumishi wako mtakatifu unamtukuza Mungu wetu mzuri ajabu. Ikiwa umefungwa gerezani kwa sababu ya imani yako, inaelekea unahubiri kuhusu kweli hali zikiruhusu na hilo hufanya moyo wa Yehova ushangilie. (Met. 27:11) Pia, unamtukuza Yehova ikiwa unadumisha ratiba ya mambo ya kiroho licha ya kuwa katika familia iliyogawanyika kidini. (1 Pet. 3:1-4) Hata chini ya hali ngumu, unaweza kumsifu Yehova na kufanya maendeleo ya kiroho.

20, 21. Ikiwa umepewa majukumu mengi zaidi katika tengenezo la Yehova, unawezaje kuwa baraka kwa wengine?

20 Bila shaka Yehova atakubariki ukizidi kufanya maendeleo ya kiroho. Labda kwa kufanya mabadiliko machache katika ratiba au maisha yako, unaweza kushiriki zaidi kueneza kweli za Mungu zenye thamani kwa watu wanaohitaji tumaini. Isitoshe, maendeleo yako ya kiroho na maisha yako ya kujidhabihu yanaweza kuwanufaisha sana waabudu wenzako. Na unapofanya kazi kwa bidii na kwa unyenyekevu kutanikoni, utafurahi kwa kuwa watu wanaompenda Yehova watakupenda, watakuthamini, na kukutegemeza.

21 Iwe tumemtumikia Yehova kwa miaka mingi au miezi michache tu, sote tunaweza kufanya maendeleo katika ibada yake. Lakini Wakristo wakomavu wanaweza kuwasaidiaje wapya wafanye maendeleo ya kiroho? Tutazungumzia jambo hilo katika makala inayofuata.