Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi ya Kufanikiwa Katika Ndoa ya Kikristo

Jinsi ya Kufanikiwa Katika Ndoa ya Kikristo

“Kila mtu mmoja-mmoja kati yenu na ampende hivyo mke wake kama vile anavyojipenda mwenyewe; . . . mke anapaswa kumheshimu sana mume wake.”—EFE. 5:33.

NYIMBO: 87, 3

1. Ingawa ndoa huwa na furaha mwanzoni, wale wanaofunga ndoa wanapaswa kutarajia nini? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

BIBI-ARUSI mrembo anaposimama kando ya bwana-arusi mtanashati siku yao ya arusi, wao huwa na furaha isiyo na kifani. Wakati wa uchumba, upendo wao ulikua sana hivi kwamba sasa wako tayari kuweka nadhiri kuwa watakuwa waaminifu katika ndoa yao. Bila shaka, wanahitaji kufanya mabadiliko kwa kuwa wameunganisha maisha yao na kuanzisha familia mpya. Lakini Neno la Mungu linatoa ushauri wenye hekima kwa wote wanaotaka kufunga ndoa, kwa kuwa Mwanzilishi wa ndoa mwenye upendo anataka zifanikiwe na ziwe na furaha. (Met. 18:22) Hata hivyo, Maandiko yanatuambia wazi kwamba wanadamu wasio wakamilifu wanaofunga ndoa “watakuwa na dhiki katika mwili wao.” (1 Kor. 7:28) Dhiki hiyo inaweza kupunguzwa jinsi gani? Ni nini kitakachofanya ndoa za Wakristo zifanikiwe?

2. Wenzi wa ndoa wanapaswa kuonyeshana aina zipi za upendo?

2 Biblia inakazia umuhimu wa upendo. Upendo mwororo (Kigiriki, phi·liʹa) unahitajika katika ndoa. Upendo wa kimahaba (eʹros) huleta raha, na upendo kuelekea watu wa familia (stor·geʹ) ni muhimu watoto wanapozaliwa. Hata hivyo, upendo unaoongozwa na kanuni (a·gaʹpe) ndio unaofanikisha ndoa. Mtume Paulo aliandika hivi kuhusu upendo huo: “Kila mtu mmoja-mmoja kati yenu na ampende hivyo mke wake kama vile anavyojipenda mwenyewe; kwa upande mwingine, mke anapaswa kumheshimu sana mume wake.”—Efe. 5:33.

WENZI WA NDOA WANA MAJUKUMU GANI HASA?

3. Upendo unapaswa kuwa wenye nguvu kadiri gani katika ndoa?

3 Paulo aliandika hivi: “Enyi waume, endeleeni kuwapenda wake zenu, kama vile Kristo pia alivyolipenda kutaniko na kujitoa mwenyewe kwa ajili yake.” (Efe. 5:25) Kuiga mfano wa Yesu kunamaanisha kwamba wanafunzi wake wanapaswa kupendana kama alivyowapenda. (Soma Yohana 13:34, 35; 15:12, 13.) Hivyo, wenzi wa ndoa Wakristo wanapaswa kupendana sana hivi kwamba kila mmoja wao awe tayari kufa kwa ajili ya mwenzake hali ikilazimu. Lakini huenda ikawa vigumu kufanya hivyo matatizo makubwa ya kutoelewana yanapotokea. Hata hivyo, upendo wa a·gaʹpe “huhimili mambo yote, huamini mambo yote, hutumaini mambo yote, huvumilia mambo yote.” Naam, “upendo haushindwi kamwe.” (1 Kor. 13:7, 8) Wenzi wa ndoa wanaomwogopa Mungu wakikumbuka nadhiri walizotoa kwamba watapendana na kuwa waaminifu katika ndoa, watajitahidi kufuata kanuni bora za Yehova kutatua matatizo yoyote yanayoweza kutokea.

4, 5. (a) Mume ana jukumu gani akiwa kichwa cha familia? (b) Mke anapaswa kuuonaje ukichwa? (c) Wenzi fulani wa ndoa walihitaji kufanya mabadiliko gani?

4 Paulo aliandika hivi kuhusu majukumu ya kila mwenzi wa ndoa: “Wake na wajitiishe kwa waume zao kama kwa Bwana, kwa sababu mume ni kichwa cha mke wake kama vile Kristo pia alivyo kichwa cha kutaniko.” (Efe. 5:22, 23) Mpango huo haumfanyi mke awe duni kuliko mume wake. Badala yake, unamsaidia kutimiza jukumu ambalo Mungu alikuwa nalo kuelekea mke, aliposema hivi: “Si vema huyo mwanamume [Adamu] aendelee kuwa peke yake. Nitamfanyia msaidizi, awe kikamilisho chake.” (Mwa. 2:18) Mume Mkristo anapaswa kutumia ukichwa wake kwa upendo jinsi ambavyo Kristo, “kichwa cha kutaniko,” anaonyesha upendo. Anapofanya hivyo, mke wake anahisi salama na anafurahia kumwonyesha heshima, kumuunga mkono, na kujitiisha.

5 Cathy [1] anakiri kwamba lazima ufanye mabadiliko unapofunga ndoa. Anasema hivi: “Nilipokuwa mseja, nilijitegemea na nilijitimizia mahitaji yangu. Nilihitaji kufanya mabadiliko baada ya kuolewa kwa kuwa nilijifunza kumtegemea mume wangu. Haijawa rahisi sikuzote, lakini kuishi kulingana na kanuni za Yehova kumetusaidia kuwa na uhusiano wa karibu zaidi.” Mume wake anayeitwa Fred, anasema hivi: “Haijawahi kuwa rahisi kwangu kufanya maamuzi. Na katika ndoa, inakuwa vigumu hata zaidi unapohitaji kufanya maamuzi yanayohusu watu wawili. Lakini ninapotafuta mwongozo wa Yehova kwa kusali na kusikiliza kwa makini mapendekezo ya mke wangu, inakuwa rahisi zaidi. Ninahisi kwamba kwa kweli tunakamilishana!”

6. Upendo unakuwaje “kifungo kikamilifu cha muungano” matatizo yanapotokea katika ndoa?

6 Ndoa imara inafanyizwa na wenzi walio tayari kupuuza udhaifu wa mwenzi wao. Wanaendelea “kuvumiliana na kusameheana kwa hiari.” Ni kweli kwamba wenzi wote wawili watakosea. Hata hivyo, hilo linapotokea, kuna nafasi za kujifunza kutokana na makosa yao, kusameheana, na kuruhusu upendo uwaongoze katika kila jambo, kwa maana huo ni “kifungo kikamilifu cha muungano.” (Kol. 3:13, 14) Isitoshe, “upendo ni wenye ustahimilivu na wenye fadhili. . . . Hauweki hesabu ya ubaya.” (1 Kor. 13:4, 5) Kutoelewana kunapaswa kusuluhishwa haraka iwezekanavyo. Kwa hiyo, wenzi wa ndoa Wakristo wanapaswa kujaribu kusuluhisha tatizo lolote la kutoelewana kabla ya jua kutua. (Efe. 4:26, 27) Unahitaji unyenyekevu na ujasiri ili useme kwa unyoofu, “Naomba msamaha kwa kukuumiza,” lakini hilo husaidia sana kusuluhisha matatizo na kuimarisha uhusiano wa wenzi wa ndoa.

UHITAJI WA PEKEE WA WORORO

7, 8. (a) Biblia inatoa ushauri gani kuhusu mahusiano ya kingono katika ndoa? (b) Kwa nini wenzi wa ndoa wanapaswa kutendeana kwa wororo?

7 Biblia inatoa ushauri mzuri unaoweza kuwasaidia wenzi wa ndoa wawe na maoni yaliyosawazika kuhusu haki ya ndoa. (Soma 1 Wakorintho 7:3-5.) Ni muhimu kufikiria kwa upendo hisia na mahitaji ya mwenzi wetu wa ndoa. Mke asipotendewa kwa wororo, huenda ikawa vigumu kwake kufurahia mahusiano hayo. Waume wanaambiwa wawatendee wake zao “kulingana na ujuzi.” (1 Pet. 3:7) Mume au mke hapaswi kumlazimisha mwenzi wake kuwa na mahusiano ya kingono, bali kila mmoja wao anapaswa kutoa haki ya ndoa kwa kupenda. Mara nyingi mwanamume anaweza kuwa tayari haraka zaidi kwa ajili ya mahusiano hayo kuliko mwanamke. Hata hivyo, wote wanapaswa kuwa tayari kihisia.

8 Ingawa Biblia haitoi sheria kuhusu mambo ambayo wenzi wa ndoa wanaweza kufanya ili kuamsha nyege kabla ya kufanya ngono, wala haisemi yanaweza kufanywa kwa kiwango gani, inataja maonyesho ya mapenzi. (Wim. 1:2; 2:6) Wenzi wa ndoa Wakristo wanapaswa kutendeana kwa wororo.

9. Kwa nini kutamani kufanya ngono na mtu asiye mwenzi wetu wa ndoa ni jambo lisilokubalika?

9 Wenzi wa ndoa wakimpenda sana Mungu na jirani hawataruhusu mtu au kitu chochote kiharibu ndoa yao. Baadhi ya ndoa zimepata mkazo au kuharibika kwa sababu ya mwenzi mmoja kuwa na uraibu wa ponografia. Mwelekeo wa kuvutiwa na mazoea hayo au kutamani kuwa na mahusiano mengine ya kingono nje ya ndoa unapaswa kupingwa kwa uthabiti. Hata kuwa na mwelekeo wa kumchezea kimapenzi mtu ambaye si mwenzi wetu wa ndoa, ni jambo linaloonyesha kwamba hatuna upendo na hivyo linapaswa kuepukwa. Kukumbuka kwamba Mungu anajua mawazo na matendo yetu yote kutaimarisha tamaa yetu ya kumpendeza na kuendelea kuwa safi kiadili.​—Soma Mathayo 5:27, 28; Waebrania 4:13.

MATATIZO YANAPOTOKEA KATIKA NDOA

10, 11. (a) Watu wanaotalikiana ni wengi kadiri gani? (b) Biblia inasema nini kuhusu kutengana? (c) Ni nini kitakachowasaidia wenzi wa ndoa wasichukue hatua ya kutengana haraka?

10 Kunapokuwa na matatizo makubwa na yanayoendelea katika ndoa, mwenzi mmoja au wote wawili wanaweza kufikiria kutengana au kutalikiana. Katika nchi fulani, zaidi ya asilimia 50 ya watu wanaofunga ndoa hutalikiana. Hilo si jambo la kawaida katika kutaniko la Kikristo, lakini ongezeko la matatizo katika ndoa za watu wa Mungu ni jambo linalohangaisha.

11 Biblia inatoa maagizo haya: “Mke hapaswi kuondoka kwa mume wake; lakini kwa kweli akiondoka, na akae mseja kama sivyo apatane tena na mume wake; na mume hapaswi kumwacha mke wake.” (1 Kor. 7:10, 11) Kutengana na mwenzi wa ndoa hakupaswi kuonwa kuwa jambo dogo. Ingawa kutengana kunaweza kuonwa kuwa suluhisho matatizo makubwa yanapotokea, mara nyingi hilo hutokeza matatizo mengi zaidi. Baada ya kurudia kile ambacho Mungu alisema kuhusu mwanamume kumwacha baba na mama yake na kushikamana na mke wake, Yesu alisema hivi: “Kile ambacho Mungu ameunganisha mtu yeyote asikitenganishe.” (Mt. 19:3-6; Mwa. 2:24) Hilo linamaanisha pia kwamba hata mume au mke hapaswi ‘kutenganisha kile ambacho Mungu ameunganisha.’ Yehova anaiona ndoa kuwa kifungo kinachodumu hadi mwenzi mmoja anapokufa. (1 Kor. 7:39) Kuzingatia kwamba sote tutatoa hesabu mbele za Mungu kunapaswa kuwachochea wenzi wa ndoa wajitahidi sana kusuluhisha matatizo haraka ili yasiwe makubwa zaidi.

12. Ni nini kinachoweza kumfanya mwenzi wa ndoa afikirie kutengana na mwenzi wake?

12 Matarajio yasiyo halisi yanaweza kuwa chanzo cha matatizo katika ndoa. Mawazo kuhusu ndoa yenye furaha yasipotimia, huenda mtu akakosa kuridhika, akahisi kuwa amedanganywa, au hata akakata tamaa. Tofauti za kihisia na malezi zinaweza kusababisha matatizo, au kutoelewana kunaweza kutokea kuhusiana na pesa, wakwe, na jinsi ya kulea watoto. Hata hivyo, inavutia kuona kwamba wenzi wengi Wakristo husuluhisha kwa umoja matatizo kama hayo kwa sababu wanamruhusu Mungu awaongoze.

13. Ni sababu gani halali za kutengana?

13 Nyakati nyingine huenda ikawa sawa kutengana. Watu fulani wameona kuwa hali zifuatazo zinawaruhusu kutengana: mwenzi mmoja kukataa kimakusudi kutegemeza familia, kuwaumiza kimwili kupita kiasi, na kuhatarisha kabisa hali yao ya kiroho. Wenzi wa ndoa Wakristo walio na matatizo makubwa wanapaswa kuomba msaada kutoka kwa wazee. Ndugu hao wenye uzoefu wanaweza kuwasaidia wenzi wa ndoa wafuate ushauri wa Neno la Mungu. Tunaposuluhisha matatizo katika ndoa, tunapaswa pia kumwomba Yehova atupe roho yake na atusaidie kutumia kanuni za Biblia na vilevile kuonyesha sifa za tunda la roho.​—Gal. 5:22, 23. [2]

14. Biblia inawaambia nini Wakristo waliofunga ndoa na wenzi ambao si waabudu wa Yehova?

14 Katika visa fulani, huenda ikawa Mkristo amefunga ndoa na mtu ambaye bado hajawa mtumishi wa Yehova. Katika hali kama hizo, Biblia inatoa sababu nzuri za kuwafanya waendelee kuwa pamoja. (Soma 1 Wakorintho 7:12-14.) Iwe mwenzi ambaye si Shahidi anatambua au la, yeye ‘ametakaswa’ kwa sababu ya kufunga ndoa na Shahidi wa Yehova. Kwa hiyo, watoto wao wanaonwa kuwa “watakatifu,” na hivyo wana ulinzi wa Mungu. Paulo anasema hivi: “Mke, unajuaje kama utamwokoa mume wako? Au, wewe mume, unajuaje kama utamwokoa mke wako?” (1 Kor. 7:16) Karibu kila kutaniko la Mashahidi wa Yehova lina wenzi Wakristo ambao wamechangia ‘kuwaokoa’ wenzi wao.

15, 16. (a) Biblia inatoa ushauri gani kwa wake Wakristo waliofunga ndoa na waume ambao si watumishi wa Mungu? (b) Mwenzi Mkristo anaweza kufanya nini “yule asiyeamini akiondoka”?

15 Mtume Petro anawashauri wake Wakristo wajitiishe kwa waume zao, “ili, ikiwa wowote si watiifu kwa lile neno, wavutwe bila neno kupitia mwenendo wa wake zao, kwa sababu wamekwisha kushuhudia kwa macho mwenendo wenu ulio safi kiadili pamoja na heshima kubwa.” Kwa mwenendo wake unaoonyesha “roho ya utulivu na ya upole, ambayo ni ya thamani kubwa machoni pa Mungu,” mke anaweza kutimiza mengi zaidi katika kumvuta mume wake kwenye ibada ya kweli kuliko kuzungumza sana kuhusu imani yake ya Kikristo.​—1 Pet. 3:1-4.

16 Namna gani ikiwa mwenzi ambaye si Shahidi anaamua kutengana na mwenzi wake? Biblia inasema hivi: “Yule asiyeamini akiondoka, acha aondoke; ndugu au dada hayumo katika utumwa chini ya hali za namna hiyo, lakini Mungu amewaita ninyi kwenye amani.” (1 Kor. 7:15) Hilo halimaanishi kwamba mwenzi Mkristo yuko huru Kimaandiko kufunga ndoa tena, hata hivyo, hana wajibu wa kumlazimisha mwenzi wake asiondoke. Huenda kutengana kukaleta amani ya kadiri. Mwenzi Mkristo anaweza kutazamia kwamba mwenzi wake atarudi akiwa tayari kushirikiana naye katika kudumisha ndoa yao na mwishowe kuwa Shahidi wa Yehova.

NDOA NA MAMBO TUNAYOPASWA KUTANGULIZA

Kutanguliza mambo ya kiroho kunaweza kuongeza furaha katika ndoa yako (Tazama fungu la 17)

17. Wenzi wa ndoa Wakristo wanapaswa kutanguliza nini?

17 Kwa kuwa tunaishi mwishoni mwa “siku za mwisho,” tunakabili “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Tim. 3:1-5) Hata hivyo, kudumisha hali nzuri ya kiroho kutatusaidia kushinda uvutano usiofaa wa ulimwengu huu. Paulo aliandika hivi: “Wakati uliobaki umepungua. Tangu sasa wale walio na wake na wawe kana kwamba hawana, . . . na wale wanaoutumia ulimwengu wawe kama wale wasioutumia kwa ukamili.” (1 Kor. 7:29-31) Paulo hakuwa akiwaambia wenzi wa ndoa wapuuze majukumu yao ya ndoa. Hata hivyo, kwa sababu wakati uliobaki umepungua, wangehitaji kutanguliza mambo ya kiroho.​—Mt. 6:33.

18. Kwa nini inawezekana kwa Wakristo kufanya ndoa zao zifanikiwe na ziwe zenye furaha?

18 Ingawa tunaishi katika kipindi kigumu sana na tunaona ndoa nyingi zikivunjika, tunaweza kufanya ndoa zetu zifanikiwe na ziwe zenye furaha. Kwa kweli, Wakristo waliofunga ndoa wakishikamana na watu wa Yehova, wakifuata ushauri wa Kimaandiko, na kukubali mwongozo wa roho takatifu ya Yehova, wanaweza kudumisha “kile ambacho Mungu ameunganisha.”—Marko 10:9.

^ [1] (fungu la 5) Majina yamebadilishwa.

^ [2] (fungu la 13) Tazama kitabu “Jitunzeni Katika Upendo wa Mungu,” nyongeza yenye kichwa, “Maoni ya Biblia Kuhusu Talaka na Kutengana.”