Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HABARI KUU | JE, KWELI BIBLIA NI KITABU CHA MUNGU?

Biblia—Ni Sahihi Katika Nyanja Zote

Biblia—Ni Sahihi Katika Nyanja Zote

Sahihi Kisayansi

INGAWA Biblia si kitabu cha sayansi, inapoeleza kuhusu ulimwengu wetu inasema mambo yaliyo sahihi. Fikiria mifano kadhaa katika nyanja ya metorolojia (elimu ya upimaji wa hali ya hewa) na ya chembe za urithi.

METOROLOJIA—JINSI MVUA INAVYOTOKEA

METOROLOJIA

Biblia inasema: “Kwa maana [Mungu] huyateka matone ya maji; yanajichuja kama mvua yawe ukungu wake, hivi kwamba mawingu yanadondoka.”—Ayubu 36:27, 28.

Katika andiko hilo, Biblia inataja hatua tatu muhimu za mzunguko wa maji. Mungu ambaye ni Chanzo cha jua, “huyateka matone ya maji” kwa (1) uvukizaji. Kisha, kwa njia ya (2) mgandamizo, maji yaliyotekwa huwa mawingu, na baadaye hushuka yakiwa (3) mvua au kwa namna nyingine. Hata sasa, wataalamu wa upimaji wa hali ya hewa hawaelewi kikamili habari zote kuhusu jinsi mvua inavyotokea. Kwa kupendeza, Biblia inauliza hivi: “Ni nani anayeweza kuelewa tabaka za mawingu?” (Ayubu 36:29) Hata hivyo, Muumba anaelewa mzunguko wa mvua naye alimwongoza mwanadamu aandike habari hizo za kweli katika Biblia. Alifanya hivyo hata kabla ya wanadamu kugundua kanuni za msingi za sayansi kuhusu mzunguko wa mvua.

CHEMBE ZA URITHI—UKUZI WA MTOTO KATIKA TUMBO LA UZAZI

CHEMBE ZA URITHI

Mfalme Daudi ambaye ni mwandikaji wa Biblia, alimwambia Mungu hivi: “Macho yako yalikiona kiini-tete changu, na katika kitabu chako sehemu zake zote zilikuwa zimeandikwa.” (Zaburi 139:16) Kwa kutumia lugha ya ushairi, Daudi alizungumzia ukuaji unaotukia tumboni kwa kufuata maagizo yaliyoandikwa katika “kitabu,” au mpangilio maalumu. Kwa kushangaza, jambo hilo liliandikwa miaka 3,000 hivi iliyopita!

Hata hivyo, mtaalamu wa mimea wa Austria, Gregor Mendel aligundua kanuni za msingi za mfumo wa chembe za urithi katika miaka ya 1800. Na mpaka kufikia mwezi Aprili 2003, watafiti hawakuwa wameelewa mpangilio kamili wa habari zilizo katika DNA ambazo zinahitajika ili kutokeza mwili wa mwanadamu. Wanasayansi wamefafanua mkusanyo wa habari zilizo kwenye chembe za urithi kuwa kama kamusi iliyojaa maneno yenye herufi za alfabeti. Maneno hayo hutokeza maagizo ya chembe za urithi. Kwa kutegemea maagizo hayo, sehemu za kiini tete, kama vile ubongo, moyo, mapafu, na mbavu, hukua kwa utaratibu na kwa muda muafaka. Kwa kufaa, wanasayansi wamefafanua mkusanyo wa habari zilizo katika DNA kuwa kama “kitabu cha uhai.” Ni nini kilichomwezesha Daudi, mwandikaji wa Biblia, kueleza jambo hilo kwa usahihi? Kwa unyenyekevu alikiri hivi: “Roho ya Yehova ndiyo iliyosema kupitia mimi, na neno lake lilikuwa kwenye ulimi wangu.” *2 Samweli 23:2.

Inatabiri Kuhusu Wakati Ujao Kwa Usahihi

NI VIGUMU sana au huenda haiwezekani kabisa kujua ni lini, jinsi gani, na kwa kiwango gani falme na majiji yatainuka au kuanguka. Lakini, Biblia ilitabiri na kueleza habari za kina kuhusu kuharibiwa kwa tawala na majiji fulani yenye nguvu. Chunguza mifano miwili.

KUANGUKA NA KUACHWA UKIWA KWA BABILONI

Kwa karne nyingi, Babiloni la kale lilikuwa kitovu cha milki yenye nguvu na ushawishi katika nchi za Asia ya magharibi. Wakati fulani lilikuwa jiji kubwa kuliko majiji yote ulimwenguni. Hata hivyo, miaka 200 hivi mapema, Mungu alimwongoza Isaya, mwandikaji wa Biblia, kutabiri mtu atakayelishinda jiji la Babiloni, yaani, Koreshi, na kwamba halitakaliwa milele. (Isaya 13:17-20; 44:27, 28; 45:1, 2) Je, ilitukia kama ilivyotabiriwa?

HISTORIA

Katika usiku mmoja, Oktoba 539 K.W.K., Koreshi Mkuu alilishinda Babiloni. Baada ya muda, mifereji ya maji ambayo wakati fulani ilizunguka eneo lenye rutuba iliziba kutokana na kutodumishwa. Kufikia mwaka wa 200 W.K., jiji hilo lilikuwa limeachwa ukiwa. Leo, Babiloni la kale limebaki magofu. Sawa na vile ambavyo Biblia ilitabiri, Babiloni limekuwa “mahame yenye ukiwa.”—Yeremia 50:13.

Mwandikaji huyo wa Biblia alipataje mapema habari hizo sahihi za kihistoria? Biblia inafunua jinsi ilivyokuwa kwa kusema: “Tangazo juu ya Babiloni ambalo Isaya mwana wa Amozi aliona katika maono.”—Isaya 13:1.

NINAWI—“ENEO LISILO NA MAJI KAMA NYIKA”

Ninawi, mji mkuu wa Milki ya Ashuru, ulionwa kuwa moja kati ya maajabu ya uhandisi. Jiji hilo lilijivunia barabara zake pana, bustani za umma, mahekalu, na majumba makubwa ya kifahari. Hata hivyo, nabii Sefania alitabiri kwamba jiji hilo mashuhuri lingekuja kuwa “ukiwa, eneo lisilo na maji kama nyika.”—Sefania 2:13-15.

Ninawi liliharibiwa kabisa na majeshi yaliyoungana ya Babiloni na Wamedi katika karne ya saba K.W.K. Kulingana na rejeo fulani, jiji hilo lililoharibiwa “lilisahaulika kwa miaka 2500.” Kwa kipindi fulani, watu walitilia shaka ikiwa kuliwahi kuwa na jiji la Ninawi! Ilikuwa katikati ya karne ya 19 wanaakiolojia walipochimbua na kupata mabaki ya jiji la Ninawi. Leo, magofu hayo yamechakaa sana na kuharibiwa vibaya na watu, hivi kwamba shirika la Global Heritage Fund limeonya hivi: “Huenda mabaki ya jiji la Ninawi yakafukiwa tena na hivyo kutoweka milele.”

Sefania alijuaje habari hizo mapema? Yeye alikiri kwamba ‘neno la Yehova lilimjia.’—Sefania 1:1.

Biblia Inajibu Maswali Muhimu Maishani

BIBLIA hutoa majibu yenye kuridhisha ya maswali muhimu maishani. Fikiria mifano kadhaa.

KWA NINI KUNA UOVU NA MATESO MENGI DUNIANI?

Maandiko mengi yanaeleza kwa kina sababu za kuwepo kwa uovu na kuteseka. Biblia inaeleza hivi:

  1. “Mwanadamu amemtawala mwanadamu kwa kumuumiza.”Mhubiri 8:9.

    Utawala wa wanadamu wasio na uwezo na ambao ni wafisadi umeiletea jamii ya wanadamu mateso mengi sana.

  2. “Wakati na tukio lisilotazamiwa huwapata wote.”Mhubiri 9:11.

    Matukio yasiyotazamiwa kama vile ugonjwa mbaya, aksidenti, au misiba ya asili, yanaweza kumkumba yeyote, mahali popote, na wakati wowote.

  3. “Kupitia mtu mmoja dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi.” Waroma 5:12.

    Hali ya kutokamilika kwa mwanadamu na kifo havikuwepo mwanzoni, mwanamume na mwanamke wa kwanza walipoumbwa. Dhambi “iliingia katika ulimwengu” wanadamu walipomwasi Muumba wao.

Biblia haielezi tu sababu inayofanya wanadamu wateseke. Inaahidi kwamba Mungu ataondoa uovu na “atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena.”—Ufunuo 21:3, 4.

NI NINI HUTUPATA TUNAPOKUFA?

Biblia inafafanua kifo kuwa hali ya kutotenda na kutokuwa na mawazo yoyote. Mhubiri 9:5 inasema hivi: “Kwa maana walio hai wanajua kwamba watakufa; lakini wafu, hawajui lolote kamwe.” Mtu anapokufa, “mawazo yake hupotea.” (Zaburi 146:4) Hivyo, utendaji wote wa ubongo, kutia ndani uwezo wa kuhisi, unakoma kufanya kazi tunapokufa. Kwa hiyo, hatuwezi kutenda, kuhisi, au kufikiri baada ya kufa.

Hata hivyo, Biblia inaeleza mengi zaidi ya kufafanua tu hali ya mtu aliyekufa. Inatoa tumaini zuri kwamba kupitia ufufuo, watu wataamshwa kutoka kwenye usingizi mzito wa kifo.—Hosea 13:14; Yohana 11:11-14.

NI NINI KUSUDI LA UHAI?

Kulingana na Biblia, Yehova Mungu alimuumba mwanamume na mwanamke. (Mwanzo 1:27) Mwanamume wa kwanza, Adamu, anatajwa kuwa “mwana wa Mungu.” (Luka 3:38) Mwanadamu aliumbwa kwa kusudi hususa, ambalo ni kusitawisha urafiki na Baba yake wa mbinguni na kuwa na maisha yenye furaha na yenye kuridhisha milele hapa duniani. Kwa maana hiyo, wanadamu wote wameumbwa wakiwa na uhitaji wa kiroho, hivyo, ni jambo la asili kutamani kujifunza kumhusu Mungu. Ndio sababu Biblia inasema hivi: “Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.”—Mathayo 5:3.

Kwa kuongezea, Biblia inasema hivi: “Wenye furaha ni wale wanaolisikia neno la Mungu na kulishika!” (Luka 11:28) Biblia haitusaidii tu kujifunza kumhusu Mungu, bali pia inatusaidia kuishi maisha yenye furaha zaidi na kutupatia tumaini la wakati ujao.

Uhusiano Wako na Mungu—Mtungaji wa Biblia

BAADA ya kuchunguza uthibitisho, mamilioni ya watu duniani kote wamefikia mkataa wa kwamba Biblia si kitabu cha kale tu. Wanaamini kwamba Biblia ni Neno la Mungu lililoongozwa na roho yake, njia ya Mungu ya kuwasiliana na wanadamu, kutia ndani wewe! Ina mwaliko wa Mungu kwako kwamba ujifunze kumhusu na uwe rafiki yake. Biblia inasema hivi: “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.”—Yakobo 4:8.

Kuchimba katika Biblia kutakusaidia kujua mambo yenye kustaajabisha. Ni mambo gani hayo? Kama vile kusoma kitabu hukusaidia kujua mawazo ya mtunzi wake, kusoma Biblia kunafunua mawazo na hisia za Mtungaji wake, yaani, Mungu. Fikiria faida ya jambo hilo kwako. Unaweza kujua hisia na mawazo ya Muumba wako! Kwa kuongezea, Biblia inafunua mambo yafuatayo:

Je, ungependa kujifunza mengi zaidi? Mashahidi wa Yehova watafurahi kukusaidia. Wanaweza kupanga kujifunza nawe Biblia bila malipo. Hilo litakusaidia kumkaribia zaidi Mtungaji wa Biblia, Yehova Mungu.

Makala hii imechunguza baadhi ya mambo yanayothibitisha kwamba Biblia ni kitabu kilichoongozwa na roho ya Mungu. Ili kupata habari zaidi, soma sura ya 2 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova, na kinachopatikana katika tovuti ya www.jw.org/sw

Pia unaweza kutazama video Ni Nani Aliyeitunga Biblia? inayopatikana kwenye www.jw.org/sw

Tafuta kwenye MACHAPISHO > VIDEO

^ fu. 10 Katika Biblia, Mungu anatajwa kwa jina lake binafsi, yaani, Yehova.—Zaburi 83:18.