Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sura ya 27

“Wema Wake, Jinsi Ulivyo Mwingi!”

“Wema Wake, Jinsi Ulivyo Mwingi!”

1, 2. Wema wa Mungu ni mwingi kadiri gani, na Biblia inakaziaje sifa hiyo?

KATIKA nuru nyangavu ya machweo, marafiki kadhaa wanafurahia kula chakula pamoja bustanini, wanacheka na kuzungumza huku wakifurahia mandhari. Mbali sana, mkulima anatazama mashamba yake na kutabasamu kwa sababu mawingu meusi yametanda angani na mvua imeanza kunyesha. Kwingineko, mume na mke wanafurahi sana kumwona mtoto wao mchanga akiyumba-yumba anapojaribu kutembea.

2 Iwe wanajua au hawajui, watu hao wote wananufaika na jambo moja—wema wa Yehova Mungu. Wanadini wengi hurudia-rudia maneno haya, “Mungu ni mwema.” Biblia inakazia sifa hiyo hata zaidi. Inasema: “Wema wake, jinsi ulivyo mwingi!” (Zekaria 9:17) Lakini yaonekana kwamba ni watu wachache sana leo wanaojua maana ya maneno hayo. Wema wa Yehova Mungu unahusisha nini, na sifa hiyo inamnufaishaje kila mmoja wetu?

Sifa Muhimu ya Upendo wa Mungu

3, 4. Wema ni nini, na kwa nini inaweza kusemwa kwamba wema wa Yehova ni wonyesho wa upendo wake?

3 Katika lugha nyingi leo, neno “wema” halina maana maalumu. Hata hivyo, Biblia inaonyesha kwamba wema ni sifa ya pekee sana. Sifa hiyo inamaanisha hasa wema wa kiadili. Kwa hivyo, tunaweza kusema kwamba Yehova ni mwema kabisa. Sifa zake zote, kutia ndani nguvu zake, haki yake, na hekima yake ni njema kabisa. Ingawa hivyo, wema unaweza kutajwa kwa kufaa kuwa wonyesho wa upendo wa Yehova. Kwa nini?

4 Wema ni sifa inayoonyeshwa kwa matendo. Mtume Paulo alisema kwamba mtu mwema huwavutia wengine zaidi kuliko mtu mwadilifu. (Waroma 5:7) Mtu mwadilifu hutii matakwa ya sheria kwa uaminifu, lakini mtu mwema hufanya mengi zaidi. Anachukua hatua na kujitahidi sana kuwasaidia wengine. Kama tutakavyoona, hapana shaka kwamba Yehova ni mwema katika njia hiyo. Kwa wazi, upendo wa Yehova usio na mipaka ndio chanzo cha wema wake.

5-7. Kwa nini Yesu alikataa kuitwa “Mwalimu Mwema,” na hivyo alithibitisha ukweli gani hakika?

5 Yehova ni mwema kwa njia isiyo na kifani. Muda mfupi kabla ya Yesu kufa, mtu fulani alimfikia ili kumwuliza swali na akamwita “Mwalimu Mwema.” Yesu akamjibu: “Kwa nini waniita mwema? Hakuna mtu aliye mwema, ila mmoja, Mungu.” (Marko 10:17, 18) Huenda ukashangazwa na jibu hilo. Mbona Yesu alimkosoa mtu huyo? Je, Yesu hakuwa “Mwalimu Mwema”?

6 Ni wazi kwamba mtu huyo alikuwa akimrairai Yesu kwa kutumia maneno “Mwalimu Mwema” kama cheo. Kwa unyenyekevu, Yesu alielekeza utukufu huo kwa Baba yake wa mbinguni, ambaye ni mwema kwa njia isiyo na kifani. (Mithali 11:2) Lakini Yesu alikuwa akithibitisha pia ukweli huu hakika: Ni Yehova peke yake anayeamua yaliyo mema. Akiwa Mwenye Enzi Kuu, ni yeye peke yake aliye na haki ya kuamua mambo mema na mabaya. Adamu na Hawa walijaribu kujitwalia haki hiyo walipoasi na kula tunda la mti wa ujuzi wa mema na mabaya. Lakini Yesu kwa unyenyekevu anamwachia Baba yake haki ya kuamua mema na mabaya.

7 Isitoshe, Yesu alijua kwamba Yehova ndiye chanzo cha vitu vyote vyema. Yeye ni Mtoaji wa “kila zawadi njema na kila upaji mkamilifu.” (Yakobo 1:17) Hebu tuone jinsi ambavyo ukarimu wa Yehova unathibitisha wema wake.

Mambo Yanayothibitisha Wema Mwingi wa Yehova

8. Yehova amewaonyeshaje wanadamu wote wema?

8 Kila mtu aliyepata kuishi amenufaishwa na wema wa Yehova. Zaburi 145:9 yasema: “BWANA ni mwema kwa watu wote.” (Italiki ni zetu.) Ni mifano ipi inayoonyesha kwamba wema wake unamnufaisha kila mtu? Biblia inasema hivi: “Hakujiacha mwenyewe bila ushahidi kwa kuwa alitenda mema, akiwapa nyinyi mvua kutoka mbinguni na majira yenye kuzaa matunda, akijaza mioyo yenu kikamili kwa chakula na uchangamfu.” (Matendo 14:17) Je, umewahi kufurahia chakula kitamu? Hakungekuwa na chakula chochote kama Yehova hangekuwa mwema na kubuni mzunguko wa maji safi na “majira yenye kuzaa matunda.” Yehova amewatendea watu wote wema, hata wale wasiompenda. Yesu alisema hivi: “Hufanya jua lake lichomoze juu ya watu waovu na wema na kufanya mvua inyeshe juu ya watu waadilifu na wasio waadilifu.”—Mathayo 5:45.

Yehova ‘anawapa nyinyi mvua kutoka mbinguni na majira yenye kuzaa matunda’

9. Tofaa linaonyeshaje wema wa Yehova?

9 Wengi hupuuza ukarimu mkubwa ambao wanadamu wanaonyeshwa kupitia jua, mvua, na majira ya matunda. Kwa mfano, fikiria tofaa, tunda linalokuzwa sana katika maeneo yenye halijoto ya wastani duniani. Ni tunda tamu sana linalovutia, lina madini muhimu na maji tosha yanayoburudisha. Je, wajua kwamba ulimwenguni pote kuna aina 7,500 hivi za matofaa yenye rangi mbalimbali kama vile nyekundu, rangi ya dhahabu, manjano, na rangi ya kijani-kibichi, na yana ukubwa mbalimbali, mengine ni makubwa kidogo kuliko cheri na mengine ni kama balungi? Tofaa lina mbegu ndogo. Lakini mojawapo ya miti maridadi zaidi hukua kutoka kwa mbegu hiyo ndogo. (Wimbo Ulio Bora 2:3, BHN) Kila mwaka mtofaa huchanua maua mengi yenye kuvutia na kuzaa matunda. Kila mwaka, kwa muda wa miaka 75 hivi, mtofaa wa wastani huzaa katoni 20 za matunda, kila katoni ikiwa na uzito wa kilogramu 19!

Mti unaoweza kulisha na kuwafurahisha watu kwa miaka mingi sana hukua kutoka kwa mbegu hii ndogo

10, 11. Hisi zetu zinathibitishaje wema wa Mungu?

10 Kwa wema wake usio na kikomo, Yehova ametupatia mwili ambao ‘umeumbwa kwa jinsi ya ajabu.’ Tuna hisi ambazo zinakusudiwa kutusaidia kutambua kazi zake na kuzifurahia. (Zaburi 139:14) Hebu fikiria tena mambo yaliyotajwa mwanzoni mwa sura hii. Tunafurahia kuona mambo gani? Uso mwangavu wa mtoto anayeangua kicheko. Mvua kubwa inaponyesha. Machweo ya rangi nyekundu, ya dhahabu, na ya urujuani. Jicho la mwanadamu linaweza kuona zaidi ya rangi 300,000! Na tunaweza kusikia na kutofautisha sauti mbalimbali zinazovutia, kama vile mvumo wa upepo katika miti, na kicheko kichangamfu cha mtoto mchanga. Ni nini kinachotuwezesha kufurahia mambo hayo? Biblia inasema: “Sikio lisikialo, na jicho lionalo, BWANA ndiye aliyeyafanya yote mawili.” (Mithali 20:12) Lakini hizo ni hisi mbili tu.

11 Hisi yetu ya kunusa huthibitisha pia wema wa Yehova. Pua ya mwanadamu inaweza kutofautisha harufu zipatazo 10,000. Baadhi ya harufu hizo ni: harufu nzuri ya chakula upendacho kinapopikwa, harufu nzuri ya maua, ya majani makavu, harufu ya moshi. Na hisi yako ya kugusa inakuwezesha kuhisi upepo unapovuma kwa wanana usoni mwako, kupata utulivu unapokumbatiwa na mpendwa wako, kuhisi tunda lenye ganda laini mkononi mwako. Unapoliuma, hisi yako ya kuonja inaanza kufanya kazi. Unafurahia ladha mbalimbali vionjio vyako vinapoonja kemikali tata za tunda hilo. Naam, tuna kila sababu ya kutangaza hivi kumhusu Yehova: “Jinsi gani ulivyo mwingi wema wako, uliowawekea wale wanaokucha!” (Zaburi 31:19, BHN) Lakini Yehova ‘amewawekeaje’ wema wale ambao wanamhofu?

Wema Unaoleta Faida za Milele

12. Ni maandalizi gani kutoka kwa Yehova yaliyo muhimu zaidi, na kwa nini?

12 Yesu alisema: “Imeandikwa, ‘Binadamu lazima aishi, si kwa mkate pekee, bali kwa kila tamko linalokuja kupitia kinywa cha Yehova.’” (Mathayo 4:4) Kwa kweli, maandalizi ya kiroho kutoka kwa Yehova yanaweza kutufaidi kuliko maandalizi ya kimwili, kwa kuwa yatatuwezesha kuishi milele. Katika Sura ya 8 ya kitabu hiki, tuliona kwamba katika siku hizi za mwisho, Yehova ametumia uwezo wake wa kurudisha hali mpya kuleta paradiso ya kiroho. Jambo muhimu zaidi ni kwamba paradiso hiyo ina chakula tele cha kiroho.

13, 14. (a) Nabii Ezekieli aliona nini katika ono, nalo linatuhusuje leo? (b) Yehova amewapa watumishi wake waaminifu maandalizi gani ya kiroho kwa ajili ya uhai?

13 Katika mojawapo ya unabii mbalimbali muhimu wa urudisho, nabii Ezekieli alipata ono la hekalu jipya lenye utukufu. Kijito kilichotiririka kutoka hekaluni humo, kilizidi kupanuka na kina chake kuongezeka hatua kwa hatua mpaka kikawa “mto.” Mto huo ulikuwa na matokeo mazuri popote ulipopitia. Miti mingi sana ambayo ilitokeza chakula na maponyo ilisitawi kwenye kingo za mto huo. Na mto huo hata ulileta uhai na ufanisi katika Bahari ya Chumvi isiyo na uhai! (Ezekieli 47:1-12) Lakini ono hilo lilimaanisha nini?

14 Ono hilo lilimaanisha kwamba Yehova angerudisha mpango wake wa ibada safi ambao unawakilishwa na hekalu aliloona Ezekieli. Maandalizi ya Mungu kwa ajili ya uhai yangewamiminikia watu wake kwa wingi zaidi kama ule mto ulio katika ono. Tangu kurudishwa kwa ibada safi mwaka wa 1919, Yehova amewabariki watu wake kwa kuwapa maandalizi ya uhai. Jinsi gani? Biblia, vichapo vya Biblia, mikutano, na makusanyiko yamewasaidia mamilioni ya watu kupata kweli muhimu sana. Kupitia njia hizo, Yehova amewafundisha watu kuhusu mpango muhimu zaidi kwa ajili ya uhai—dhabihu ya fidia ya Kristo. Dhabihu hiyo huwawezesha wote wanaompenda na kumhofu Yehova kikweli wawe na uhusiano mzuri naye na kuwa na tumaini la kuishi milele. * Kwa hiyo, watu wa Yehova wamekuwa wakifurahia karamu ya kiroho katika siku hizi za mwisho, huku ulimwengu ukiteseka kwa sababu ya njaa ya kiroho.—Isaya 65:13.

15. Wema wa Yehova utawanufaishaje wanadamu waaminifu wakati wa Utawala wa Kristo wa miaka elfu moja?

15 Lakini mto alioona Ezekieli hautakoma kutiririka huu mfumo wa kale wa mambo utakapoharibiwa. Kinyume chake, utaendelea kutiririka kwa wingi zaidi wakati wa Utawala wa Kristo wa miaka elfu moja. Wakati huo, kupitia Ufalme wa Kimesiya, Yehova atatumia manufaa kamili ya dhabihu ya Yesu ili wanadamu waaminifu wafikie ukamilifu hatua kwa hatua. Ndipo tutakaposhangilia sana kwa sababu ya wema wa Yehova!

Sifa Nyingine za Wema wa Yehova

16. Biblia inaonyeshaje kwamba wema wa Yehova unatia ndani sifa nyingine? Taja baadhi ya sifa hizo.

16 Wema wa Yehova watia ndani sifa nyingine mbali na ukarimu. Mungu alimwambia Musa hivi: “Nitapitisha wema wangu wote mbele yako, nami nitalitangaza jina la BWANA mbele yako.” Simulizi hilo lasema kwamba baadaye ‘BWANA alipita mbele yake, akatangaza, BWANA, BWANA, Mungu mwingi wa huruma, mwenye fadhili, si mwepesi wa hasira, mwingi wa rehema na kweli.’ (Kutoka 33:19; 34:6) Kwa hiyo, wema wa Yehova unatia ndani sifa kadhaa zenye kuvutia. Hebu tuchunguze sifa mbili tu kati ya sifa hizo.

17. Fadhili ni nini, na Yehova amewaonyeshaje fadhili wanadamu duni wasiokamilika?

17 “Mwenye fadhili.” Sifa hii inatuonyesha jinsi ambavyo Yehova anashughulika na viumbe wake. Badala ya kuwa mkali sana, na asiyejali, au kuwa katili kama watu wengi wenye mamlaka, Yehova ni mpole na mwenye fadhili. Kwa mfano, Yehova alimwambia hivi Abramu: “Tafadhali inua macho yako ukatazame kutoka hapo ulipo, upande wa kaskazini na wa kusini na wa mashariki na wa magharibi.” (Mwanzo 13:14, NW) Tafsiri nyingi hazitaji neno “tafadhali.” Lakini wasomi wa Biblia wanasema kwamba maandishi ya awali ya Kiebrania yana kishirikishi cha neno ambacho kinabadili taarifa hiyo kuwa ombi la heshima badala ya amri. Kuna mifano mingine. (Mwanzo 31:12, NW; Ezekieli 8:5, NW) Hebu wazia, Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu anasema “tafadhali” anapoongea na wanadamu duni. Katika ulimwengu ambamo watu wengi ni wakali, wachokozi na wasio na adabu, inatia moyo kutafakari fadhili ya Mungu wetu Yehova.

18. Yehova ni “mwingi wa . . . kweli” katika maana gani, na kwa nini maneno hayo yanatia moyo?

18 “Mwingi wa . . . kweli.” Kusema uwongo ni zoea la kawaida ulimwenguni leo. Lakini Biblia inatukumbusha hivi: “Mungu si mtu, aseme uongo.” (Hesabu 23:19) Isitoshe, andiko la Tito 1:2 linasema kwamba ‘Mungu hawezi kusema uwongo.’ Hawezi kusema uwongo kwa sababu yeye ni mwema sana. Kwa hivyo, ahadi za Yehova zinategemeka kabisa; maneno yake hayawezi kamwe kukosa kutimia. Yehova anaitwa pia “Mungu wa kweli.” (Zaburi 31:5) Mbali na kutosema uwongo, anaeneza ukweli kwa wingi. Yeye hafanyi mambo kwa kujificha au kisirisiri, bali yeye huwafundisha watumishi wake waaminifu hekima yake isiyo na mipaka. * Hata anawafundisha jinsi ya kuishi kupatana na kweli hizo ili ‘waendelee kutembea katika kweli.’ (3 Yohana 3) Kwa ujumla, kila mmoja wetu anapaswa kuitikiaje wema wa Yehova?

‘Ukimbilieni Wema wa Bwana’

19, 20. (a) Shetani alidhoofishaje tumaini la Hawa katika wema wa Yehova, na matokeo yalikuwa nini? (b) Wema wa Yehova unapaswa kutuchochea tufanye nini, na kwa nini?

19 Shetani alipomshawishi Hawa katika bustani ya Edeni, alianza kwa kudhoofisha kwa hila tumaini lake katika wema wa Yehova. Yehova alikuwa amemwambia Adamu hivi: “Matunda ya kila mti wa bustani waweza kula.” Yehova alimkataza kula matunda ya mti mmoja tu kati ya maelfu ya miti yenye kuvutia iliyokuwa bustanini. Hata hivyo, angalia swali ambalo Shetani alimwuliza Hawa: “Ati! hivi ndivyo alivyosema Mungu, Msile matunda ya miti yote ya bustani?” (Mwanzo 2:9, 16; 3:1) Shetani alipotosha maneno ya Yehova ili amsadikishe Hawa kwamba Yehova alikuwa akimnyima kitu fulani kizuri. Kwa kusikitisha, Hawa alidanganyika. Hawa alianza kutilia shaka wema wa Mungu ambaye alikuwa amempa kila kitu alichokuwa nacho. Wanaume na wanawake wengi walioishi baadaye walifuata mfano wake.

20 Tunajua huzuni na taabu nyingi sana zilizosababishwa na shaka hiyo. Basi na tutii maneno ya Yeremia 31:12: “Wataukimbilia wema wa BWANA.” Bila shaka tunapaswa kuukimbilia wema wa Yehova kwa shangwe. Hatupaswi kamwe kutilia shaka makusudi ya Mungu wetu ambaye ni mwema sana. Tunaweza kumtumaini kabisa kwa sababu anataka wale wanaompenda wawe na maisha bora.

21, 22. (a) Ungependa kuonyesha katika njia zipi kwamba unathamini wema wa Yehova? (b) Tutazungumzia sifa gani katika sura inayofuata, na sifa hiyo inatofautianaje na wema?

21 Zaidi ya hayo, tunafurahi tunapopata nafasi ya kuwaambia wengine kuhusu wema wa Mungu. Zaburi 145:7 yasema hivi kuhusu watu wa Yehova: “Watalihubiri kumbukumbu la wema wako mkuu.” Kila siku tunafaidika kwa njia fulani na wema wa Yehova. Kwa nini usimshukuru Yehova kila siku kwa sababu ya jambo hususa linaloonyesha wema wake? Kutafakari na kumshukuru Yehova kila siku kwa sababu ya wema wake, na kuwaambia wengine kuhusu sifa hiyo kutatusaidia kumwiga Mungu wetu mwema. Tutamkaribia Yehova zaidi tukitafuta njia za kuiga wema wake. Mtume Yohana aliyezeeka aliandika hivi: “Mpendwa, uwe mwigaji, si wa lililo baya, bali wa lililo jema. Yeye ambaye atenda mema hutokana na Mungu.”—3 Yohana 11.

22 Wema wa Yehova unahusiana pia na sifa nyingine. Kwa mfano, Mungu ni “mwingi wa fadhili-upendo,” au upendo mshikamanifu. (Kutoka 34:6, NW) Tofauti na wema, Yehova hawaonyeshi watu wote sifa hiyo bali anawaonyesha hasa watumishi wake waaminifu. Katika sura inayofuata, tutajifunza jinsi anavyofanya hivyo.

^ fu. 14 Fidia ndiyo uthibitisho bora zaidi wa wema wa Yehova. Ajapokuwa na mamilioni ya viumbe wa roho, Yehova alimchagua Mwanaye mpendwa aliye mzaliwa-pekee afe kwa ajili yetu.

^ fu. 18 Kwa kufaa, Biblia inaonyesha kwamba kweli inahusiana na nuru. Mtunga-zaburi aliimba hivi: ‘Niletee nuru yako na kweli yako.’ (Zaburi 43:3) Yehova anawaangazia nuru nyingi ya kiroho wale walio na nia ya kufundishwa au kuelimishwa naye.—2 Wakorintho 4:6; 1 Yohana 1:5.