Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sura ya 22

Je, “Hekima ya Kutoka Juu” Inakuongoza Maishani?

Je, “Hekima ya Kutoka Juu” Inakuongoza Maishani?

1-3. (a) Solomoni alionyeshaje hekima ya pekee katika kuamua ni nani aliyekuwa mama ya mtoto? (b) Yehova anaahidi kutupatia nini, na ni maswali gani yanayozuka?

ILIKUWA kesi ngumu sana—wanawake wawili walibishania mtoto mmoja mchanga. Wanawake hao waliishi pamoja, na mmoja wao alijifungua mwana siku chache tu baada ya mwingine kujifungua. Mtoto mmoja alikuwa amekufa, na kila mwanamke alidai kwamba mtoto aliyekuwa hai alikuwa wake. * Hapakuwa na watu wengine walioshuhudia lililotukia. Yaelekea kwamba kesi hiyo ilikuwa imesikilizwa katika mahakama ya chini lakini haikusuluhishwa. Mwishowe, kesi hiyo ilipelekwa kwa Solomoni, mfalme wa Israeli. Je, angefunua ukweli wa mambo?

2 Baada ya kuwasikiliza wanawake hao wakibishana kwa muda, Solomoni aliomba upanga. Kisha, akaamuru mtoto huyo akatwe vipande viwili na kila mwanamke apewe kipande kimoja. Mara moja mama ya mtoto huyo akamsihi mfalme amkabidhi yule mwanamke mwingine mtoto wake mpendwa. Lakini mwanamke yule mwingine aliendelea kusisitiza mtoto huyo akatwe vipande viwili. Sasa Solomoni akajua ukweli wa mambo. Alijua jinsi ambavyo mama humhurumia na kumpenda sana mtoto wake, naye alitumia ujuzi huo kutatua kesi hiyo. Hebu wazia furaha ya mama huyo Solomoni alipompa mtoto wake na kusema: “Yeye ndiye mama yake.”—1 Wafalme 3:16-27.

3 Solomoni alikuwa na hekima ya pekee, sivyo? Watu walistaajabu sana waliposikia jinsi Solomoni alivyosuluhisha kesi hiyo, “maana waliona ya kuwa hekima ya Mungu ilikuwa ndani yake.” Naam, hekima ya Solomoni ilikuwa zawadi kutoka kwa Mungu. Yehova alikuwa amempa “moyo wa hekima na wa akili.” (1 Wafalme 3:12, 28) Lakini vipi sisi? Je, Mungu anaweza pia kutupatia hekima? Ndiyo. Solomoni aliongozwa kuandika hivi: “BWANA huwapa watu hekima.” (Mithali 2:6) Yehova aahidi kuwapa hekima, yaani, uwezo wa kutumia ujuzi, ufahamu, na utambuzi, wale wanaoitafuta kwa unyofu. Tunawezaje kupata hekima inayotoka juu? Na tutaitumiaje maishani mwetu?

Unawezaje ‘Kujipatia Hekima’?

4-7. Ni matakwa gani manne yanayohitajiwa ili kujipatia hekima?

Je, ni lazima tuwe na akili nyingi au elimu ya juu ili Mungu atupatie hekima yake? La. Yehova yu tayari kutupatia hekima bila kujali malezi au elimu yetu. (1 Wakorintho 1:26-29) Lakini ni lazima tuchukue hatua fulani, kwa sababu Biblia inatuhimiza ‘tujipatie hekima.’ (Mithali 4:7) Tutajipatiaje hekima?

5 Kwanza, ni lazima tumhofu Mungu. “Kumhofu Yehova ni mwanzo wa hekima [“hatua ya kwanza ya kupata hekima,” The New English Bible],” yasema Mithali 9:10, NW. Kumhofu Mungu ndio msingi wa hekima ya kweli. Kwa nini? Kumbuka kwamba hekima inatia ndani uwezo wa kutumia ujuzi kwa mafanikio. Kumhofu Mungu si kutetemeka kwa wasiwasi, bali ni kumsujudia kwa kicho, heshima, na kumtumaini. Hofu ya aina hiyo inafaa na humchochea sana mtu. Hutuchochea kuishi kupatana na ujuzi tulio nao kuhusu mapenzi ya Mungu na njia zake. Hilo ndilo jambo la hekima zaidi tuwezalo kufanya, kwa sababu sikuzote kanuni za Yehova huwafaidi kabisa wale wanaozifuata.

6 Pili, ni lazima tuwe wanyenyekevu na wenye kiasi. Hatuwezi kuwa na hekima ya Mungu tusipokuwa wanyenyekevu na wenye kiasi. (Mithali 11:2) Kwa nini? Tukiwa wanyenyekevu na wenye kiasi, tutakuwa tayari kukubali kwamba hatujui kila jambo. Tutakubali kwamba nyakati nyingine maoni yetu si sawa na hivyo tunahitaji kujifunza maoni ya Yehova. Yehova “huwapinga wenye kiburi,” lakini hufurahi kuwapa hekima wale walio wanyenyekevu moyoni.—Yakobo 4:6.

Ili kupata hekima ya Mungu, ni lazima tuitafute kwa bidii

7 Jambo la tatu muhimu ni kujifunza Neno la Mungu. Hekima ya Yehova imefunuliwa katika Neno lake. Ili kupata hekima hiyo, ni lazima tujitahidi kabisa kuitafuta. (Mithali 2:1-5) Takwa la nne ni sala. Tukimwomba Yehova hekima kwa unyofu, atatupatia kwa ukarimu. (Yakobo 1:5) Tukiomba msaada wa roho yake hatakosa kujibu sala zetu. Na roho yake itatuongoza kupata hazina zilizo katika Neno lake ambazo zinaweza kutusaidia kutatua matatizo, kuepuka hatari, na kufanya maamuzi ya hekima.—Luka 11:13.

8. Ni nini kitakachoonyesha kwamba tumejipatia hekima ya Mungu?

8 Kama tulivyoona katika Sura ya 17, hekima ya Yehova inazaa matunda. Kwa hiyo, mwenendo wetu utaonyesha wazi kwamba tumejipatia hekima ya Mungu. Mwanafunzi Yakobo alitaja sifa za hekima ya Mungu alipoandika hivi: “Hekima ya kutoka juu kwanza kabisa ni safi kiadili, kisha yenye kufanya amani, yenye kukubali sababu, tayari kutii, yenye kujaa rehema na matunda mema, isiyofanya tofauti zenye ubaguzi, si ya kinafiki.” (Yakobo 3:17) Tunapozungumzia kila moja ya sifa hizo za hekima ya Mungu, huenda tukajiuliza, ‘Je, hekima ya kutoka juu inaniongoza maishani?’

“Ni Safi Kiadili, Kisha Yenye Kufanya Amani”

9. Kuwa safi kiadili kwamaanisha nini, na kwa nini inafaa kwamba usafi wa kiadili ndiyo sifa inayotajwa kwanza katika orodha ya sifa za hekima?

9 “Kwanza kabisa ni safi kiadili.” Kuwa safi kiadili kwamaanisha kutakata na kuwa bila unajisi, si kwa nje tu bali pia moyoni. Biblia inahusianisha hekima na moyo, lakini hekima itokayo mbinguni haiwezi kuingia katika moyo uliotiwa unajisi na tamaa na mawazo maovu, na nia mbovu. (Mithali 2:10; Mathayo 15:19, 20) Lakini, kama moyo wetu ni safi kiadili—yaani, kwa kadiri ambavyo wanadamu wasiokamilika wanaweza kuwa safi—‘tutajiepusha na uovu na tutatenda mema.’ (Zaburi 37:27; Mithali 3:7) Kwa kufaa, usafi wa kiadili unatajwa kwanza katika orodha ya sifa za hekima. Hatuwezi kuwa na sifa nyingine za hekima ya kutoka juu tusipokuwa safi kiadili na kiroho.

10, 11. (a) Kwa nini ni muhimu tuwe watu wanaofanya amani? (b) Ukigundua kwamba umemkosea mwabudu mwenzako, utaonyeshaje kwamba wewe ni mtu anayefanya amani? (Ona pia kielezi-chini.)

10 “Kisha yenye kufanya amani.” Hekima ya kutoka mbinguni hutuchochea kufuatia amani, ambayo ni tunda la roho ya Mungu. (Wagalatia 5:22) Tunajitahidi sana kutoharibu ‘kifungo cha amani’ kinachowaunganisha watu wa Yehova. (Waefeso 4:3) Sisi pia hujitahidi kabisa kurudisha amani inapovurugwa. Kwa nini ni muhimu kufanya hivyo? Biblia inasema: “Endeleeni . . . kuishi kwa kufanya amani; na Mungu wa upendo na amani atakuwa pamoja nanyi.” (2 Wakorintho 13:11) Mungu wa amani atakuwa pamoja nasi maadamu tunaendelea kufanya amani. Uhusiano wetu na Yehova unategemea jinsi tunavyowatendea waabudu wenzetu. Tunawezaje kuwa watu wanaofanya amani? Fikiria mfano ufuatao.

11 Unapaswa kufanya nini ukigundua kwamba umemkosea mwabudu mwenzako? Yesu alisema: “Basi, ikiwa wewe unaleta zawadi yako kwenye madhabahu na huko wakumbuka kwamba ndugu yako ana jambo fulani dhidi yako, acha zawadi yako hapo mbele ya madhabahu, na uende zako; kwanza fanya amani yako na ndugu yako, na ndipo, ukiisha kurudi, toa zawadi yako.” (Mathayo 5:23, 24) Unaweza kutumia shauri hilo kwa kuchukua hatua ya kwenda kumwona ndugu yako. Ukiwa na kusudi gani? Ili ‘ufanye amani yako’ naye. * Ili kutimiza kusudi hilo, huenda ukahitaji kukubali kwamba umemwumiza kihisia. Ukimfikia kwa kusudi la kufanya amani na udumishe mtazamo huo, yaelekea kwamba tatizo litasuluhishwa, utaomba msamaha na utasamehewa. Unapochukua hatua ya kufanya amani, unaonyesha kwamba unaongozwa na hekima ya Mungu.

“Yenye Kukubali Sababu, Tayari Kutii”

12, 13. (a) Neno linalotafsiriwa “-enye kukubali sababu” katika Yakobo 3:17 linamaanisha nini? (b) Tunawezaje kuonyesha kwamba sisi ni wenye kukubali sababu?

12 “Yenye kukubali sababu.” Ni nini maana ya kukubali sababu? Wasomi wa Biblia wanasema kwamba si rahisi kutafsiri neno la awali la Kigiriki linalotafsiriwa “-enye kukubali sababu” kwenye Yakobo 3:17. Watafsiri wametumia maneno kama vile “upole,” “ustahimilivu,” na “mwenye kujali.” Neno la Kigiriki linamaanisha kihalisi “mwenye kukubali maoni ya wengine.” Tunawezaje kuonyesha kwamba tunaongozwa na sifa hiyo ya hekima ya kutoka juu?

13 Andiko la Wafilipi 4:5 lasema: “Hali yenu ya kukubali sababu na ijulikane kwa watu wote.” Tafsiri nyingine inasema: “Mjulikane kuwa watu wenye kukubali sababu.” (The New Testament in Modern English, ya J. B. Phillips) Ona kwamba jambo muhimu si jinsi tunavyojiona; bali ni jinsi wengine wanavyotuona. Mtu mwenye kukubali sababu hafuatilii mambo madogo-madogo ya sheria au hasisitizi mambo yafanywe jinsi anavyopenda. Badala yake, yuko tayari kuwasikiliza wengine na kukubali maoni yao inapowezekana. Yeye pia ni mpole, si mkali au mkatili. Hiyo ni sifa muhimu kwa Wakristo wote, lakini hasa kwa wazee wa kutaniko. Upole huvutia, kwa hiyo watu hujihisi huru kuongea na wazee wapole. (1 Wathesalonike 2:7, 8) Ni muhimu sote tujiulize hivi: ‘Je, wengine huniona kuwa mtu mwenye kuwajali wengine, mwenye kukubali sababu, na mpole?’

14. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tuko “tayari kutii”?

14 “Tayari kutii.” Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “tayari kutii” linapatikana mara moja tu katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Msomi mmoja anasema kwamba neno hilo “hutumiwa mara nyingi kuhusiana na nidhamu ya kijeshi.” Linaweza kumaanisha “mtu anayeshawishiwa kwa urahisi” na “mtiifu.” Mtu anayeongozwa na hekima ya kutoka juu huwa tayari kutii Maandiko. Hashikilii sana maoni yake na kukataa hoja zozote ambazo zinapinga maoni yake. Badala yake, yeye hubadili maoni mara moja anapothibitishiwa kwa Maandiko kwamba amefanya uamuzi mbaya au maoni yake ni yenye kosa. Je, ndivyo wengine wanavyokuona?

“Yenye Kujaa Rehema na Matunda Mema”

15. Rehema ni nini, na kwa nini inafaa kwamba andiko la Yakobo 3:17 linataja “rehema” pamoja na “matunda mema”?

15 “Yenye kujaa rehema na matunda mema.” * Rehema ni sifa muhimu ya hekima ya kutoka juu, kwa sababu inasemekana kwamba hekima hiyo ‘imejaa rehema.’ Ona kwamba “rehema” inatajwa pamoja na “matunda mema.” Jambo hilo linafaa kwa sababu katika Biblia, mara nyingi rehema humaanisha kuwajali sana wengine na kuwatendea mambo mengi ya fadhili kwa huruma. Kichapo kimoja cha marejeo chafafanua rehema kuwa “hali ya kuhuzunishwa na hali mbaya ya mtu mwingine na kujaribu kumsaidia.” Kwa hiyo, hekima ya Mungu si baridi wala haitegemei akili tu. Badala yake, ni yenye upendo na huruma, na inawajali wengine. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tumejaa rehema?

16, 17. (a) Mbali na kumpenda Mungu, ni nini kinachotuchochea tushiriki kazi ya kuhubiri, na kwa nini? (b) Ni katika njia zipi tunaweza kuonyesha kwamba tumejaa rehema?

16 Bila shaka njia bora ya kuonyesha sifa hiyo ni kuwahubiria wengine habari njema za Ufalme wa Mungu. Ni nini kinachotuchochea kufanya kazi hiyo? Hasa ni kwa sababu tunampenda Mungu. Tunachochewa pia na rehema, au huruma. (Mathayo 22:37-39) Watu wengi leo ‘wamechunwa ngozi na kutupwa huku na huku kama kondoo wasio na mchungaji.’ (Mathayo 9:36) Wamepuuzwa na kupofushwa kiroho na wachungaji wa uwongo wa kidini. Ndiyo sababu hawajui mwongozo wenye hekima ulio katika Neno la Mungu wala hawajui baraka zitakazoletwa duniani na Ufalme huo hivi karibuni. Kwa hiyo, tunapozingatia mahitaji ya kiroho ya jirani zetu, tunachochewa na huruma kutoka moyoni kujitahidi kadiri tuwezavyo kuwaambia kusudi la Yehova lenye upendo.

Tunapowaonyesha wengine rehema, au huruma, tunadhihirisha “hekima ya kutoka juu”

17 Ni katika njia zipi nyingine tunaweza kuonyesha kwamba tumejaa rehema? Kumbuka mfano wa Yesu wa yule Msamaria aliyemkuta msafiri fulani aliyelala kando ya barabara baada ya kupigwa na kuporwa. Msamaria huyo alimhurumia na ‘akatenda kwa rehema.’ Alimfunga majeraha na kumtunza. (Luka 10:29-37) Mfano huo waonyesha kwamba kuwa na rehema kwahusisha kuwasaidia wenye uhitaji. Biblia inatuambia “tufanye lililo jema kuelekea wote, lakini hasa kuelekea wale ambao katika imani ni jamaa zetu.” (Wagalatia 6:10) Fikiria mifano kadhaa. Huenda mwamini mwenzako aliye mzee kwa umri anahitaji kusaidiwa kusafiri kwenda kwenye mikutano ya Kikristo na kurudi. Huenda mjane fulani kutanikoni anahitaji kusaidiwa kurekebisha nyumba yake. (Yakobo 1:27) Huenda mtu fulani aliyeshuka moyo anahitaji kuambiwa “neno jema” la kumfariji. (Mithali 12:25) Tunapoonyesha rehema katika njia hizo, tunathibitisha kwamba tunaongozwa na hekima ya kutoka juu.

‘Isiyobagua, Si ya Kinafiki’

18. Ikiwa tunaongozwa na hekima ya kutoka juu, tunapaswa kujitahidi kuondoa nini mioyoni mwetu, na kwa nini?

18 “Isiyobagua.” Hekima ya Mungu hushinda kabisa ubaguzi wa kikabila na uzalendo. Ikiwa tunaongozwa na hekima hiyo, tunapaswa kujitahidi kuondoa kabisa mioyoni mwetu mwelekeo wowote wa kuonyesha upendeleo. (Yakobo 2:9) Hatuwapendelei watu fulani kwa sababu ya elimu yao, utajiri wao, au madaraka yao kutanikoni; wala hatumdharau mwabudu mwenzetu, hata ikiwa anaonekana kuwa na cheo cha chini sana katika jamii. Ikiwa Yehova anawapenda watu hao, hapana shaka kwamba sisi tunapaswa kuwapenda pia.

19, 20. (a) Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “mnafiki” latokana na nini? (b) Tunaonyeshaje “shauku ya kidugu isiyo na unafiki,” na kwa nini jambo hilo ni muhimu?

19 “Si ya kinafiki.” Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “mnafiki” linaweza kurejelea “mwigizaji katika mchezo wa kuigiza.” Katika nyakati za kale, waigizaji Wagiriki na Waroma walivaa vinyago vikubwa usoni katika michezo ya kuigiza. Kwa hiyo, neno la Kigiriki linalotafsiriwa “mnafiki” likaanza kutumiwa kumaanisha mtu anayejifanya, au mtu anayejisingizia. Hekima ya Mungu inapaswa kuongoza jinsi tunavyowatendea waabudu wenzetu na pia jinsi tunavyowaona.

20 Mtume Petro alisema kwamba ‘tukitii ile kweli’ tutakuwa na “shauku ya kidugu isiyo na unafiki.” (1 Petro 1:22) Naam, shauku yetu kwa ndugu zetu haipaswi kuwa ya kujionyesha tu. Hatujifanyi wala kujisingizia ili tuwadanganye wengine. Ni lazima shauku yetu iwe ya kweli, ya kutoka moyoni. Tukiwa na shauku ya aina hiyo, waamini wenzetu watatuamini kwa sababu watajua kwamba sisi si wanafiki. Unyofu wa aina hiyo hutokeza uhusiano mzuri kati ya Wakristo na pia huchangia hali ya kuaminiana kutanikoni.

“Shika Hekima Kamili”

21, 22. (a) Solomoni alishindwaje kushika hekima kamili? (b) Tunawezaje kushika hekima, na tutapata faida gani tukifanya hivyo?

21 Tunahitaji kushika hekima kwa sababu ni zawadi kutoka kwa Yehova. Solomoni alisema: “Mwanangu, . . . shika hekima kamili na busara.” (Mithali 3:21) Kwa kusikitisha, Solomoni mwenyewe alishindwa kufanya hivyo. Alikuwa mwenye hekima maadamu alitii kutoka moyoni. Lakini mwishowe, wake zake wengi wa kigeni waliugeuza moyo wake kutoka kwa ibada safi ya Yehova. (1 Wafalme 11:1-8) Hali iliyompata Solomoni inaonyesha kwamba tusipotumia ifaavyo ujuzi tulio nao hautatufaidi.

22 Tunawezaje kushika hekima kamili? Haitoshi tu kusoma kwa ukawaida Biblia na vichapo vya Biblia vinavyotayarishwa na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” Ni lazima pia tujitahidi kutumia mambo tunayojifunza. (Mathayo 24:45) Tuna kila sababu ya kutumia hekima ya Mungu. Tukifanya hivyo, tutakuwa na maisha bora sasa. Inatuwezesha “kuwa na mshiko imara juu ya uhai ulio halisi,” yaani, uhai katika ulimwengu mpya wa Mungu. (1 Timotheo 6:19) Na jambo la muhimu hata zaidi ni kwamba tunapokuza hekima ya kutoka juu tunamkaribia zaidi Yehova Mungu, chanzo cha hekima yote.

^ fu. 1 Andiko la 1 Wafalme 3:16 linasema kwamba wanawake hao walikuwa makahaba. Kichapo Insight on the Scriptures chasema: “Huenda wanawake hao hawakuwa makahaba wa kulipwa bali walikuwa wamefanya uasherati. Labda walikuwa wanawake Wayahudi au wanawake wa kigeni.”—Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 11 Usemi wa Kigiriki unaotafsiriwa “fanya amani yako” unatokana na kitenzi kinachomaanisha “‘kuleta badiliko, kubadilishana,’ na hivyo, ‘kupatanisha.’” Kwa hiyo, kusudi lako ni kubadilisha hali, na ikiwezekana, kuondoa chuki iliyo moyoni mwa yule aliyekosewa.—Waroma 12:18.

^ fu. 15 Biblia Habari Njema inatafsiri hivi maneno hayo: “Imejaa huruma na huzaa matunda ya matendo mema.”