Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Uzima wa Milele Duniani—Je, Ni Tumaini la Kikristo?

Uzima wa Milele Duniani—Je, Ni Tumaini la Kikristo?

Uzima wa Milele Duniani—Je, Ni Tumaini la Kikristo?

“[Mungu] atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena.”—UFU. 21:4.

1, 2. Tunajua jinsi gani kwamba Wayahudi wengi wa karne ya kwanza walitumaini kupata uzima milele duniani?

KIJANA mmoja tajiri na mashuhuri alimkimbilia Yesu, akapiga magoti mbele yake na kumuuliza hivi: “Mwalimu Mwema, nifanye nini ili niurithi uzima wa milele?” (Marko 10:17) Kijana huyo alikuwa akiuliza kuhusu kurithi uzima wa milele, lakini wapi? Kama tulivyozungumzia katika habari iliyotangulia, karne nyingi mapema Mungu aliwapa Wayahudi tumaini la ufufuo na la uzima wa milele duniani. Wayahudi wengi wa karne ya kwanza bado walikuwa na tumaini hilo.

2 Inaelekea Martha, rafiki ya Yesu, alikuwa akifikiria tumaini la watu kufufuliwa duniani aliposema hivi kuhusu ndugu yake aliyekufa: “Ninajua atafufuka katika ufufuo siku ya mwisho.” (Yoh. 11:24) Kwa kweli, wakati huo Masadukayo hawakuamini ufufuo. (Marko 12:18) Hata hivyo, katika kitabu chake (Judaism in the First Centuries of the Christian Era), George Foot Moore anasema hivi: “Maandishi . . . ya karne ya pili au ya kwanza kabla ya wakati wetu yanathibitisha imani ya kwamba katika wakati uliotarajiwa wa mabadiliko katika historia ya ulimwengu wale waliokufa katika vizazi vya zamani watafufuliwa na kuishi tena duniani.” Yule mwanamume tajiri aliyemwendea Yesu alitaka kupata uzima wa milele duniani.

3. Tutazungumzia maswali gani katika habari hii?

3 Leo, dini nyingi na wasomi wengi wa Biblia wanapinga kwamba tumaini la kuishi milele duniani ni fundisho la Kikristo. Watu wengi wanatumaini kuishi mbinguni baada ya kufa. Hivyo, wasomaji wa Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo wanapoona maneno “uzima wa milele,” wengi wanafikiri kwamba sikuzote yanamaanisha kuishi mbinguni. Je, ni kweli? Yesu alimaanisha nini aliposema kuhusu uzima wa milele? Wanafunzi wake waliamini nini? Je, Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yanafundisha kuhusu tumaini la kuishi milele duniani?

Uzima wa Milele “Katika Uumbaji-Mpya”

4. Ni mambo gani yatakayotukia “katika uumbaji-mpya”?

4 Biblia inafundisha kwamba Wakristo watiwa-mafuta watafufuliwa ili watawale juu ya dunia wakiwa mbinguni. (Luka 12:32; Ufu. 5:9, 10; 14:1-3) Hata hivyo, Yesu alipozungumza kuhusu uzima wa milele, sikuzote hakuwa tu akifikiria kikundi hicho. Fikiria yale aliyowaambia wanafunzi wake baada ya yule kijana tajiri kukataa kwa huzuni mwaliko wa kuacha mali yake yote na kuwa mfuasi wa Kristo. (Soma Mathayo 19:28, 29.) Yesu aliwaambia mitume wake kwamba watakuwa kati ya wale ambao watatawala wakiwa wafalme na kuyahukumu “makabila kumi na mawili ya Israeli,” yaani, ulimwengu wa wanadamu bila kutia ndani wale watakaotawala wakiwa mbinguni. (1 Kor. 6:2) Pia, alisema kwamba “kila mtu” ambaye atamfuata atapata thawabu. Watu hao pia ‘watarithi uzima wa milele.’ Mambo hayo yote yatatukia “katika uumbaji-mpya.”

5. “Uumbaji-mpya” ni nini?

5 Yesu alimaanisha nini aliposema “uumbaji-mpya”? Maneno hayo yanatafsiriwa kuwa “ulimwengu mpya” katika Biblia Habari Njema. Katika Biblia ya The Jerusalem Bible yanatafsiriwa kuwa “mambo yote yatakapofanywa mapya,” na katika Biblia ya The Holy Bible—New International Version yanatafsiriwa kuwa “kufanywa upya kwa mambo yote.” Kwa kuwa Yesu alitumia maneno hayo bila kuyafafanua, ni wazi kwamba alikuwa akizungumza kuhusu tumaini ambalo Wayahudi walikuwa nalo kwa karne nyingi. Kungekuwa na uumbaji-mpya wa hali za dunia, hivi kwamba mambo yangekuwa kama yalivyokuwa katika bustani ya Edeni kabla ya Adamu na Hawa kutenda dhambi. Uumbaji-mpya utatimiza ahadi ya Mungu ya ‘kuumba mbingu mpya na dunia mpya.’—Isa. 65:17.

6. Mfano wa kondoo na mbuzi unatufundisha nini kuhusu tumaini la uzima wa milele?

6 Yesu alitaja pia uzima wa milele katika hotuba yake kuhusu umalizio wa mfumo wa mambo. (Mt. 24:1-3) Alisema hivi: “Wakati Mwana wa binadamu atakapofika katika utukufu wake, na malaika wote pamoja naye, ndipo atakapoketi juu ya kiti chake cha ufalme chenye utukufu. Na mataifa yote yatakusanyika mbele yake, naye atawatenganisha watu, mmoja kutoka kwa mwenzake, kama vile mchungaji anavyotenganisha kondoo na mbuzi.” Wale watakaohukumiwa adhabu “watakatiliwa mbali milele, lakini waadilifu wataingia katika uzima wa milele.” “Waadilifu” ambao watapokea uzima wa milele ni wale ambao wanawaunga mkono kwa ushikamanifu “ndugu” za Kristo waliotiwa-mafuta kwa roho. (Mt. 25:31-34, 40, 41, 45, 46) Kwa kuwa watiwa-mafuta wanachaguliwa ili wawe watawala katika Ufalme wa mbinguni, “waadilifu” hao ni lazima wawe raia wa kidunia wa Ufalme huo. Biblia ilitabiri hivi: “[Mfalme wa Yehova] atakuwa na raia kutoka bahari mpaka bahari na kutoka ule Mto mpaka miisho ya dunia.” (Zab. 72:8) Raia hao watafurahia uzima wa milele duniani.

Injili ya Yohana Inaonyesha Nini?

7, 8. Yesu alizungumza na Nikodemo kuhusu matumaini gani mawili tofauti?

7 Kama ilivyoandikwa katika Injili ya Mathayo, Marko, na Luka, Yesu alitumia maneno “uzima wa milele” katika pindi zilizotajwa hapo juu. Injili ya Yohana inanukuu mara 17 maneno ya Yesu kuhusu kuishi milele. Acheni tuchunguze baadhi ya manukuu hayo ili tuone yale ambayo Yesu alisema kuhusu tumaini la kuishi milele duniani.

8 Kulingana na Yohana, mtu wa kwanza ambaye Yesu alizungumza naye kuhusu uzima wa milele alikuwa Farisayo aliyeitwa Nikodemo. Alimwambia Nikodemo hivi: “Mtu asipozaliwa kwa maji na roho, hawezi kuingia katika ufalme wa Mungu.” Ni lazima wale wanaoingia katika Ufalme wa mbinguni ‘wazaliwe tena.’ (Yoh. 3:3-5) Yesu hakusema hayo tu. Pia, alisema kuhusu tumaini ambalo watu wote ulimwenguni wanaweza kupata. (Soma Yohana 3:16.) Yesu alikuwa akizungumza kuhusu tumaini la uzima wa milele huko mbinguni kwa ajili ya wafuasi wake watiwa-mafuta na kwa wengine duniani.

9. Yesu alizungumza na mwanamke Msamaria kuhusu tumaini gani?

9 Baada ya kuzungumza na Nikodemo huko Yerusalemu, Yesu alisafiri upande wa kaskazini kuelekea Galilaya. Njiani, alikutana na mwanamke mmoja kwenye chemchemi ya Yakobo karibu na jiji la Sikari huko Samaria. Alimwambia hivi: “Yule atakayekunywa maji ambayo nitampa hatapatwa na kiu hata kidogo, lakini maji ambayo nitampa yatakuwa chemchemi ya maji ndani yake, inayobubujika ili kutokeza uzima wa milele.” (Yoh. 4:5, 6, 14) Maji hayo yanawakilisha maandalizi ya Mungu ya kuwarudishia wanadamu wote uzima wa milele, kutia ndani wale ambao wataishi duniani. Katika kitabu cha Ufunuo, Mungu mwenyewe anasema hivi: “Kwa yeyote aliye na kiu mimi nitampa maji bure kutoka kwenye chemchemi ya maji ya uzima.” (Ufu. 21:5, 6; 22:17) Kwa hiyo, Yesu alizungumza na yule mwanamke Msamaria kuhusu uzima wa milele si tu kwa ajili ya warithi wa Ufalme watiwa-mafuta bali pia kwa ajili ya wanadamu waaminifu ambao wana tumaini la kuishi duniani.

10. Baada ya kumponya mtu fulani mgonjwa karibu na dimbwi la Bethzatha, Yesu aliwaambia nini wapinzani wa kidini kuhusu uzima wa milele?

10 Mwaka uliofuata, Yesu alirudi tena Yerusalemu. Akiwa huko, alimponya mtu fulani mgonjwa karibu na dimbwi la Bethzatha. Yesu aliwaambia hivi Wayahudi ambao walishutumu jambo alilofanya: “Mwana hawezi kufanya hata jambo moja kwa uamuzi wake mwenyewe, ila tu lile analomwona Baba akifanya.” Baada ya kuwaambia kwamba Baba “amemkabidhi Mwana kazi yote ya kuhukumu,” Yesu alisema: “Yule ambaye husikia neno langu na kumwamini yule aliyenituma ana uzima wa milele.” Pia, Yesu alisema hivi: “Saa inakuja ambayo wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti [ya Mwana wa binadamu] na kutoka, wale waliotenda mambo mema kwenye ufufuo wa uzima, wale waliokuwa na zoea la kutenda mambo maovu kwenye ufufuo wa hukumu.” (Yoh. 5:1-9, 19, 22, 24-29) Yesu alikuwa akiwaambia Wayahudi waliokuwa wakimtesa kwamba yeye ndiye aliyewekwa rasmi na Mungu kutimiza tumaini la Wayahudi la kupata uzima wa milele duniani na kwamba angefanya hivyo kwa kuwafufua wafu.

11. Tunajua jinsi gani kwamba maneno ambayo Yesu alisema kwenye Yohana 6:48-51 yanahusu pia tumaini la kuishi milele duniani?

11 Akiwa Galilaya, maelfu ya watu waliotaka mikate ambayo Yesu aliandaa kimuujiza walianza kumfuata. Yesu akawaambia kuhusu mkate wa aina nyingine—“mkate wa uzima.” (Soma Yohana 6:40, 48-51.) Alisema hivi: “Mkate ambao nitatoa ni mwili wangu.” Yesu alitoa uhai wake si kwa ajili tu ya wale ambao atatawala nao katika Ufalme wake wa kimbingu, bali pia “kwa ajili ya uzima wa ulimwengu” wa wanadamu wanaoweza kukombolewa. “Yeyote akila mkate huu,” yaani, akionyesha imani katika uwezo wa kukomboa wa dhabihu ya Yesu, atakuwa na tumaini la kupata uzima wa milele. Kwa kweli, maneno ‘kuishi milele’ yalitia ndani tumaini ambalo Wayahudi walikuwa nalo kwa muda mrefu la kuishi milele duniani chini ya utawala wa Masihi.

12. Yesu alikuwa akizungumza kuhusu tumaini gani alipowaambia wapinzani wake kwamba ‘atawapa kondoo wake uzima wa milele’?

12 Baadaye, kwenye Sherehe ya Wakfu huko Yerusalemu, Yesu aliwaambia hivi wapinzani wake: “Hamwamini, kwa sababu ninyi hamko kati ya kondoo wangu. Kondoo wangu huisikiliza sauti yangu, nami ninawajua, nao wananifuata. Nami ninawapa hao uzima wa milele.” (Yoh. 10:26-28) Je, Yesu alikuwa akizungumza tu kuhusu uzima wa milele mbinguni, au alikuwa pia akizungumzia uzima wa milele katika paradiso duniani? Muda mfupi kabla ya hapo, Yesu alikuwa amewafariji wafuasi wake kwa maneno haya: “Msiogope, kundi dogo, kwa sababu Baba yenu amekubali kuwapa ninyi ufalme.” (Luka 12:32) Hata hivyo, wakati wa Sherehe hiyo ya Wakfu, Yesu alisema: “Nina kondoo wengine, ambao si wa zizi hili; hao pia nitawaleta.” (Yoh. 10:16) Kwa hiyo, Yesu alipozungumza na wapinzani hao, alimaanisha tumaini la kuishi mbinguni kwa ajili ya “kundi dogo” na tumaini la kuishi milele duniani kwa ajili ya mamilioni ya “kondoo wengine.”

Tumaini Ambalo Halikuhitaji Kufafanuliwa

13. Yesu alimaanisha nini aliposema: “Utakuwa pamoja nami katika Paradiso”?

13 Yesu alipokuwa akiteseka kwenye mti wa mateso, alitoa uthibitisho usioweza kupingwa wa tumaini la wanadamu. Mtenda-maovu mmoja aliyetundikwa kando yake alimwambia hivi: “Yesu, unikumbuke utakapoingia katika ufalme wako.” Yesu alimwahidi hivi: “Kwa kweli mimi nakuambia leo, Utakuwa pamoja nami katika Paradiso.” (Luka 23:42, 43) Kwa kuwa ni wazi kwamba mtu huyo alikuwa Myahudi, hakuhitaji kufafanuliwa kuhusu Paradiso. Alijua kuhusu tumaini la uzima wa milele duniani wakati ujao.

14. (a) Ni nini kinachoonyesha kwamba ilikuwa vigumu kwa mitume kuelewa maelezo kuhusu tumaini la kwenda mbinguni? (b) Ni wakati gani wafuasi wa Yesu walipoelewa vizuri kabisa tumaini la kwenda mbinguni?

14 Hata hivyo, yaliyohitaji kufafanuliwa ni maelezo ya Yesu kuhusu tumaini la kwenda mbinguni. Alipowaambia wanafunzi wake kwamba anaenda mbinguni ili kuwatayarishia mahali, hawakuelewa kile alichomaanisha. (Soma Yohana 14:2-5.) Baadaye aliwaambia hivi: “Bado nina mambo mengi ya kuwaambia, lakini hamwezi kuyastahimili kwa sasa. Hata hivyo, huyo atakapofika, roho ya ile kweli, atawaongoza ninyi ndani ya kweli yote.” (Yoh. 16:12, 13) Ni baada tu ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K. walipotiwa mafuta kwa roho ya Mungu ili kuwa wafalme wakati ujao ndipo wafuasi wa Yesu walipoelewa kwamba viti vyao vya ufalme vitakuwa mbinguni. (1 Kor. 15:49; Kol. 1:5; 1 Pet. 1:3, 4) Tumaini la urithi wa kimbingu lilikuwa jambo jipya, na lilikaziwa zaidi katika barua zilizoongozwa na roho ya Mungu ambazo ni sehemu ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Je, barua hizo zinathibitisha tumaini la wanadamu la kuishi milele duniani?

Barua Zilizoongozwa na Roho ya Mungu Zinasema Nini?

15, 16. Barua kwa Waebrania iliyoongozwa na roho ya Mungu na maneno ya Petro yanaonyesha jinsi gani tumaini la kuishi milele duniani?

15 Katika barua yake kwa Waebrania, mtume Paulo aliwaita waamini wenzake “ndugu watakatifu, washiriki wa mwito wa mbinguni.” Hata hivyo, alisema pia kwamba Mungu ameitiisha chini ya Yesu “dunia yenye kukaliwa inayokuja.” (Ebr. 2:3, 5; 3:1) Katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, neno la awali linalotafsiriwa “dunia yenye kukaliwa” sikuzote linamaanisha dunia inayokaliwa na wanadamu. Kwa hiyo, “dunia yenye kukaliwa inayokuja” ni mfumo wa mambo wa wakati ujao duniani chini ya utawala wa Yesu Kristo. Wakati huo, Yesu atatimiza ahadi hii ya Mungu: “Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.”—Zab. 37:29.

16 Mtume Petro pia aliongozwa na roho ya Mungu kuandika kuhusu wakati ujao wa wanadamu. Aliandika hivi: “Mbingu na dunia za sasa zimewekwa akiba kwa ajili ya moto nazo zinahifadhiwa mpaka ile siku ya hukumu na ya kuangamizwa kwa watu wasiomwogopa Mungu.” (2 Pet. 3:7) Ni nini kitakachochukua mahali pa mbingu za kiserikali na jamii ya sasa ya wanadamu waovu? (Soma 2 Petro 3:13.) Zitaondolewa na mahali pake kuchukuliwa na “mbingu mpya,” yaani, Ufalme wa Kimasihi wa Mungu, na “dunia mpya,” yaani, jamii ya wanadamu waadilifu ambao ni waabudu wa kweli.

17. Tumaini la wanadamu linaelezwa jinsi gani kwenye Ufunuo 21:1-4?

17 Mioyo yetu inachochewa na maono ya kitabu cha mwisho cha Biblia yanayohusu kurudishwa kwa wanadamu kwenye hali ya ukamilifu. (Soma Ufunuo 21:1-4.) Wanadamu waaminifu wamekuwa na tumaini hilo tangu ukamilifu wa wanadamu ulipopotezwa katika bustani ya Edeni. Watu waadilifu wataishi milele katika Paradiso duniani bila kuzeeka. Tumaini hilo linategemea kabisa Maandiko ya Kiebrania na pia Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, na linaendelea kuwatia nguvu watumishi waaminifu wa Yehova mpaka leo.—Ufu. 22:1, 2.

Je, Unaweza Kueleza?

• Yesu alimaanisha nini aliposema kuhusu “uumbaji-mpya”?

• Yesu alizungumza na Nikodemo kuhusu nini?

• Yesu alimwahidi nini mtenda-maovu fulani aliyetundikwa kando yake?

• Barua kwa Waebrania na maneno ya Petro yanathibitisha jinsi gani tumaini la kuishi milele duniani?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 8]

Wanadamu walio mfano wa kondoo watapewa uzima wa milele duniani

[Picha katika ukurasa wa 10]

Yesu aliwaambia wengine kuhusu uzima wa milele