Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Umewahi Kuwa na Mapendeleo ya Utumishi? Je, Unaweza Kutumikia Tena?

Umewahi Kuwa na Mapendeleo ya Utumishi? Je, Unaweza Kutumikia Tena?

Umewahi Kuwa na Mapendeleo ya Utumishi? Je, Unaweza Kutumikia Tena?

JE, WAKATI fulani ulikuwa na pendeleo la utumishi katika kutaniko la Kikristo? Labda ulikuwa mtumishi wa huduma au mzee. Au huenda ulitumikia katika aina fulani ya utumishi wa wakati wote. Bila shaka, migawo yako ilikuletea shangwe na uradhi mwingi sana, hata hivyo, ulilazimika kuacha migawo hiyo kwa sababu fulani.

Huenda uliacha pendeleo lako ili uwatunze washiriki wa familia. Au labda uliacha kwa sababu ya umri au kwa sababu ya matatizo ya afya. Maamuzi kama hayo si ishara ya kwamba hukufanikiwa. (1 Tim. 5:8) Katika karne ya kwanza, Filipo alitumikia akiwa mmishonari, lakini baadaye aliishi huko Kaisaria ambako aliitunza familia yake. (Mdo. 21:8, 9) Alipozeeka, Mfalme Daudi wa Israeli la kale alifanya mipango ili mwanawe Sulemani awe mfalme baada yake. (1 Fal. 1:1, 32-35) Ingawa hivyo, bado Yehova alimpenda Filipo na pia Daudi na wanaheshimiwa na watu leo.

Hata hivyo, huenda ikawa kwamba uliachishwa pendeleo fulani la utumishi. Je, ilikuwa ni kwa sababu ya mwenendo usiofaa? Au je, matatizo ya familia yalichangia? (1 Tim. 3:2, 4, 10, 12) Hata inawezekana kwamba hukukubaliana na uamuzi uliofanywa, na huenda ikawa umekasirishwa na jambo hilo mpaka leo.

Unaweza Kufikia Mapendeleo Tena

Je, mtu anaweza kupata tena pendeleo ambalo alipoteza? Katika visa vingi inawezekana. Hata hivyo, ili uweze kutumika tena, ni lazima uwe na tamaa ya kufikia mapendeleo. (1 Tim. 3:1) Lakini kwa nini uwe na tamaa hiyo? Kwa sababu ileile ambayo ilikufanya ujiweke wakfu kwa Mungu, yaani, upendo wako kwa Yehova na kwa wale wanaomtumikia. Ikiwa uko tayari kuonyesha upendo huo kwa kutumikia tena, hilo litamruhusu Yehova atumie uzoefu uliokuwa nao kabla ya kuachishwa pendeleo fulani na uzoefu ambao umepata baada ya kuachishwa pendeleo hilo.

Hebu kumbuka uhakikisho ambao Yehova aliwapa Waisraeli baada ya taifa lao kupoteza kwa haki pendeleo la kuwa na uhusiano wa pekee pamoja naye. Neno lake linasema hivi: “Mimi ni Yehova; sikubadilika. Nanyi ni wana wa Yakobo; hamjafikia mwisho wenu.” (Mal. 3:6) Yehova aliwapenda Waisraeli na alitamani kuwatumia zaidi. Vivyo hivyo, Yehova angependa kukutumia wakati ujao. Kwa sasa unaweza kufanya nini? Kupata mapendeleo ya kitheokrasi hakutegemei vipawa vyetu tu bali kwa kiwango kikubwa kunategemea hali yetu ya kiroho. Hivyo, kwa kuwa sasa huna madaraka mengi katika kutaniko, jitahidi kuboresha hali yako ya kiroho.

Ili ‘uwe na nguvu’ katika imani, ni lazima ‘umtafute Yehova na nguvu zake.’ (1 Kor. 16:13; Zab. 105:4) Njia moja ambayo unaweza kufanya hivyo ni kusali kutoka moyoni. Unapozungumza na Yehova kuhusu hali yako, mweleze hisia zako na umwombe akupe roho yake takatifu. Ukifanya hivyo, utamkaribia Yehova zaidi, na hilo litakutia nguvu. (Zab. 62:8; Flp. 4:6, 13) Njia nyingine ya kutia nguvu hali yako ya kiroho ni kuboresha funzo lako la Neno la Mungu. Kwa kuwa sasa una madaraka machache, unaweza kufanya mengi zaidi kuhusiana na funzo lako la kibinafsi na la familia, labda hata unaweza kurudia ratiba ambayo ulishindwa kudumisha.

Bila shaka, bado unamwakilisha Yehova ukiwa mmoja wa Mashahidi wake. (Isa. 43:10-12) Pendeleo kubwa zaidi ambalo kila mmoja wetu anaweza kuwa nalo ni kuwa ‘mfanyakazi mwenzi wa Mungu.’ (1 Kor. 3:9) Kuongeza utendaji katika utumishi wa shambani ni njia nzuri ya kuboresha uhusiano wako pamoja na Yehova na uhusiano wako pamoja na wale unaoshirikiana nao katika huduma.

Kukabiliana na Hisia Zako

Huenda ukaona aibu au kujuta baada ya kupoteza pendeleo. Huenda ukawa na mwelekeo wa kutetea matendo yako. Lakini, namna gani ikiwa ndugu walio na mamlaka walisikiliza sababu ulizotoa na bado wakaonelea kwamba hupaswi kuendelea kuwa na pendeleo fulani? Huenda ukawa na maoni mabaya kuelekea ndugu hao, na hilo linaweza kukuzuia usijitahidi tena kufikia mapendeleo au hata kukuzuia kujifunza kutokana na jambo lililokupata. Acheni tuchunguze jinsi mambo yaliyompata Ayubu, Manase, na Yosefu yanavyoweza kutusaidia kukabiliana na hisia zisizofaa.

Ayubu aliwawakilisha wengine mbele za Yehova na alitumika akiwa mzee na hakimu katika jamii ya kiukoo. (Ayu. 1:5; 29:7-17, 21-25) Kisha, katika kipindi kigumu zaidi cha maisha yake, Ayubu alipoteza mali yake, watoto wake, na afya yake nzuri. Zaidi ya matatizo hayo, alipoteza pia sifa yake nzuri mbele ya wengine. “Wamenicheka,” Ayubu akasema, “wale wenye siku chache kuliko mimi.”—Ayu. 30:1.

Ayubu alihisi kwamba hakuwa na hatia hata kidogo na alitaka kujitetea mbele za Mungu. (Ayu. 13:15) Ingawa hivyo, Ayubu alikuwa tayari kumngojea Yehova, naye alibarikiwa kwa kufanya hivyo. Alitambua kwamba alihitaji kurekebishwa, hasa kwa sababu ya jinsi alivyotenda alipokuwa akijaribiwa. (Ayu. 40:6-8; 42:3, 6) Mwishowe, Ayubu alibarikiwa sana na Mungu kwa sababu ya unyenyekevu wake.—Ayu. 42:10-13.

Ikiwa ulipoteza pendeleo kwa sababu ulifanya kosa fulani, huenda ukajiuliza ikiwa Yehova na ndugu zako Wakristo wanaweza kukusamehe kikweli na kusahau jambo hilo. Ikiwa unahisi hivyo, hebu sasa chunguza kisa cha Mfalme Manase wa Yuda. “Alifanya kwa kiasi kikubwa yale yaliyokuwa mabaya machoni pa Yehova, na kumtia uchungu.” (2 Fal. 21:6) Hata hivyo, kufikia wakati wa kifo chake, Manase alikuwa mwanamume mwaminifu, akitawala kama mfalme. Hilo lilifanyika jinsi gani?

Mwishowe, Manase alikubali nidhamu. Baada ya kupuuza maonyo, Yehova aliwaruhusu Waashuru wamshambulie, wakamfunga kwa pingu na kumpeleka uhamishoni huko Babiloni. Akiwa huko, Manase ‘aliutuliza uso wa Yehova Mungu wake, akaendelea kujinyenyekeza sana kwa sababu ya Mungu wa mababu zake. Naye akaendelea kusali kwake Yeye.’ Kutubu kutoka moyoni kulimchochea achukue hatua ili kurekebisha mambo, na Manase akasamehewa.—2 Nya. 33:12, 13.

Si rahisi kupata tena mara moja mapendeleo yote uliyopoteza. Hata hivyo, baada ya muda, huenda ukapewa mapendeleo machache. Kukubali mapendeleo hayo na kuyashughulikia vizuri kabisa kutafanya upewe mapendeleo zaidi. Hilo halimaanishi kwamba ni rahisi kufikia tena mapendeleo. Huenda utakabiliana na mambo yenye kuvunja moyo. Hata hivyo, ukiendelea kuvumilia na kuwa tayari kutumika utapata matokeo mazuri.

Kwa mfano, mfikirie Yosefu mwana wa Yakobo. Yosefu alipokuwa na umri wa miaka 17, ndugu zake walimuuza isivyo haki kuwa mtumwa. (Mwa. 37:2, 26-28) Bila shaka hakutarajia kutendewa hivyo na ndugu zake. Hata hivyo, alikuwa tayari kukabiliana na hali hiyo, na kwa baraka za Yehova “akaja kusimamia nyumba ya bwana wake.” (Mwa. 39:2) Baadaye, Yosefu alifungwa gerezani. Lakini aliendelea kuwa mwaminifu, na Yehova alikuwa pamoja naye, hivi kwamba mwishowe alipewa daraka la kusimamia mambo gerezani.—Mwa. 39:21-23.

Yosefu hakujua kwamba miaka yote aliyokuwa gerezani ingetimiza kusudi fulani. Aliendelea tu kufanya mambo aliyoweza. Hivyo, Yehova alimtumia katika kuulinda ukoo ambao ungetokeza Uzao ulioahidiwa. (Mwa. 3:15; 45:5-8) Ingawa hakuna mmoja wetu anayeweza kutarajia kutimiza daraka kubwa kama Yosefu alivyofanya, simulizi hilo lililoongozwa na roho ya Mungu linaonyesha kwamba mkono wa Yehova unahusika katika mapendeleo ambayo watumishi Wake wanapewa. Mwige Yosefu kwa kuendelea kuacha mlango wa kupata mapendeleo ukiwa wazi.

Kujifunza Kutokana na Hali Ngumu

Ayubu, Manase, na Yosefu walikabili hali zenye kuvunja moyo. Wanaume hao wote watatu walikubali hali ambazo Yehova aliruhusu ziwapate, na kila mmoja wao alijifunza mambo ya maana. Unaweza kujifunza nini?

Tambua jambo ambalo huenda Yehova anajaribu kukufundisha. Alipokuwa akikabiliana na mfadhaiko, Ayubu alijifikiria mwenyewe kupita kiasi naye hakutambua masuala makubwa zaidi. Hata hivyo, kwa sababu alirekebishwa na Yehova kwa upendo, alipata usawaziko tena, naye akakubali hivi: “Nilisema, lakini sikuwa ninaelewa.” (Ayu. 42:3) Ikiwa unaumia kihisia kwa sababu ya kupoteza mapendeleo, ‘usijifikirie mwenyewe zaidi kuliko ilivyo lazima kufikiri; bali fikiri ili uwe na akili timamu.’ (Rom. 12:3) Huenda Yehova anajaribu kukurekebisha katika njia ambayo kwa sasa huielewi vizuri kabisa.

Kubali nidhamu. Huenda mwanzoni Manase alihisi kwamba hakustahili adhabu kali aliyopewa. Hata hivyo, aliikubali, akatubu, na kuacha mwenendo wake mbaya. Hata iwe unahisi jinsi gani kuhusu nidhamu ambayo umepewa, ‘jinyenyekeze machoni pa Yehova, naye atakuinua.’—1 Pet. 5:6; Yak. 4:10.

Uwe na subira na uwe tayari kutumika. Kwa sababu ya mambo yaliyompata, ingekuwa rahisi kwa Yosefu kuwa na chuki na tamaa ya kulipiza kisasi. Badala yake, alisitawisha ufahamu na rehema. (Mwa. 50:15-21) Ikiwa umevunjwa moyo, uwe na subira. Uwe tayari kuzoezwa na Yehova.

Je, wakati fulani ulitumikia ukiwa na pendeleo katika kutaniko la Kikristo? Mpe Yehova nafasi ya kukupa mapendeleo wakati ujao. Itie nguvu hali yako ya kiroho. Kabiliana na hisia zako kwa subira na unyenyekevu. Uwe tayari kukubali mgawo wowote ambao utapewa. Uwe na hakika kwamba “Yehova mwenyewe hatawanyima jambo lolote jema wale wanaotembea bila kosa.”—Zab. 84:11.

[Blabu katika ukurasa wa 30]

Uwe na nguvu katika imani kwa kusali kutoka moyoni

[Picha katika ukurasa wa 31]

Kuongeza utendaji katika utumishi wa shambani ni njia nzuri ya kuboresha hali yako ya kiroho

[Picha katika ukurasa wa 32]

Mpe Yehova nafasi ya kukupa mapendeleo wakati ujao