Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ufalme wa Mungu Ni Bora Katika Njia Zote

Ufalme wa Mungu Ni Bora Katika Njia Zote

YESU KRISTO aliwafundisha wafuasi wake hivi: “Basi, ninyi msali hivi: ‘Baba yetu uliye mbinguni, jina lako na litakaswe. Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.’” (Mathayo 6:9, 10) Sala hiyo ambayo wengi wanaiita Baba Yetu, au Sala ya Bwana, inaeleza kusudi la Ufalme wa Mungu.

Kupitia Ufalme huo, jina la Mungu litatakaswa. Shutuma zote ambazo uasi wa Shetani na wa wanadamu umeleta dhidi ya jina lake zitaondolewa. Hilo ni jambo muhimu. Furaha ya viumbe wote wenye akili inategemea kuliona jina la Mungu kuwa takatifu na kukubali kwa hiari kwamba yeye ndiye mwenye haki ya kutawala.—Ufunuo 4:11.

Pia, Ufalme huo umesimamishwa ili “mapenzi [ya Mungu] yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.” Mapenzi hayo ni nini? Ni kurudisha uhusiano kati ya Mungu na wanadamu, ambao Adamu alipoteza. Isitoshe, Ufalme huo utatimiza kusudi la Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote, Yehova, la kufanya dunia kuwa paradiso ambapo wanadamu wazuri wanaweza kuishi milele. Naam, Ufalme wa Mungu utaondoa uovu wote ambao umesababishwa na ile dhambi ya kwanza nao utatimiza kusudi la Mungu kwa ajili ya dunia. (1 Yohana 3:8) Kwa kweli, Ufalme huo na mambo utakayotimiza ndio ujumbe mkuu zaidi katika Biblia.

Ni Bora kwa Njia Gani?

Ufalme wa Mungu ni serikali halisi yenye mamlaka kubwa. Nabii Danieli alituonyesha kidogo jinsi ulivyo na mamlaka. Alitabiri hivi zamani za kale: “Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao . . . utazivunja na kuzikomesha falme . . . zote [za wanadamu].” Isitoshe, tofauti na serikali za wanadamu ambazo husimama na kuanguka, Ufalme wa Mungu “hautaharibiwa kamwe.” (Danieli 2:44) Na si hayo tu. Katika kila njia, Ufalme huo ni bora kuliko serikali yoyote ya wanadamu.

Ufalme wa Mungu una Mfalme bora.

Fikiria mambo yafuatayo kuhusu Mfalme huyo. Katika “ndoto na maono” aliyoonyeshwa, Danieli alimwona “mtu fulani kama mwana wa binadamu,” ambaye ni Mtawala wa Ufalme wa Mungu, akiletwa mbele ya Mungu Mweza-Yote na kupewa “utawala na heshima na ufalme.” (Danieli 7:1, 13, 14) Huyo Mwana wa binadamu si mwingine ila Yesu Kristo, au Masihi. (Mathayo 16:13-17) Yehova Mungu alimchagua Mwana wake, Yesu, kuwa Mfalme wa Ufalme Wake. Alipokuwa duniani, Yesu aliwaambia Mafarisayo waovu hivi: “Ufalme wa Mungu umo katikati yenu,” akimaanisha kwamba yeye, akiwa Mfalme wa wakati ujao wa Ufalme huo alikuwa katikati yao.—Luka 17:21.

Ni mwanadamu gani anayeweza kuwa na sifa kama za Yesu akiwa Mtawala? Tayari Yesu amethibitika kuwa Kiongozi mwadilifu sana, anayetegemeka, na mwenye huruma. Vitabu vya Injili vinamfafanua kuwa mtu wa vitendo, mchangamfu, na mwenye hisia sana. (Mathayo 4:23; Marko 1:40, 41; 6:31-34; Luka 7:11-17) Isitoshe, akiwa mbinguni baada ya kufufuliwa, Yesu hawezi kufa wala kuwa na udhaifu wowote wa kibinadamu. —Isaya 9:6, 7.

Yehova amemchagua Yesu Kristo kuwa Mfalme wa Ufalme Wake

Yesu na wale watakaotawala pamoja naye wanatawala wakiwa mahali bora zaidi.

Katika ndoto na maono yake, Danieli aliona kwamba ‘ufalme na utawala ulipewa watu ambao ni watakatifu.’ (Danieli 7:27) Yesu hatatawala akiwa peke yake. Kuna wengine watakaotawala pamoja naye wakiwa wafalme na makuhani. (Ufunuo 5:9, 10; 20:6) Mtume Yohana aliandika hivi kuwahusu: “Nikaona, na, tazama! Mwana-Kondoo amesimama juu ya Mlima Sayuni, na pamoja naye 144,000 . . . ambao wamenunuliwa kutoka duniani.”—Ufunuo 14:1-3.

Mwana-Kondoo ni Yesu Kristo akiwa Mfalme aliyetawazwa wa Ufalme wa Mungu. (Yohana 1:29; Ufunuo 22:3) Mlima Sayuni unarejelea mbinguni. * (Waebrania 12:22) Yesu pamoja na washirika wenzake 144,000 wanatawala wakiwa mbinguni. Hapo ni mahali penye utukufu kama nini! Wakiwa mbinguni, wanaona mambo mengi. Kwa kuwa kiti cha ufalme huo kiko mbinguni, “ufalme wa Mungu” huitwa pia “ufalme wa mbinguni.” (Luka 8:10; Mathayo 13:11) Hakuna silaha zozote, hata za nyuklia, zinazoweza kuifikia na kuiharibu serikali hiyo ya mbinguni. Haiwezi kushindwa, nayo itatimiza kusudi la Yehova.—Waebrania 12:28.

Ufalme wa Mungu una wawakilishi waaminifu duniani.

Tunajuaje? Andiko la Zaburi 45:16 linasema: ‘Utawaweka wakuu katika dunia yote.’ Katika unabii huo, ‘anayewaweka’ ni Mwana wa Mungu. (Zaburi 45:6, 7; Waebrania 1:7, 8) Hivyo, Yesu Kristo mwenyewe atawaweka rasmi wakuu watakaomwakilisha. Tuna uhakika kwamba watafuata mwongozo wake kwa uaminifu. Hata leo, wanaume wanaostahili ambao wanatumikia wakiwa wazee katika makutaniko ya Kikristo wanafundishwa ‘wasipige ubwana’ juu ya waamini wenzao, badala yake wawalinde, wawaburudishe, na kuwafariji. —Mathayo 20:25-28; Isaya 32:2.

Ufalme una raia waadilifu.

Mungu anawaona kuwa wanyoofu na wasio na lawama. (Methali 2:21, 22) Biblia inasema: “Wapole wataimiliki dunia, nao watapata furaha yao tele katika wingi wa amani.” (Zaburi 37:11) Raia wa Ufalme huo ni wapole, yaani, wanakubali kufundishwa na ni wanyenyekevu. Wanahangaikia hasa mambo ya kiroho. (Mathayo 5:3) Wanapenda kufanya mema nao hukubali mwongozo wa Mungu.

Ufalme wa Mungu una sheria bora zaidi.

Sheria na kanuni zinazoongoza Ufalme huo zinatoka kwa Yehova Mungu mwenyewe. Badala ya kutulemea isivyo haki, sheria na kanuni hizo hutufaidi. (Zaburi 19:7-11) Tayari watu wengi wanafaidika kwa kuishi kulingana na matakwa ya uadilifu ya Yehova. Kwa mfano, tunapotii shauri la Biblia kwa waume, wake, na watoto, tunaboresha maisha ya familia zetu. (Waefeso 5:33–6:3) Tunapotii amri ya ‘kujivika upendo,’ tunaboresha uhusiano wetu na wengine. (Wakolosai 3:13, 14) Tunapoishi kulingana na kanuni za Kimaandiko, tunakuwa wenye bidii kazini na kuwa na maoni yaliyosawazika kuhusu pesa. (Methali 13:4; 1 Timotheo 6:9, 10) Kujiepusha na ulevi, ukosefu wa maadili katika ngono, tumbaku, na dawa za kulevya hutusaidia kutunza afya yetu.—Methali 7:21-23; 23:29, 30; 2 Wakorintho 7:1.

Ufalme wa Mungu ni serikali iliyosimamishwa na Mungu. Mungu anataka Mfalme wake, yaani, Masihi, Yesu Kristo, na wale watakaotawala pamoja naye watekeleze sheria Zake za haki na kanuni Zake za upendo. Raia wa Ufalme huo, kutia ndani wawakilishi wake duniani, hufurahia kuishi kulingana na sheria za Mungu. Hivyo, hangaiko kuu la watawala na raia wa Ufalme huo ni kumpendeza Mungu. Kwa kweli, Mungu ndiye mtawala wa Ufalme huo. Bila shaka, ufalme huo utafanikiwa kutimiza kusudi lililofanya usimamishwe. Hata hivyo, Ufalme wa Mungu, unaoitwa pia Ufalme wa Kimasihi, utaanza kutawala wakati gani?

Ufalme Unaanza Kutawala

Maneno ya Yesu yanaweza kutusaidia kuelewa wakati ambapo Ufalme ungeanza kutawala. Alisema: “Yerusalemu litakanyagwa-kanyagwa na mataifa, mpaka nyakati zilizowekwa za mataifa zitimie.” (Luka 21:24) Yerusalemu ndilo jiji pekee lililohusianishwa moja kwa moja na jina la Mungu. (1 Wafalme 11:36; Mathayo 5:35) Lilikuwa jiji kuu la ufalme wa kidunia uliokubaliwa na Mungu. Jiji hilo lingekanyagwa-kanyagwa na mataifa katika maana ya kwamba utawala wa Mungu juu ya watu wake ungekatizwa na serikali za ulimwengu. Hilo lingeanza wakati gani?

Mfalme wa mwisho aliyekalia kiti cha enzi cha Yehova huko Yerusalemu aliambiwa hivi: “Kiondoe kilemba, na kulivua taji. . . . Hakika hili halitakuwa la mtu yeyote mpaka atakapokuja yule aliye na haki ya kisheria, nami nitampa yeye.” (Ezekieli 21:25-27) Taji lilipaswa kuondolewa kwenye kichwa cha mfalme huyo, na Ufalme wa Mungu juu ya watu wake kukatizwa. Hilo lilitukia mwaka wa 607 K.W.K., wakati Wababiloni walipoharibu Yerusalemu. Katika “nyakati zilizowekwa” ambazo zingefuata, Mungu hangekuwa na serikali duniani ambayo ingewakilisha utawala wake. Mwishoni mwa nyakati hizo ndipo Yehova angempa Yesu Kristo, “yule aliye na haki ya kisheria,” mamlaka ya kutawala. Kipindi hicho kingekuwa na urefu gani?

Unabii katika kitabu cha Danieli unasema hivi: “Ukateni mti uanguke, na kuuharibu. Hata hivyo, kiacheni kisiki chake katika udongo, lakini kikiwa na pingu ya chuma na ya shaba . . . mpaka nyakati saba zipite juu yake.” (Danieli 4:23) Kama tutakavyoona, “nyakati saba” zinazotajwa hapa zinalingana na “nyakati zilizowekwa za mataifa.”

Katika Biblia, nyakati nyingine watu, watawala, na falme huwakilishwa na miti. (Zaburi 1:3; Yeremia 17:7, 8; Ezekieli, sura ya 31) Mti huo wa mfano “ulikuwa unaonekana mpaka sehemu za mwisho za dunia nzima.” (Danieli 4:11) Hivyo, utawala uliowakilishwa na mti huo na ambao ungekatwa uanguke na kufungwa pingu ulifika “mpaka sehemu za mwisho za dunia,” kutia ndani ufalme wote wa wanadamu. (Danieli 4:17, 20, 22) Kwa hiyo, mti huo unawakilisha utawala mkuu zaidi wa Mungu, hasa kuhusiana na dunia. Utawala huo uliwakilishwa kwa muda na ufalme ambao Yehova alisimamisha katika taifa la Israeli. Mti huo wa mfano ulikatwa, na pingu za chuma na shaba zikafungwa kwenye kisiki chake ili kuuzuia usikue. Hilo lilimaanisha kwamba ufalme ambao Mungu alitumia kutawala duniani ungekoma kwa muda, kama ilivyotukia mwaka wa 607 K.W.K. Mti huo ungefungwa pingu mpaka “nyakati saba” zipite. Mwishoni mwa kipindi hicho, Yehova angempa utawala mrithi halali, Yesu Kristo. Basi, “nyakati saba” na “nyakati zilizowekwa za mataifa” zinawakilisha kipindi kilekile cha wakati.

Biblia hutusaidia kujua urefu wa “nyakati saba.” Inalinganisha siku 1,260 na “wakati [mmoja] na nyakati [mbili, wingi wa wakati] na nusu ya wakati,” kwa jumla, “nyakati” tatu na nusu. (Ufunuo 12:6, 14) Hiyo inamaanisha kwamba mara mbili ya namba hiyo, au nyakati saba, ni siku 2,520.

Tukihesabu siku halisi 2,520 kutoka mwaka wa 607 K.W.K., tunafikia mwaka wa 600 K.W.K. Hata hivyo, nyakati saba zilichukua muda mrefu zaidi. Bado zilikuwa zinaendelea wakati Yesu aliposema kuhusu “nyakati zilizowekwa za mataifa.” Kwa hiyo, hizo nyakati saba ni za kinabii. Hivyo, ni lazima tutumie kanuni hii ya Kimaandiko: “Siku moja kwa mwaka mmoja.” (Hesabu 14:34; Ezekieli 4:6) Hivyo basi, nyakati saba, ambazo zinawakilisha muda ambao dunia imetawaliwa na serikali za ulimwengu bila Mungu kuingilia kati, ni jumla ya miaka 2,520. Tukihesabu miaka 2,520 kuanzia mwaka wa 607 K.W.K., tunafikia mwaka wa 1914 W.K. Huo ndio mwaka ambao “nyakati zilizowekwa za mataifa” au nyakati saba zilimalizika. Hiyo inamaanisha kwamba Yesu Kristo alianza kutawala akiwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu mwaka wa 1914.

“Ufalme Wako na Uje”

Kwa kuwa Ufalme wa Kimasihi tayari umesimamishwa mbinguni, je, tunapaswa kuendelea kuomba uje kama Yesu alivyofundisha katika sala ya kielelezo? (Mathayo 6:9, 10) Ndiyo. Ombi hilo linafaa na bado lina maana kubwa. Hivi karibuni Ufalme wa Mungu utatawala dunia hii kwa ukamili.

Wanadamu waaminifu watafurahia baraka nyingi wakati huo utakapofika! Biblia inasema: “Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.” (Ufunuo 21:3, 4) Wakati huo, “Hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’” (Isaya 33:24) Wale wanaompendeza Mungu watapata uzima wa milele. (Yohana 17:3) Tunapongojea kutimizwa kwa unabii huo wa Biblia wenye kuvutia na mwingine mwingi, acheni ‘tuendelee kuutafuta kwanza ufalme wa Mungu na uadilifu wake.’—Mathayo 6:33.

^ fu. 10 Mfalme Daudi wa Israeli la kale aliiteka ngome ya Mlima Sayuni wa kidunia kutoka kwa Wayebusi na kuifanya kuwa jiji lake kuu. (2 Samweli 5:6, 7, 9) Pia, alilipeleka Sanduku takatifu huko. (2 Samweli 6:17) Kwa kuwa Sanduku lilihusianishwa na kuwapo kwa Yehova, Sayuni liliitwa mahali pa makao ya Mungu, nalo linafaa kabisa kuwakilisha mbinguni.—Kutoka 25:22; Mambo ya Walawi 16:2; Zaburi 9:11; Ufunuo 11:19.