Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Mungu Wetu Anaweza Kutuokoa’

‘Mungu Wetu Anaweza Kutuokoa’

“Lazima Tumtii Mungu Kuwa Mtawala Kuliko Wanadamu”

‘Mungu Wetu Anaweza Kutuokoa’

TUKIO hilo lilikusudiwa liwe lenye kustaajabisha. Sanamu kubwa ya dhahabu ilikuwa imesimamishwa katika nchi tambarare ya Dura, yaelekea karibu na jiji la Babiloni. Sanamu hiyo ilipaswa kuzinduliwa wakati wa sherehe ya pekee iliyohudhuriwa na wakuu ambao walitazamiwa kuiinamia baada ya kusikia sauti ya vyombo mbalimbali vya muziki. Mfalme Nebukadneza wa Babiloni alikuwa ametangaza kwamba yeyote ambaye hangeiabudu sanamu hiyo, angeuawa kwa kutupwa ndani ya tanuru yenye moto mkali. Ni nani angethubutu kuvunja amri hiyo?

Watazamaji walishangaa kuona kwamba waabudu watatu wa Yehova, Shadraki, Meshaki, na Abednego, hawakuiinamia sanamu hiyo. Walijua kwamba kuiinamia kungekuwa kinyume cha ujitoaji wao kwa Yehova Mungu peke yake. (Kumbukumbu la Torati 5:8-10) Walipoamriwa waeleze msimamo wao imara, bila kuogopa walimwambia hivi Nebukadneza: “Kama ni hivyo, Mungu ambaye tunamtumikia anaweza kutuokoa. Yeye atatuokoa kutoka katika tanuru inayowaka moto na kutoka mkononi mwako, Ee mfalme. Lakini kama sivyo, ujue hivi, Ee mfalme, kwamba sisi hatuitumikii miungu yako, na sanamu ambayo umeisimamisha hatutaiabudu.”—Danieli 3:17, 18.

Waebrania hao watatu waliokolewa kimuujiza baada ya kutupwa ndani ya tanuru ya moto. Mungu alimtuma malaika awalinde watumishi Wake waaminifu. Hata hivyo, walikuwa tayari kufa badala ya kumwasi Yehova. * Hali yao ilikuwa sawa na ya mitume wa Yesu Kristo ambao zaidi ya karne sita baadaye walitangaza hivi mbele ya mahakama kuu ya Kiyahudi: “Lazima tumtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.”—Matendo 5:29.

Mambo Muhimu Tunayojifunza

Shadraki, Meshaki, na Abednego ni mifano mizuri ya watu wenye imani, utii, na ushikamanifu. Waebrania hao watatu walikuwa na imani katika Yehova. Dhamiri yao iliyozoezwa na Maandiko haikuwaruhusu kufanya tendo lolote la ibada ya uwongo au la kutukuza taifa. Vivyo hivyo, Wakristo leo humtegemea kabisa Mungu wa kweli. Wanaongozwa na dhamiri yao iliyozoezwa na Biblia, nao hukataa kushiriki katika matendo ya ibada ya uwongo au sherehe ambazo hazipatani na sheria na kanuni za Mungu.

Waebrania hao watatu waaminifu, walimtegemea Yehova nao hawakuruhusu mambo yoyote ambayo yangewapa umashuhuri, cheo, au utukufu katika Milki ya Wababiloni yawazuie wasimtii Yehova. Vijana hao walikuwa tayari kuteseka na kufa badala ya kuharibu uhusiano wao pamoja na Mungu. Kama vile Musa aliyeishi kabla yao, ‘waliendelea kuwa imara kama wanaomwona Yeye asiyeonekana.’ (Waebrania 11:27) Iwe Yehova alichagua kuwaokoa kutokana na kifo au la, Waebrania hao watatu waliazimia kudumisha utimilifu wao kwake badala ya kuvunja sheria ya Yehova ili kuokoa uhai wao. Yaelekea mtume Paulo alikuwa akizungumzia mfano wao alipotaja watu waaminifu ambao ‘walizuia nguvu za moto.’ (Waebrania 11:34) Katika siku zetu, watumishi wa Yehova huonyesha imani na utii kama huo wanapokabili majaribu ya utimilifu wao.

Kisa cha Shadraki, Meshaki, na Abednego kinatufundisha kwamba Mungu huwapa thawabu wale walio washikamanifu kwake. Mtunga-zaburi aliimba hivi: “Yehova . . . hatawaacha washikamanifu wake.” (Zaburi 37:28) Leo, hatutazamii Mungu atuokoe kimuujiza kama alivyowaokoa wale Waebrania watatu. Hata hivyo, tunaweza kuwa na uhakika kwamba Baba yetu wa mbinguni atatusaidia tunapokabili matatizo mbalimbali. Mungu anaweza kutuondolea tatizo, kutupa nguvu za kulivumilia, au kutufufua iwapo tutadumisha utimilifu wetu hadi kifo. (Zaburi 37:10, 11, 29; Yohana 5:28, 29) Kila wakati utimilifu wetu unapojaribiwa na tunapochagua kumtii Mungu kuliko wanadamu, imani, utii, na ushikamanifu hushinda.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Ona Kalenda ya Mashahidi wa Yehova 2006, Julai/Agosti.

[Picha katika ukurasa wa 9]

JE, ULIJUA?

• Wale Waebrania watatu walikuwa na umri wa karibu miaka 30 walipokabili jaribu la utimilifu.

• Inaonekana tanuru iliongezwa moto mwingi.—Danieli 3:19.