Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutembea Katika Njia za Yehova Huthawabisha Sana

Kutembea Katika Njia za Yehova Huthawabisha Sana

Kutembea Katika Njia za Yehova Huthawabisha Sana

JE, UMEWAHI kupanda mlima? Ikiwa umewahi, yaelekea ulihisi kana kwamba ulikuwa kwenye paa la dunia. Ilifurahisha kama nini kuvuta hewa safi, kuona mbali, kuangalia uumbaji wenye kuvutia! Labda hukutilia maanani mahangaiko ya kila siku.

Watu wengi huwa hawapandi milima, lakini kama wewe ni Mkristo aliyejiweka wakfu, huenda ikawa kwa muda fulani umefuata mwendo wa maisha ambao waweza kulinganishwa na kupanda mlima. Kama mtunga-zaburi wa kale, labda umesali hivi: “Ee BWANA, unijulishe njia zako, unifundishe mapito yako.” (Zaburi 25:4) Je, unakumbuka jinsi ulivyohisi ulipokwenda mlimani pa nyumba ya Yehova mara ya kwanza na kuanza kuupanda? (Mika 4:2; Habakuki 3:19) Labda ulitambua upesi kwamba ulipata ulinzi na shangwe kwa kutembea katika njia hizo za juu za ibada safi. Ulianza kuhisi kama mtunga-zaburi: “Heri watu wale waijuao sauti ya shangwe, Ee BWANA, huenenda katika nuru ya uso wako.”—Zaburi 89:15.

Hata hivyo, nyakati nyingine, lazima wapanda-milima wajitahidi kushuka miteremko mikali. Miguu yao huanza kuuma, nayo huchoka. Sisi pia tunaweza kupatwa na magumu katika utumishi wetu kwa Mungu. Huenda ikawa tumeanza kuchoka hivi karibuni. Twaweza kupataje tena nguvu na shangwe yetu? Hatua ya kwanza ni kutambua ubora wa njia za Yehova.

Sheria za Yehova za Juu

Njia za Yehova zi ‘juu sana kuliko za mwanadamu,’ na ibada yake ‘imewekwa imara juu ya milima, na kuinuliwa juu ya vilima.’ (Isaya 55:9; Mika 4:1) Hekima ya Yehova ni “hekima ya kutoka juu.” (Yakobo 3:17) Sheria zake ni za juu kuliko zote. Kwa mfano, wakati ambapo Wakanaani walitoa dhabihu za watoto, Yehova aliwapa Waisraeli sheria ambazo zilikuwa za juu kiadili na zenye huruma. Aliwaambia hivi: “Usimpendelee mtu maskini, wala kumstahi mwenye nguvu. . . . Mgeni . . . kama mzalia kwenu; mpende kama nafsi yako.”—Mambo ya Walawi 19:15, 34.

Karne 15 baadaye, Yesu alitoa mifano mingine ya ‘sheria tukufu ya Yehova.’ (Isaya 42:21) Katika Mahubiri yake ya Mlimani, aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Endeleeni kupenda maadui wenu na kusali kwa ajili ya wale wanaowanyanyasa nyinyi; ili mpate kujithibitisha wenyewe kuwa wana wa Baba yenu aliye katika mbingu.” (Mathayo 5: 44, 45) Kisha akaongeza “Mambo yote mtakayo watu wawafanyie nyinyi, lazima mwafanyie wao pia hivyohivyo, hili, kwa kweli, ndilo ambalo Sheria na Manabii humaanisha.”—Mathayo 7:12.

Sheria hizo za juu zimeathiri watu wenye mioyo mikunjufu, zikiwachochea wamwige Mungu wanayemwabudu. (Waefeso 5:1; 1 Wathesalonike 2:13) Fikiria jinsi ambavyo Paulo aligeuzwa. Jina lake linapotajwa mara ya kwanza, ni wakati alipokuwa ‘akikubali kuuawa kimakusudi’ kwa Stefano na akilitendea “kutaniko kwa njia mbaya kabisa.” Miaka michache baadaye, alikuwa anawatendea kwa uanana Wakristo Wathesalonike kama vile “mama mwenye kunyonyesha atunzavyo sana watoto wake.” Mafundisho ya Mungu yalimgeuza Paulo aliyekuwa mnyanyasaji, akawa Mkristo mwenye kujali. (Matendo 8:1, 3; 1 Wathesalonike 2:7) Kwa hakika alishukuru kwamba utu wake ulikuwa umegeuzwa na mafundisho ya Kristo. (1 Timotheo 1:12, 13) Shukrani kama hizo zaweza kutusaidiaje tutembee katika njia za Mungu za juu?

Kutembea kwa Shukrani

Wapanda-milima hufurahia mandhari nzuri wakiwa juu ya milima. Pia hujifunza kufurahia polepole vitu vidogo-vidogo njiani, kama vile miamba ya pekee, maua mazuri, au mnyama. Katika maana ya kiroho, twahitaji kuwa macho kuona thawabu—kubwa na ndogo—zinazotokana na kutembea pamoja na Mungu. Kujua hivyo kwaweza kutufanya tutembee tukiwa na nguvu mpya na kufanya mwendo wenye kuchosha uwe wenye kuburudisha. Tutakubaliana na maneno ya Daudi yasemayo: “Unifanye kusikia fadhili zako asubuhi, kwa maana nimekutumaini wewe. Unijulishe njia nitakayoiendea.”—Zaburi 143:8.

Mary, ambaye ametembea kwa miaka mingi katika njia za Yehova, asema hivi: “Ninapotazama uumbaji wa Yehova, sioni tu ubuni wake ulio tata bali pia utu wa Mungu wenye upendo. Iwe ni mnyama, ndege, au mdudu, kila mmoja wao ni tofauti, ni mwenye kupendeza sana. Ndivyo kweli za kiroho zinavyofurahisha zinapoendelea kueleweka mwaka baada ya mwaka.”

Twaweza kuonyeshaje shukrani zaidi? Kwa kutopuuza yale ambayo Yehova anatufanyia. “Salini bila kukoma,” akasema Paulo. “Kuhusiana na kila jambo toeni shukrani.”—1 Wathesalonike 5:17, 18; Zaburi 119:62.

Funzo la kibinafsi hutusaidia kuwa na roho ya shukrani. Paulo aliwasihi Wakristo Wakolosai hivi: “Endeleeni kutembea katika muungano na yeye [Kristo Yesu], . . . mkifurikwa na imani katika utoaji-shukrani.” (Wakolosai 2:6, 7) Kusoma Biblia na kutafakari yale tunayosoma huimarisha imani yetu na kutufanya tuwe na uhusiano wa karibu na Mtungaji wa Biblia. Katika Biblia nzima tunapata hazina ambazo zaweza kutuchochea ‘tufurikwe na shukrani.’

Pia kutumikia Yehova pamoja na ndugu zetu hufanya njia iwe rahisi kutembea. Mtunga-zaburi alisema hivi kujihusu: “Mimi ni mwenzao watu wote wakuchao.” (Zaburi 119:63) Baadhi ya nyakati tunazokuwa na furaha zaidi ni wakati tunapokuwa kwenye makusanyiko ya Kikristo au wakati tunapokuwa na ndugu zetu. Twatambua kwamba familia yetu ya Kikristo yenye thamani inayopatikana ulimwenguni pote ipo kwa sababu ya Yehova na njia zake za juu.—Zaburi 144:15b.

Zaidi ya kuwa wenye shukrani, tukihisi kuwa tuna wajibu tutaimarishwa kufanya maendeleo tunapotembea katika njia za Yehova za juu.

Kutembea Tukiwa na Wajibu

Wapanda-milima wanaojiona kuwa na wajibu hutambua uhitaji wa kutembea kwa uangalifu ikiwa wataepuka kupotea au kujikuta kwenye miamba yenye miteremko mikali. Tukiwa viumbe wenye uhuru wa kuchagua, Yehova anatupatia uhuru wa kadiri. Lakini uhuru huo hutaka tuone wajibu wetu wa kutimiza madaraka yetu ya Kikristo.

Kwa mfano, Yehova anatumaini kwamba watumishi wake watatimiza madaraka yao. Hasemi ni nguvu na wakati kadiri gani tunaopaswa kutumia katika utendaji wa Kikristo au ni kiasi gani cha fedha tunachopaswa kuchanga au utoaji mwingineo. Badala yake, maneno ya Paulo kwa Wakorintho yanatuhusu sote: “Acheni kila mmoja afanye kama vile ameazimia moyoni mwake.”—2 Wakorintho 9:7; Waebrania 13:15, 16.

Mkristo anayeona wajibu wa kutoa huwahubiria wengine habari njema. Pia twaonyesha tunawajibika kwa kutoa michango kwa ajili ya kazi ya Ufalme ya ulimwenguni pote. Gerhardt, mzee wa kutaniko, anaeleza kwamba yeye na mke wake waliongeza michango yao zaidi baada ya kuhudhuria kusanyiko huko Ulaya Mashariki. Alisema hivi: “Tuliona kwamba ndugu zetu huko wana vitu vichache sana vya kimwili, lakini wanathamini sana vichapo vyetu vya Biblia. Kwa hiyo tukaamua kwamba tungetaka kutegemeza kadiri tuwezavyo ndugu zetu wenye uhitaji katika nchi nyingine.”

Kuendelea Kuvumilia

Kutembea milimani kwahitaji nguvu. Wapanda-milima hufanya mazoezi wanapoweza, na wengi hutembea miendo mifupi ili wajitayarishe kutembea miendo mirefu. Vivyo hivyo, Paulo alipendekeza kwamba twendelee kuwa wenye shughuli nyingi katika utendaji wa kitheokrasi ili tudumishe hali nzuri ya kiroho. Wale wanaotaka ‘kutembea kwa kumstahili Yehova’ na wanaotaka ‘kufanywa wenye nguvu,’ Paulo alisema, wanapaswa ‘kuendelea kuzaa matunda katika kila kazi njema.’—Wakolosai 1:10, 11.

Ili mpandaji mlima avumilie na kupata matokeo mazuri anahitaji kichocheo. Jinsi gani? Kukazia fikira lengo hususa, kama vile kutazama mlima ulio mbali, kunaleta kichocheo. Na mpandaji mlima anapofika sehemu anazofahamu, anaweza kukadiria maendeleo yake kuelekea mradi wake. Anapotazama nyuma kuona mahali ambapo ametoka, yeye huhisi ameridhika.

Vivyo hivyo, tumaini letu la uhai udumuo milele hutuimarisha na kutuchochea. (Waroma 12:12) Kwa wakati uliopo, tunapotembea katika njia za Yehova, twatimiza na kufikia miradi yetu ya Kikristo. Na tunakuwa na shangwe kama nini tunapokumbuka miaka yetu ya utumishi mwaminifu au kuona mabadiliko ya utu wetu ambayo tumefanya!—Zaburi 16:11.

Watembeaji hutembea mwendo ulio imara ili wasafiri mbali na kuhifadhi nguvu yao. Hali kadhalika, mpango mzuri unaotia ndani kuhudhuria mikutano kwa ukawaida na utumishi wa shambani utatusaidia kusonga kwa makini kuelekea mradi wetu. Hivyo, Paulo aliwatia moyo Wakristo wenzake: “Acheni tuendelee kutembea kwa utaratibu katika kawaida hiyohiyo.”—Wafilipi 3:16.

Bila shaka, hatutembei peke yetu katika njia za Yehova. “Tukaangaliane sisi kwa sisi na kuhimizana katika upendo na kazi nzuri,” aandika Paulo. (Waebrania 10:24, Union Version) Mashirika mazuri ya kiroho yatafanya iwe rahisi kwetu kuendelea kutembea pamoja na waamini wenzetu.—Mithali 13:20.

Hatimaye, jambo la maana zaidi ni kwamba hatupaswi kamwe kusahau nguvu ambayo Yehova hutupatia. Wale ambao wanategemezwa na Yehova ‘wataendelea toka nguvu hata nguvu.’ (Zaburi 84:5, 7) Ingawa huenda lazima nyakati nyingine tupitie magumu, tunaweza kufaulu kwa msaada wa Yehova.